Wednesday, May 19, 2021

WATANZANIA WAHIMIZWA KUCHANGAMKIA FURSA ZINAZOPATIKANA SADC


Watanzania wamehimizwa kuchangamkia fursa mbalimbali zinazopatina kwenye mtangamano wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ikiwemo biashara, uwekezaji na soko la bidhaa mbalimbali za Tanzania ili kunufaika na Jumuiya hiyo.

Rai hiyo imetolewa leo tarehe 19 Mei 2021 na Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Prof. Davis Mwamfupe wakati akifungua rasmi Kongamano la Maadhimisho ya Miaka 40 ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini  mwa Afrika (SADC)  lililofanyika kwenye Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali.

Mhe. Prof. Mwamfupe amesema kwamba, katika kipindi cha miaka 40 tangu kuanzishwa kwa SADC mwezi Aprili  1980, wigo wa fursa umeongezeka ambapo sasa Jumuiya imejikita katika kuwanufaisha  wananchi wake kiuchumi baada ya kukamilisha jukumu la kuzikomboa kisiasa  Nchi za Kusini mwa Afrika ambalo lilikuwa moja ya lengo la kuanzishwa kwa Jumuiya ya SADC.

Kadhalika alisema kuwa maadhimisho ya miaka 40 ambayo yamebeba kaulimbiu isemayo “Miaka 40 SADC ya Kuimarisha Amani na Usalama, Kuhamasisha Maendeleo na Ustahimilivu wa Changamoto Zinazoikabili Dunia” yanalenga pamoja na mambo mengine kuenzi mchango wa waaanzilishi wa SADC, lakini pia kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu Mtangamano wa SADC na faida za uanachama wa Tanzania kwenye Jumuiya hiyo ikiwa ni pamoja na kuwaeleza wananchi fursa zinazopatikana za kiuchumi, kijamii na kisiasa.

Pia aliongeza kuwa, maadhimisho haya yanalenga kuangazia mafanikio yaliyofikiwa pamoja na kuongeza hamasa kwa makundi mbalimbali kama vile wafanyabiashara, vijana, wanawake, makundi maalum na wananchi kwa ujumla kuchangamkia fursa za kiuchumi na kijamii zinazopatikana SADC.

“Leo tunaposherehekea miaka 40 ya SADC tunafungua wigo kwa wadau mbalimbali hususan wafanyabiasha na vijana kuwaonesha namna gani wanaweza kunufaika na Jumuiya hiyo kutoka ile ya kufundishwa darasani hadi SADC inayotuwezesha kupanga mipango yetu ya maendeleo kwa kuwashirikisha wadau mbalimbali wakiwemo wafanyabiashara, vijana na makundi mengine. Hivyo tuna kazi kubwa moja ya kuhakikisha elimu kuhusu fursa zinazopatikana SADC inawafikia wananchi wote” alisema Prof. Mwamfupe.

Awali akizungumza kuwakaribisha Washiriki wa Kongamano hilo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Prof. Faustine Bee alisema anashukuru Chuo hicho kuwa sehemu ya maadhimisho ya miaka 40 ya SADC kwani ni heshima kubwa kwao ambayo imewezesha wadau mbalimbali kukutana na kubadilisha mawazo ya namna ya kuiimarisha Jumuiya hiyo.

Aliongeza kusema kwamba, wakati Nchi Wanachama wa SADC zikiadhimisha miaka 40 ya Jumuiya hiyo, Chuo hicho kinatambua faida za SADC kwani tayari kinashirikiana na Nchi za Jumuiya hiyo ambapo Tanzania kwa sasa inapokea wanafunzi kupitia ushirikiano huo. Alisema mfano mzuri ni ule uliopo kati ya Tanzania na Msumbiji ambazo tayari zinashirikiana katika kubadilishana wanafunzi kupitia utaratibu wa TAMOSE (Tanzania –Mozambique Students Exchange Program) ambapo tayari wanafunzi kutoka Msumbiji wanasoma UDOM na Vyuo vingine hapa nchini na vivyo hivyo wapo wanafunzi kutoka Tanzania wanaosoma nchini Msumbiji.

Kadhalika alisema, Chuo hicho ambacho kinapokea wanafunzi kutoka Nchi zingine za SADC kama Comoro, Afrika Kusini, Zambia, Malawi, DRC na zingine kimejiwekea malengo ya kuingia kwenye vyuo bora 20 katika Afrika kufikia mwaka 2030. Alisisitiza kuwa, lengo hilo litafanikiwa endapo Chuo kitapokea wanafunzi wengi kutoka nje ya nchi ikiwa ni moja ya kigezo  cha kupima ubora wa chuo na alitoa ombi kwa Serikali kukisaidia Chuo hicho kuongeza wanafunzi kupitia ushirikiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na nchi zingine na ule wa kikanda na kimataifa.

Wakati wa Kongamano hilo, ambalo limeandaliwa kwa uratibu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, mada mbalimbali ziliwasilishwa na kujadiliwa ikiwemo “Kuimarisha Amani na Usalama katika Kukabiliana na Changamoto za Ulimwengu” iliyowasilishwa na Mkuu wa Chuo cha Diplomasia Mstaafu, Dkt. Mohammed  Maundi na mada isemayo          “Kuhamasisha Maendeleo na Uhimilivu katika kukabiliana na Changamoto za Ulimwengu” ambayo iliwasilishwa na  Mhadhiri na Mkuu wa Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Dkt. Ajali Mustafa.

Viongozi wengine walioshiriki Kongamano hilo ni Mkuu wa Chuo cha Mipango, Prof. Hozen Mayaya, Mkuu wa Chuo cha Serikali za Mitaa cha Hombolo, Dkt. Michael Msendekwa, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo cha Dodoma anayeshughulikia Taaluma, Prof. Alexander Makulilo na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Agnes Kayola. Pia, kongamano lilihudhuriwa na Wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma, Chuo Kikuu cha Mipango na Chuo cha Serikali za Mitaa kilichopo Hombolo jijini Dodoma.


Mgeni Rasmi ambaye ni Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Prof. Davis Mwamfupe akifungua rasmi Kongamano la Maadhimisho ya Miaka 40 ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) lililofanyika katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) tarehe 19 Mei 2021. Kongamano hilo ambalo liliandaliwa chini ya uratibu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki lilihudhuriwa na wadau mbalimbali wakiwemo wanafunzi kutoka UDOM na Vyuo vingine vya Dodoma. 

Makamu Mkuu wa Chuo cha Dodoma (UDOM), Prof. Faustine Bee akiwakaribisha Washiriki wa Kongamano la Maadhimisho ya Miaka 40 ya SADC Chuoni hapo

Mkuu wa Chuo cha Diplomasia Mstaafu, Dkt. Mohammed Maundi akiwasilisha mada kwa Washiriki kuhusu Kuimarisha Amani na Usalama katika Kukabiliana na Changamoto za Ulimwengu wakati wa Kongamano la Maadhimisho ya Miaka 40 ya SADC lilifanyika UDOM

Mhadhiri Mkuu wa Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala wa Umma wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Dkt. Ajali Mustafa nae akiwasilisha mada kuhusu Kuhamasisha Maendeleo na Uhimilivu katika Kukabiliana na Changamoto za Ulimwengu wakati wa Kongamano la kuadhimisha miaka 40 ya SADC.

Sehemu ya Washiriki waliohuria Kongamano la Maadhimisho ya Miaka 40 ya SADC. Kutoka kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bibi Agnes Kayola, Mkuu wa Chuo cha Serikali za Mitaa cha Hombolo, Dkt. Michael Msendekwa  na Mkuu wa Chuo cha Mipango, Prof. Hozen Mayaya 

Sehemu nyingine ya Washiriki wa Kongamano

Washiriki wa Kongamno wakiwemo wahadhiri wakifuatialia uwasilishwaji wa mada mbalimbali

Sehemu ya Wanafunzi wakifuatilia matukio mbalimbali wakati wa Kongamano la Maadhimisho ya miaka 40 ya SADC

Sehemu nyingine ya Washiriki

Washiriki wa Kongamano la maadhimisho ya miaka 40 ya SADC kama wanavyoonekana pichani

Sehemu nyingine ya washiriki

Waandishi wa Habari wakifuatilia matukio mbalimbali wakati wa Kongamano la Maadhimisho ya miaka 40 ya SADC

Washiriki kama wanavyoonekana pichani

Mmoja wa Wahadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma akichangia jambao wakati wa Kongamano la Maadhimisho ya Miaka 40 ya SADC

Mmoja wa Wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma akiuliza swali wakati wa Kongamano la Maadhimisho ya Miaka 40 ya SADC

Mwanafunzi kutoka Chuo cha Mipango nae akichangia jambo wakati wa Kongamano la Maadhimisho ya Miaka 40 ya SADC

Picha ya pamoja

Meza Kuu katika picha ya pamoja na wadau mbalimbali



 

Tuesday, May 18, 2021

BALOZI MULAMULA AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA BALOZI WA POLAND, USWISI

Na Mwandishi wetu, Dar

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Poland nchini, Mhe. Krzystof Buzalski pamoja na Balozi wa Uswisi nchini Mhe. Didier Chassot katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Waziri Mulamula amesema kuwa mazungumzo yake na mabalozi hao yalilenga kujadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa uwili (bilateral cooperation) baina ya Tanzania na nchi hizo katika sekta za afya, elimu, utalii pamoja na biashara na uwekezaji.

Akiongelea uhusiano baina ya Tanzania na Poland Balozi Mulamula amesema kuwa wapoland walikuja kwa kasi katika uwekezaji ambapo wana kampuni zao zinazozalisha matreka Kibaha, na kuanzisha miradi katika sekta ya maji, miradi katika uwekezaji wa nafaka pamoja na kutoa ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wa kitanzania nchini Poland.

“Sasa hivi Balozi amenijulisha kuwa fursa hizo za watanzania kusoma Poland na kutuhamasisha kuzichangamkia fursa hizo, lakini pia tumeongelea jinsi ya kukuza biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Poland,” Amesema Balozi Mulamula

Akiongelea kuhusu ushirikiano wa Tanzania na Uswisi Mhe. Mulamula amesema kuwa ushirikiano wa Tanzania na Uswisi umekuwa ni wa muda mrefu na wamekuwa wakisaidia sana Tanzania katika sekta ya Afya hasa katika kupambana na Malaria.

“……..Uswisi imekuwa ikisaidia mikopo mbalimbali lakini pia ni mwenyekiti mwenza katika kuunganisha Tanzania na nchi wadau/zinzaotoa misaada, pamoja na mambo mengine, madhumuni ya kukutana leo ni kuangalia jinsi gani ya kukuza sekta ya uwekezaji na biashara,” Amesema Balozi Mulamula

Kwa upande wake Balozi wa Poland nchini, mhe. Krzystof Buzalski amesema kuwa wamekubaliana kuendelea kuimarisha ushirikiano baina ya Poland na Tanzania katika sekta ya uchumi, maendeleo, utalii na siasa.

“Leo tumekubaliana kuendelea kuimarisha ushirikiano baina ya Poland na Tanzania katika sekta ya uchumi, maendeleo, utalii pamoja na siasa kati ya Poland na Tanzania,” amesema Balozi Buzalski.

Nae balozi wa Uswisi Mhe. amesema kuwa Uswisi na Tanzania zimekuwa na ushirikiano wa siku nyingi kwa zaidi ya miaka 40 na viongozi hawa wamejadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa uwili (Bilateral cooperation) katika masuala ya kiuchumi na kisiasa.

“Mimi na Mhe. Waziri tumekubaliana kuendeleza ushirkiano baina ya nchi zetu mbili katika sekta ya afya; elimu; biashara; uwekezaji pamoja na maliasili na utalii,” amesema Balozi Chassot.

Balozi wa Poland nchini, Mhe. Krzystof Buzalski akiongea na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akimuelezea jambo Balozi wa Poland nchini, Mhe. Krzystof Buzalski katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akiteta jambo Balozi wa Uswisi nchini, Mhe. Didier Chassot katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam


Kikao cha Mhe. Waziri Balozi Mulamula na Balozi wa Uswisi kikiendelea 


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Mulamula katika picha ya pamoja na Balozi wa Uswisi nchini, Mhe. Chassot pamoja na maafisa kutoka Ubalozi wa Uswisi na Wizara ya Mambo ya Nje


 

Monday, May 17, 2021

TANZANIA YAENDELEA KUFANYA VYEMA UTAWALA BORA, HAKI ZA BINADAMU

Na Mwandishi wetu, Dar 

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imesema Tanzania imeendelea kufanya vizuri katika viwango vya Utawala Bora na Haki za Binadamu hususani katika maeneo ya haki za kijamii pamoja na haki za kisiasa.

Mwenyekiti wa Tume hiyo (Jaji Mstaafu) Mathew Mwaimu ameyasema hayo Jijini Dar es Salaam alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (Mb) na kuongeza kuwa licha ya uwepo wa baadhi ya maeneo ya maboresho kwa sasa Tanzania iko katika daraja “A” miongoni mwa nchi zinazofanya vizuri katika masuala ya Utawala Bora na Haki za Binadamu.

“Licha ya uwepo wa baadhi ya maeneo ya maboresho kwa sasa Tanzania iko katika daraja “A” miongoni mwa nchi zinazofanya vizuri katika masuala ya Utawala Bora na Haki za Binadamu,” amesema Jaji Mwaimu.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula ameipongeza Tume hiyo kwa kutekeleza majukumu yake ikiwemo kuishauri Serikali katika kuzingatia na kutekeleza masuala ya haki za binadamu na utawala bora kama ilivyoridhia katika majukwaa ya kimataifa. 

“Naipongeza Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kwa kutekeleza majukumu yake vizuri ikiwemo kuishauri Serikali katika kuzingatia na kutekeleza masuala ya haki za binadamu na utawala bora kama ilivyoridhia katika majukwaa ya kimataifa,” amesema Balozi Mulamula. 

Balozi Mulamula ameongeza kuwa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ya Tanzania ni mwanachama katika tume nyingine za kikanda na kimataifa ambazo hupima viwango vya utekelezaji wa Haki za binadamu na Utawala Bora ambapo kwa sasa Tanzania ina kiwango “A”.

Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (Jaji Mstaafu) Mathew Mwaimu akimueleza jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula wakati walipokutana kwa maongezi katika ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula akiteta jambo na Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (Jaji Mstaafu) Mathew Mwaimu wakati walipokutana kwa maongezi katika ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Mazungumzo baina ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula na Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (Jaji Mstaafu) Mathew Mwaimu yakiendelea katika ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (Jaji Mstaafu) Mathew Mwaimu, Kamishna kutoka Tume ya haki za Binadamu na Utawala Bora Bw. Nyanda Shuli na maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki



Sunday, May 16, 2021

TANZANIA YAZINDUA RASMI MAADHIMISHO YA MIAKA 40 YA SADC

 Na Mwandishi wetu, Dar

Tanzania imezindua rasmi maadhimisho ya kitaifa ya Kumbukumbu ya Maadhimisho ya Miaka 40 tangu kuanzishwa kwa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) tarehe 1 Aprili 1980. 

Akiongelea uzinduzi wa maadhimisho hayo Jijini Dar es Salaam, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) amesema Tanzania ikiwa ni miongoni mwa nchi 16 wanachama wa SADC inajivunia mafanikio yaliyopatikana ambayo yanaenzi mchango mkubwa wa Viongozi Wakuu waanzilishi wa SADC ambao maono yao yaliweka msingi wa ukombozi wa kisiasa na kiuchumi kwa nchi za Kanda ya Kusini mwa Afrika. 

Balozi Mulamula amesema wakati SADC ikiadhimisha miaka 40 tangu kuanzishwa kwake, Tanzania imejipanga kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu SADC  na fursa zake kiuchumi, kijamii na kisiasa na itaongeza hamasa kwa raia wake ili wachangamkie fursa zinazopatikana ndani ya jumuiya hiyo.

“Pamoja na mambo mengine, tumejipanga kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu mtangamano wa SADC na faida za uanachama kwenye Jumuiya hii ikiwa ni pamoja na fursa zilizopo za kiuchumi, kijamii na kisiasa, kuangazia mafanikio yaliyofikiwa katika masuala ya amani na usalama na pia maendeleo ya kiuchumi kwa watu wote katika Kanda ya Kusini mwa Afrika; na kuongeza hamasa kwa makundi mbalimbali kama wafanyabiashara, vijana, wanawake, makundi maalum na wananchi kwa ujumla kuchangamkia fursa za kiuchumi na kijamii zinazopatikana kupitia uanachama wa SADC,” amesema Balozi Mulamula. 

Waziri Mulamula amesema katika kuadhimisha miaka 40 ya SADC, Tanzania imeandaa mihadhara kuhusu umuhimu wa SADC kwa Tanzania na Kanda ya Kusini mwa Afrika ambapo mihadhara hiyo itafanyika katika baadhi ya vyuo vikuu vya hapa nchini. Amesema mhadhara wa kwanza utafanyika tarehe 19 Mei, 2021 katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) mhadhara wa pili utafanyika katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) tarehe 21 Mei, 2021 mhadhara wa tatu utafanyika katika Chuo Kikuu cha Zanzibar (SUZA) tarehe 26 Mei 2021 na mhadhara wa hitimisho utafanyika katika Chuo cha Diplomasia (CFR) tarehe 27 Mei, 2021  

Balozi Mulamula ameyataja mafanikio yaliyopatikana ndani ya miaka hiyo 40 ya SADC kuwa ni pamoja na harakati za ukombozi hususan kwa nchi za Kusini mwa Afrika na kuimarika kwa hali ya Ulinzi na Usalama na masuala ya demokrasia na utawala bora katika nchi za SADC

“Itakumbukukwa kuwa, Tanzania wakati wa uongozi wa Hayati Mwalimu Julius Nyerere ilifanya kazi kubwa ya kusaidia harakati za ukombozi hususan kwa nchi za Kusini mwa Afrika. Kadhalika,. Kadhalika, Tanzania chini ya Uongozi wa Rais wa Awamu ya Tano Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ilikuwa Mwenyekiti wa Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC kwa kipindi cha mwaka mmoja kuanzia mwezi Agosti 2018 hadi Agosti 2019 ambapo katika kipindi hicho cha uenyekiti mchango wa Tanzania ulifanikisha masuala mbalimbali ndani ya SADC kukamilika ikiwa ni pamoja na kuimarika kwa hali ya Ulinzi na Usalama na masuala ya demokrasia na utawala bora katika nchi za SADC,” amesema Waziri Mulamula

Ameyataja mafanikio mengine kuwa ni pamoja na kuzinduliwa kwa mfumo wa uombaji na utoaji vyeti vya utambuzi wa Uasili wa Bidhaa kwa njia ya mtandao, kuzinduliwa kwa Baraza la Biashara la SADC, kuongezeka kwa uzalishaji wa umeme wa SADC wa megawati 3,595 sawa na asilimia 90 ya lengo la kuzalisha megawati 4000, kuandaliwa kwa Dira ya maendeleo ya SADC ya mwaka 2050 pamoja na Mpango Elekezi wa Maendeleo ya Kikanda (RISDP) wa Mwaka 2020-2030. 

“Mafanikio mengine ni kuridhiwa kwa lugha ya Kiswahili kuwa miongoni mwa lugha nne za SADC, kupitishwa kwa Azimio la Kuondolewa Vikwazo vya iuchumi vilivyowekwa dhidi ya Zimbabwe tangu mwaka 2000. Azimio hilo liliridhia  tarehe 25 Oktoba ya kila mwaka kuwa siku maalum ya kupinga vikwazo vya kiuchumi dhidi ya Zimbabwe,” amesema Balozi Mulamula.

Aidha, kumbukumbu ya maadhimisho hayo kwa ngazi ya kikanda itahitimishwa tarehe 5 Juni, 2021 kwa mhadhara wa umma utakaofanyika pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC utakaofanyika kuanzia tarehe 30 Mei hadi 8 Juni 2021 jijini Maputo, Msumbiji.

Kaulimbiu ya maadhimisho haya ni:  “Miaka 40 ya SADC ya Kuimarisha Amani na Usalama, Kuhamasisha Maendeleo na Ustahimilivu wa  Changamoto Zinazoikabili Dunia” . 

SADC ilianzishwa kutoka kwa uliokuwa Mkutano wa Uratibu wa Maendeleo Kusini mwa Afrika (Southern African Development Coordination Conference-SADCC) (SADCC) ambao ilianzishwa rasmi Lusaka, Zambia mwezi Aprili 1980 baada ya Nchi za Mstari wa Mbele kuridhia Azimio la Lusaka lililojulikana kama “Kusini mwa Afrika: Kuelekea Ukombozi wa Kiuchumi  ambao pamoja na mambo mengine, ulilenga kuimarisha sekta muhimu za kuchochea maendeleo ya kanda kama vile Uchukuzi na Mawasiliano, Kilimo na Chakula, Viwanda, Maendeleo ya Rasilimali Watu na Nishati. Nchi Wanachama waanzilishi wa SADCC ni Angola, Botswana, Lesotho, Malawi, Msumbiji, Swaziland, Tanzania, Zambia na Zimbabwe.

Mwezi Agosti 1992, Wakuu wa Nchi na Serikali waliokutana jijini Windhoek, Namibia walisaini Mkataba wa kuibadilisha SADCC kuwa SADC na kutoa fursa ya kutafsiri upya misingi ya ushirikiano miongoni mwa Nchi Wanachama kutoka kwenye muungano usio rasmi na kuwa muungano wa kisheria. SADC ina wanachama 16 ambao ni Angola, Botswana, Comoros, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Eswatini, Lesotho, Madagascar, Malawi, Mauritius, Msumbiji, Namibia, Ushelisheli, Afrika Kusini, Tanzania, Zambia na Zimbabwe.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula


Saturday, May 15, 2021

URUSI: MATATIZO YA AFRIKA YATATULIWE NA WAAFRIKA WENYEWE

 Na Mwandishi wetu, Dar

Shirikisho la Urusi limesema linaunga mkono jitihada zinazofanywa na Umoja wa Afrika katika kutatua changamoto zinazolikabili bara hilo kwa kuwa matatizo ya Afrika yanahitaji kutatuliwa na Waafrika wenyewe bila kuingiliwa na Mataifa mengine.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Mjumbe Maalum wa Rais wa Shirikisho Urusi kuhusu masuala ya Afrika na Mashariki ya Kati Mhe. Mikhail Bogdanov ameyasema hayo jijini Dar es Salaam alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (Mb) na kupongeza jitihada zinazofanywa na Tanzania na Afrika kwa ujumla katika kutatua changamoto za kiusalama katika eneo la maziwa makuu.

“Tunaunga mkono jitihada zinazofanywa na Umoja wa Afrika katika kutatua changamoto zinazolikabili Afrika kwa kuwa matatizo ya Afrika yanahitaji kutatuliwa na Waafrika wenyewe,” amesema Bogdanov. Pia Naibu waziri huyo amepongeza jitihada zinazofanywa na Tanzania na Afrika kwa ujumla katika kutatua changamoto za kiusalama katika eneo la maziwa makuu.

Aidha, Bogdanov ameongeza kuwa Urusi ni moja kati ya nchi zinazoamini kuwa Afrika inaweza kutatua matatizo yake bila ya kuingiliwa kutokana na mazingira yaliyopo na kwamba nchi hiyo ipo tayari kushirikiana na Afrika hususani Tanzania katika kuleta amani na usalama sambamba na kuchochea jitihada za maendeleo ikiwemo biashara na uwekezaji.

Kwa upande wake waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula amemuomba Waziri huyo kuimarisha zaidi mahusiano ya diplomasia ya Uchumi hususani katika sekta ya biashara na uwekezaji kutokana na takwimu zilizopo kuonesha kiwango kidogo cha mahusiano ya kibiashara na uwekezaji.

“Tumejadili masuala la kuimarisha uhusiano wa Tanzania na Urusi hasa katika sekta ya biashara na uwekezaji, ambapo Mhe. Bogdanov ameahidi kulifanyia kazi suala hilo na kuhakikisha kuwa tunakuza biashara na uwekezaji,” amesema Balozi Mulamula  

Pia Balozi Mulamula amesema Tanzania iko tayari kuwa mwenyeji wa mkutano wa ushirikiano kati ya Urusi na Afrika ambao umepangwa kufanyika Afrika ambapo Umoja wa Afrika unajukumu la kupendekeza nchi moja ambayo itakuwa mwenyeji wa mkutano huo.

Balozi Mulamula amemuomba pia Naibu Waziri huyo wa Mambo ya Nje wa Shirikisho la Urusi kuhamasisha watalii kutoka Urusi kuja kwa wingi hapa nchini na kwamba licha ya ugonjwa wa COVID 19 Tanzania imechukua tahadhari zote zinazosisitizwa na Shirika la Afya Duniani.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) akimkaribisha Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Mjumbe Maalum wa Rais wa Shirikisho Urusi kuhusu masuala ya Afrika na Mashariki ya Kati Mhe. Mikhail Bogdanov pamoja na ujumbe wake katika Ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) akiteta jambo na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Mjumbe Maalum wa Rais wa Shirikisho Urusi kuhusu masuala ya Afrika na Mashariki ya Kati Mhe. Mikhail Bogdanov katika Ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Mjumbe Maalum wa Rais wa Shirikisho Urusi kuhusu masuala ya Afrika na Mashariki ya Kati Mhe. Mikhail Bogdanov akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula katika Ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam


Kikao kikiendelea 



PONGEZI

 


Wednesday, May 12, 2021

JAJI IMANI ABOUD APENDEKEZWA KUGOMBEA URAIS WA MAHAKAMA YA AFRIKA

 

Jaji wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu kutoka Tanzania Mhe. Jaji Imani Aboud 


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) akizungumza na Jaji wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu kutoka Tanzania Mhe. Jaji Imani Aboud katika ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Tuesday, May 11, 2021

TANZANIA MBIA MUHIMU WA UINGEREZA, JUMUIYA YA MADOLA

 Na Mwandishi wetu, Dar

Uingereza imesema Tanzania ni mbia wake muhimu wa miaka mingi katika maendeleo na Jumuiya ya Madola na kuahidi kuwa itaendelea kushirikiana na Tanzania katika masuala ya kidiplomasia, biashara na uwekezaji.

Waziri wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Afrika Mhe. James Duddridge ameyasema hayo jijini Dar es Salaam katika mazungumzo rasmi aliyoyafanya na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula muda mfupi baada ya kuwasili nchini kwa ziara ya kikazi ya siku mbili

“Lengo la ziara yangu hapa Tanzania ni kuendelea kuimarisha mahusiano baina ya Uingereza na Tanzania licha ya changamoto ya ugonjwa wa COVID – 19 ambapo Uingereza tumekusudia kuisaidia Tanzania kuboresha mifumo ya ukusanyaji kodi, mapambano dhidi ya rushwa lakini pia katika sekta za afya na elimu,” amesema Mhe. Duddridge.

Akizungumzia ziara hiyo ya waziri wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Afrika, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (Mb) amesema ziara hiyo ni kielelezo cha Tanzania kuheshimika na kukubalika miongoni mwa Jumuiya za Kimataifa na Mataifa ya nje na kwamba kipaumbele cha Serikali ya awamu ya sita ni diplomasia ya uchumi ambapo Uingereza ni moja kati ya nchi tatu kubwa zinazowekeza hapa nchini na hivyo kuwa ni miongoni mwa Mataifa muhimu kwa Tanzania katika kukuza diplomasia ya uchumi.

Balozi Mulamula ameongeza kuwa katika mazungumzo yao msisitizo mkubwa umewekwa katika uchumi na kukuza biashara pamoja na kuiendeleza miradi mikubwa iliyokuwa ikitekelezwa na Uingereza ikiwemo miradi ya kiwanda cha sukari na madini.

“Ujio wa Waziri wa Uingereza  anayeshughulikia masuala ya Afrika Mhe. Duddridge hapa nchini inathibitisha kuwa mahusiano ya Tanzania nje ya mipaka yake bado ni imara licha ya taarifa potofu zilizokuwa zikisambaa katika mitandao ya kijamii na vyombo vya habari vya nje zikitilia mashaka juu ya diplomasia ya Tanzania nje ya nchi,” amesema Balozi Mulamula.

Aidha, kuhusu masuala ya biashara na uwekezaji Balozi Mulamula amemuhakikishia Mhe. Duddridge kuwa mazingira ya uwekezaji ni salama na yanavutia baada ya kuboreshwa na hivyo kumtaka kuwahamasisha wawekezaji kutoka Uingereza kuja hapa nchini kuwekeza katika sekta mbalimbali.

Mara baada ya mazungumzo na Balozi Mulamula Waziri Duddridge amekutana na Waziri wa Viwanda na Biashara Prof. Kitila Mkumbo pamoja na Waziri wa Uwekezaji Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Uwekezaji, Mhe. Geoffrey Mwambe na baadae kukutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan na kesho (Jumatano) anatarajia kwenda Zanzibar kukutana na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Ali Mwinyi kabla ya kuhitimisha ziara yake ya kikazi ya siku mbili hapa nchini.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) akimkaribisha Waziri wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Afrika Mhe. James Duddridge katika Ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam. Waziri Duddridge ameambatana na Balozi wa Uingereza hapa nchini Mhe. David Concar


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) akiteta jambo na Waziri wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Afrika Mhe. James Duddridge wakati wa kikao chao kilichofanyika katika Ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam 


Waziri wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Afrika Mhe. James Duddridge akimueleza jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula wakati wa kikao chao kilichofanyika katika Ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam 


Kikao kikiendelea 


Sehemu ya wakurugenzi na maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakifuatilia kikao cha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula na Waziri wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Afrika Mhe. James Duddridge



Balozi wa Uingereza hapa nchini Mhe. David Concar (wa kwanza kulia) na baadhi ya maafisa kutoka ubalozi wa Uingereza wakifuatilia kikao cha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula na Waziri wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Afrika Mhe. James Duddridge


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Afrika Mhe. James Duddridge (mwenye tai ya bluu) pamoja na Balozi wa Uingereza Mhe. David Concar, Maafisa kutoka Ubalozi wa Uingereza, Wakurugenzi kutoka Wizarani