Wednesday, December 21, 2016

Katibu Mkuu wa Mambo ya Nje akutana na ujumbe wa UNMICT



Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Aziz P. Mlima (katikati) akizungumza na Bwana Samuel Akorimo, Mkuu wa Ofisi ya Arusha kutoka Mahakama ya Umoja wa Mataifa (UNMICT) iliyopo Arusha walipomtembelea  Wizarani kwa lengo la kushukuru kwa mchango wa Serikali na Wizara kufanikisha ujenzi na uzinduzi wa Majengo ya Umoja wa Mataifa Jijini Arusha, eneo la Lakilaki. Wengine katika picha ni Balozi Baraka Luvanda, Mkurugenzi wa Kitengo cha Sheria (kulia) na Bi.Bi Blandina Kasagama, Afisa Mambo ya Nje. Kushoto ni Bw. Samwel Algozin Afisa Sheria Mkuu kutoka (UNMICT)


Katibu Mkuu, Balozi Mlima na Ujumbe kutoka UNMICT wakiwa  katika picha ya pamoja baada ya kikao

Friday, December 16, 2016

Tanzania na Kenya zasaini Makubaliano ya Tume ya Pamoja ya Ushirikiano


 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,  Balozi Dkt. Augustine Mahiga kwa pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya, Mhe. Balozi Dkt. Amina Mohammed wakisaini Makubaliano ya Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Kenya.  Makubaliano hayo yamesainiwa kufuatia Kikao cha Tume ya Pamoja ya Ushirikiano (JCC) kati ya Tanzania na Kenya kilichofanyika tarehe 1 hadi 3 Desemba, 2016 ambapo masuala mbalimbali ya ushirikiano baina ya nchi hizi mbili yalijadiliwa na kukubaliwa. Masuala ya ushirikiano ni pamoja na kilimo, uchukuzi, utalii, nishati na madini na uvuvi. Hafla hiyo fupi ya uwekaji saini makubaliano hayo imefanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini  Dar es Salaam tarehe 16 Desemba, 2016.
Waziri Mahiga na Waziri Mohammed wakibadilishana makubaliano hayo mara baada ya kusaini.
Waziri Mahiga akizungumza katika hafla hiyo.Katika hotuba yake Mhe. Mahiga alisisitiza kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana kwa karibu na Kenya na kwamba makubaliano yaliyosainiwa yataimarisha mahusiano hayo kwa kuboresha mazingira ya uwekezaji, kurahisisha ufanyaji biashara na kuongeza fursa za ajira kwa vijana wa nchi hizi mbili.
Waziri Amina naye  akizungumza kwenye hafla hiyo. Katika hotuba yake aliahidi Kenya kuendelea kushirikiana na Tanzania kwa karibu katika masuala yote yaliyokubaliwa.
Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhani Muombwa Mwinyi akitoa neno la shukrani katika hafla hiyo ya uwekaji saini Makubaliano ya Tume ya Pamoja ya Ushirikiano
Sehemu ya wajumbe kutoka Kenya waliohudhuria  hafla ya uwekwaji saini wa Makubaliano ya Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Kenya.  Kulia ni Balozi wa Kenya nchini Tanzania, Mhe. Chirau Ali Mwakwere
Sehemu ya ujumbe wa Tanzania nao wakishuhudia uwekwaji  saini katika makubaliano ya tume ya pamoja ya ushirikiano kati ya Tanzania na Kenya. Kushoto ni Balozi Samwel Shelukindo, Mkurugenzi wa Idara ya Afrika akifuatiwa na Bw. Stephen Mbundi, Mkurugenzi wa Idara ya Siasa, Ulinzi na Usalama katika Wizara ya mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Masahriki
Mshereheshaji ambaye pia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Mindi Kasiga akiwakaribisha wageni wakati wa hafla ya uwekaji saini Makubaliano ya Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Kenya.
Sehemu ya maafisa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Waandishi wa Habari waliohudhuria  hafla hiyo.
Picha ya Pamoja

Wednesday, December 14, 2016

Wizara ya Mambo ya Nje yapokea kifaa cha kutunza data za mtandao kutoka IOM

Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika, Balozi Joseph Sokoine (katikati) akimwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki  kupokea kifaa cha kulinda na kutunza data za mtandao (router) za   Wizara kutoka kwa Mwakilishi Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) nchini Tanzania, Bw. Qasim Sufi ( kulia)Kushoto ni Mkurugenzi wa Idara ya Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Anisa Mbega.
 Balozi Sokoine (katikati) akizungumza na Bw. Sufi mara baada ya kupokea kifaa cha kutunza na kulinda data za mtandao wa Wizara (Router)
Balozi Mbega naye akichangia jambo wakati wa mazungumzo hayo
Picha ya pamoja

Balozi wa Tanzania nchini Malaysia, Mhe. Dkt. Dau awasilisha Hati za Utambulisho

Balozi wa Tanzania nchini Malaysia, Mhe. Dkt Ramadhani Dau akikabidhi  hati zake za utambulisho kwa mfalme na mkuu wa nchi hiyo  Abdul Halim Mu'adzam Shah katika kasri ya Istana Negara jijini Kuala Lumpur  mapema mwezi huu.

Balozi wa Tanzania nchini Malaysia, Mhe. Dkt Ramadhani Dau akikabidhi  Hati za Utambulisho kwa Mfalme na Mkuu wa Nchi hiyo,  Abdul Halim Mu'adzam Shah katika kasri ya Istana Negara jijini Kuala Lumpur  mapema mwezi huu.



Kikosi cha askari kikitoa saluti wakati nyimbo za Taifa za Tanzania na Malayasia zikipigwa mara baada ya Balozi wa Tanzania nchini humo  Mhe. Dkt Ramadhani Dau kuwasili katika kasri ya Istana Negara jijini Kuala Lumpur kukabidhi Hati za Utambulisho kwa Mfalme na Mkuu wa nchi hiyo aliyemaliza muda wake Abdul Halim Mu'adzam Shah mapema mwezi huu.

Tuesday, December 13, 2016

Wizara ya Mambo ya Nje yakutana uongozi wa Taasisi ya Aga Khan kujadili masuala ya ushirikiano

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga akitoa hotuba ya ufunguzi katika kikao cha wadau kilichoandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje kwa  ajili ya kujadili masuala ya ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na Uongozi wa Taasisi ya Maendeleo ya Aga Khan "The Aga Khan Development Network" (AKDN). Kikao hicho kilifanyika tarehe 13 Disemba, 2016 katika ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam.
Mkuu wa masuala ya Diplomasia katika Taasisi wa Maendeleo wa Aga Khan, Balozi Arif Lalani  akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi ya Taasisi hiyo iliyopo nchini. Balozi Lalani alieleza kuwa wataendelea kushirikiana na Tanzania katika kuhakikisha wanatoa huduma nzuri na zenye ubora hususan katika sekta za Elimu, Afya na masuala ya Utalii sambamba na kuangalia namna ya kuanzisha maeneo mengine zaidi ya uwekezaji.
Waziri Mahiga akifuatilia ya taarifa iliyokuwa ikiwasilishwa na Mratibu wa Mradi wa Chuo cha Aga Khan kinachotarajiwa kujengwa Jijini Arusha. Pembeni yake kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhan Muombwa Mwinyi na kushoto ni Mkurugenzi wa Idara ya Sheria, Balozi Baraka Luvanda.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali na Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Mindi Kasiga (kulia) pamoja na Bi Lilian Kimaro, Afisa Mambo ya Nje wakifuatilia kikao.
Sehemu nyingine ya Maafisa wa Wizara ya Mambo ya Nje  na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakifuatilia kikao.
Kikao cha wadau kikiendelea.

Friday, December 9, 2016

Naibu Waziri ashiriki maadhimisho ya siku ya Kitaifa ya Japan


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Susan Kolimba akisalimiana na Balozi wa Japan nchini, Tanzania Mhe. Masaharo Yoshida mara alipowasili kushiriki hafla fupi ya maadhimisho ya siku ya Japan iliyofanyika  nyumbani kwa Balozi huyo Oysterbay, Jijini Dar es Salaam 
Mkurugenzi na Idara ya Asia na Australasia, Balozi Mbelwa Kairuki akisalimiana na Balozi wa Japan nchini Mhe. Masaharn Yoshida alipowasili nyumbani kwake Jijini Dar es Salaam kushiriki hafla fupi ya maadhimisho ya siku ya Japan
Kutoka kulia; Rais Mstaafu wa Serikali ya Awamu ya Pili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Ali Hassan Mwinyi, Naibu Waziri Mhe.Dkt. Susan Kolimba na Balozi wa Japan nchini Mhe.Masaharo Yoshida wakiwa wamesimama wakati wimbo wa Taifa unapigwa
Balozi wa Japan nchini Mhe.Masaharo Yoshida akiongea na hadhira iliyohudhuria hafla ya siku ya Japan 
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Susan Kolimba akiongea na hadhira iliyohudhuria hafla hiyo

Thursday, December 8, 2016

Naibu Waziri akutana na Kaimu Balozi wa Marekani nchini


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Susan Kolimba akisalimiana na Kaimu Balozi wa Marekani nchini, Bi. Virginia M. Blaser walipokutana kwa mazungumzo Wizarani Jijini Dar es Salaam

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Susan Kolimba akizungumza na Kaimu Balozi wa Marekani nchini Bi.Virginia M. Blaser walipokutana Wizarani mapema leo asubuhi.

Naibu Waziri Mhe. Dkt. Susan Kolimba akimsikiliza Kaimu Balozi wa Marekani Bi. Virgnia M Blaser walipokutana kwa mazungumzo Wizarani
Balozi Joseph Sokoine (wa kwanza kulia) akifafanua jambo wakati wa mazungumzo 
Mazungumzo yakiendelea

Katibu Mkuu na "TUNATEKELEZA" leo


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki leo saa 3.30 hadi 4.30 usiku atazungumza kwenye kipindi cha "TUNATEKELEZA" kitakacho rushwa  kupitia TBC1, akielezea majukumu mbalimbali ya Wizara. Tafadhali fuatilia bila kukosa

Afrika ijifunze kutoka Korea, Mawaziri





TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Afrika ijifunze kutoka Korea, Mawaziri.


Nchi za Afrika zimehimizana kutumia sera , mbinu na mfumo wa maendeleo uliotumiwa na Jamhuri ya Korea kufanya mapinduzi makubwa ya uchumi, viwanda na teknolojia katika kipindi cha miongo michache iliyopita.

Hayo yamejiri kwenye Mkutano wa  Mawaziri wa  nchi za Afrika na Korea uliohitimishwa leo jijini Addis Ababa, Ethiopia.

"Katika miaka ya 1960 hali ya uchumi na mazingira ya Korea yalikuwa yanalingana na bara la Afrika, hivyo, mfumo ulioifanya Korea kufanya mapinduzi ya uchumi unafaa kutumiwa na bara la Afrika kwa kuwa mazingira yetu yanafanana".

Katika mkutano huo ambaoTanzania iliwakilishwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Augustine Mahiga, Mawaziri walielezea kuridhishwa na ushirikiano huo tokea ulipoanzishwa mwaka 2006, kwa kuwa unazingatia maslahi ya pande zote na haufungamani na masharti ya aina yoyote.

Walisema kuwa Bara la Afrika lina fursa lukuki zikiwemo maliasiri kama madini, mafuta na ardhi nzuri kwa kilimo.

 Rasilimali hizo miaka yote zimekuwa zikiuzwa nje bila kuendelezwa kutokana na ukosefu wa viwanda na teknolojia, hali iliyochangia  kwa kiasi kikubwa kulifanya bara hilo kubaki nyuma kimaendeleo.
Hivyo, kupitia jukwaa hilo la ushirikiano na Korea, bara la Afrika litapokea misaada ya fedha za maendeleo na teknolojia  itakayotumiwa kujenga viwanda vya kusindika rasilimali ili kuziongezea thamani.

Kwa kuwa maendeleo na amani na usalama ni vitu vinavyotegemeana, Mawaziri walisisitiza umuhimu wa kutunza amani barani Afrika kwa kushirikiana na Korea.

 Walibainisha masuala mbalimbali yanayotishia amani ya  dunia likiwemo tatizo la ugaidi wa kimataifa. Walikubaliana kuwa ugaidi ni changamoto ya ulimwengu mzima na ili ufumbuzi wake upatikane lazima wadau duniani kote washirikiane.

Ushirikiano wa nchi za Afrika na Korea unatimiza miaka 10 mwaka huu tokea ulipoanzishwa mwaka 2006. Kwa muktadha huo, ulisisitizwa umuhimu wa kufanya tathmini na ufuatiliaji wa miradi ya utekelezaji ili kubaini mafanikio mapungufu na changamoto.  Hiyo itasaidia kuchukua hatua stahiki katika kufikia malengo yaliyowekwa na umoja huo.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Korea, Mhe. Yun Byung-se alieleza mafanikio ya ushirikiano huo tokea kunzishwa kwake. Alisema katika eneo la ushirikiano wa kiuchumi na Afrika, Korea ilikuwa mwenyeji wa Mkutano wa tano wa Mawaziri wa ushirikiano wa kiuchumi kati ya Korea na Afrika mwezi Oktoba 2016.

 Katika mkutano huo, Korea iliahidi kutoa Dola za Marekani bilioni 5 kwa ajili ya kusaidia masuala ya kiuchumi barani Afrika. Fedha hizo zinatarajiwa kuongezeka  mara dufu katika kipindi kijacho. Aidha, Korea inatarajia kuwa mwenyeji wa Mkutano wa Jukwaa la ushirikiano wa viwanda kati ya Korea na Afrika katika wiki mbili zijazo.

Vile vile, Korea imeongeza mara dufu misaada ya maendeleo kwa bara la Afrika na ile misaada ya maendeleo inayohusisha nchi mbili (bilateral)  itaongezeka kutoka asilimia 24 hadi kufikia asilimia 35 itakapofika mwaka 2020.

Waheshimiwa Mawaziri walihitimisha mkutano wao kwa kuridhia nyaraka mbili ambazo ni Tamko la Addis Ababa na Mwongozo wa Ushirikiano kati ya Korea na Afrika. Mwongozo huo umeainisha miradi mbali mbali itakayotekelezwa katika kipindi cha miaka mitano 2017 - 2021. Maeneo hayo ni pamoja na: biashara, kuendeleza viwanda na uwekezaji; uzalishaji katika kilimo na kiwango cha mavuno; uchumi wa bahari, uendeshaji wa bandari na usafiri wa majini; kuwaendeleza vijana na kuwajengea uwezo wanawake.

Wajumbe walikubaliana kuwa mkutano ujao utafanyika Seoul, Korea mwaka 2021.


Imetolewa na: KITENGO CHA MAWASILIANO YA SERIKALI, WIZASRA YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI.
TAREHE 08 DESEMBA 2016

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga akisoma hotuba ya Tanzania kwenye Mkutano wa Nne wa Ushirikiano wa nchi za Afrika na Jamhuri ya Korea uliofanyika jijini Addis Ababa, Ethiopia tarehe 06 na 07 Desemba 2016.
Mhe. Waziri Mahiga akipitia makabrasha ya mkutano. Nyuma ya Mhe. Waziri ni Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia na kwenye Umoja wa Afrika, Mhe. Naimi Aziz na Afisa wa Ubalozi huo, Bi Suma Mwakyusa.

Maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje nao wakifuatilia mkutano huo. Kutoka kushoto ni Bw. Gerlad Mbwafu, Katibu wa Waziri, Bi. Berther Makilagi, Afisa Dawati la Korea na Bw. Benedict Msuya anayemwakilishsa Mkurugenzi wa Asia na Australasia.

Picha ya pamoja