Thursday, January 5, 2017

Waziri wa Mambo ya Nje wa China kufanya ziara nchini

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,  Bi. Mindi Kasiga akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari kuhusu  ziara ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Watu wa China atakayoifanya hapa nchini tarehe 09 Januari, 2017.Mkutano huo umefanyika katika Ukumbi wa  Mikutano wa Kimataifa wa JNICC Jijini Dar es Salaam leo.
Sehemu ya Waandishi wa Habari wakifuatilia kwa makini wakati Bi. Mindi Kasiga (hayupo pichani) akiendelea kuzungumza nao.
Sehemu nyingine ya Waandishi wa Habari wakifuatilia mkutano.
Mkutano na Waandishi wa Habari ukiendelea.



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI 
Ziara ya Waziri wa Mambo ya Nje wa China nchini
Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. WANG Yi anatarajiwa kufanya ziara ya kikazi nchini tarehe 09 Januari 2017. Mhe. Waziri Wang Yi atapokelewa na mwenyeji wake Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga.
  
Madhumuni ya  ziara hiyo ni kukuza mahusiano mazuri na ya kihistoria baina ya China na Tanzania ambayo yamedumu kwa zaidi ya miaka hamsini tangu kuanzishwa kwake pamoja ‎na kuangalia maeneo mapya ya ushirikiano wa kiuchumi baina ya Tanzania na China.
Wakati wa ziara hiyo Mhe. Wang Yi atakutana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa lengo la kumsalimia. 
Aidha, Mhe. Wang Yi atafanya mazungumzo rasmi na Mhe. Dkt. Mahiga kuhusu masuala mbalimbali ya ushirikiano baina ya Tanzania na China na ushirikiano wa kimataifa.
Itakumbukwa kwamba mwezi Desemba 2015 kwenye Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika na China, China iliichagua Tanzania kuwa miongoni mwa nchi nne Barani Afrika zitakazowezeshwa kupiga hatua kwenye maendeleo ya viwanda. Kupitia mpango huo inatarajiwa viwanda takriban 200 vitajengwa au kuwekezwa nchini kutoka China kabla ya mwaka 2020.
Mpango huu unaenda sambamba na Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa mwaka 2016/2020 na pia ahadi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ya kujenga Tanzania ya viwanda. Ni matarajio yetu ni kuwa, Watanzania takriban laki mbili watanufaika na ajira kupitia mpango huu mahsusi wa kuendeleza viwanda.
Mbali na mpango wa uendelezaji wa viwanda, viongozi hawa wawili watazungumzia miradi mingine ya miundombinu ambapo China imeahidi kuisadia Tanzania ikiwa ni pamoja na maboresho makubwa ya Reli ya TAZARA; Ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo pamoja na ujenzi wa Reli ya Kati.
Aidha, Mhe. Wang anatarajiwa kuzungumza na Mwenyeji wake kuhusu masuala ya ushirikiano wa kimataifa ikiwa ni pamoja na mageuzi ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ambapo China inaunga mkono msimamo wa Afrika na wa Tanzania wa kutaka Afrika ipewe viti viwili vya kudumu kwenye Baraza hilo na kura ya turufu. 
Vilevile viongozi hao watazungumzia masuala ya amani na usalama katika eneo la Afrika Mashariki pamoja na eneo la Bahari ya Kusini mwa China.
Mazungumzo hayo yatafuatiwa na Mkutano wa Mawaziri na Vyombo vya Habari (Joint Press Conference) ambapo wataeleza makubaliano waliyofikia kwenye mazungumzo yao.
-Mwisho-
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dar es Salaam
05 Januari, 2017



No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.