Friday, October 18, 2024

Tanzania na Iran kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia katika biashara na uwekezaji


Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Kiislam ya Irani zimekusudia kusaini hati mbalimbali za makubaliano ili kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia katika biashara na uwekezaji kwa manufaa ya pande zote mbili.

Mkurugenzi wa Idara ya Mashariki ya Kati wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Abdalah Kilima amesema hayo leo 17 Oktoba, 2024, katika kikao cha ngazi ya Wataalamu na Maafisa Waandamizi kutoka Tanzania na Iran, kilichofanyika katika Kituo cha Mikutano  cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), kilichojikita katika kuandaa ajenda za kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia kwa manufaa ya nchi hizo.

Balozi Kilima ambaye pia alikuwa mwenyekiti mwenza katika kikao hicho, amesema hatua ya ukuzaji Biashara na Uwekezaji baina ya Tanzania na Iran, itahusisha maeneo ya kipaumbele katika sekta ya Kilimo, Mifugo, Uvuvi, Nishati, Teknolojia ya Habari na Utunzaji wa Maji Kale.

Maeneo mengine ni mafuta na gesi, ulinzi na usalama, maeneo ya kupambana na majanga na sheria; hatua ambayo itaziwezesha nchi hizi kutia saini hati za makubaliano ya ushirikiano kwa utekelezaji. 

Hati hizo za makubaliano zitatiwa saini na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa Tanzania Mhe. Balozi Thabit Kombo (Mb) na Naibu Waziri wa Kilimo wa Iran Mhe. Dkt. Gholamreza Nouri katika kikao cha kilele cha Mawaziri wa nchi hizo kitakachofanyika tarehe 19 Octoba 2024, JNICC, jijini Dar es Salaam.

Balozi Kilima amesema hati zitakazosainiwa ni pamoja na hati ya kutotoza kodi mara mbili, ushirikiano katika sekta ya ulinzi, kupambana na majanga, Sanaa na Michezo na ushirikino katika sekta ya kumbukumbu na nyaraka.

Naye Mwenyekiti mwenza wa Kikao hicho cha Wataalam na Maafisa Wandamizi kwa upande wa Iran, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Kilimo wa nchi hiyo Mhe. Dkt. Gholamreza Nouri ameishukuru Tanzania kwa kuimarisha ushirikiano wa kimataifa na Iran kwani utawezesha mataifa hayo kukuza na kuendeleza mahusiano mema yaliyopo ya kidiplomasia.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.