|
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Liberata Mulamula (kulia) wakiweka saini Mkataba wa Hati ya Makubaliano (MoU) na Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Umoja Unit Trust (UTT/PID), Dkt. Gration Kamugisha,
Makubaliano
hayo yatatoa fursa kwa Mfuko wa UTT/PID kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje katika kuendeleza viwanja na majengo mengine ya Ofisi za Balozi zilizopo nje ya
nchi. |
|
Balozi Mulamula na Dkt. Kamugisha wakibadilisha Mkataba huo mara baada ya kuweka saini |
|
Viongozi mbalimbali wa Wizara ya Mambo ya Nje nao wakishuhudia zoezi hilo la uwekaji saini. Kutoka kulia ni Bi. Mindi Kasiga, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. James Lugaganya, Mkurugenzi wa Sera na Mipango, Balozi Baraka Luvanda, Mkurugenzi wa Kitengo cha Sheria na Bw. Gerald Mbwafu, Afisa Mambo ya Nje. |
|
Ujumbe ulioambatana na Dkt. Kamugisha nao wakishuhudia tukio hilo |
|
Balozi Mulamula akiwa katika picha ya pamoja na Dkt. Kamugisha |
|
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Balozi Liberata Mulamula na Mtendaji Mkuu Dkt. Kamugisha wakiwa katika picha ya pamoja na Balozi Luvanda (wa tatu kutoka kulia), Bi. Kasiga (wa kwanza kulia), na Maafisa Mambo ya Nje, Bw. Mbwafu (wa pili kutoka kulia) na Bi. Happy Ruangisa (wa kwanza kushoto) |
Picha na Reginald Philip
========================
TAARIFA
YA KATIBU MKUU WA WIZARA YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA KWA VYOMBO
VYA HABARI KUHUSU KUSAINIWA KWA HATI YA MAKUBALIANO KATI YA WIZARA NA MFUKO WA
UTT/PID
Ndugu wanahabari nimewaita leo ili
mshuhudie tukio muhimu la uwekaji saini wa Hati ya Makubaliano (MoU) kati ya
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na Mfuko wa Umoja Unit Trust
(UTT/PID).
Makubaliano haya yatatoa fursa kwa Mfuko wa UTT/PID kwa kushirikiana
na Wizara yangu kuendeleza viwanja na majengo mengine ya Ofisi zetu za Balozi
zilizopo nje ya nchi.
Kama mnavyofahamu, Serikali ina
Balozi 35 katika nchi mbalimbali duniani. Tumefanikiwa kuwa na majengo yetu
wenyewe kwa ajili ya ofisi na makazi ya maafisa wetu katika Ofisi za Balozi za
baadhi ya nchi. Majengo hayo yamejengwa au kununuliwa kwa kutumia fedha za
Bajeti ya Maendeleo za Serikali na imesaidia kupunguza mzigo mkubwa kwa
Serikali wa kulipa gharama kubwa za kodi ya pango katika nchi hizo.
Ieleweke kwamba, nia ya Wizara ni
kuendeleza viwanja na majengo yote yanayomilikiwa na Ofisi za Balozi nje ya
nchi. Hivyo, Wizara imebuni mkakati wa
kushirikiana na wabia mbalimbali kuhakikisha kuwa viwanja au majengo
yanayomilikiwa na Balozi nje ya nchi vinaendelezwa.
UTT/PID ni mmoja wa washirika
aliyeitikia wito wa mkakati huo wa Wizara ambapo baada ya kusainiwa kwa
Makubaliano haya, Wizara katika siku chache zijazo itakabidhi kwa UTT/PID
ripoti ya viwanja na majengo mengine inayomiliki nje ya nchi ili waainishe
maeneo watakayoanza kuyaendeleza kwa kuzingatia kigezo cha fursa za kiuchumi.
Lengo la Wizara kuviendeleza
viwanja hivyo, sio tu kupata ofisi na makazi ya kudumu ya maafisa wa Ubalozi
bali pia kwa ajili ya vitega uchumi ambapo ofisi za ziada zitapangishwa kwa
ajili ya kuingizia mapato Serikali.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya
Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa,
Dar es Salaam
08 Desemba, 2015