Saturday, July 16, 2022

MAKATIBU WAKUU WA SADC WAANZA MAANDALIZI YA MKUTANO WA 24 WA KAMATI YA MAWAZIRI

Mkutano wa 24 wa Kawaida wa Kamati ya Mawaziri wa Asasi ya Ushirikiano katika masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (MCO) utafanyika jijini Pretoria, Afrika Kusini kuanzia tarehe 16 hadi 19 Julai, 2022. 

 

Mkutano huo umetanguliwa na Mkutano wa Makatibu Wakuu unaofanyika tarehe 16 na 17 Julai 2022 ambapo ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano wa Kamati hii unaongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma M. Rajab ambaye anamwakilisha Katibu Mkuu, Balozi Joseph Sokoine. 

 

Mkutano wa 24 unalenga pamoja na mambo mengine kupokea na kujadili agenda mbalimbali zikiwemo mapitio ya utekelezaji wa maamuzi ya Mkutano wa 23 wa MCO na Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC; Hali ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya kanda; na tathmini ya hali ya Ulinzi na Usalama katika Kanda pamoja na Tathmini ya athari zitokanazo na mgogoro unaoendelea katika bara la Ulaya.

 

Viongozi wengine kutoka Tanzania wanaoshiriki Mkutano wa Makatibu Wakuu ni pamoja na Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Makakala, Mwakilishi wa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Mnadhimu Mkuu wa Jeshi, Lt. Jenerali Salum Othman, Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, Mhe. Meja Jenerali (Mst) Gaudence Milanzi, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Kuzuia na  Kupambana na Rushwa,  Kamishna wa Polisi Salum  Hamduni, Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Agnes Kayola na Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga.

 

Ujumbe wa Tanzania kwa ngazi ya Mawaziri unatarajiwa kuongozwa na Mhe. Balozi Liberata Mulamula, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambaye ataambatana na Mhe. Dkt. Stergomena Tax, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Mohammed Rajab akiongoza ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano wa Makatibu Wakuu unaofanyika kwa ajili ya kuandaa Mkutano wa 24 wa Kawaida wa Kamati ya Mawaziri wa Asasi ya Ushirikiano katika masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC MCO) utakaofanyika jijini Pritoria, Afrika Kusini kuanzia tarehe 16 hadi 19 Julai 2022.

Mwenyekiti wa Mkutano wa Makatibu Wakuu (kulia) na Mjumbe kutoka Sekretarieti ya SADC  wakati wa ufunguzi wa mkutano huo unaofanyika jijini Pretoria, Afrika Kusini tarehe 16 na 17 Julai 2022 kwa ajili ya kuandaa Mkutano wa 24 wa Kamati ya Mawaziri wa Asasi ya Ushirikiano katika masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC.

Sehemu ya Ujumbe wa Serikali ya Angola ukishiriki Mkutano wa Makatibu Wakuu

Sehemu ya Ujumbe wa Serikali ya Botswana ukishiriki Mkutano wa Makatibu Wakuu

Wakati huohuo Mhe. Balozi Fatma ameongoza kikao kati yake na ujumbe wa Tanzania unaoshiriki Mkutano wa Makatibu Wakuu. Pichani Balozi Fatma akizungumza na ujumbe huo (hawapo pichani) kuhusu namna ya kushiriki kikamilifu kama Tanzania kwenye Mkutano wa 24 wa Kawaida wa Kamati ya Mawaziri wa Asasi ya Ushirikiano katika masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC. Kushoto ni Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Agnes Kayola.

Viongozi mbalimbali kutoka Serikalini akiwemo Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Kuzuia na  Kupambana na Rushwa,  Kamishna wa Polisi Salum  Hamduni (kushoto) wakimsikiliza kiongozi wa ujumbe wa Tanzania, Balozi Fatma (hayupo pichani) wakati wa kikao cha maandalizi ya ushiriki wa Tanzania kwenye Mkutano wa Makatibu Wakuu

Viongozi wengine akiwemo Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Makakala (kushoto) wakati wa kikao cha maandalizi

Kaimu Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, Bw. Shija akifuatilia kikao cha maandalizi cha ujumbe wa Tanzania unaoshiriki Mkutano wa Makatibu Wakuu

Mkurugenzi wa Mawasiliano katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga akishiriki kikao cha maandalizi kilichohusisha ujumbe wa Tanzania.


 

TANZANIA YATOA WITO KWA BARA LA AFRIKA KUIMARISHA AMANI NA USALAMA


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) ametoa wito kwa nchi za Umoja wa Afrika (AU) kuendelea kuunga mkono juhudi mbalimbali zinazofanywa na umoja huo katika kutafuta suluhu ya migogoro ili kudumisha amani na usalama barani Afrika. 

Waziri Mulamula ametoa wito huo alipokuwa akichangia ajenda iliyohusu masula ya nafasi za uanachama katika Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika kwenye Mkutano wa 41 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika uliofanyika jijini Lusaka Zambia tarehe15 Julai 2022.

Akitoa mchango wake kwa lugha ya Kiswahili Waziri Mulamula alieleza kuwa Tanzania inaunga mkono juhudi zinazofanywa na AU kwa lengo la kuimarisha utendaji wa Baraza la Umoja na Usalama la Umoja wa Afrika ikiwemo kuendelea kuwa na idadi ya wanachama waliopo katika baraza hilo. 

“Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni muumini mkubwa wa usawa wa uwakilishi wa kanda na nchini wanachama ndani ya Umoja wa Afrika na Taasisi nyingine za kimataifa. Hii ni kutokana na imani yetu kuwa endapo usawa utazingatiwa tutaendelea kudumisha umoja na mshikamano wetu ambao kwa muda mrefu umeendelea kuwa nguzo ya amani na usalama katika bara letu” Alieleza Waziri Mulamula. 

Sambamba na hilo katika Mkutano huo wa Baraza la Mawaziri miongoni mwa ajenda zilizojadiliwa ilikuwa ni kupitisha bajeti ya Umoja wa Afrika kwa mwaka 2023. Kitu muhimu katika mkutano huu ni kuwa bajeti hiyo imeweka kifungu kwa ajili ya utekelezaji wa maamuzi ya Mkutano wa 35 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika yaliyopitsha Kiswahili kuwa Lugha ya Kazi ya Umoja wa Afrika. 

Akizungumzia suala hilo Waziri Mulamula ameeleza kuwa amefarijika kuona kipengele maalumu cha kutekeleza maamuzi ya kukifanya Kiswahili kuwa lugha ya kazi ya Umoja wa Afrika inafanyiwa kazi kwa vitendo. Aliongeza kusema hatua hiyo itaharakisha utekelezaji wa maamuzi hayo kwa kuwa itarahishisha utendaji wa shughuli mbalimbali muhimu kama vile kugharamia zoezi la kutafsiri nyaraka mbalimbali, kulipa au kuajili wakalimani na kuwajengea uwezo wa lugha hiyo wataalamu wa ngazi mbalimbali katika Kamisheni ya Umoja wa Afrika na Taasisi nyingine za umoja huo. 

Aidha katika mkutano huo wa 41 wa Baraza la Mawaziri la Umoja wa Afrika kwa mara ya kwanza wameanda baadhi ya taarifa zinazotokana na mkutano huo kwa lugha ya Kiswahili.

Vilevile Waziri Mulamula kwenye Mkutano huo alichangia mjadala wa kupitisha bajeti ya Umoja wa Afrika kwa mwaka 2023 ambapo kwa niaba ya Tanzania ameunga mkono mapendekezo ya bajeti ya umoja huo. Pia alitumia nafasi hiyo kutoa wito kwa Kamisheni ya Umoja wa Afrika na Taasisi zake kuendelea kuchukua hatua za kupunguza matumizi ili kuendana na uhalisia wa hali ya uchumi wa nchi zetu za Afrika katika nyakati hizi.

 

“Tunatoa wito kwa Kamisheni na Taasisi nyingine za Umoja wa Afrika kuweka mipango mizuri ya miradi na shughuli zake ili kuendana na uwezo wa kutekeleza miradi hiyo na kuweka kipaumbele kwa miradi yenye tija kwa wananchi wa Bara la Afrika” Alisema Waziri Mulamula.

Mkutano wa 41 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika umeongozwa na mwenyekiti wake Mhe. AissataTall Sall ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje wa Senegal.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) akichangia jambo kwenye Mkutano wa 41 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika (AU) uliofanyika jijini Lusaka, Zambia
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akifuatilia mjadala uliokuwa ukiendelea kwenye Mkutano wa 41 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika uliofanyika jijini Lusaka, Zambia.
Mkutano wa 41 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika uliofanyika jijini Lusaka, Zambia ukiendelea. 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akiwa katika picha ya pamoja na ujumbe wa Tanzania ulioshiriki katika Mkutano wa 41 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika (AU) uliofanyika jijini Lusaka, Zambia.

Friday, July 15, 2022

TANZANIA, UBELGIJI ZAKUBALIANA KUANZA MASHAURIANO YA KUANZISHA USHIRIKIANO UBORESHAJI WA HUDUMA ZA BANDARI

 








TANZANIA, UFARANSA ZAAHIDI KUENDELEZA USHIRIKIANO

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Ufaransa zimeahidi kuendeleza ushirikiano katika nyanja za elimu, afya, maji, usafirishaji, kilimo na utalii kwa maslahi mapana ya pande zote mbili.

Ahadi hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk aliposhiriki hafla ya kuandimisha Siku ya Taifa ya Ufaransa  iliyofanyika Jijini Dar es Salaam tarehe 14 Julai 2022.

Balozi Mbarouk alisema Tanzania na Ufaransa zimekuwa na uhusiano mzuri tangu mwaka 1961 na mataifa hayo yamekuwa na ushirikiano katika nyanja za elimu, afya, maji, usafirishaji, mawasiliano, utalii, kilimo, biashara na uwekezaji.

“Ufaransa imekuwa mdau mkubwa katika masuala ya uchumi ambapo kampuni mbalimbali kutoka Ufaransa zimewekeza nchini na zimekuwa zikichangia kutoa ajira kwa watanzania na kuongeza pato la taifa,” alisema Balozi Mbarouk 

Balozi Mbarouk aliongeza kuwa Ufaransa imekuwa mdau mkubwa wa utalii ambapo idadi ya watalii imekuwa ikiongezeka kutoka 25,000 kwa mwaka 2020 hadi 50,000 kwa mwaka 2022.

“Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan imekuwa ikiboresha mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuwavutia zaidi wawekezaji kutoka nje kuja kuwekeza  nchini…….pia Serikali inatambua na kuthamini mchango wa wafanyabishara wa Ufaransa katika kukuza sekta uchumi,” alisema Balozi Mbarouk.

Awali Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Nabil Hajlaoui alisema Ufaransa imefurahishwa na ushirikiano mzuri inaoupata kutoka Serikali ya Tanzania na kuahidi kuwa Ufaransa itaendelea kudumisha uhusiano huo kwa maslahi ya mataifa yote mawili.

Balozi Hajlaoui aliongeza kuwa Ufaransa itaendelea kushirikiana na Tanzania kuunga mkono juhudi mbalimbali za kukuza maendeleo ya kijamii, kisiasa na kiuchumi zinazofanywa na Serikali ya Tanzania.

“Tanzania imekuwa na uhusiano mzuri na Ufaransa kwa muda mrefu nawaahidi hapa kuwa uhusiano huu tutaendelea kuudumisha na kuulinda wakati wote,” alisema Balozi Hajlaoui

Balozi Hajlaoui aliongeza kuwa Ufaransa inaridhishwa na jitihada za Tanzania katika kuhakikisha usawa wa kijinsia katika jamii, uhuru wa demokrasia, kulinda amani na usalama ndani na kwenye kanda.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Mizengo Pinda, Mabalozi mbalimbali na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa wanaoziwakilisha nchi zao hapa nchini, asasi za kiraia, viongozi wa vyama vya siasa na wafanyabiashara.  
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akisalimiana na Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Nabil Hajlaoui wakati wa hafla ya kuandimisha Siku ya Taifa ya Ufaransa  iliyofanyika Jijini Dar es Salaam tarehe 14 Julai 2022

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akitoa hotuba yake katika hafla ya kuandimisha Siku ya Taifa ya Ufaransa  iliyofanyika Jijini Dar es Salaam tarehe 14 Julai 2022

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akitoa hotuba yake katika hafla ya kuandimisha Siku ya Taifa ya Ufaransa  iliyofanyika Jijini Dar es Salaam tarehe 14 Julai 2022

Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Nabil Hajlaoui akiwasilisha hotuba yake katika hafla ya kuandimisha Siku ya Taifa ya Ufaransa  iliyofanyika Jijini Dar es Salaam tarehe 14 Julai 2022


Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda akijadili jambo na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk katika hafla ya kuandimisha Siku ya Taifa ya Ufaransa  iliyofanyika Jijini Dar es Salaam tarehe 14 Julai 2022

Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Mizengo Pinda katika picha ya pamoja na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk, Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Nabil Hajlaoui na Afisa Mtendaji Mkuu NMB Bank, Bibi. Ruth Zaipuna pamoja na maafisa kutoka Ubalozi wa Ufaransa na Wasanii wa muziki wa kizazi kipya

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akiteta jambo na Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Nabil Hajlaoui wakati wa hafla ya kuandimisha Siku ya Taifa ya Ufaransa  iliyofanyika Jijini Dar es Salaam tarehe 14 Julai 2022



TANGAZO LA KAZI KATIKA SEKRETARIETI YA JUMUIYA YA MADOLA


 

Thursday, July 14, 2022

WAZIRI MULAMULA ASHIRIKI MKUTANO WA 41 WA BARAZA LA MAWAZIRI WA UMOJA WA AFRIKA


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) akichangia jambo kwenye Mkutano wa 41 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika unaoendelea jijini Lusaka, Zambia.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) yupo jijini Lusaka, Zambia kushiriki Mkutano wa 41 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika (AU) ulioanza leo tarehe 14 jijini humo.

Mkutano huo wa siku mbili umepokea na kujadili taarifa za kiutendaji za Taasisi za Umoja wa Afrika ikiwemo Kamati ya Wawakilishi wa Kudumu (Mabalozi) kwenye Umoja wa Afrika na Kamisheni ya Umoja wa Afrika katika kipindi cha Februari-Juni 2022.

Mkutano huo pia utapitisha Bajeti ya Umoja wa Afrika kwa mwaka 2023 pamoja na bajeti ya kifungu cha utekelezaji wa maamuzi ya Mkutano wa 35 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika yaliyopitisha Kiswahili kuwa Lugha ya Kazi ya Umoja huo.

Katika mkutano huo Waziri Mulamula amesisitiza Kamisheni ya Umoja wa Afrika kutoa kipaumbele katika utekelezaji wa maamuzi ya Kiswahili kuwa Lugha ya Kazi ya Umoja wa Afrika, kuhimiza matumizi sahihi ya rasilimali fedha na kusisitiza umuhimu wa uwazi na usawa kwenye mchakato wa ajira ili kuwezesha Watanzania kupata ajira kwenye umoja huo. 

Mkutano huo wa Mawaziri wa Mambo ya Nje utafuatiwa na Mkutano wa 4 wa Kamati ya Uratibu ya Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika utakaofanyika tarehe 17 Julai 2022. 

Kamati hiyo inaundwa na nchi za Senegal (Mwenyekiti); Libya (Makamu wa Pili wa Mwenyekiti); Angola (Makamu wa Tatu wa Mwenyekiti); Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (Katibu) na Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya za Kikanda za Umoja wa Afrika. 

Umoja wa Afrika una Jumuiya nane za kikanda ambazo ni Arab Maghreb Union (AMA), COMESA, Community of Sahel-Saharan States (CEN-SAD), EAC, ECCAS, IGAD na SADC.

Waziri Mulamula katika Mkutano huo ameambatana na Balozi wa Tanzania nchini Zambia Mhe. Hassan Simba Yahya, Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia na mwakilishi wa Kudumu katika Umoja wa Afrika Mhe. Innocent Shiyo, Mkurugenzi wa Idara ya Afrika Balozi Naimi Aziz, Mkurugenzi wa Sheria Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Balozi Caroline Chipeta na Maafisa wengine Waandamizi.
Mkutano wa 41 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika (AU) ukiendelea jijini Lusaka, Zambia.
Picha ya pamoja ya Mawaziri, Viongozi waandamizi wa Serikali, Taasisi mbalimbali za Kimataifa na Watendaji wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika kwenye Mkutano wa 41 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika (AU) unaoendelea jijini Lusaka, Zambia.
Mkutano wa 41 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika (AU) ukiendelea jijini Lusaka, Zambia.

SERIKALI YAIPONGEZA TAASISI YA MAENDELEO YA AGA KHAN KWA KUCHANGIA MAENDELEO NCHINI

  

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk ameipongeza Taasisi ya Maendeleo ya Aga Khan (AKDN) kwa mchango wake mkubwa katika kukuza na kuendeleza sekta za elimu, afya, miundombinu, utalii na utamaduni hapa nchini. 


Balozi Mbarouk ameyasema hayo wakati wa maadhimisho ya miaka 65 ya Uimamu wa Kiongozi wa Kiroho wa Madhehebu ya Shia Ismailia duniani, Mhe. Karim  Aga Khan. 


Balozi Mbarouk ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho hayo yaliyoandaliwa na Taasisi hiyo, amesema Taasisi hiyo ambayo kupitia miradi mbalimbali iliyopo Tanzania Bara na Zanzibar ikiwemo ya elimu na afya na ile ya kujikwamua kiuchumi imewasaidia watu wengi ambapo hadi sasa takriban watoto 10,000 nusu ya hao wakiwa wasichana wamefaidika kwa kupata elimu bora kupitia taasisi hiyo


"Kupitia uongozi mzuri wa Mheshimiwa Aga Khan, Taasisi ya AKDN imekuwa mstari wa mbele kuchangia katika sekta za elimu, afya, maendeleo ya uchumi na kuondoa umaskini kwa upande wa Tanzania Bara na Zanzibar. Hivyo ninayo furaha kuungana na jamii ya Ismailia ya hapa nchini na duniani kwa ujumla kusherehekea siku hii muhimu ya miaka 65 ya Mhe. Aga Khan kuwa Imam wa Madhehebu ya Shia Imailia” alisema Balozi Mbarouk. 


Kadhalika, Mhe. Balozi Mbarouk alisema anapongeza jitihada zinazoendelea kufanywa na AKDN katika kuboresha huduma za afya nchini ambapo kupitia jitihada hizo, mwezi Aprili 2022, Mkuu wa Kamati ya Maendeleo ya Jamii ya AKDN, Mhe. Zahra Aga Khan, Mkuu wa Kamati ya Jamii ya AKDN alitembelea Tanzania na kuweka jiwe la msingi kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Kituo cha Huduma za Saratani jijini Dar es Salaam cha kiwango cha kimataifa ambacho kitakuwa na uwezo wa kutoa huduma mbalimbali kuhusu ugonjwa wa saratani ikiwemo kinga, utambuzi wa mapema wa ugonjwa, matibabu na huduma  za nyumbani kwa wagonjwa 


 Kwa upande wake, Mwakilishi Mkazi wa Taasisi ya AKDN hapa nchini, Mhe. Balozi Amin Kurji amesema Taasisi yake itaendelea kushirikiana na Serikali katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia sekta mbalimbali zikiwemo za afya na elimu. Amesema, kupitia taasisi hiyo tayari miradi mbalimbali ikiwemo ya Vyuo Vikuu, Vyuo vya Afya vya wauguzi na wakunga vimeanzishwa nchini. 


Aidha,  ameishukuru na kuipongeza Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa maendeleo makubwa ya uchumi na jamii yaliyopatikana nchini katika kipindi kifupi tangu aingie madarakani na kwamba Taasisi ya AKDN itaendelea kushirikiana na Serikali ili kuunga mkono jitihada hizo. 


“Nampongeza Mhe. Rais Samia na Serikali yake kwa ujumla. Tumeshuhudia uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika kuboresha sekta za afya, elimu maji, umeme, miundombinu na sekta za uzalishaji. AKDN inaahidi kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuboresha maisha ya Watanzania” alisisitiza Balozi Kurji. 


Maadhimisho hayo ambayo yalifanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam yalihudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali akiwemo Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye, Mabalozi, Wabunge na Wageni wengine waalikwa.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akizungumza wakati wa maadhimisho ya miaka 65 ya Uimamu wa Kiongozi wa Kiroho wa Madhehebu ya Shia Ismailia duniani, Mheshimiwa Karim Aga Khan. Pamoja na mambo mengine Mhe. Balozi Mbarouk aliipongeza Taasisi ya Maendeleo ya Aga Khan (AKDN) kwa mchango wake katika kuboresha na kuendeleza sekta za elimu, afya na miundombinu. Maadhimisho hayo ambayo yalihudhuriwa na  viongozi mbalimbali wa Serikali yalifanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam
Mhe. Balozi Mbarouk akihutubia wageni waalkiwa wakati wa maadhimisho ya miaka 65 ya Imam Aga Khan

Mwakilishi Mkazi wa Taasisi ya AKDN nchini, Mhe. Balozi Amin Kurji naye akizungumza wakati wa maadhimisho hayo

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye akifuatilia maadhimisho ya miaka 65 ya Imam Aga Khan

Wageni waalikwa wakifuatilia maadhimisho ya miaka 65 ya Uimamu wa Aga Khan

Mhe. Naibu Waziri akipata maelezo kuhusu kazi mbalimbali za uchapishaji  vitabu unaofanywa na Taasisi ya AKDN

Mhe. Balozi Mbarouk akiwa katika picha ya pamoja

 

Wednesday, July 13, 2022

BALOZI MUSHY AKUTANA NA MEYA WA JIJI LA Linz

Balozi wa Tanzania nchini Austria, Mhe. Celestine Mushy (kushoto)  akutana na kufanya mazungumzo na Meya wa Jiji la Linz, Mhe. Mstahiki Klaus Luger. Balozi alimshukuru kwa mapemzi yake kwa Tanzania ambayo yaliwezesha Jiji la Dodoma kuwa na mahusiano na Jiji la Linz (Sister Cities).   Balozi alimuomba kuimarisha mahusiano hayo zaidi kwa kusainiana makubalino ya ushirikiano kati ya hospitali na vyuo vikuu vya Linz na Tanzania ili kuweza kubadilishana utaalamu, teknolojia, mafunzo, wanafunzi na wahadhiri. Aidha, Balozi alimuomba kuandaa mkutano wa wadau wote ili aweze kuongea nao. Mhe. Mstahiki Meya alikubali maombi hayo.

Balozi wa Tanzania nchini Austria, Mhe. Celestine Mushy na Meya wa Jiji la Linz, Mhe. Mstahiki Klaus Luger wakiwa katika picha ya pamoja na wasaidizi wao baada ya kufanya mazungumzo.



 

BALOZI MULAMULA AKUTANA NA RAIS WA CARE INTERNATIONAL

Shirika lisilo la kiserikali la Care International limetakiwa kupanua huduma zake katika mikoa mingi zaidi badala ya mikoa tisa tu ambayo shirika hilo kwa sasa linatoa huduma zake hapa nchini.

Wito huo umetolewa leo tarehe 13 Julai 2022 jijini Dar Es Salaam na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula, wakati wa mazungumzo yake na Rais na Mtendaji Mkuu wa Shirika hilo, Bi. Michelle Nunn

Bi. Nunn ametaja baadhi ya shughuli ambazo shirika lake inazifanya hapa nchini kuwa ni pamoja na utunzaji wa mazingira, afya, elimu, kuwawezesha wanawake kiuchumi, kilimo, haki za kijamii na usawa wa kijinisa. Amesema utekelezaji wa shughuli hizo umezingatia kipaumbele cha mwanamke.

“Tunasaidia watoto wa maeneo ya vijijini kupata elimu bora, tunasaidia jamii kutumia aridhi yao vizuri ili izalishe chakula, wakati huo huo ikitunzwa vizuri na programu zetu za kutoa mikopo na kuwasaidia wanawake wa vijijini kujiwekea akiba kwa kutumia teknolojia ya kisasa ya kidigitali zimewawezesha wanawake wengi kumiliki rasilimali na kunyanyuka kiuchumi”, Alisema Bi. Nunn.

Kwa upande wake, Balozi Mulamula alilishukuru shirika hilo kwa misaada inayotoa nchini na kueleza kuwa programu zao za misaada zinaenda sanjari na dira ya maendeleo ya Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan.

Aliendelea kueleza kuwa changamoto kwa wanawake ni nyingi zikiwemo za afya ya uzazi na ugonjwa wa malaria ambao bado unakatisha maisha ya watu wengi katika nchi za Afrika, hivyo alishauri umuhimu wa “Care International” kuangalia kwa jicho la pekee eneo hilo.

Aidha, Balozi Mulamula alilipongeza shirika hilo kwa kujikita katika utunzaji wa mazingira kwa kuwa tatizo hilo ni kubwa na watu wengi hawalioni, ingawa madhara ya uharibifu wa mazingira yanamfikia kila mmoja wetu.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (kulia) akiwa katika mazungumzo na Rais na Mtendaji Mkuu wa Care International, Bi. Michelle Nunn kuhusu huduma zinazotolewa na shirika hilo nchini Tanzania

Ujumbe ulioambatana na Rais na Mtendaji Mkuu wa Care International, Bi. Michelle Nunn ukifuatilia mazungumzo yake na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (kulia) akiwa katika mazungumzo na Rais na Mtendaji Mkuu wa Care International, Bi. Michelle Nunn huku maafisa walio chini yao wakifuatilia mazungumzo hayo.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (katikati) akifurahia jambo na Rais na Mtendaji Mkuu wa Care International, Bi. Michelle Nunn (kulia) na Mkurugenzi Mkazi wa Care International, Bi. Prudence Masako

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula na Rais na Mtendaji Mkuu wa Care International, Bi. Michelle Nunn wakiwa katika picha ya pamoja na watumishi walioambatana nao wakati walipofanya mazungumzo jijini Dar Es Salaam.