Friday, June 26, 2020

IMF YAAHIDI KUIPATIA TANZANIA FEDHA ITAKAYOIHITAJI


Shirika la Fedha Duniani (IMF) limeahidi kuipatia Tanzania fedha itakayoihitaji ili iweze kuendelea kukabiliana na athari zitokanazo na janga la Covid 19 kwa ajili ya kuimarisha uchumi wake.

Mkurugenzi Mkazi wa IMF nchini Tanzania Bw. Jens Reinke ameyasema hayo wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi leo katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam.

Pia Bw. Reinke ameipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua madhubuti inazozichukua katika kukabiliana na janga la Covid 19 ili kuepusha madhara ya kiuchumi na kijamii.

Mazungumzo hayo pia yamelenga miradi ya maendeleo, msamaha wa madeni kwa nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania, ushirikiano baina ya IFM na Tanzania, biasara na utalii. 
  
Kwa upande wake, Prof. Kabudi ameishukuru (IMF) kwa msamaha wa madeni ambao umetolewa kwa Tanzania na nchi nyingine, fedha zitakazoziwezesha nchi hizo kuendelea kukabiliana na Covid 19.

"Tumeongelea mambo mbalimbali yanayohusu ushirikiano hasa katika kuimarisha uchumi wetu baada ya janga la covid 19, usirikiano kati ya Tanzania na IMF unafahamika na tumekubaliana baadhi ya mambo ambayo tutayafanyia kazi kwa kina ili tuweze kuimarisha uchumi wetu baada ya corona hasa katika sekta ya utalii, biashara na miundombinu," amesema Prof. Kabudi.

Katika hatua nyingine, Waziri Kabudi amekutana na kumuaga Balozi wa Vietnam nchini, Mhe. Nguyen Kim Doanh ambaye amemaliza muda wake wa utumishi na amemtakia maisha mema na kumsihi kuendelea kuwa balozi mwema kwa Tanzania nchini Vietnam na duniani kwa ujumla.

"Kwa niaba ya Serikali napenda kukuhakikishia kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na Vietnam katika nyanja mbalimbali za kimataifa ikiwemo kuiunga mkono Vietnum katika kugombea nafasi mbalimbali katika Masirika ya KImataifa," Amesema Prof. Kabudi.

Nae Balozi Doanh ameishukuru Tanzania kwa ushirikiano ambao imekuwa ikimpatia alipokuwa akitekeleza majukumu yake nchini wakati wote na kuahidi kuwa ushirikiano kati ya nchi hizo mbili utaendelea kuimarishwa.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Kabudi akisalimiana na Mkurugenzi Mkazi wa IMF nchini Tanzania Bw. Jens Reinke 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi akimuelezea jambo Mkurugenzi Mkazi wa IMF nchini Tanzania Bw. Jens Reinke leo katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam 


Mkurugenzi Mkazi wa IMF nchini Tanzania Bw. Jens Reinke akiongea na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi leo katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam



Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi akiongea na Balozi wa Vietnam  nchini, Mhe. Nguyen Kim Doanh ambaye amemaliza muda wake wa utumishi nchini Tanzania 


Balozi wa Vietnam nchini, Mhe. Nguyen Kim Doanh akipokea zawadi kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Kabudi  


Balozi wa Vietnam nchini, Mhe. Nguyen Kim Doanh akimkabidhi zawadi Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Kabudi  



No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.