Friday, October 4, 2024

MKUU WA MISHENI YA UANGALIZI WA UCHAGUZI YA SADC NCHINI MSUMBIJI AFANYA MAZUNGUMZO NA MGOMBEA URAIS WA CHAMA CHA FRELIMO

Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mkuu wa Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC –SEOM) nchini Msumbiji, Mhe. Dkt. Amani Abeid Karume ameendelea kukutana na wadau mbalimbali wa uchaguzi mkuu wa Msumbiji ambapo leo tarehe 04 Oktoba, 2024 jijini Maputo amekutana na kufanya mazungumzo na Mgombea urais wa Chama cha FRELIMO, Mhe. Daniel Francisco Chapo.

 

Katika mazungumzo yao, Mhe. Chapo alimweleza Mhe. Dkt. Karume masuala mbalimbali kuhusu maandalizi ya chama hicho kuelekea uchaguzi mkuu wa rais na wabunge unaotarajiwa kufanyika nchini humo tarehe 09 Oktoba 2024.


Kwa upande wake,  Mhe. Dkt. Karume alimshukuru Mhe. Chapo kwa taarifa yake na kumweleza lengo la Misheni anayoiongoza  kuwa ni kuangalia uchaguzi kwa mujibu wa Kanuni na Miongozo  ya SADC inayoongoza Uchaguzi wa Kidemokrasia iliyorekebishwa mwaka 2021 na kuridhiwa na nchi wanachama. Pia alitumia nafasi hiyo kuwatakia  wananchi wa Msumbiji uchaguzi mwema wa amani na utulivu.

 

Wakati wa Mkutano huo, Mhe. Dkt. Karume aliambatana na Wajumbe wa Troika kutoka Tanzania, Zambia na Malawi, Sekretarieti ya SADC akiwemo Mwenyekiti wa Troika, Prof. Kula Ishmael Theletsane na  Wajumbe wa Baraza la Ushauri wa masuala ya Uchaguzi la SADC (SEAC). Wajumbe  wa Troika kutoka Tanzania walioshiriki ni pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushiriano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaibu Mussa na  Mshauri wa Rais masuala ya Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Sofia Mjema.

 

Mhe. Dkt. Karume kwa nafasi yake ya Mkuu wa Uangalizi wa Uchaguzi ya SADC ameendelea  kukutana na wadau mbalimbali wa uchaguzi ambapo hadi sasa amekutana na Mwenyekiti wa  Tume ya Uchaguzi ya Msumbiji (CNE), Mabalozi wa Nchi za SADC waliopo Msumbiji, Waziri wa Mambo ya Nje wa Msumbiji na Kamishna Msidizi wa Jeshi la Polisi la Msumbiji.

 

Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mkuu wa Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC-SEOM) nchini Msumbiji, Mhe. Dkt. Amani Abeid Karume akizungumza na Mgombea urais wa Chama cha FRELIMO, Mhe. Daniel Francisco Chapo.  Mazungumzo yao yamefanyika tarehe 04 Oktoba 2024 jijini Maputo. Uchaguzi wa Rais na Wabunge nchini Msumbiji utafanyika tarehe 09 Oktoba 2024.

Mazungumzo yakiendelea ambapo Mhe. Chapo amemweleza Mhe. Dkt. Karume kuhusu maandalizi ya uchaguzi ya Chama chake kuelekea uchaguzi tarehe 09 Oktoba 2024

Mhe. Chapo akizungumza

Wajumbe wa Troika kutoka Tanzania ambao walishiriki mazungumzo kati ya Mkuu wa Misheni ya SADC ya Uangalizi wa Uchaguzi nchini Msumbiji, Mhe. Dkt Karume na mgombea urais wa Chama cha FRELIMO, Mhe. Chapo (hawapo pichani). Kushoto ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaibu Mussa na Mshauri wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania masuala ya Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Sofia Mjema

Wajumbe wa Troika kutoka Zambia nao wakishiriki mazungumzo kati ya Mkuu wa Misheni ya SADC ya Uangalizi wa Uchaguzi nchini Msumbiji, Mhe. Dkt Karume na mgombea urais wa Chama cha FRELIMO, Mhe. Chapo (hawapo pichani). 
Wajumbe wakishiriki mazungumzo kati ya Mkuu wa Misheni ya SADC ya Uangalizi wa Uchaguzi nchini Msumbiji, Mhe. Dkt Karume na mgombea urais wa Chama cha FRELIMO, Mhe. Chapo (hawapo pichani). 
Mkuu wa Misheni ya SADC ya Uangalizi wa Uchaguzi nchini Msumbiji, Mhe. Dkt Karume akiagana na  mgombea urais wa Chama cha FRELIMO, Mhe. Chapo baada ya kumaliza mazungumzo yao 
Picha ya pamoja




















MISHENI YA UANGALIZI WA UCHAGUZI YA SADC NCHINI MSUMBIJI YAZINDULIWA RASMI

Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mkuu wa Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC-SEOM) nchini Msumbiji, Mhe. Dkt. Amani Abeid Karume amezindua rasmi Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi  leo tarehe 03 Oktoba 2024 katika hafla iliyofanyika jijini Maputo.

 

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo uliowashirikisha wadau mbalimbali muhimu wakiwemo Mabalozi wanaowakilisha nchi zao nchini Msumbiji, Wawakilishi kutoka Serikali ya Msumbiji, Tume ya Taifa ya Uchaguzi ya Msumbiji (CNE), Vyama vya Siasa, Viongozi wa Dini, Jumuiya za Kiraia na waandishi wa habari, Mhe. Dkt. Karume ameishukuru Serikali ya Msumbiji kwa kuialika Misheni hiyo ambayo ina jukumu la kuangalia namna misingi ya demokrasia, taratibu na kanuni za uchaguzi za SADC zinavyotekelezwa.


Amesema Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya SADC pamoja na mambo mengine itatathmini mwenendo wa uchaguzi kulingana na  Kanuni na Miongozo ya SADC inayoongoza Uchaguzi wa Kidemokrasia iliyorekebishwa mwaka 2021 na kuridhiwa na Nchi Wanachama.


Amesema pamoja na mambo mengine, Kanuni na Miongozo hiyo inazitaka nchi wanachama kushirikisha wananchi  katika mchakato wa demokrasia, kuwawezesha  wananchi kufurahia  haki za binadamu na kuwa huru katika kushirikiana, kukusanyika  na kujieleza. Kadhalika kanuni na miongozo hiyo imeweka mikakati ya kuzuia rushwa, upendeleo, migogoro ya kisiasa, kutovumiliana na kuhakikisha zinakuwepo fursa sawa  kwa vyama vyote vya siasa katika kutumia vyombo vya habari vinavyomilikiwa na Serikali na kuhakikisha  uhuru wa wananchi kupata taarifa kuhusu masuala ya uchaguziunazingatiwa.

 

Mhe. Dkt. Karume pia alitumia fursa hiyo kupongeza kazi kubwa iliyofanywa  na Misheni ya Ulinzi wa Amani ya SADC nchini Msumbiji (SAMIM), ambayo ilifanikiwa kudhibiti  vikundi vya kigaidi vilivyoibka katika maeneo ya Kaskazini mwa Msumbiji na kuishukuru Serikali ya Msumbiji kwa kuahidi kuendelea kulinda mafanikio yaliyofikiwa na SAMIM katika eneo hilo.

 

Vilevile, Mhe. Dkt. Karume alilipongeza Jeshi la Ulinzi la Msumbiji na vyombo vingine vya Usalama vya nchi hiyo kwa jitihada zao zilizofanikisha Wananchi katika maeneo ya Kaskazini mwa nchi hiyo wanajiandikisha kwa ajii ya kupiga kura licha  ya changamoto za kiusalama.

 

Mhe. Dkt. Karume alitumia nafasi hiyo pia kuwatakia uchaguzi wa amani na utulivu wananchi wa Msumbiji na kutoa wito kwa wale wote waliojiandikisha kujitokeza  kwa wingi siku ya tarehe 09 Oktoba 2024 na kupiga kura. Pia alitoa rai kwa wadau wote wa siasa nchini Msumbiji kuheshimu maoni na mitazamo tofauti ya kisiasa miongoni mwao na kujua wajibu wao katika kipindi chote cha uchaguzi na baada ya uchaguzi.

 

Naye Mkurugenzi wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama, Prof. Kula Ishmael Theletsane alieleza umuhimu wa Misheni za Uangalizi kuwa zinalenga  kufikia malengo  mahsusi ya mafanikio hususan kwa mtangamano wa SADC kupitia kanuni ya ustahimilivu, utekelezaji wa demokrasia, utwala bora na amani.

 

Misheni  ya SADC, iliwasili nchini Msumbiji tarehe 24 Septemba, 2024 na itakuwepo nchini humo hadi tarehe 20 Oktoba, 2024 kwa lengo la kuangalia uchaguzi kwa mujibu  wa Kanuni na Miongozo ya SADC inayoongoza Uchaguzi  wa Kidemokrasia iliyorekebishwa mwaka 2021.

 

Misheni hiyo ya SADC ina jumala ya wajumbe 97 ambapo miongoni mwao 52 ni waangalizi wa uchaguzi ambao watasambazwa kwenye majimbo 11 ya uchaguzi nchini Msumbiji ambayo ni Cabo Delgado, Nampula, Niassa, Maputo City, Maputo, Tete, Gaza, Inhambane, Sofala, Manica na Zambezia.

Waangalizi hao wanatoka katika Nchi 10 ambazo ni wanachama wa SADC. Nchi hizo ni Tanzania, Angola, Botswana, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Eswatini, Malawi, Namibia, Afrika Kusini, Zambia na Zimbabwe.


Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mkuu wa Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC-SEOM) nchini Msumbiji, Mhe. Dkt. Amani Abeid Karume akizindua rasmi Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi tarehe 03 Oktoba 2024 katika hafla iliyofanyika jijini Maputo. Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge nchini Msumbiji unatarajiwa kufanyika tarehe 09 Oktoba 2024

Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mkuu wa Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC-SEOM) nchini Msumbiji, Mhe. Dkt. Amani Abeid Karume akizindua rasmi Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi tarehe 03 Oktoba 2024 katika hafla iliyofanyika jijini Maputo. Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge nchini Msumbiji unatarajiwa kufanyika tarehe 09 Oktoba 2024

Mkurugenzi wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama , Prof. Kula Ishmael Theletsane akizungumza wakati wa uzinduzi wa  Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya SADC nchini Msumbiji. Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge nchini humo unatarajiwa kufanyika tarehe 09 Oktoba 2024
Mjumbe wa Troika ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaibu Mussa akichangia jambo wakati wa uzinduzi wa Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya SADC nchini Msumbiji. Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge nchini humo unatarajiwa kufanyika tarehe 09 Oktoba 2024

Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mkuu wa Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC-SEOM) nchini Msumbiji, Mhe. Dkt. Amani Abeid Karume akizungumza na na Waangalizi 52 wa SADC kwa lengo la kuwaaga kabla ya kusambazwa katika majimbo 11 ya uchaguzi nchini Msumbiji kwa ajili ya kuangalia uchaguzi. Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge nchini Msumbiji unatarajiwa kufanyika tarehe 09 Oktoba 2024

Balozi wa Tanzania nchini Msumbiji, Mhe. Phaustine Kasike akishiriki hala ya uzinduzi wa 
Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya SADC nchini Msumbiji. Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge nchini humo unatarajiwa kufanyika tarehe 09 Oktoba 2024
Mjumbe wa Troika ambaye pia ni Mshauri wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika masuala ya Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Sofia Mjema akishiriki hafla ya uzinduzi wa
Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya SADC nchini Msumbiji. Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge nchini humo unatarajiwa kufanyika tarehe 09 Oktoba 2024
Mjumbe wa Troika ambaye ni Mkurugenzi wa Ushirikiano wa Kikanda katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Talha Waziri akifuatilia uzinduzi wa 
Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya SADC nchini Msumbiji. Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge nchini humo unatarajiwa kufanyika tarehe 09 Oktoba 2024
Sehemu ya Waangalizi wa Uchaguzi wa SADC wakifuatilia hafla ya uzinduzi wa
Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya SADC nchini Msumbiji. Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge nchini humo unatarajiwa kufanyika tarehe 09 Oktoba 2024

Sehemu nyingine ya waangalizi
Waangalizi wa Uchaguzi wa SADC nchini Msumbiji wakishiriki uzinduzi wa 
Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya SADC nchini Msumbiji. Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge nchini humo unatarajiwa kufanyika tarehe 09 Oktoba 2024
Sehemu nyingine ya waangalizi wa uchaguzi 
Meza kuu katika picha ya pamoj
Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mkuu wa Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC-SEOM) nchini Msumbiji, Mhe. Dkt. Amani Abeid Karume akiwa katika picha ya pamoja na Mabalozi wanaowakilisha nchi zao Msumbiji walioshiriki hafla ya uzinduzi wa misheni hiyo
Picha ya pamoja ya kundi la waangalizi wa uchaguzi
Picha ya pamoja ya waangalizi wa uchaguzi

Wageni waalikwa wakifuatilia uzinduzi

Tuesday, October 1, 2024

NAIBU WAZIRI LONDO AWAPONGEZA NJE – SPORTS KWA KUFANYA VIZURI SHIMIWI


 NAIBU WAZIRI LONDO AWAPONGEZA NJE – SPORTS KWA KUFANYA VIZURI SHIMIWI

 

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki, Mhe. Denis Londo amewapongeza wanamichezo wa timu ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki (Nje - Sports), kwa kufanya vizuri katika michezo ya SHIMIWI inayoendelea mjini Morogoro.

Mhe. Londo amezipongeza Timu ya Mpira wa miguu wanaume kwa kuingia Nusu fainali , Timu ya Kamba wanawake na Timu ya Mpira wa pete kwa kuingia 16 Bora ya michuano ya SHIMIWI yanayoendelea Mkoani Morogoro

 Mhe. Londo ametoa pongezi hizo tarehe 30 Septemba, 2024 alipokutana na wachezaji wa Nje – Sports katika hafla ya Chakula cha jioni kilichoandaliwa kwa ajili yao mjini Morogoro. 

Hafla hiyo imefanyika maalum kuwapa hamasa wachezaji ili waendelee kufanya vizuri kwenye michuano hiyo. 

Katika hafla hiyo Mhe. Londo alifikisha salam za Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Thabit Kombo ambaye aliwataka wachezaji hao waendelee kupambana hadi mwisho.

 “Nilimweleza Mhe. Waziri kuwa naenda Mikumi lakini nitarudi jioni kwa ajili ya chakula cha jioni na Ninyi. amefurahia na ameniambia niwaletee salamu za upendo na kusema kwamba yupo pamoja na ninyi na muendelee kupambana hadi mwisho na anawatakia kila la kheri” Amesema Mhe. Londo

 Naye Mwenyekiti wa Michezo Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Ismail Abdallah, ameupongeza na kuushukuru uongozi wa Wizara kwa namna wanavyo wapa miongozo na namna wanavyo wapa hamasa ambayo imekuwa chachu ya wao kufanya vizuri kwenye michezo hiyo.  

Pia amempongeza Naibu Waziri Mhe. Londo kwa kufika uwanjani kujionea pamoja na kuzungumza na wachezaji kitu kilichowapa hamasa kubwa wachezaji na kupelekea kufanya vizuri kwenye mchezo wao.

 “Mafanikio haya Mheshimiwa yamechagizwa sana na kitendo ulichokifanya juzi, kitendo cha kutenga muda wako na kuja kututembelea na hukuja kambini bali umekuja Uwanjani, kwakweli toka tumefika hapa sidhani kama kuna Timu Waziri wao amekuja kuwatembelea kama ulivyo fanya, kwakweli umetujengea hamasa kubwa, heshima kubwa mpaka tumeonekana Watoto pendwa sijui nitumie neno gani lakini tumeonekana wakipekee. Tunashukuru sana” Amesema Bwa. Ismail

 Nje – Sports inatarajia kuingia dimbani hapo kesho kwa Mchezo wa Nusu Fainal dhidi ya mpinzani Wake Wizard ya Maji.