Friday, January 17, 2020

KAMPUNI YA ALRIFAI YA KUWAIT YATEMBELEA TANZANIA, KUANGALIA FURSA ZA UWEKEZAJI


Na Mwandishi wetu,

Kampuni ya Alrifai inayojihusisha na biashara ya mazao mchanganyiko iko nchini kwa lengo la kuangalia fursa za uwekezaji hususani kununua zao la korosho na kahawa na kuangalia uwezekano wa kujenga kiwanda cha kuchakata zao la korosho nchini.

Ujumbe wa watu watatu (3) ukiongozwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni hiyo ya Alrifai, Bwn. Abdellah Foaud, Meneja Viwango Bwn. Ahmed Mohamed Bahie pamoja na Meneja wa Manunuzi Bwn. M. K Hussin uko nchini tangu tarehe 13 Januari, 2020 kwa lengo kuu la kuangalia uwezekano wa Kununua korosho zilizokwisha chakatwa pamoja na kahawa zilizokobolewa na pia kuona maeneo ambayo wanaweza kuwekeza katika kiwanda cha kuchakata korosho.

Ujumbe huo ulifanya kikako na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Bodi ya Kahawa (TCB), Mamlaka ya Maendeieo ya Biashara Tanzania (TanTrade) pamoja na Bodi ya Mazao Mchanganyiko na kuweza kupata fursa ya kufahamu kwa undani juu ya taratibu za ununuzi wa mazao hayo pamoja na taratibu za uwekezaji wa kiwanda cha kuchakata korosho hapa nchini.

Akitoa maelezo juu ya uzalishwaji wa zao la Korosho nchini, Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Biashara wa TanTrade, Bi. Twilumba Mlelwa alisema kuwa korosho ghafi kwa mwaka huzalishwa kati ya tani 250,000 na tani 300,000 ambapo kiasi kikubwa huzalishwa Mtwara, Lindi, Ruvuma (Tunduru), Pwani (Mkuranga na Kibaha) pamoja na Tanga.

"Naomba niwatoe shaka juu ya zao la korosho kwani kwa sasa viwanda vya korosho ni 18 ambapo vinauwezo wa huhifadhi tani 63,000 za korosho lakini kwa sasa vinavyofanya kazi ni 13 na vina uwezo wa kubangua tani 43,000" Amesema Bi. Mlelwa

Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni hiyo ya Alrifai, Bwn. Abdellah Foaud,ameushukuru Ubalozi wa Tanzania nchini Kuwait kwa ushirikiano alioupata kutoka ubalozini hadi kwa viongozi wa Wizara ya Mambo ya Nje kwa kuweza kuratibu zoezi la kukuagua zao la Korosho, kahawa pamoja na karafuu.

"Binafsi nashukuru kwa ushirikiano nilioupata kwa viongozi wa Mkoa wa Lindi na Mtwara, Bodi ya Mazao Mchanganyiko, TIC, TanTrade, Bodi ya Kahawa pamoja na Balozi Mhandisi Aisha Amour kwa namna alivyolisimamia jambo hili tangu likiwa wazo mpaka sasa tunapoelekea kwenye utekelezaji niwaahidi tu kuwa utekelezaji wa kununua mazao haya utaanza mara moja mara tu baada ya kufanya maamuzi na mikataba itasainiwa kwa mujibu wa sheria," amesema Bwn. Foaud

Aidha, mbali na maelezo ya uzalishaji wa zao la Korosho nchini, ujumbe huo pia ulipata fursa ya kuona zao la korosho lililohifadhiwa katika ghala la Serikali eneo la Kurasini jijini Dar es Salaam na uliridhishwa na zao hilo na kuahidi kuwekeza nchini kwani korosho zinzazalishwa ni nzuri na bora.

Meneja Viwango Bwn. Ahmed Mohamed Bahie amesema "tumejionea wenyewe ubora wa korosho, kahawa na karafuu kwa kweli ni nzuri sana na sote tumeridhika na ubora huo. Tutajitahidi kukamilisha taratibu zote muhimu na kuanza mara moja uagizaji wa korosho na baadae kujenga kiwanda cha kuchakata korosho hapa Tanzania,".  

Ujumbe huo ulipata fursa ya kutembelea maeneo kadhaa kwa lengo la kupata maelezo kuhusu taratibu na fursa za uwekezaji zinazopatikana nchini, maeneo hayo ni pamoja na mikoa ya Lindi, Mtwara na Kilimanjaro pamoja na Zanzibar ambapo waliweza kuona uzalishaji wa Karafuu.

Ujio wa kampuni hiyo ni matokeo ya juhudi za Ubalozi wa Tanzania nchini Kuwait ambapo ulifanya mazungumzo na Kampuni ya Alrifai inayojihusisha na biashara ya mazao mchanganyiko kuhusu nia yao ya kununua zao la korosho na kahawa na kuangalia uwezekano wa kujenga kiwanda cha kuchakata zao la korosho nchini Tanzania.
Kaimu Mkurugenzi wa Bodi ya kahawa nchini(TCB),Primus Kimaryo akiwaelezea jambo viongozi wa Kampuni Alrifai juu ya upatikanaji wa zao la kahawa nchini

Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Alrifai, Bwn. Abdellah Foaud, akiongea na viongozi kutoka TIC, TCB, TanTrade pamoja na Bodi ya Mazao Mchanganyiko wakati walipokutana katika mkutano uliofanyika Jijini Dar es Salaam

Add caption

Meneja Viwango Bwn. Ahmed Mohamed Bahie akikagua korosho zinazozalishwa hapa nchini, kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mazao Mchanganyiko, Dkt. Anselm Moshi na kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Biashara TanTrade, Bi. Twilumba Mlelwa



Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Alrifai, Bwn. Abdellah Foaud pamoja na Meneja wa Manunuzi Bwn. Hussain wakikagua korosho zilizohifadhiwa kwenye moja ya ghala hapa nchini, kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mazao Mchanganyiko, Dkt. Anselm Moshi

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mazao Mchanganyiko, Dkt. Anselm Moshi akimuonyesha Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Alrifai, Bwn. Abdellah Foaud jinsi korosho zinavyohifadhiwa


 Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mazao Mchanganyiko, Dkt. Anselm Moshi akimfafanulia jambo Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Alrifai, Bwn. Abdellah Foaud pamoja na Meneja Viwango Bwn. Ahmed Mohamed Bahie


Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Alrifai, Bwn. Abdellah Foaud akiuliza kitu wakati alipotembelea moja kati ya viwanda vya kubangua korosho Mkoani Mtwara


Ujumbe wa Kampuni ya Alrifai ukiwa katika moja ya kiwanda cha kubangua korosho mkoani Mtwara
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Bwn. Gelasius Byakanwa (kulia) akiwa ofisini kwake na Ujumbe wa Kampuni ya Alrifai ambapo ujumbe huo ulitembelea pia chuo cha utafiti wa Korosho Nariendele na baadhi ya viwanda vya kubangua korosho

Ujumbe wa Kampuni ya Alrifai ukiwa katika moja ya duka la kuuza karafuu Mjini Zanzibar 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.