Tuesday, September 3, 2024

WAZIRI KOMBO AONGOZA UJUMBE WA TANZANIA KWENYE MKUTANO WA MAWAZIRI WA FOCAC.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji Prof. Kitila Mkumbo wakipitia nyaraka za mkutano wa Mawaziri wa FOCAC muda mfupi kabla ya kuanza kwa mkutano huo. 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) ameongoza ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano 9 wa Mawaziri wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (9th Ministerial Conference of the Forum on China-Africa Cooperation) uliofanyika tarehe 3 Septemba 2024 jijini Beijing, China.

Mkutano huo pamoja na masuala mengine umejadili na kupitisha agenda za Mkutano wa Kilele wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (Forum on China-Africa Cooperation-FOCAC) unaotarajiwa kufanyika jijini humo kuanzia Septemba 4-6, 2024. 

Akizungumza kwenye ufunguzi wa mkutano huo Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Watu wa China ambaye pia ni mwenyeki mwenza wa mkutano huo Mhe. Wang Yi ameeleza kuwa ushirikiano wa China na Afrika hautazamwi kuwa ni wakindugu na urafiki pekee bali unalenga kuchagiza kasi ya maendeleo ya pande zote mbili kwa kutatua changamoto zinazokabili jamii.

Ameongeza kuwa FOCAC limekuwa jukwaa muhimu linalotoa fursa hadhimu kwa Viongozi wa China na Afrika kukutana na kujadili kwa pamoja masuala muhimu ya kimkakati kwa mustakabali mwema wa mataifa hayo na watu wake. 

Vilevile Waziri Wang ameeleza kuridhishwa kwake na kupongeza hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa masuala yaliyokubaliwa katika mkutano wa 8 wa FOCAC uliofanyika jijini Dakar, Senegal ikiwemo kwenye sekta ya ujenzi wa miundombinu,viwanda na kilimo, biashara na uwekezaji, ubunifu na teknolojia. 

Kwa upande wake Waziri Mambo ya Nje wa Senegal ambaye pia ni mwenyeketi mwenza wa mkutano huo Mhe. Yacine Fall ameeleza kuwa China ni mshirika wa kimkakati wa maendeleo kwa Mataifa ya Afrika hivyo uhusiano wa kindungu uliopo kati ya pande hizo mbili unapaswa kudumishwa na kulindwa daima kwa manufaa ya pande zote mbili. 

Aidha, mkutano huo kwa kauli moja umepitisha rasimu ya agenda ya Mkutano wa Kilele wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa FOCAC, rasimu ya tamko na mpango wa utekelezaji na tathimini ya utekelezaji wa masuala yaliyofikiwa katika mkutano wa 8 wa FOCAC.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo umejumuisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji Prof. Kitila Mkumbo, Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Samwel Shelukindo, Balozi wa Tanzania nchini China Mhe. Khamis Mussa Omar na Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia Bi. Felista Lugabwa ukiongozwa na Waziri Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo. 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) akifuatilia Mkutano 9 wa Mawaziri wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika uliofanyika jijini Beijing, China, tarehe 3 Septemba 2024.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Watu wa China Mhe. Wang Yi akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano 9 wa Mawaziri wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika uliofanyika jijini Beijing, China, tarehe 3 Septemba 2024.
 Mkutano 9 wa Mawaziri wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika ukiendelea jijini Beijing, China.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo akifurahia jambo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya Mhe. Musalia Mudavadi muda mfupi kabla ya kuanza kwa Mkutano 9 wa Mawaziri wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.