Friday, April 24, 2015

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje akutana kwa mazungumzo na CEO wa Standard Chartered nchini

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Dkt. Mahadhi Juma Maalim (Mb.) akimkaribisha Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Standard Chartered nchini Bi. Liz Lloyd alipomtembelea Wizarani kwa ajili ya mazungumzo na Mhe. Maalim. 
Mhe. Maalim akimtambulisha kwa Bi. Llyoid Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Simba Yahya. 
Mhe. Dkt.  Maalim akizungumza na Bi. Lloyd
Ujumbe alioambatana nao Bi. Lloyd wakifuatilia mazungumzo.
Bi. Lloyd nae alipata wasaa wa kuchangia hoja wakati wa mazungumzo na Dkt.  Maalim 
Balozi  Yahya (kushoto) akiwa na Katibu wa Naibu Waziri Bw. Adam Isara wakisikiliza mazungumzo kati ya Dkt. Maalim na Bi. Lloyd (hawapo pichani)
Mazungumzo yakiendelea.


Picha na Reginald Kisaka.

Membe awahimiza Watanzania kuchangamkia fursa Comoro


Mhe. Bernard Membe, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Tanzania akihutubia Kongomano la Biashara baina ya Tanzania na Comoro jijini Moroni Alhamis tarehe 23 Aprili 2015



Membe awahimiza Watanzania kuchangamkia fursa za kibiashara na kuwekeza katika Visiwa vya Comoro

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb.)  amewahimiza wafanyabiashara wa Tanzania kuchangamkia fursa za biashara na uwekezaji Visiwani Comoro kwani uhusiano baina ya nchi hizi mbili umeimarika.

Mhe. Membe alitoa kauli hiyo wakati akilihutubia Kongamano la Biashara baina ya Tanzania na Comoro lililoandaliwa na Balozi za Tanzania na Comoro kwa kushirikiana na sekta binafsi za nchi hizo mbili jijini Moroni, Comoro tarehe 23 Aprili, 2015.

 “Watanzania tunathaminiwa sana hapa kutokana na mchango wetu mwaka 2008 tulipokikomboa Kisiwa cha Anjouan kutoka kwa Kanali Bacar. Sasa Serikali ya Umoja wa Visiwa vya Comoro imeimarika na uhusiano wetu umeshamiri. Wanatukaribisha sisi kwanza kushirikiana kibiashara, tuchangamkie fursa hii” alisema Waziri Membe.


Vilevile,  Mhe. Membe alisifu jitihada za ofisi za ubalozi wa nchi hizi mbili kwa kuitikia wito wa kuimarisha uhusiano wa kibiashara kwa kuandaa kongamano hilo la kihistoria.

“Rais Kikwete alipofanya ziara yake hapa mwaka 2014, aliahidi kukuza uhusiano wetu na kutoa wito wa kushirikiana kibiashara kwa manufaa ya nchi zetu. Nawapongeza sana Balozi Kilumanga na Balozi Fakih kwa kushirikiana na sekta binafsi na kutekeleza hili kwa wakati”alisema Waziri Membe, ambaye aliongoza ujumbe wa Tanzania kwenye kongamano hilo.

Kwa upande wake, Rais wa Visiwa vya Comoro, Mhe. Ikililou Dhoinine alisema kuwa yeye na Serikali yake wanathamini mchango mkubwa wa Tanzania kwa watu wa Comoro na hivyo atahakikisha uhusiano wetu unakua kwenye nyanja zote, Serikalini, sekta binafsi na hata baina ya watu wa nchi zote mbili.

Aidha, baada ya ufunguzi rasmi wa kongamano hilo, wafanyabiashara wa Tanzania walikutanishwa na wenzao wa Comoro kwenye makundi madogo madogo ili kuibua changamoto zinazokwaza biashara baina ya nchi hizo. Mikutano hiyo inatarajiwa kuibua njia bora zaidi ya kuwezesha biashara baina yao na kuimarisha uhusiano baina ya watu wake.

Akiwa jijini Moroni, Mhe. Membe alipata fursa ya kutembelea fukwe za bahari ambazo ni vivutio vikubwa vya utalii kwenye nchi hiyo ya visiwa akiwa na mwenyeji wake Mhe. Dkt. Alanrif Said Hussane, Waziri wa Mambo ya Nje wa Visiwa vya Comoro.

Serikali ya Tanzania ilifungua ofisi zake za ubalozi mwaka 2013 ambapo inawakilishwa nchini humo na Mhe. Chabaka Kilumanga, Balozi wa Tanzania, mwenye makazi yake Moroni. Kwa upande wa Serikali ya Comoro ilifungua Ubalozi wake nchini Tanzania mwaka 2014 na inawakilishwa na Mhe. Ahamed El Badaoui Mohamed Fakih Balozi wa Comoro mwenye makazi yake Dar es salaam.

Kongamano hilo la siku mbili lililofunguliwa na Mhe. Ikililou Dhoinine, Rais wa Visiwa vya Comoro, lilifanyika kwenye ukumbi wa bunge jijini Moroni, mojawapo ya visiwa vitatu vinavyounda Umoja wa Visiwa vya Comoro, na kuhudhuriwa na wafanyabiashara takriban mia moja kutoka Tanzania. Visiwa vingine vinavyounda umoja huo wa Comoro ni Ngazija (Grand Comoro), Anjouan na Moheli huku mji mkuu ukiwa Moroni.

-Mwisho-

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali kwa Umma,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa

Sehemu ya Wafanyabiashara waliohudhuria Kongamano hilo wakimsikiliza Mhe. Membe 

 Picha ya meza kuu ya viongozi wa Tanzania na Comoro,

katikati ni Rais wa Visiwa vya Comoro Mhe. Dk. Ikililou Dhoinine, 
akiwa na Mhe. Bernard Membe, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa 
Kimataifa wa Tanzania na Kiongozi wa Ujumbe wa Tanzania kwenye 
Kongomano la Biashara wakifuatilia ufunguzi.

 Rais wa Visiwa vya Comoro Mhe. Dk. Ikililou Dhoinine, akizungumza na Mhe. Bernard Membe, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Tanzania wakati wa ufunguzi rasmi wa Kongamano la BIashara baina ya Tanzania na Comoro tarehe 23 Aprili 2015 Moroni.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje amuaga Mwakilishi wa FAO nchini

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Mahadhi Juma Maalim (Mb.) akimkaribisha Mwakilishi wa Shirika la Chakula la Umoja wa Mataifa (F.A.O) nchini Bi. Diana E. Tempelman alipomtembelea ofisini kwake kwa ajili ya kumuaga baada ya kumaliza muda wake wa uwakilishi wa Shirika hilo hapa nchini. 
Mhe. Dkt. Mahadhi akizungumza na Bi. Diana kwa kumpongeza kwa uwakilishi wake mzuri wa Shirika la FAO hapa nchini
Bi. Diana nae akitoa neno la shukrani kwa Naibu Waziri kwa Ushirikiano mzuri aliokuwa akiupata kutoka Wizarani wakati wote akiwa hapa nchini.  

Picha na Reginald Philip

Wednesday, April 22, 2015

Waziri Membe azungumza na Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa UN eneo la Maziwa Makuu

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb.), akizungumza na Mwakilishi  Maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwenye Ukanda wa Maziwa Makuu, Bw.  Said Djinnit walipokutana kwa mazungumzo tarehe 22 Aprili, 2015. Katika mazungumzo yao waligusia masuala ya usalama katika Ukanda huo hususan hali ilivyo nchini DRC.
Waziri Membe akimweleza jambo Bw. Said Djinnit (katikati) huku Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilshi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini Bw. Alvaro Rodriguez akisikiliza kwa makini.
Waziri Membe (kulia) akiagana na Bw. Said Djinnit mara baada ya kumaliza mazungumzo yao


Picha na Reginald Philip

Tuesday, April 21, 2015

Watanzania 18 warejeshwa nchini kutokea Yemen

Kiongozi wa Msafara wa Watanzania waliorejeshwa nchini kutokea Yemen Bw. Abdul Twahid Said akizungumza na Waandishi wa Habari  kwa niaba ya wenzake mara baada ya kuwasili leo kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere  jijini Dar es Salaam kwa ndege ya Shirika la Emirates. Bw. Said alitoa shukrani kwa jitihada za Serikali za kuwarejesha nchini Watanzania wote kufuatia machafuko yanayoendelea nchini Yemen.
 Bw. Sabri Hery Omari ambaye ni miongoni mwa Watanzania waliorejea nae  akizungumza na Waandishi wa Habari huku sehemu nyingine ya Watanzania hao wakionekana kwa nyuma.
Watanzania waliurudishwa Nchini wakitokea nchini Yemeni kutokana na machafuko yanayoendelea huko wakifurahi kuwa nyumbani salama
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikali na Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Bi. Mindi Kasiga akizungumza mara baada ya Watanzania hao kuwasili nchini. Anayeonekana pembeni mwenye miwani ni Bw. Elibariki Maleko, Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Mashariki ya Kati katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ambaye alikuwepo wakati wa mapokezi hayo


Picha na Reginald Philip
============================================


Na. Reuben Mchome

Watanzania kumi na nane warejea kutoka Yemen.

Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania imefanikiwa kuwarejesha nyumbani jumla ya Watanzania kumi na nane kutoka nchini Yemen kufuatia mapigano yanayoendelea nchini humo ya wenyewe kwa wenyewe.

Watanzania hao ambao wamewasili nchini leo kwa ndege ya shirika la emirates namba EK 725 wameishukuru serikali kutokana na jitihada za haraka zilizofanywa kupitia ubalozi wa Tanzania nchini Oman na kufanikiwa kuwarejesha salama pasipo gharama zozote .

Akizungumza na waandishi wa habari kwa niaba ya Watanzania hao Bw. Sabri Abeid Almaghi ambaye alikua anafanya biashara nchini Yemen amesema kuwa anaishukuru Serikali ya Tanzania kwa namna ya pekee kwa kuwajali wananchi wake bila kujali wapo nchini au nje ya nchi na kutoa msaada  kwa wakati.

“Tunaishukuru sana serikali yetu ya Tanzania kwa jinsi ambavyo wanajali wananchi wake bila kujali wapo ndani au nje ya nchi,  kweli kama sio jitihada za ubalozi wetu pale mjini Muscat, sijui leo tungekua katika hali gani, tunaomba shukrani zetu mzifikishe kwa Rais Kikwete, Waziri Membe na wahusika wengine wote waliofanikisha kuturejesha nyumbani” alisema Mzee Saleh Mbaraka Jabri mmoja wa watanzania hao waliorejea kutoka Yemen.

Aidha, akizungumzia hali ya usalama ilivyo nchini Yemen, Bw. Almaghi amesema kuwa hali ni mbaya sana kufuatia mapigano ya anga yanayoendelea hivi sasa na muda wowote yataanza mapigano ya ardhini. Aidha amesema kuwa kufuatia hali hiyo huduma zote za kijamii pamoja na biashara zimesimama.

Akizungumza mara baada ya kuwapokea watanzania hao Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano serikalini Bi. Mindi Kasiga amesema mpaka hivi sasa watanzania ambao wamesharejeshwa nchini kutoka Yemen ni 23, kati ya   Watanzania 69 ambao wamejiandikisha  na jitihada  zinaendelea.

“Awamu ya kwanza ya Watanzania waliorejeshwa na serikali kutoka nchini Yemen ni familia moja ya watu watano ambao walirudi wiki chache zilizopita” alimalizia Bi. Mindi Kasiga.

Hivi karibuni Serikali kupitia Waziri wa Mambo  na Ushirikiano wa Kimataifa Mhe. Bernard Membe ilitangaza kuwarejesha nchini Watanzania waliopo Yemen kufuatia machafuko yanayoendelea nchini humo.


Tanzania yashiriki mkutano wa ushirikiano wa Afrika na Asia unaofanyika Indonesia

Mhe. Dkt. Mary M. Nagu (Mb) Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- Uratibu na Mahusiano akichangia hoja katika moja ya mijadala kwenye Mkutano wa Kuadhimisha miaka 60 ya Ushirikiano kati ya Bara la Asia na Afrika unaoendelea jijini Jakarta nchini Indonesia kuanzia tarehe 19 hadi 24 Aprili 2015. Kulia kwa Waziri ni Mhe. Aziz Mlima, Balozi wa Tanzania nchini Indonesia mwenye makazi yake ya kudumu nchini Malaysia, Bw. Khatibu Makenga, Afisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa pamoja na Bw. Dismas Assenga, Afisa katika Ubalozi wa Tanzania nchini Malaysia.
Mkutano huo kwa ngazi ya Mawaziri ukiendelea.
==============================
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Mkutano wa Wakuu wa Nchi kuadhimisha miaka 60 ya ushirikiano kati ya Asia na Afrika kufanyika Indonesia

Mkutano wa Maadhimisho ya Miaka 60 ya ushirikiano kati ya Asia na Afrika pamoja na Miaka 10 ya Mkakati Mpya wa Ubia Kati ya Asia na Afrika umeanza tarehe 19 Aprili 2015 hapa Jakarta, Indonesia.

Mkutano huo umetanguliwa na kikao cha Maafisa Waandamizi kinachojadili maazimio mbalimbali yaliyofikiwa mwaka 2005 pamoja na kutengeneza Agenda za Mkutano wa Ngazi ya Mawaziri na Wakuu wa Nchi na Serikali kuanzia tarehe 19 mpaka 24 Aprili 2015.

Kaulimbiu ya mkutano huu ni Kupanua wigo wa Ushirikiano kwa nchi wanachama “Advancing South - South Cooperation”.

Lengo kuu la mkutano huu ni kujadili kwa kina na kupitisha maazimio yatakayodumisha ushirikiano miongoni kwa nchi wanachama katika masuala ya ustawi wa amani, kuimarisha Mkakati Mpya wa Ubia kati ya Asia na Afrika na Azimio la Palestina. Maazimio yote hayo matatu yalijadiliwa na Maafisa Waandamizi kutoka Serikali za nchi wanachama na kisha kupitishwa na Mkutano wa Mawaziri.

Mkutano wa Wakuu wa nchi na Serikali utafanyika tarehe 22 na 23 Aprili 2015, ambapo Rais wa Jamhuri ya Indonesia, Mheshimiwa Joko Widodo anatarajiwa kuufungua kwa kutoa hotuba kwa wageni kabla ya kupitisha na kusaini Maazimio tajwa hapo juu.

Aidha, pamoja na mambo mengine, viongozi hao pia watajadili mustakabali mzima wa masuala mbalimbali yanayoendelea duniani katika Nyanja ya usalama, ubaguzi wa rangi, matabaka baina ya jamii, usafirishaji haramu wa binadamu, ugaidi na mengineyo. Siku ya mwisho, Mkutano unatarajia kukamilika kwa Wakuu wa nchi na Serikali kutembele jiji la kihistoria la Bandung ambako ndiko ulifanyika Mkutano wa kwanza wa ushirikiano kati ya Asia na Afrika miaka 60 iliyopita.

Ujumbe wa Serikali ya Tanzania kwenye mkutano huo, uliongozwa na Mheshimiwa Dkt Mary M. Nagu (Mb), Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu, Balozi, Mbelwa Kairuki, Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mheshimiwa Aziz Mlima, Balozi wa Tanzania nchini Indonesia mwenye makazi yake nchini Malaysia pamoja na Maafisa wengine katika taasisi hizo. 

Imetolewa na:
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Dar es Salaam
Tarehe 21 Aprili, 2015

Monday, April 20, 2015

Hakuna Mtanzania aliepoteza Maisha kwenye vurugu nchini Afrika Kusini - Membe



Waziri Membe: Hakuna Mtanzania katika mauaji ya Wageni Afrika Kusini

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Mhe. Benard K. Membe (Mb.) akizungumza na Waandishi wa Habari nchini kuhusiana machafuko yanayoendelea nchini Afrika ya Kusini.
Mkurugenzi wa Kitengo cha Sheria katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,  Balozi Irene Kasyanju (wa kwanza kulia) akiwa na  Mkurugenzi Idara ya Amerika na Ulaya Balozi Joseph Sokoine (kushoto) na Balozi wa Tanzania nchini Uswisi, Mhe. Modest Mero wakimsikiliza Waziri Membe (hayupo pichani) alipokuwa anazungumza na Waandishi wa Habari.   
Waandishi wa Habari wakimsikiliza na kunukuu taarifa kutoka kwa Waziri Membe ambaye hayupo pichani
Waziri Membe akiendelea kuzungumza na Waandishi wa Habari.
Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa nao wakimsikiliza Waziri Membe (Hayupo pichani) 
Mwandishi wa Habari mkongwe  Bw. Jackton Manyerere akiuliza swali kwa Mhe. Membe
Mwandishi wa Habari kutoka Gazeti la Mawio Bi. Pendo Omary naye akiuliza swali kwa Waziri Membe.
Waziri Membe akijibu Maswali yaliyo ulizwa na Waandishi wa Habari 
Mazungumzo yakiendelea

Picha na Reginald Philip

==============================

TAARIFA KWA  VYOMBO VYA HABAR

Waziri Membe: Hakuna Mtanzania katika mauaji ya Wageni Afrika Kusini

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard Membe, amesema leo kuwa hakuna Mtanzania kati ya watu wanane waliouawa katika mashambulizi dhidi ya wageni huko Durban na Johannesburg nchini Afrika ya Kusini.

Mhe. Membe amewaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salaam kuwa taarifa zilizosambazwa na baadhi ya vyombo vya habari kwamba Watanzania watatu wameuwawa katika mashambulizii hayo siyo za kweli.


"Nimehakikishiwa na Waziri wa Usalama wa Afrika kusini, David Mahlobo, asubuhi hii kuwa hakuna Mtanzania kati ya watu wanane waliouwawa, ambao ni raia wa Ethiopia, Zimbabwe, Malawi na Swaziland," ametaarifu Mhe. Waziri.

Amesema serikali ina taarifa kuwa kuna Watanzania watatu waliofariki dunia nchini Afrika Kusini, lakini hawakuuwawa katika mashambulizi ya wenyeji dhidi ya wageni.

"Watanzania hao ni Rashidi Jumanne, ambaye imetaarifiwa alipigwa risasi katika tukio la ujambazi, kilometa 90 nje ya mji wa Durban; mfungwa Athumani China Mapepe, aliyeripotiwa kuchomwa kisu gerezani wakati wa vurugu za wafungwa, na Ali Heshima Mohamed, ambaye alifariki hospitalini kutokana na ugonjwa wa TB," alieleza Mhe. Membe.

Mwili wa marehemu Mohamed ulirejeshwa nchini jana kwa mazishi. Mhe. Waziri alitaarifu kuwa kuna Watanzania 23 katika kambi iliyotayarishwa na serikali ya Afrika Kusini huko Durban kuhudumia wageni wanaokimbia mashambulizi hayo ya wenyeji, na kuwa utaratibu unafanywa kuwarejesha nyumbani raia 21 walioomba. "Wawili wamesema hawako tayari kurudi."

Mhe. Membe amesema taarifa ya Serikali ya Afrika Kusini inaonyesha kuwa hali ya utulivu imerejea Durban na Johannesburg katika saa 48 zilizopita kutokana na juhudi za Rais Jacob Zuma na kamati maalum ya mawaziri aliyoiteua kushughulikia mashambulizi hayo.

Mapema jana, Mhe. Membe alimwita Balozi wa Afrika Kusini nchini Tanzania, Mhe. Thamsanqa Dennis Mseleku,       na kuelezea kukerwa kwa Serikali na mauaji ya wageni na akataka hatua madhubuti zichukuliwe kuhakikisha usalama wa Watanzania nchini Afrika Kusini.

Alisema Tanzania inaunga mkono taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe, ambayo imelaani vikali mashambulizi ya Waafrika kutoka nje ya Afrika Kusini. Hata hivyo, Rais Mugabe, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Umoja mwa Afrika (AU), amesifia hatua zinazochukuliwa na serikali ya Afrika Kusini kukomesha mashambulizi hayo na kurejesha utulivu.

Mhe. Membe aliwataka Watanzania waishio Afrika Kusini na kwingineko nje ya nchi, kujitambulisha kwenye Balozi zetu ili iwe rahisi kufuatilia usalama wao na kuwasaidia yatokeapo majanga.

"Hatuna takwimu sahihi za idadi ya Watanzania waishio Afrika kusini kwa sababu wengi wao wamekwenda huko kwa njia za panya," alisema. Inakadiriwa kuna Watanzania 10,000 waishio Johannesburg na Durban. 

Akijibu swali, Mhe. Membe alisema Tanzania inapaswa kutumia utajiri mkubwa wa gesi asilia ilionao kuendeleza viwanda vidogo, vya kati na vikubwa vitakavyotengeneza ajira za kuvutia kwa vijana ili wasikimbilie nchi za nje na kuhatarisha maisha yao.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali kwa Umma,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,
Dar es Salaam
20 Aprili, 2015.




Waziri wa Mambo ya nje akiwasili katika ukumbi wa mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC) kwaajili ya kuzungumza na waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam
Waziri Membe akiingia katika ukumbi wa Mkutano kwaajili ya kuzungumza na waandishi we habari (hawapo pichani).
Waziri akizungumza na waandishi wa Habari  
Waziri Membe (Wa kwanza kulia) akiendelea kuzungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani), Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini Mhe. Radhia Msuya (Wa kwanza kushoto) na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Mambo ya Nje Bi. Mindi Kasiga 
Mazungumzo yakiendelea
Waziri Membe akiongozana na Viongozi wa Wizara na baadhi ya Waandishi wa habari kuelekea nje ya Ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere.