Monday, June 22, 2020

BARAZA LA MAWAZIRI WA SADC KUKUTANA KWA DHARURA 23 JUNI 2020

Mkutano wa Dharura wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) utafanyika tarehe 23 Juni, 2020 kwa njia ya Mtandao (Video Conferencing) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikali, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Emmanuel Buhohela, mkutano huo utatanguliwa na kikao cha Kamati ya Kudumu ya Maafisa Waandamizi/ Makatibu Wakuu chini ya uenyekiti wa Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge, Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na kufuatiwa na Mkutano wa Baraza la Mawaziri.
Mkutano wa Baraza la Mawaziri utajadili utekelezaji wa maazimio ya Baraza la Mawaziri dhidi ya mapambano ya ugonjwa wa COVID 19, kupokea taarifa ya Mkutano wa Kamati ya Wataalamu ya SADC ya kusimamia utekelezaji wa Itifaki ya Afya ya SADC uliofanyika tarehe 05 Juni 2020 na upendeleo utakaotolewa na India kwa nchi za SADC zitakaponunua dawa, vifaa kinga na vifaa tiba kwa ajili ya COVID 19.
Mkutano pia utapitia na kujadili Mwongozo wa Kikanda wa Urazinishaji {harmonization) na uwezeshaji wa shughuli za usafirishaji ndani ya SADC pamoja na masuala ya uratibu, usimamizi na uangalizi wa usafirishaji kwa njia ya barabara katika vituo vya kuingilia, ukaguzi dhidi ya Virusi vya Corona vinavyotambuliwa na SADC na namna ya kuendeleza shughuli za biashara wakati huu wa janga la CORONA ili kunusuru uchumi na kupunguza umasikini ndani ya jumuiya.
Mkutano huo utakuwa chini ya Uenyekiti wa Prof. Palamagamba John Kabudi, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na utakutanisha Mawaziri wenye dhamana ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Fedha na Mipango, Viwanda na Biashara, Uchukuzi, Utalii na Afya kutoka nchi 16 wanachamawa SADC ambazo ni Angola, Afrika Kusini, Botswana, Comoro, DRC, Eswatini, Lesotho, Malawi, Mauritius, Msumbiji, Madagascar, Namibia, Visiwa vya Shelisheli, Zambia, Zimbabwe na Mwenyekiti Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.