Tuesday, July 16, 2019

Wawekezaji kutoka Jamhuri ya Czech watua nchini kutafuta fursa za biashara na uwekezaji



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Wafanyabiashara na wawekezaji kutoka Jamhuri ya Czech watafuta fursa za biashara na uwekezaji nchini Tanzania

Ujumbe wa wafanyabiashara na wawekezaji kutoka Jamhuri ya Czech wamewasili nchini tarehe 13 Julai, 2019 kwa lengo la kukutana na kufanya mazungumzo na wadau mbalimbali nchini ili kujadili fursa za biashara na uwekezaji nchini katika sekta mbalimbali hususan afya, kilimo, miundombinu ya barabara na reli,nishati, madini,utalii na wa ujenzi wa viwanda vya madawa na vifaa tiba.

Ziara hiyo inatokana na juhudi za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kupitia Ubalozi wa Tanzania uliopo nchini Ujerumani ambao pia unawakilisha Tanzania katika Jamhuri ya Czech na wadau wengine muhimu katika kushawishi wafanyabiashara wakubwa kuja kuwekeza nchini katika sekta mbalimbali.

Ujumbe huo wa watu kumi na mbili (12) ukiwa nchini, pamoja na masuala mengine, unategemea kukutana na uongozi wa Wizara naTaasisi mbalimbali zikiwemo, Wizara ya Viwanda na Biashara, Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Wizara ya Nishati, Wizara ya Madini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Bohari Kuu ya Dawa na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam. 

Vilevile, ujumbe huo unategemea kushiriki katika Kongamano la Uwekezaji wa Viwanda vya Kutengeneza Madawa na Vifaa Tiba kwa ubia kati ya Serikali na Sekta Binafsi, lililoandaliwa na Bohari Kuu ya Dawa. Kongamano hilo limepangwa kufanyika tarehe 17 Julai, 2019 katika Ukumbi wa Mkutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.

Ziara ya ujumbe huo nchini ni chachu ya kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na Czech. Kadhalika, ziara ya ujumbe huo ni moja ya mikakati ya utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje inayojikita katika diplomasia ya uchumi na kuhamasisha uwekezaji katika sekta ya viwanda ili kutimiza azma ya Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda na uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.

Mhe. Dkt. Abdallah Saleh Possi, Balozi wa Tanzania nchini Ujerumani ambaye pia ni Balozi wa Tanzania asiye na makazi nchini Czech ameambatana na ujumbe huo wa wafanyabiashara na wawekezaji.

Ujumbe huo kutoka Jamhuri ya Czech unategemea kukamilisha ziara yao nchini tarehe 17 Julai, 2019.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma.

16 Julai 2019


Mhe. Dkt. Abdallah Saleh Possi, Balozi wa Tanzania nchini Ujerumani ambaye pia ni Balozi wa Tanzania asiye na makazi nchini Czech akiwa kwenye mkutano kati ya ujumbe wa wafanyabiashara na wawekezaji kutoka Jamhuri ya Czech na Kituo cha UwekezajiTanzania (TIC) uliofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 15 Julai 2019. Mhe. Balozi Possi ameambatana na ujumbe huo hapa nchini ambao una lengo la kutafuta fursa za biashara na uwekezaji kwenye sekta za afya, kilimo, nishati na madini na ujenzi wa viwanda vya madawa na vifaa tiba.
Sehemu ya Wafanyabiashara na Wawekezaji kutoka Jamhuri ya Czech ukufuatilia mada mbalimbali zilizowasilishwa kwao na Wataalam kutoka Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC)
Sehemu nyingine ya Wafanyabiashara na wawekezaji kutoka Jamhuri ya Czech 
Mkutano ukiendelea
Mhe. Balozi Possi (wa tatu kulia) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Viongozi wa TIC na wafanyabiashara na wawekezaji kutoka Jamhuri ya Czech.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.