Friday, June 9, 2017

Siku ya Kongamano la Biashara ya Kilimo na Uwekezaji kati ya Tanzania na Uholanzi yafana



 TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Siku ya Kongamano la Biashara ya Kilimo na Uwekezaji kati ya Tanzania na Uholanzi yafana

Katika kutekeleza Sera ya Diplomasia ya Uchumi, Ubalozi wa Tanzania kwa kushirikiana na Ubalozi wa Uholanzi uliopo Tanzania, Wizara ya Masuala ya Uchumi na Wizara ya Mambo ya Nje za Uholanzi na Taasisi ya Netherlands–African Business Council (NABC)kwa pamoja ziliandaa Kongamano la Biashara na Uwekezaji lililofanyika hapa The Hague, Uholanzi tarehe 31 Mei 2017. Lengo kuu la Kongamamo hilo, pamoja na kuendeleza na kukuza uhusiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na Uholanzi, nikutangaza fursa mbalimbali za biashara na uwekezaji zilizopo nchini Tanzania hususan katika Sekta za Kilimo, Ufugaji, Uvuvi na Miundombinu ya Kilimo. Aidha, Kongamano hilo lililohudhuriwa na Wawakilishi wa Makampuni takriban mia moja (100) ni mwendelezo wa utekelezaji wa makubaliano yaliyofikiwa kwenye Mkataba kati ya Tanzania na Uholanzi kuhusu Uingizwaji wa Mbegu za Viazi kutoka Uholanzi uliosainiwa kwenye ziara ya Mhe. Martijn Van Dam, Waziri wa Kilimo wa Uholanzi nchini Tanzania tarehe 16 Juni 2016. Aidha, Kongamano hii lilitanguliwa na ziara ya ujumbe kutembelea maeneo mbalimbali ikiwemo mashamba yanayomilikiwa na wakulima na wafugaji binafsi nchini Tanzania pamoja na kupata fursa za kusikiliza mada mbalimbali zilizotolewa na wakulima/wafugaji na wakufunzi wa Chuo Kikuu cha Wageningen kinachohusika na kufanya tafiti za Kilimo na Ufugaji.
Ujumbe kutoka Tanzania uliongozwa na Mhe.Eng. Mathew Mtigumwe, Katibu Mkuu anayeshughulikia Kilimo kutoka Wizara ya Kilimo, Ufugaji na Uvuvi, akimwakilisha Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi.
Wajumbe wengine ni:
ü  Mhe. Yohana Budeba, Katibu Mkuu anayeshughulikia Uvuvi, Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi,
ü  Mhe. Irene F.M. Kasyanju, Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi,
ü  Bw. Twahir Nzallawahe, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Mazao, Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi,
ü  Bibi Anuciata Njombe, Mkurugenzi wa Uzalishaji wa Mifugo na Masoko, Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi,
ü  Bw. Geoffrey Kirenga, Mtendaji Mkuu wa Kituo cha kuendeleleza Kilimo Ukanda wa Kusini (SAGCOT),
ü  Bibi Jennifer Baarn, Naibu Mtendaji Mkuuwa Kituo cha kuendeleleza Kilimo Ukanda wa Kusini (SAGCOT),
ü  Professa Andrew Temu, Mkurugenzi wa Diligent Consulting Ltd na Mwanachama wa Bodi ya SAGCOT,
ü  Bibi Jacqueline Mkindi, Mtendaji Mkuu wa Tanzania Horticulture Association (TAHA),
ü  Bw. Hussein Sufiani Ally, Mkurugenzi wa AZAM Bakhresa Group,
ü  Bibi Mona Mahecha, Afisa Mambo ya Nje Mwandamizi, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
ü  Maafisa wa Ubalozi wa Tanzania Uholanzi Bw. Matiku Kimenya (MC), Bibi Naomi Z. Mpemba (CO) na Bibi Agnes K. Tengia (FS).
Kwa upande wa Serikali ya Uholanzi, ujumbe uliongozwa na Mhe. Bibi Marjolijn Sonnema, Katibu Mkuu anayeshughulikia masuala ya Kilimo, Wizara ya Masuala ya Uchumi ya Uholanzi ambaye pia anakaimu kama Naibu Waziri wa Kilimo. Wengine ni;
ü  Mhe. Jaap Fredericks, Balozi wa Uholanzi nchini Tanzania,
ü  Bw. Bert Rikken, Afisa anayeshughulikia Masuala ya Kilimo, Ubalozi wa Uholanzi nchini Tanzania/Kenya,
ü  Bibi Ingrid Korving, Afisa Sera Mwandamizi, Wizara ya Masuala ya Uchumi ya Uholanzi,
ü  Bibi Hennie Wellen, Mratibu Wageni wa Kimataifa, Wizara ya Masuala ya Uchumi ya Uholanzi,
ü  Bibi Theresia Mcha, Afisa Kilimo, Ubalozi wa Uholanzi nchini Tanzania.
Katika Kongamano hili, Viongozi wa Ujumbe wa Serikali ya Tanzania na Uholanzi walionesha dhamira ya kuendelea kushirikiana kwa pamoja kwa kusaini Barua (Letter of Intent) ya kuanzishwa kwa Kituo cha Kuendeleza Zao la Viazi nchini Tanzania (Centre for Development of the Potato Industry in Tanzania- CD PIT). Aidha, Makampuni takriban kumi (10) yanayojishughulisha na kilimo cha viazi, yalionesha utayari wa kuwa wanachama kwa kushirikiana na Serikali za nchi hizi mbili katika uanzishwaji wa Kituo hicho. Tukio hilo lilikamilishwa kwa Wawakilishi wa Makampuni hayo kuweka saini kwenye Kadi/Bango kuonesha utayari wao.
Kituo cha CD PIT kinatarajiwa kuanzishwa Mkoani Mbeya ambapo pamoja na kukuza maendeleo ya sekta binafsi na kutoa ajira, kitatoa mafunzo ya kujenga uwezo hususan katika uzalishaji na utafutaji masoko, kitaendesha tafiti mbalimbali za kilimo ikiwemo pia kukuza uhusiano wa kibiashara kati ya  Tanzania na Uholanzi. 
Ubalozi kwa upande wake umeridhishwa na mwitikio mkubwa uliooneshwa na wadau mbalimbali waliojitokeza kushiriki katika Kongamano hilo. Hii inadhihirisha kuzidi kuimarika kwa mahusiano mazuri yaliyopo kati ya nchi hizi mbili.
Pamoja na kubadilishana uzoefu, kujifunza na kufahamiana, Kongamano hilo liliwezesha wadau kupata fursa ya kujadili pia changamoto wanazokabiliana nazo katika shughuli mbalimbali za biashara na uwekezaji wanazoziendesha nchini Tanzania.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
The Hague, Uholanzi, 09 Juni 2017
Mhe. Mathew Mtigumwe, Katibu Mkuu wa Wizara Kilimo, Mifugo na Uvuvi akisoma hotuba.
Mhe. Irene Kasyanju, Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi akisoma hotuba ya ufunguzi.

Mhe. Marjolijn Sonnema, Katibu Mkuu na Kaimu Naibu Waziri wa Kilimo wa Uholanzi  akisoma hotuba
Picha ya Pamoja ya Waheshimiwa Mabalozi wa Tanzania na Uhoalnzi na Makatibu Wakuu wa Kilimo na Uvuvi na Mkurugenzi wa TAHA.

Uwekaji saini wa makubaliano (letter of intent) ya kuanzishwa kwa kituo cha kuendeleza zao la viazi Tanzania


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.