Thursday, May 18, 2017

Mkutano wa 34 wa Dharura wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki wamalizika

Mkutano wa 34 wa Dharura wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofanyika leo Jijini Dar es Salaam umefikia tamati. Mkutano huu uliofanyika katika Hoteli ya Serena umehudhuriwa na Mawaziri wanaoshughulikia masuala ya Mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kutoka nchi wanachama, watendaji mbalimbali wa Wizara, mashirika ya umma, Watendaji wa Sekretariati ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, na taasisi mbalimbali za Serikali ndani ya Jumuiya. 

Pamoja na mambo mengine Mkutano huu ulikuwa ni maalum kwa ajili ya kuandaa agenda zinazohitaji maamuzi ya Wakuu wa nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Agenda hizo zinatokana na taarifa ya utekelezaji wa maagizo na maelekezo mbalimbali ya Mkutano uliopita wa Wakuu wa nchi wa Jumuiya wa mwaka 2015/2016, iliyo andaliwa na Mkutano wa ngazi ya wataalamu. 

Baadhi ya mambo yaliyopo kwenye taarifa hiyo ya utekelezaji wa maagizo na maelekezo mbalimbali ya Mkutano uliopita wa Wakuu wa nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ya mwaka 2015/2016 ambayo imekabidhiwa kwa Baraza la Mawaziri yanajumuisha mambo yafuatayo;

·     Taarifa ya namna ya kuwezesha uundaji wa magari katika   Jumuiya ya Afrika Mashariki na kupunguza uagizaji wa         magari yaliyotumika kutoka nje ya Jumuiya



· Taarifa ya mapitio kuhusu sekta ya nguo na ngozi juu ya       kuzuia/kuondoa uagizaji wa nguo na viatu vilivyotumika       kutoka nje     na;

· Taarifa ya namna endelevu ya Uchangiaji wa bajeti ya         Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Aidha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga akizungumza na wanahabari punde baada ya mkutano amesema  Mkutano huo wa Baraza la Mawaziri umekuwa  na mafanikio makubwa kwanza, kutokana na idadi kubwa na yakuridhisha ya wajumbe walioshiriki Mkutano kutoka nchi wanachama ,na pili  ni kutokana na mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi chote cha miaka miwili ambayo Tanzania ilikuwa mwenyekiti wa Jumuiya hadi sasa inapokabidhi kwa nchi ya Jamhuri ya Uganda.  

Mfanikio yaliyopatikana katika kipindi cha uwenyekiti;
Waziri Mahiga ameyataja mafanikio yaliyopatikana ndani ya kipindi cha miaka miwili Tanzania ikiwa mwenyekiti wa Jumuiya kuwa ni; kuongezeka kwa nchi ya Sudan Kusini katika Jumuiya, kuboreka kwa mfumo wa elimu kwa ngazi ya elimu ya juu katika Jumuiya na kupungua kwa vikwazo vya biashara vinavyotokana na vikwazo visivyokuwa vya kiforodha ndani ya Jumuiya vilivyopelekea kurahisisha na kuhamasisha biashara katika Jumuiya.

Mkutano huu wa Baraza la Mawaziri utafuatiwa na Mkutano wa 18 wa Kaiwada  wa Wakuu wa nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki uanaotarajiwa kufanyika tarehe 20 Mei, 2017 Ikulu Jijini Dar es Salaam. 

Pamoja na mambo mengine Mkutano wa Wakuu wa nchi unatarajiwa kupokea ripoti ya usuluhishi ya kamati inayoongozwa na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Benjamini William Mkapa.

Tanzania ilikabidhiwa uwenyekiti wa Jumuiya mwishoni mwa mwaka 2014 katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi uliofanyika Nairobi, Kenya; na ikapewa tena nafasi ya kuendelea kushikilia kiti hicho mwaka 2015, ambapo mpaka sasa Tanzania wakati inaelekea kukabidhi nafasi hii ya uwenyekiti kwa nchi ya Uganda, Tanzania imekuwa mwenyekiti wa Jumuiya kwa kipindi cha miaka miwili mfululizo.


Waheshimiwa Mawaziri wa Tanzania waliohudhuria Mkutano wakiwa wamesimama wakati wimbo wa Afrika Mashariki unapigwa kabla ya kuanza kwa Mkutano
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga akizungumza wakati wa Mkutano wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofanyika Hotel ya Serena jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga akisalimiana na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wamasuala ya Afrika Mashariki wa Uganda Mhe.Dkt.A.M Kirunda Kivejinja kabla ya kuanza kwa Mkutano wa Baraza la Mawaziri uliofanyika Hoteli ya Serena Jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Aziz P. Mlima (wakwanza kushoto) akifuatilia Mkutano.


Balozi wa Tanzania nchini Kenya Mhe. Pindi Chana (wakwanza kushoto) akifuatilia Mkutano wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki
Mkutano ukiwa ukiendelea, Hoteli ya Serena Jijini Dar es Salaam






Balozi wa Tanzania katika Muungano wa Visiwa vya Komoro awasilisha Hati za Utambulisho.



Balozi wa Tanzania katika Muungano wa Visiwa vya Komoro Mhe. Sylvester M. Mabumba (kulia) akiwasili katika Ikulu ya Komoro kwaajili ya hafla ya kuwasilisha Hati za Utambulisho, kushoto ni Mnikulu  wa Ikulu ya Komoro Bw.Hashim Mohamed. Hafla ya kukabidhi Hati hizo ilifanyika mapema wiki hii katika Ikulu hiyo.



Mhe. Balozi Mabumba akijitambulisha sambamba na kutoa salamu za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kabla ya kukabidhi Hati za Utambulisho.
Mhe. Balozi Mabumba akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika  Ukumbi wa Ikulu ya Komoro. Pembeni yake ni Wakurugenzi wa Wizara ya Mambo Mambo ya Nje ya Komoro.


==================================================
TANZANIA NA KOMORO ZAAHIDI KUENDELEA KUIMARISHA USHIRIKIANO.
Balozi wa Tanzania katika Muungano wa Visiwa vya Komoro, Mhe. Sylvester M. Mabumba mapema wiki hii alikabidhi hati za utambulisho  kwa Rais wa Muungano wa Visiwa vya Komoro Mhe. Azali Assoumani. Hafla ya kukabidhi hati hizo ilifanyika kwenye Ukumbi wa Ikulu ya Komoro ijulikanayo kama  Beit.

Wakati akihutubia, Mhe. Mabumba alijitambulisha kwa Mhe. Rais na kueleza furaha yake ya kuteuliwa kuwa Balozi wa pili kutoka Tanzania kuja kutumikia nchini Komoro. Aidha, alieleza furaha yake kwa mapokezi mazuri aliyoyapata tangu kuwasili kwake Visiwani  humo na kwamba yamemfanya ajisikie yupo nyumbani.

Alieleza kuwa anatambua kazi kubwa iliyopo mbele yake na kuahidi kuwa katika kipindi chake wakati akiwa Balozi nchini humo atajitahidi kukuza mahusiano yaliyopo baina ya Tanzania na Komoro. Sambamba na hilo, Mhe. Balozi alieleza dhamira yake ya kutaka kuona mahusiano baina ya nchi hizi mbili yanakuwa na manufaa kwa pande zote halikadhalika kukua kwa uhusiano wa kindugu kwani mahusiano baina ya Tanzania na Komoro ni ya kihistoria.

Pia Mhe. Rais Assoumani katika hotuba yake naye alianza kwa kuonyesha furaha yake ya kuwasili kwa Balozi pamoja na kukiri kupokea barua ya kurejea Balozi aliyepita na ya kuwasili kwa Balozi wa sasa. Vilevile alieleza kuwa kila Mkomoro hujisikia nyumbani pindi anapo tembelea Tanzania kutokana na ukarimu wanao onyeshwa wanapokuwa huko. Aidha Mhe. Rais alimuhakikishia Mhe. Balozi kuwa atarajie kupata ushirikiano wake pamoja na wa Serikali yake katika kipindi chote atakapo kuwa nchini humo.

Mhe. Balozi Mabumba alitumia fursa hiyo pia  kumuomba Mhe. Rais Assoumani kufanye ziara ya kikazi nchini Tanzania ili kuweza kudumisha mahusiano yaliyopo baina ya nchi hizo mbili.

Zanzibar haibaguliwi katika EAC,

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, akimkaribisha Mkurugenzi wa Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Jamii, Bw. Eliabi Chodota kutoa mada kwenye semina ya mtangamano inayoendelea Kisiwani Pemba. Ushiriki na mwitikio katika semina hiyo umekuwa mkubwa kwa washiriki ambapo wameonekana kuvutiwa sana na semina hii pia wamekuwa wadadisi wazuri wa kutaka kujua zaidi fursa zinazo patikana kwenye mtangamano huo.
Bw. Chodota akitoa mada kwenye semina ya mtangamano inayoendelea Pemba.
Sehemu ya washiriki wakisikiliza kwa makini mada iliyokuwa ikitolewa na Bw. Chodota (hayupo pichani).
Bw. Chodota akiendelea kutoa mada yake.
Mmoja wa washiriki Bi. Kauthari akiuliza swali mara baada ya mada kumalizika kutolewa na Bw. Chodota hayupo pichani.
Sehemu nyingine ya washiriki wakimsikiliza kwa makini.
Bw. Chodota akijibu swali lililokuwa limeulizwa na Bi Kauthari (hayupo pichani).
Bw. Suleimani Haji kutoka ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar naye akitoa mada kuhusu nafasi ya Zanzibar kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Sehemu ya washiriki wakimsikiliza kwa makini Bw. Suleimani (hayupo pichani).
Washiriki wakisikiliza kwa makini mada na maswali yaliyo kuwa yakiulizwa na washiriki wengine.
Mhe. Mbarouk Salim Ali Mbunge wa Jimbo la Wete akiuliza swali kwenye semina. Pembeni yake ni Mbunge wa Jimbo la Konga, Mhe. Mbarouk Ali akisikiliza kwa makini.
Meneja wa TRA kwa upande wa Kisiwani Pemba Bw. Habibu Saleh naye akiuliza swali kwa mtoa mada, Bw. Suleimani (hayupo pichani).
Bw. Salehe akijibu maswali hayo na kutolea ufafanuzi kwa baadhi ya mambo.


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Zanzibar haibaguliwi katika EAC,

Serikali ya Zanzibar inashiriki moja kwa moja bila ukomo katika masuala yote ya Mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), hivyo Wazanzibari wamehimizwa kuchangamkia fursa zilizopo kwenye Jumuiya hiyo na kuondokana na dhana kuwa eti, Serikali yao inabaguliwa.



Akiwasilisha mada leo kuhusu ushiriki wa Zanzibar katika Jumuiya ya Afrika Mashariki kwenye semina ya masuala ya  mtangamano wa EAC inayofanyika Pemba, Afisa wa Ushirikiano wa Kimataifa kutoka Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Bw. Suleima Haji alitoa ufafanuzi wa kina kuonesha namna Zanzibar inavyoshiriki katika EAC.



Bw. Haji alieleza kuwa  licha ya Zanzibar kuwa  sehemu ya muungano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ushiriki wake umedhihirika katika mgawanyo wa miradi ya maendeleo ya EAC, hususan miradi ya Miundombinu.  Alisema Zanzibar iliwasilisha mapendekezo ya miradi 10 kwenye Sekretarieti ya EAC na kutokana na vipaumbe vilivyowekwa miradi 3 imekubaliwa na mchakato wa kuitekeleza unaendelea. Miradi hiyo ni ujenzi wa Bandari ya  Marhubi kisiwani Pemba, upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Pemba na ununuzi wa meli kubwa zitakazosafirisha abiria na mizigo kwenye nchi wanachama wa EAC.



 Aidha, kwenye miradi inayofadhiliwa na washirika wa maendeleo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Zanzibar haijasahaulika. Zanzibar inanufaika na miradi inayofadhiliwa na taasisi inayojihusisha na masuala ya kukuza biashara na kupunguza umasikini katika nchi za EAC inayoitwa "East Africa Trademark" (TMEA).  TMEA ambayo ni mdau mkubwa wa EAC inafadhili mradi ambao unawawezesha Wazanzibari kufanya maombi kwa njia ya mtandao ili kupata cheti cha uasili wa bidhaa. Cheti hicho ni muhimu kwa wafanyabiashara kwani kinatambulisha bidhaa yako ilipotengenezwa na kupata msamaha wa kodi ya forodha inapoingia nchi nyingine za EAC.



Mradi mwingine unaofadhiliwa na TMEA huko Zanzibar ni ule wa kuwasilisha malamiko kwa njia ya mtandao au ujumbe mfupi wa simu pale inapotokea mfanyabiashara amekumbana na vikwazo visivyo vya forodha katika kusafirisha bidhaa zake ndani ya Jumuiya. Ujumbe huo utakapopokelewa, kikwazo kilicholalamikiwa kitafanyiwa kazi na taasisi husika mara moja.


Benki ya dunia pia inaendesha mradi wa kutathmini utekelezaji wa Soko la Pamoja kwa upande wa Zanzibar. Kama inavyotambulika soko la pamoja lina vipengele vingi vikiwemo; usafirishaji huru wa bidhaa, huduma, mtaji na watu. Hivyo kuna umuhimu wa kupima namna nchi wanachama zinavyotekeleza vipengele hivyo.



Ushiriki wa Zanzibar unapatikana pia kwenye uenyeji wa taasisi za Jumuiya ya Afrika Mashariki. Zanzibar imebahatika kuwa mwenyeji wa Kamisheni ya  Kiswahili ya EAC. Kuwa mwenyeji wa taasisi kuna faida kubwa zikiwemo kujitangaza na ajira. Kwa upande wa ajira, Bw. Haji alisema sio tu Wazanzibari wanafaidikia na ajira za  Kamisheni ya Kiswahili, bali wanapata ajira hata katika Sekretarieti ya EAC na kutolea mfano kuwa Mhasibu Mkuu wa kwanza wa Sekretarieti hiyo alikuwa Mzanzibari.


Vile vile, Zanzibar imekuwa mwenyeji wa vikao mbalimbali vya taasisi za Jumuiya. Mwaka 2010 Mahakama ya Afrika Mashariki ilifanya kikao chake Zanzibar, Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) lilifanya kikao chake Zanzibar mwaka 2016 na mwezi Agosti mwaka huu utafanyika mkutano mkubwa wa masuala ya Kiswahili mjini Zanzibar. Aliendelea kusema kuwa katika Bunge la EALA la kipindi hiki,  Zanzibar ina wabunge watatu, wawili wakitokea CCM na mmoja CUF.



Alihitimisha mada yake kwa kuwasihi Wazanzibari waache fikra potofu za kujihisi kubaguliwa badala yake waunganishe nguvu kuchangamkia fursa lukuki za kibiashara zilizopo kwenye mtangamano wa EAC. Alisema Serikali ya Zanzibar inashiriki katika kila jambo ikiwemo kushiriki mikutano ya Marais. Mawaziri na Wataalamu ili kutetea maslahi ya Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.



 -Mwisho-

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar es Salaam, 18 Mei, 2017


Wednesday, May 17, 2017

Maandalizi ya Mkutano wa 34 wa Dharura wa Baraza la Mawaziri la Afrika Mashariki yakamilika.


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Aziz P. Mlima akizungumza kwenye kikao cha Wataalamu ngazi ya Makatibu Wakuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofanyika katika Hoteli ya Serena Jijini Dar es Salaam.
 Mkutano huu ni maandalizi ya Mkutano wa 34 wa Dharura wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki unaotarajiwa kufanyika tarehe 18 Mei, 2017 Hoteli ya Serena Jijini Dar es Salaam. 

Mkurugenzi wa Siasa, Ulinzi na Usalama Bw. Stephene Mbundi akisisitiza wakati wa Mkutano wa ngazi ya Wataalam kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofanyika Hoteli ya Serena Jijini Dar es Salaam



Sehemu ya wajumbe wakifuatilia mkutano

Katibu Mkuu Sekretariati ya Jumuiya ya Afrika Mashariki Bw. Liberat Mfumukeko akifuatilia Mkutano.

Tuesday, May 16, 2017

Watumishi wa umma kuweni karibu na wananchi, Balozi Mwinyi

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhani Mwinyi akitoa mwongozo kwa wajumbe wa semina ya Mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki  inayoendelea kufanyika kisiwani Pemba. Pamoja na mambo mengine amewahimiza wananchi kuchangamkia fursa zinazopatikana kwenye mtangamano.
Mbunge wa jimbo la Konga, Mhe. Mbarouk Ali akichangia jambo kwenye semina.
Sehemu ya wajumbe wakiendelea kusikiliza mada mbalimbali zilizokuwa zikiendelea kutolewa kwenye semina.
Afisa kutoka Ofisi za Uhamiaji Pemba Bw. Haji Kassim Haji akijibu hoja mbalimbali zilizokuwa zikitolewa na wajumbe kwenye semina juu ya upatikanaji wa Hati ya Kusafiria ya Afrika Mashariki.
Bw. Amedeusi Mzee akitoa mada kuhusu Soko la Pamoja na faida zinazopatikana kwenye soko hilo.
Luteni Kamanda. Hassan Hussein  wa KMKM naye akitolea ufafanuzi kwenye maswala mbalimbali yenayohusiana na maswala ya magendo.
Wajumbe wakisikiliza kwa makini mada na majibu ya hoja mbalimbali walizokuwa wakihitaji kufahamu kutoka kwa Bw. Amedeusi (hayupo pichani) na mjumbe kutoka JKU.

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI



Watumishi wa umma kuweni karibu na wananchi,  Balozi Mwinyi



Taasisi za Serikali zimehimizwa ziwe karibu na wananchi ili ziweze kuwahudumia na kuwaelimisha juu ya huduma inazozitoa. Wananchi wengi wamekuwa wakilalamika mara kwa mara kuhusu watumishi wa umma kutotumia weledi na ubunifu katika kuwahudumia wananchi jambo ambalo likiachwa liendelee, Tanzania itaachwa nyuma ndani ya Mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na ulimwengu mzima kwa ujumla.

         Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhan Mwinyi katika semina kuhusu elimu ya mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na fursa zake inayotolewa na wataalamu wa Wizara yake kisiwani Pemba.    Semina hiyo  iliyoanza jana inafanyika kwenye uwanja wa Gombani, Pemba na itamalizika tarehe 18 Mei 2017.

         "Kuna fursa nyingi za kiuchumi katika Mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki lakini kama wananchi wetu hatutawasaidia na kuwaelimisha kuhusu nyaraka na masharti yanayokidhi vigezo wataachwa nyuma na kubaki kuwa watazamaji na walalamikaji" Balozi Mwinyi alisema.

         Wajasiriamali walielezea masikitiko yao juu ya ugumu wa kupata hati za kusafiria kutokana na mlolongo wa masharti hususan, inapotokea kuwa safari ni ya ghafla. Aidha, wajasiriamali wamekuwa wakilalamika kuwa wanapata tabu kusajili bidhaa zao katika mamlaka zinazosimamia ubora wa viwango wa bidhaa, chakula na madawa kwa kuelezwa kwamba bidhaa zao ni duni, hivyo wameiomba Serikali iwawezeshe kupata teknolojia ya kisasa ikiwa ni pamoja na vifungashio.

         Balozi Mwinyi alisisitiza umuhimu wa taasisi zote bila kukiuka Sheria, kanuni na vigezo vilivyowekwa kurahisisha taratibu zao ili wananchi wapate nyaraka zinazotakiwa kwa urahisi ili iwe wepesi kwao kuchangamkia fursa za kiuchumi na kibiashara katika soko la pamoja la Afrika Mashariki.

         Akitoa ufafanuzi kuhusu upatikanaji wa hati za kusafiria, Afisa Uhamiaji, Bw. Haji Kassim Haji alisema kuwa taratibu zilizowekwa hazina lengo la kukwamisha shughuli ya mtu yeyote isipokuwa zimewekwa kwa kuzingatia maslahi mapana ya nchi. Katika ulimwengu wa leo ambao unakabiliwa na changamoto nyingi za kiusalama kama, ugaidi, uharamia, Biashara haramu ya binadamu, uhamiaji haramu, lazima masharti yazingatiwe ili kuepuka uwezekano wa kutokea uovu huo.

         Aidha, Balozi Mwinyi alishauri wajasiriamali wajiunge katika vikundi ili  masuala yao ikiwa ni pamoja na maombi ya hati za kusafiria yafanywe kwa pamoja wakidhaminiwa na taasisi zinazosimamia shughuli zao.



 -Mwisho-



Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,

Pemba, 16 Mei, 2017



Wananchi wa Pemba wahimizwa kuchangamkia fursa za EAC



Waziri wa Mambo ya nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Augustine Mahiga (Mb.), akizungumza kwenye ufunguzi wa semina ya Mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Kisiwani Pemba. Semina hiyo inatolewa kwa wajasiriamali wa Pemba ili waweze kuchangamkia fursa za mtangamano. Semina hiyo inafanyika katika Ukumbi wa Mikutano uliopo katika Uwanja wa mpira wa Gombani.
Sehemu ya wajumbe waliohudhuria semina hiyo, wa kwanza kushoto ni Mbunge wa Konde Mhe. Mbarouk Ali akiwa pamoja na washiriki wengine wakifuatilia kwa makini ufunguzi huo
Sehemu nyingine ya wajumbe wakimsikiliza kwa makini Waziri Mahiga hayupo pichani.
Naibu Waziri wa Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora wa Serikali ya Zanzibar Mhe. Khamis Juma Maalim akisoma hotuba ya ukaribisho.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhan Mwinyi naye akielezea jambo kwenye ufunguzi wa semina hiyo ya Mtangamano wa Afrika Mashariki.
Mwenyekiti wa wafanyabiashara wa Sanday markert  kutoka Pemba, Bw.Khamis Suleiman Masoud akitoa neno la shukrani kwa Mhe. Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki (hayupo pichani).
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Mindi Kasiga akitoa ufafanuzi masuala mbali mbali kuhusiana na semina hiyo.
Ufunguzi wa Semina ukiendelea
Wakiwa katika picha ya pamoja.

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Wananchi wa Pemba wahimizwa kuchangamkia fursa za kiuchumi katika Soko la EAC

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Augustine Mahiga amewataka wakazi wa Pemba na Tanzania kwa ujumla  kuchangamkia ipasavyo fursa za Soko la Pamoja la Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa ajili ya kujiongezea kipato.

Mhe. Waziri alieleza kuwa katika ulimwengu wa leo hakuna nchi duniani itakayoweza kujiimarisha kiuchumi peke yake bila kushirikiana na nchi nyingine.  Ndio maana hata zile nchi zilizoendekea kama Marekani na nchi za Ulaya wana umoja wao kwa madhumuni ya kuongeza nguvu na kasi ya maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kisiasa.

Waziri Mahiga aliyasema hayo alipokuwa anafungua semina kuhusu elimu ya Mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na fursa zake kwa wananchi wa Pemba ambayo itatolewa na wataalamu wa Wizara yake kwa siku nne kuanzia leo kwenye Uwanja wa Mpira wa Miguu wa  Gombani.

Mhe. Waziri alieleza kuwa kabla, wakati na baada ya ukoloni nchi za Afrika Mashariki zilikuwa na aina moja au nyingine ya Ushirikiano kwa madhumuni ya kuimarisha uchumi wa nchi zao, waliotutawala.  Aina moja ya Ushirikiano ni ule Umoja wa Huduma ambao ulianzishwa mwaka 1961. Umoja huo ulianzisha mashirika mbalimbali kama vile bandari, ndege, hali ya hewa, posta na reli ambayo yalikuwa yanaendeshwa kwa pamoja.

Alisema Tanzania ipo katika eneo la kimkakati ndani ya Jumuiya ikiwa ni pamoja na kuwa na eneo kubwa kuliko nchi zote, idadi kubwa ya watu, ukanda mkubwa wa bahari na ardhi nzuri yenye rutuba na kihistoria Pemba ni eneo lenye rutuba nzuri kuliko maeneo yote ya Afrika Mashariki. Hivyo, kutokana na sifa hizo hakuna budi wananchi wa Pemba na Tanzania kwa ujumla kujipanga vizuri ili kuchangamkia fursa hizo badala ya kubaki kuwa watazamaji na walalamikaji.

Waziri Mahiga aliongeza kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ina sifa nyingine ya pekee ya kuwa Muungano wa nchi mbili na kutoa wito kwa washiriki wa semina hiyo kutumia sifa ya umoja wao kuziendea na kuzichangamkia fursa za kiuchumi zilizopo kwenye Mtangamano.

"Nchi nyingi barani Afrika na duniani kwa ujumla zilijaribu kuungana lakini zilishindwa, kwa mfano nchi za Ghana, Mali na Guinea, nchi za Afrika zinazozungumza kifaransa, nchi za Misri na Syria, nchi za Afrika ya Kati na nchi za Pembe ya Afrika". “Ni sisi peke yetu hadi leo tumedumisha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo juzi tu tuliadhimisha miaka 53 ya muungano huo”. Waziri Mahiga alisema. 

Aliendelea kuueleza kuwa ni jukumu la kila Mtanzania kudumisha Muungano huo ambapo kwa maneno yake alisema kuwa unaonewa wivu Afrika na duniani kote.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora wa Serikali ya Zanzibar, Mhe. Khamisi Juma Mwalim aliwasihi washiriki wa semina hiyo kuzingatia mafunzo yanayotolewa katika semina hiyo ili waweze kunufaika katika shughuli zao ikiwemo ujasiriamali.



-Mwisho-



Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,

Dar es Salaam, 15 Mei, 2017