Thursday, June 25, 2020

MKUTANO WA MAWAZIRI WA KAMATI YA SADC YA ASASI YA USHIRIKIANO WA SIASA, ULINZI NA USALAMA KWA NGAZI YA MAKATIBU WAKUU WAFANYIKA JIJINI DAR ES SALAAM


Mkutano wa Mawaziri wa Kamati ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ya Asasi ya Ushirikiano wa Siasa, Ulinzi na Usalama kwa ngazi ya Makatibu Wakuu/ Maafisa Waandamizi umefanyika Jijini Dar es Salaam kwa njia ya Mtandao (Video Conferencing).

Mhimili wa Asasi ya Ushirikiano wa Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC unaongozwa na mfumo wa Utatu (Troika) ambapo kwa sasa Mwenyekiti ni Zimbabwe, mkutano wa ngazi ya Makatibu Wakuu unaofanyika leo ni maandalizi ya mkutano wa Mawaziri utakaofanyika tarehe 26 Juni 2020 chini ya Uenyekiti wa Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara ya Kimataifa wa Jamhuri ya Zimbabwe, Mhe. Sibusiso Busi Moyo na utakutanisha Mawaziri wenye dhamana ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mambo ya Ndani, Ulinzi na Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama kutoka nchi wanachama wa SADC.

Pamoja na mambo mengine mkutano umepokea na kujadili agenda zinazohusu masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama katika Ukanda wa SADC.
Mkutano wa leo umehudhuriwa na nchi wanachama wa SADC ambazo ni Angola, Afrika Kusini, Botswana, DRC,  Eswatini, Lesotho, Malawi, Mauritius, Msumbiji, Madagascar, Namibia, Zambia, Zimbabwe na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


Asasi ya Ushirikiano wa Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC ni moja ya mihimili ya SADC inayosimamia masuala ya Usirikiano wa Siasa, Ulinzi na Usalama katika Kanda. Mhimili huu unatekeleza majukumu yake kwa kuzingatia Mkataba wa uanzishwaji wa SADC wa mwaka 1992 na Itifaki ya Asasi ya Ushirikiano wa Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC ya mwaka 2001.


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge (katikati), kushoto kwake ni Katibu  Mkuu Wizara ya Ulinzi, Dkt. Faraji Mnyepe , mwisho kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Christopher Kadio wakifuatilia mkutano  huo kwa njia ya video conference, Jijini Dar es salaam




Wakuu wa vyombo vya Ulinzi na Usalama pamoja na baadhi ya Maafisa waandamizi kutoka Tanzania wakifuatilia mkutano huo kwa njia ya Video Conference, jijini Dar es Salaam

                                  Mkutano ukiendelea

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.