Wednesday, October 23, 2019

MAADHIMISHO YA SIKU YA UMOJA WA MATAIFA KUFANYIKA KESHO, DODOMA

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe akizungumza na wanahabari  (hawapo pichani) kwenye ukumbi wa mikutano wa Wizara, jijini Dodoma.

Katika mkutano huo Dkt. Mnyepe amewajulisha waandishi wa habari kuhusu kufanyika kwa maadhimisho ya siku ya Umoja wa Mataifa tarehe 24 Oktoba, 2019
jijini Dodoma kwenye uwanja wa Nyerere square.  

Dkt. Mnyepe amebainisha kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Prof. Palamagamba John Kabudi anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika sherehe za maadhimisho hayo, yatakayofanyika kuanzia saa 2.30 asubuhi hadi 5.00 asubuhi.

Maadhimisho ya mwaka huu yataongozwa na kauli mbiu isemayo "Wanawake na Wasichana kuwa Kipaumbele katika kufikia Malengo ya Dunia. Kauli mbiu hii inalenga kusisitiza uwajibikaji na ushirikishwaji wa Wanawake katika kufikia malengo ya dunia.

Aidha, Katibu Mkuu Dkt. Mnyepe amebainisha kuwa Tanzania itaendelea kuwa mstari wa mbele katika kuheshimu na kusimamia misingi ya kulinda na kutetea maslahi ya Wanawake na Wasichana ikiwemo kuwashirikisha katika mipango ya maendeleo ya kijamii na uchumi.

Maadhimisho ya Siku ya Umoja wa Mataifa hufanyika kila mwaka tarehe 24 Oktoba. Maadhimisho ya mwaka huu ambayo yatapambwa na shamrashamra kutoka vikundi mbalimbali vya sanaa, yanatarajiwa kuhudhuriwa na Viongozi na Watendaji Wakuu wa Serikali, Wawakilishi kutoka ofisi za Umoja wa Mataifa nchini, vijana, asasi za kiraia na wadau wengine mbalimbali.
Bw. Michael Dunford Kaimu Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini, akizungumza na waandishi wa habari kwenye mkutano uliofanyika ofisi za Wizara ya Mambo Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki jijini Dodoma.   
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe (katikati) Bw. Deusdedit Kaganda Kaimu Mkurugenzi wa Uhusiano wa Kimataifa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, na Bw. Michael Dunford Kaimu Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini wakisikiliza maswali kutoka kwa Wanahabari (hawapo pichani).
Picha ya pamoja baada ya mkutano na waandishi wa habari

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.