Sunday, October 13, 2019

Mkutano wa Baraza la Kisekta la Mawaziri wanaoshughulikia masuala ya Afrika Mashariki wamalizika Jijini Arusha.

12 Oktoba 2019, Arusha.
Mkutano wa 30 wa Baraza la kisekta la Mawaziri wanaoshughulikia masuala ya Afrika Mashariki na Mipango umemalizika tarehe 12 Oktoba 2019 kwenye Makao Makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jijini Arusha - Tanzania. Mkutano huu wa siku sita (06) umefanyika katika Ngazi zifuatazo:
  1. Mkutano katika Ngazi ya Maafisa Waandamizi tarehe 7 na 8 Oktoba, 2019;
  2. Mkutano katika Ngazi ya Makatibu Wakuu tarehe 9 na 10 Oktoba 2019 na
  3. Mkutano katika Ngazi ya Mawaziri tarehe 11 na 12 Oktoba 2019.
Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huu umeongozwa na Naibu Waziri wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Damas D. Ndumbaro (Mb) akisaidiana na Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Innocent L. Bashungwa (Mb); Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Balozi Dkt. Augustine P. Mahiga (Mb); Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaju (Mb); Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mary Mwanjelwa pamoja na viongozi wengine waandamizi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano  Tanzania.

Mkutano huu umetoa maamuzi na maelekezo mbalimbali ya kisera na kimkakati kwa Nchi Wanachama pamoja na Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kuhusu Utekelezaji wa maamuzi na maelekezo ya mikutano ya Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyopita pamoja na mkutano wa 10 hadi 28 wa Baraza la kisekta la Mawaziri wanaoshughulikia masuala ya Afrika Mashariki na Mipango; Utekelezaji wa Soko la pamoja la Afrika Mashariki; Utekeleaji wa maagizo katika taarifa ya mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (2000 – 2017); Vipaumbele vya Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa mwaka 2020/21; Maelekezo kuhusiana na mikutano ya Wakuu wa taasisi za masuala ya Uhamiaji na Kazi za Jumuiya, na maagizo ya hadidu za rejea za maandalizi ya mkakati wa mpango wa sita wa maendeleo ya Afrika Mashariki (2021/22).

Aidha, mkutano huu ulitoa mapendekezo katika taarifa ya hali ya ulipaji wa michango ya Nchi Wanachama katika Jumuiya; Taarifa ya uhamasishaji katika masuala ya rasilimali za jumuiya ya Afrika Mashariki na mikakati ya ushirikiano; Taarifa ya Tume ya Ukaguzi ya Jumuiya kwa mwaka 2017/18; Taarifa ya maendeleo ya makubaliano ya maeneo huru ya biashara katika utatu wa COMESA-EAC-SADC;Taarifa ya maendeleo ya makubaliano kuhusu eneo huru la kibiashara barani Afrika (AFCFTA); Taarifa ya maendeleo ya masuala ya kisiasa, na Kalenda ya majukumu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa kipindi cha mwezi Julai hadi Desemba 2019.

Vilevile, wajumbe wa mkutano wamejadili kuhusiana na maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwa jumuiya ya Afrika Mashariki mwaka 2000, baada ya kuvunjika kwa jumuiya ya awali iliyoundwa mwaka 1967 na kuvunjika mwaka 1977.

Mkutano wa Baraza la Kisekta la Mawaziri wanaoshughulikia masuala ya Afrika Mashariki umemalizika tarehe 12 Oktoba 2019 Jijini Arusha, Tanzania.
Pichani ni viongozi wa ujumbe kutoka Nchi Wanachama katika ngazi ya Mawaziri wakisaini maamuzi na mapendekezo waliyoyatoa katika mkutano wa 30 wa Baraza la Kisekta la Mawaziri wanaoshughulikia masuala ya Afrika Mashariki na Mipango.
Kutoka kulia ni Naibu Waziri Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Damas D. Ndumbaro (Mb); Waziri anayeshughulikia masuala ya Jumuiya ya Afrika Mshariki, Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa kutoka Rwanda, Mhe. Balozi Olivier J.P Nduhungiuhe; Katibu Mkuu Wizara ya Afrika Mashariki na Maendeleo ya Kikanda kutoka Kenya, Mhe. Ken M. Obura; Waziri Ofisi ya Rais anayeshughulikia masuala ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kutoka Burundi, Mhe. Isabelle Ndahayo; Waziri wa Masuala ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kutoka Uganda, Mhe. Rt. Dkt. Kirunda Kivejinja; pamoja na Waziri wa Biashara, Viwanda na masuala ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kutoka Sudan Kusini, Mhe. Paul Mayom Akec kutoka.

Mawaziri wa Serikali ya Tanzania walioshiriki katika mkutano wa 30 wa Baraza la Kisekta la Mawaziri wanaoshughulikia masuala ya Afrika Mashariki na Mipango wakiwa katika kikao cha ndani cha maandalizi pamoja na maafisa wengine waandamizi kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (hawapo pichani).

Pichani; Kutoka kushoto ni Naibu Waziri Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Damas D. Ndumbaro, Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Innocent L. Bashungwa (Mb); Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Balozi Dkt. Augustine P. Mahiga (Mb); Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mary Mwanjelwa na Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaju (Mb). 

Mkurugenzi wa Idara ya Siasa, Ulinzi na Usalama wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Stephen P. Mbundi akijadili jambo pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya MiundombinuMhandisi Steven D. M. Mlote (kulia) na Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki anayeshughulikia sekta za uzalishaji na jamii, Mhe. Christophe Bazivamo (kushoto). 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.