Wednesday, October 19, 2022

Come to invest in Tanzania, Dr. Bana tells Nigerian investors

Ambassador Dr. Benson Alfred Bana, High Commissioner of the United Republic of Tanzania to the Federal Republic of Nigeria was special guest at the 50th AGM of the Manufacturers Association of Nigeria in Lagos. Alhaji Aliko Dangote, GCON, President/CE Dangote Industries Ltd, delivered a lecture on *”Agenda Setting for Industrializing Nigeria the Next Decade.”* The High Commissioner seized the opportunity to invite captains of industries in Nigeria and West African countries to invest in Tanzania, illuminating opportunities and incentives provided by the Government of the United Republic of Tanzania and the Revolutionary Government of Zanzibar.

Tanzanian Ambassador to Nigeria, H.E Dr. Benson Bana (c) in attendance to the 50th AGM of the Manufacturers Association of Nigeria in Lagos held  on 18th October 2022.

Tanzanian Ambassador to Nigeria, H.E Dr. Benson Bana is in group photo with other dignitaries who attended the
50th AGM of the Manufacturers Association of Nigeria in Lagos held on 18th October 2022.


 

Tuesday, October 18, 2022

TANZANIA NA POLAND ZAKUBALIANA KUIMARISHA USHIRIKIANO

Serikali ya Tanzania na Poland zimekubaliana kuendelea kuimarisha ushirikiano kwenye sekta mbalimbali zenye manufaa kwa nchi hizi mbili ikiwemo kilimo, elimu,  nishati, utalii, biashara na uwekezaji.


Makubaliano hayo yamefikiwa leo tarehe 18 Oktoba 2022 jijini Warsaw,  Poland wakati wa mazungumzo rasmi  yaliyofanyika kati ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax na Waziri wa Mambo ya Nje wa Poland, Mhe. Zbigniew Rau.


Wakizungumza na waandishi wa habari mara baada ya mazungumzo hayo,  Mawaziri hao  wamesema Tanzania na Poland ambazo zinaadhimisha miaka 60 ya ushirikiano, zina fursa nyingi zenye manufaa kwa pande zote mbili na kwamba  wamekubaliana kuweka mikakati madhubuti ya utekelezaji wa makubaliano hayo ikiwa ni pamoja na kuanzisha ushirikiano kwenye maeneo mapya ya ulinzi na usalama pamoja na nishati.


Akizungumza,  Mhe. Dkt. Tax amesema Poland imeandelea kuwa mshirika muhimu wa kimkakati kwa Tanzania katika kipindi chote cha miaka 60 ya ushirikiano wa kidiplomasia, na kwamba wamekubaliana kuendelea kushirikiana kwenye sekta ambazo zimekuwa na tija kubwa kwenye ushirikiano huo ikiwemo kilimo, elimu, utalii, biashara na uwekezaji.

 

"Katika majadiliano yetu leo, tumetathmini ushirikiano wetu katika maeneo ambayo tayari tunashirikina na Poland kama kilimo, elimu, biashara na uwekezaji na utalii. Pia tumekubaliana kuongeza maeneo ya  ushirikiano katika masuala ya nishati na ulinzi na usalama ambayo ni muhimu katika kukuza ushirikiano wetu” amesema Dkt. Tax.

 

Kadhalika Mhe. Dkt. Tax ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji na wafanyabiashara kuja nchini kuwekeza kwani Tanzania bado inazo fursa nyingi za uwekezaji. Aidha, Mhe. Dkt. Tax ameipongeza Serikali ya Poland na Wananchi wake kwa kuendelea kuichagua Tanzania kama kituo chao muhimu cha utalii ambapo nchi hiyo ni miongoni mwa nchi tano  za juu zenye idadi kubwa ya  watalii waliotembelea nchini mwaka 2022.

 

“Ni imani yangu kuwa, baada ya ziara yangu hii biashara, uwekezaji, utalii na ushirikiano wa kisiasa kati ya Tanzania na Poland utaimarika zaidi. Pia kipekee nitumie fursa hii kuwashukuru wananchi wa Poland kwa upendo wao kwa Tanzania. Kwani kwa mwaka huu 2022, Poland ni miongoni mwa nchi tano zilizoshika nafasi ya juu kwa wananchi wake kutembelea nchini kwetu nawashukuru sana na karibuni tena, alisisitiza Dkt. Tax.

 

 Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Poland, Mhe. Zbigniew Rau amesema kuwa nchi yake inathamini ushirikiano wa kihistoria uliopo kati yake na Tanzania na kwamba maeneo muhimu yaliyojadiliwa na kukubaliwa wakati wa mkutano wao yatatekelezwa na Serikali ya nchi hiyo.

 

“Tanzania ni mshirika muhimu sana kwa Poland na miongoni mwa nchi zinazopewa kipaumbele katika program za muda mrefu za maendeleo ikiwemo uwekezaji kwenye sekta ya kilimo,” amesema Mhe. Rau.

 

Pia alitumia fursa hiyo kumshukuru Mhe. Dkt. Tax kwa kukubali mwaliko wake na kuitembelea Poland ambapo alisema hatua hiyo ni muhimu katika kukuza ushirikiano kati ya nchi mbili kwani utaharakisha utekelezaji wa makubalino mbalimbali ambayo tayari yapo na mapya.

 

“Tumekuwa na mazungumzo yenye tija na Mhe. Waziri Dkt. Tax. Kupitia mazungumzo hayo ushirikiano wetu utaimarika zaidi. Nitumie fursa hii kumshukuru Mhe. Waziri na ujumbe wake kwa kukubali mwaliko wangu na kututembelea”, amesema Mhe. Rau.

 

Wakati huohuo,  Mhe. Dkt. Tax ametembelea na kuweka shada la maua kwenye kaburi la askari mashujaa wa nchi hiyo lililopo jijini Warsaw.

 

Mhe. Dkt. Tax yupo nchini Poland kwa ziara ya kikazi ya siku tatu kuanzia tarehe 17 hadi 19 Oktoba, 2022, ambayo pamoja na mambo mengine inalenga kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia na kiuchumi baina ya nchi hizi mbili.

Katika ziara hiyo Mhe. Waziri Tax amefuatana na Wajumbe kutoka Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Wizara ya Mambo ya  Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC),  Mamlaka ya Ukuzaji  Biashara na Uwekezaji Zanzibar (ZIPA), Wakala wa Taifa wa Hifadi ya Chakula (NFRA), Benki Kuu ya Tanzania (BOT) na Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC).

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akipokelewa rasmi na Waziri wa Mambo ya Nje wa Poland, Mhe. Zbiniew Rau mara baada ya kuwasili katika Ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje za nchi hiyo tarehe 18 Oktoba 2022. Akiwa Wizarani hapo, Mhe. Waziri Dkt. Tax na Mhe. Rau walikutana kwa mazungumzo rasmi na kukubaliana kuimarisha ushirikiano katika sekta za kilimo, nishati, elimu, biashara na uwekezaji. Mhe. Dkt. Tax yupo nchini Poland kwa ziara ya kikazi ya siku tatu kuanzia tarehe 17 hadi 19 Oktoba 2022.

Mhe. Dkt. Tax akiwa katika picha ya pamoja namwenyeji wake Mhe. Rau mara baada ya kuwasili katika Ofisi za Mambo ya Nje zilizopo Warsaw nchini Poland

Mhe. Dkt. Tax na ujumbe wake akiwa kwenye mazungumzo rasmi na Mhe. Rau na ujumbe wake.
Sehemu ya ujumbe wa Tanzania ulioshiriki mazungumzo kati ya Mhe. Dkt. Tax na Mhe. Rau. Kulia ni balozi wa Tanzania nchini Ujerumani na Poalnd, Mhe. Abdallah Possi

Sehemu ya ujumbe wa Poland wakati wa mazungumzo hayo
Mhe. Waziri Dkt. Tax na mwenyeji wake, Mhe. Rau wakizungumza na waandishi wa habari kuhusu masuala mbali mbali ya ushirikiano waliyojadili na kukubaliana

Sehemu ya Ujumbe wa Tanzania akiwemo Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikisno wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme (Kushoto)

Mhe. Waziri akisindikizwa  na Naibu Mkuu wa Itifaki wa Poland, Bw. Artur Harazim kwenye kaburi la askari mashujaa wa Poland kwa ajili ya kuweka shada la maua kwa lengo la kuwaenzi na kuwakumbuka

Gwaride la heshima liloandaliwa rasmi kwa ajili ya Mhe. Dkt. Tax alipofika eneo hilo kwa ajili kuwakumbuka mashujaa wa Poland


Mhe. Dkt. Tax akisaini kitabu cha wageni alipowasili kwenye eneo hilo la makumbusho ya mashujaa

Mhe. Waziri Dkt. Tax akiwa na ujumbe wa Tanzania na Poland mara baada ya kukamilisha shughuli ya uwekaji shada la maua kuwakumbuka askari mashujaa wa Poland




 

MALKIA MAXIMA AWASILI DAR ES SALAAM KWA ZIARA YA KIKAZI

Malkia wa Uholanzi, Malkia Maxima amewasili Jijini Dar es Salaam akitokea mkoani Kilimanjaro ambapo alianzia ziara yake jana tarehe 17 Oktoba 2022 baada ya kuwasili nchini kwa ziara ya kikazi ya siku tatu kuanzia tarehe 17 – 19 Oktoba, 2022.

Mara baada ya Malkia Maxima kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam, alipokelewa na Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Robert Kahendaguza.

Malkia Maxima ambaye pia ni Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Mfumo Jumuishi wa Fedha katika Maendeleo anatarajia kukutana kwa mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan tarehe 19 Oktoba 2022.

Mbali na kukutana na Mhe. Rais Samia pia Malkia Maxima kabla ya kuhitimisha ziara yake hapa nchini, anatarajia pia kukutana na viongozi mbalimbali waandamizi wa Serikali.

Malkia wa Uholanzi, Malkia Maxima akipokelewa na Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Robert Kahendaguza baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam

Malkia wa Uholanzi, Malkia Maxima akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam. Pembeni yake mwenye suti ya kijivu ni Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Robert Kahendaguza

Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Robert Kahendaguza akiteta jambo na Malkia wa Uholanzi, Malkia Maxima baada ya Malkia kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam

Malkia wa Uholanzi, Malkia Maxima akimueleza jambo Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Robert Kahendaguza baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam



Monday, October 17, 2022

TANZANIA KUSHIRIKIANA NA WADAU MBALIMBALI KUBORESHA SEKTA YA MAJI NCHINI

Tanzania ipo tayari kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuboresha sekta ya maji na usafi wa mazingira nchini ili kuwawezesha wananchi wa mijini na vijijini kuondokana na changamoto ya ukosefu wa maji safi na salama. 

 

Hayo yamesemwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax leo tarehe 17 Oktoba 2022 alipotembelea Chuo Kikuu cha Sayansi za Maisha cha Warsaw nchini Poland katika siku yake ya kwanza ya ziara ya kikazi nchini humo.

 

Mhe. Dkt. Tax ambaye alikutana na Menejimenti ya Chuo hicho pamoja na wamiliki wa kampuni mbalimbali za Poland zenye nia ya kuwekeza katika sekta ya maji nchini, amesema, sekta ya maji na usafi wa mazingira ni miongoni mwa sekta za kipaumbele nchini, kwani zinagusa maisha ya wananchi wote wa mijini na vijijini na kwamba  wanahitajika wawekezaji makini na wenye tija kutoka ndani na nje ya nchi ili kuendelea kuiboresha.

 

Amesema miji mbalimbali nchini ikiwemo Dodoma na Dar es Salaam inaendelea kukua kwa kasi hivyo upo umuhimu wa kuwekeza zaidi kwenye sekta hiyo ili kuwawezesha wananchi kupata maji safi na salama lakini pia kuendelea kutunza mazingira.

 

“Maji na usafi wa mazingira ni miongoni mwa sekta za kipaumbele kwa   Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tutaendelea kushirikiana na nchi mbalimbali ili kuhakikisha sekta hii inaboreshwa zaidi hususan kwenye teknolojia ya kisasa ya usimamizi wa maji  ikiwa ni pamoja na kuwajengea uwezo wataalam wetu” alisema Dkt. Tax.

 

Pia amesema Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki itaendelea kushirikiana na  Taasisi mbalimbali zinazosimamia sekta ya maji nchini ikiwemo Wizara ya Maji ili kwa pamoja kuendelea kutafuta suluhu ya kudumu kwa changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta hiyo kwa kuwashirikisha wadau wa ndani na nje ya nchi.

 

Awali akimkaribisha Mhe. Waziri chuoni hapo, Mkuu wa Chuo, Prof. Michal Zasada amesema chuo hicho ambacho kimejikita katika ufundishaji wa Teknolojia mpya ya usimamizi wa maji na utunzaji wa mazingira, kipo tayari kushirikiana na Tanzania katika kutoa mafunzo ya kuwajengea uwezo wataalam wa sekta hiyo kutoka nchini.

 

“Tumefarijika kutembelewa na wewe Mhe. Waziri na ujumbe wako kutoka Tanzania. Chuo chetu kinatoa kozi mbalimbali za Shahada na Shahada ya Uzamili katika masuala mbalimbali ikiwemo sekta ya maji. Tayari wataalam kadhaa kutoka sekta ya maji wamewahi kupata mafunzo ya kuwajengea uwezo hapa chuoni. Tunaendelea kuwakaribisha Watanzania kujiunga na program mbalimbali za mafunzo hususan za sekta ya maji zinazotolewa chuoni hapa” alisema Prof.  Zasada.

 

Wakati wa Mkutano huo Kampuni mbalimbali zinazojishughulisha na sekta ya maji na usafi wa mazingira za Poland ikiwemo ile ya Asseco ziliwasilisha mada na kueleza utayari wao wa kuwekeza katika sekta ya maji kwa kuanza na miji ya Dodoma na Dar es Salaam.

 

Akiwa chuoni hapo Mhe. Dkt. Tax alipata fursa ya kutembelea maabara za kisasa za usimamizi wa maji pamoja na  kujionea mradi wa maji unaotumia teknolojia ya kisasa unaotekelezwa na chuo hicho.

 

Mhe. Dkt. Tax yupo nchini Poland kwa ziara ya kikazi ya siku tatu kuanzia tarehe 17 hadi 19 Oktoba, 2022, ambayo pamoja na mambo mengine inalenga kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia na kiuchumi baina ya nchi hizi mbili.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Stergomena Tax akisalimiana na Mkuu wa Chuo cha Sayansi za Maisha cha Warsaw nchini Poland, Prof. Michal Zasada mara baada ya kuwasili Chuoni hapo leo tarehe 17 Oktoba 2022. Pamoja na ambo mengine Mhe. Waziri Tax alizungumza na menejimenti ya chuo hicho kuhusu masuala mbalimbali ya ushirikiano katika sekta ya elimu na maji pamoja na kutembelea miradi ya maji inayotekeelzwa na chuo hicho. Mhe. Dkt. Tax yupo nchini poland kwa ziara ya kikazi ya siku tatu kuanzia tarehe 17 hadi 19 Oktoba 2022


Mhe Waziri Dkt. Tax akizungumza na Menejimenti ya Chuo Kikuu cha Sayansi za Maisha cha Warsaw cha nchini Poland kuhusu masuala ya ushirikiano katika sekta za elimu na maji. Kushoto kwake ni Prof. Zasada, Mkuu wa Chuo hicho akifuatiwa na Makamu Mkuu wa Chuo, Dkt. Marta Mendel na Balozi wa Poland nchini Tanzania, Mhe. Krystof Buzalski. Kushoto ni Balozi wa Tanzania nchini Ujerumani anayewakilisha pia nchini Poland, Mhe. Balozi Abdallah Possi
Mkuu wa Chuo cha Sayansi za Maisha cha Warsaw, Prof. Zasada akizungumza kumkaribisha Mhe. Dkt Tax alipotembelea Chuoni hapo

Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirkiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme (kulia) akiwa pamoja na Wajumbe kutoka Tanzania walioambata na Mhe. Waziri Tax nchini Poland.

Sehemu ya Wajumbe kutoka Chuo Kikuu cha Sayansi za Maisha cha Warsaw na wamiliki wa Kampuni zinazojishughulisha na masuala ya maji wakifuatilia kikao
 
Sehemu nyingine ya Wajumbe kutoka Tanzania
 
Sehemu ya washirki kutoka Chuoni hapo
Sehemu ya Washiriki kutoka Tanzania
 
Mkutano ukiendelea
 
Sehemu ya wajumbe kutoka Chuoni hapo
 
Sehemu nyingine ya washiriki
 
Mada kuhusu masuala ya maji na usafi wa mazingir aikiwasilishwa na mmoja wa washiriki kutoka Poland
 
Mhe. Dkt. Tax akimweleza Prof. Zasada kuhusu zawadi  kutoka Tanzania kabla ya kumkabidhi. Zawadi hiyo ni mkusanyiko wa bidhaa za Tanzania zikiwemo Kahawa, Korosho, batiki, Vikoi na Viungo vya chakula.
 
 
Prof. Zasada naye akimkabidhi zawadi Mhe. Waziri Dkt. Tax
Picha ya pamoja
Mhe. Dkt. Tax akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Kituo cha Maji kilicho chini ya Chuo Kikuu cha Sayansi za Maisha cha Warsaw, Prof. Wojciech Sas alipofika kukitembelea kituo hicho na kujionea maabara mbalimbali za maji

Mhe. Dkt Tax na ujumbe wake wakipata maelezo kutoka kwa mtaalam wa mitambo na teknolojia mbalimbali za maji Prof. Adam Kiszko


Mhe. Dkt. Tax akipata maelezo kutoka kwa mtaalam wa maabara ya maji alipotembelea maabara hiyo

Mhe. Dkt. Tax akiangalia bwawa lililochimbwa kitaalam bila kuharibu mazingira na viumbehai  alipotembelea Kituo cha Maji kilicho chini ya Chuo Kikuu cha Sayansi za maisha cha Warsaw, Poland




 

TANZANIA YATWAA TUZO KATIKA MAONESHO YA UTALII NCHINI KOREA KUSINI ’THE 23RD BUSAN INTERNATIONAL TRAVEL FAIR’

 


MAKAMPUNI YA JAPAN YAVUTIWA NA KAHAWA YA TANZANIA

Makampuni ya Japan yameonesha kuvutiwa na kahawa ya Tanzania katika maonesho ya Kimataifa ya Kahawa Japan yajulikanayo kama 2022 Japan Specialty Coffee Conference & Exhibition yaliyofanyika jijini Tokyo tarehe 12 – 14 Oktoba, 2022. 

Maonesho hayo ambayo yalishirikisha taasisi zipatazo 235 zinazoshughulika na kahawa kutoka kote duniani, yaliandaliwa na kusimamiwa na Taasisi ya Kahawa ya Japan (Specialty Coffee Association of Japan – SCAJ). 

Kutokana na mapokeo mazuri ya kahawa ya Tanzania miongoni watumiaji na makampuni ya Japan katika maonesho hayo, soko la kahawa ya Tanzania nchini humo linatarajiwa kuongezeka kutoka asilimia 32 ya sasa, ambayo ni sawa na wastani wa kilogramu 15,000,000 zinazounzwa nchini humo kwa mwaka. Kiwango hiki kimeelezwa kuifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi tatu duniani zinazouza kahawa kwa wingi nchini Japan.

Maonesho hayo imekuwa ni fursa adhimu katika kukuza wigo wa soko na kujihakikishia soko la kudumu la kahawa ya Tanzania nchini Japan, ikiwa ni miongoni mwa kahawa pendwa nchini humo iliyopewa jina maarufu la kibiashara “Tanzania Kilimanjaro Coffee”.Ujumbe wa Tanzania katika maonesho hayo uliongozwa na Bodi ya Kahawa Tanzania ikiwa imeambatana na wawakilishi wa vyama viwili vya ushirika na makampuni matatu ya Kitanzania yanayohusika na uzalishaji na uuzaji wa kahawa ikiwemo; Kagera Cooperative Union (KCU), Karagwe District Cooperative Union (KDCU), Kampuni ya Kaderes Peasants Development (KPD),Kampuni ya Acacia na Kampuni ya Touton Tanzania Ltd
Balozi wa Tanzania nchini Japan Mhe.Balozi Baraka Luvanda (wanne kulia) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Maafisa wa ubalozi na wadau wa zao la kahama kutoka Tanzania katika Maonesho ya Kimataifa ya Kahawa yaliyofanyika jijini Tokyo

Sehemu ya walaji wa kahawa wa nchini Japan wakionja bidhaa hiyo kutoka Tanzania kwenye Maonesho ya Kimataifa ya Kahawa yaliyofanyika jijini Tokyo hivi karibuni
Wadau wa kahawa wa nchini Japan wakifuatilia wasilisho (presentation) kuhusu kahawa inayozalishwa hapa nchini lililowasilishwa na wataalam wa Bodi ya Kahawa Tanzania 

Wadau wa kahawa wa nchini Japan wakifuatilia wasilisho (presentation) kuhusu kahawa inayozalishwa hapa nchini lililowasilishwa na wataalam wa Bodi ya Kahawa Tanzania