Thursday, July 6, 2017

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Taarifa ya Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania na Kenya kuhusu utekelezaji wa maamuzi ya Wakuu wa Nchi Mhe. Rais John Pombe Magufuli wa Tanzania na Mhe. Rais Uhuru Kenyatta wa Jamhuri Kenya
  
Itakumbukwa kuwa tarehe 28 Juni, 2017 Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilitoa taarifa kwa umma kuhusu vikwazo vya kibiashara ambavyo nchi ya Kenya iliweka katika baadhi ya bidhaa kwa kipindi cha hivi karibuni. Katika taarifa ile, Serikali ya Tanzania ilibainisha dhamira yake ya kufanya mazungumzo na Serikali ya Kenya kwa lengo la kumaliza tofauti hizo za kibiashara baina ya nchi hizi mbili kwa kuzingatia taratibu za kibiashara tulizokubaliana katika Jumuiya yetu ya Afrika ya Mashariki.
Bidhaa za Tanzania ambazo ziliwekewa vikwazo na nchi ya Kenya ni unga wa ngano pamoja na gesi ya kupikia (LPG). Aidha, juhudi za awali za Serikali ya Tanzania kuona vikwazo hivyo vinaondelewa na Serikali ya Kenya kwa wakati hazikuzaa matunda. Hali hiyo ilipelekea Serikali ya Tanzania nayo kuchukua hatua.
Kwa kuzingatia mahusiano mazuri ya kindugu yaliyopo kati ya nchi zetu mbili na kwa kujali manufaa mapana ya Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki, Viongozi Wakuu wa nchi hizi mbili Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mhe. Uhuru Muigai Kenyatta, Rais wa Jamhuri ya Kenya walizungumza na kukubaliana kuondoleana vikwazo hivyo maramoja, Vikwazo hivyo ni;

1.     Serikali ya Kenya kuondoa vikwazo kwa bidhaa za unga wa ngano na gesi ya kupikia (LPG) kutoka Tanzania.

2.     Serikali ya Tanzania kuondoa vikwazo kwa bidhaa za maziwa zinazozalishwa nchini Kenya.

3.     Serikali za Kenya na Tanzania kuondeleana vikwazo vyovyote vile ambavyo vinaweza kuathiri biashara ya bidhaa na huduma kati ya nchi zetu mbili.

4.     Sigara ni kati ya mambo yaliyojadiliwa. Hata hiyo utekelezaji wake utafuata taratibu za ndani

Hivyo, Viongozi Wakuu wa nchi zetu mbili waliwaelekeza Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Nchi wa Tanzania na Kenya, Mhe. Dkt. Augustine Philip Mahiga (Mb) na Dkt. Amina Mohammed, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Jamhuri ya Kenya kuutarifu umma kwamba pande zote mbili zimekubaliana kumaliza tofauti hizo za kibiashara zilizojitokeza hapo awali.
Katika kutekeleza hilo, Mhe. Waziri Dkt. Amina Mohamed alimwalika Mhe.Waziri Dkt. Mahiga nchini Kenya tarehe 23 Julai, 2017 ambapo walifanya Mkutano wa Pamoja na waandishi wa habari kuutangaza uamuzi wa Viongozi Wakuu wa Kenya na Tanzania kuondoleana vikwazo hivyo maramoja.

Kufuatia makubaliano haya ya pamoja kati ya nchi hizi majirani ambazo ni waasisi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, pia, tunapenda kutaarifu kwamba Mataifa haya mawili yamekubaliana kuunda Tume ya Pamoja ambayo itakuwa na jukumu la kuepusha tofauti za kibiashara kati ya Tanzania na Kenya pamoja na kutolea ufumbuzi changamoto za kibiashara kati ya nchi hizi mbili pindi zinapojitokeza. Tume hii itaongozwa na Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania na Kenya na kujumuisha Mawaziri wanaohusika na masuala yaJumuiya ya Afrika Mashariki, Biashara, Fedha, Mambo ya Ndani ya Nchi, Kilimo, Uchukuzi na Utalii wa nchi zote mbili.
Vilevile, Mawaziri hawa wataunda mfumo wa kupeana taarifa mara kwa mara kuhusu masuala yenye changamoto za kibiashara kwa lengo la kuepusha kujirudia kwa tofauti kama hizi. Ni matarajio yetu kuwa uamuzi huu wa pamoja utakuza zaidi mahusiano ya kibiashara baina ya nchi hizi mbili. Aidha, tunapenda kuwashukuru wafanyabiashara wa nchi zetu mbili kwa uvumulivu.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar es Salaam, 24 Julai, 2017



MASWALI NA MAJIBU BAADA YA TAARIFA YA MSINGI
SWALI:  Je ni kwa nini Kenya waliweka vikwazo hivyo hapo awali?
JIBU: Sababu za awali zilizotolewa na Serikali ya Kenya zilidai kwamba bidhaa hizo hazikidhi viwango vya ubora wa kimataifa. Hata hivyo, Wataalamu wa Tanzania wameihakikishia Kenya kuwa bidhaa za unga wa ngano kutoka Tanzania zina ubora  unaokubalika Kimataifa na huuzwa nchi nyingine za Jumuiya ya afrika Mashariki na Afrika ya Kati. Halikadhalika bidhaa ya gesi ya kupikia (LPG) inakidhi viwango vya ubora vya Kimataifa
.
SWALI: Nini msimamo wa Serikali ya Tanzania kuhusu tuhuma za baadhi ya wanasiasa wa Kenya na baadhi ya vyombo vya habari kuhusu Tanzania kuingilia uchaguzi wa Kenya.
JIBU: Tuhuma hizi hazina ukweli wowote, na hata nilipokuwa  nchini Kenya juzi niliona zimeripotiwa tena na vyombo vya habari vya Kenya. Naomba nikanushe tena kwa mara nyingine, kwa niaba ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, haijawahi, na wala haifikirii kuingilia maswala ya ndani ya nchi nyingine tunazoshirikiana nazo ikiwemo maswala ya uchaguzi. Hatujawahi kuingilia uchanguzi wa Kenya na hututegemei kufanya hivyo kwenye uchaguzi huu na chaguzi nyingine zozote. Naomba waandishi wa habari, kabla ya kuandika taarifa hizi, wazihakiki mara mbili, na watutafute kutoa ufafanuzi kabla ya kuwapelekea wananchi taarifa hizi za kupotosha. Natoa rai, tuwe waangalifu na walaghai wa nje  wanaotaka kutugombanisha. Nichukue pia fursa hii kuwatakia wananchi wa Kenya uchaguzi mwema wa amani na huru.


SWALI:  Je ni kwanini Tanzania inaonekana kuweka vizingiti vingi vya kibiashara ikilinganishwa na nchi nyingine kwenye ukanda wa Afrika Mashariki na Afrika ya kati kwenye siku za hivi karibuni? Je hii haitakwaza ukuaji wetu wa uchumi kama nchi?
JIBU: Hapana, hata kidogo. Serikali ya Tanzania inaendelea kuweka mazingira wezeshi ya biashara ili kuwezesha uchumi wa nchi kukua na kuendelea, kutokana na biashara ndani ya bara la Afrika na hususan ukanda wetu wa Afrika Mashariki na Kati. Tanzania kwa siku za hivi karibuni chini ya uongozi wa Rais wa Awamu ya Tano, Mhe. John Joseph Pombe Magufuli, imefanya mageuzi makubwa kwenye taasisi zetu za bandari na ushuru yaani TRA. Hatua hizi zinalenga kwenye kuziba mianya iliyokuwepo huko nyuma ambayo ilisababisha ukusanywaji hafifu wa mapato. Ni wazi sasa mambo yanaenda kwa uwazi zaidi na ushuru unatozwa na kukusanywa kwa wakati. Tuna hakika sasa changamoto hizi zimepungua na nchi jirani zitaendelea kufanya biashara na sisi bila vikwazo.

SWALI: Kabla ya kuunda hii kamati ya kutatua changamoto zilizojitokeza hivi karibuni, Jumuiya ya Afrika Mashariki imekua ikitatua vipi changamoto kama hizi za kibiashara hususan kwenye nchi zenye ushindani mkubwa kama Kenya na Tanzania?
JIBU: Jumuiya ya Afrika Mashariki imejiwekea misingi imara na muhimu ya kutatua changamoto pindi zinapojitokeza. Hivyo ukiacha jopo la wataalam wa Serikalini kuna Baraza la Mawaziri wa Biashara wa Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki  ambao pia huweza kupendekeza ufumbuzi wa changamoto mbalimbali kwa wakuu wa nchi ili kutatua changamoto hizi. Lakini kutokana na ukaribu uliopo baina ya Tanzania na Kenya, hili la sasa tumelitatua kwa haraka na kwenda mbele zaidi kuunda tume ya mawaziri wa nchi zetu mbili ili huko baadae tuweze kutatua masuala kama haya mapema sana kabla ya kuathiri biashara kati ya nchi zetu mbili.

Ni dhahiri kwamba nchi zetu mbili ni jirani na tunalindwa na Itifaki za Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki, lakini pia tuna ushindani kati yetu. Na ili tupate maendeleo ni lazima kuweka ushindani wenye tija kwa manufaa ya ukanda wetu na wananchi wetu. Japo kuwa Kenya ipo kwenye kundi la nchi zenye kipato cha kati, uchumi wa Tanzania unakua kwa kasi kubwa na ni hali ya kawaida kwa changamoto kama hizi kujitokeza pindi nchi zinapokuwa katika ushindani wa kiuchumi.Kwa namna ya pekee naomba kusifu tena hekima za Viongozi wetu wa Juu kwa kutatua changamoto hizi kwa wakati.

Friday, June 30, 2017

Tanzania na Norway kushirikiana katika masuala ya siasa na diplomasia

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga (kulia) na Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufalme wa Norway, Mhe. Borge Brende wakiweka saini Mkataba wa Makubaliano kuhusu kushirikiana katika Mashauriano ya Kisiasa na Kidiplomasia kati ya Tanzania na Norway.Ttukio hilo lilifanyika jijini Dar Es Salaam kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere na kuhudhuriwa na Balozi wa Tanzania nchini Norway mwenye makazi yake nchini Sweden, Mhe. Dora Msechu, Balozi wa Norway nchini Tanzania, Mhe. Hanne Marie Kaarstad, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Amerika na Ulaya, Bi. Mary Matari, pamoja na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Mindi Kasiga (hawapo pichani).
Waheshimiwa Mawaziri wakibadilishana mikataba mara baada ya kuweka saini
Dkt. Mahiga akizungumza kwenye mkutano na Waandishi wa Habari mara baada ya kumaliza zoezi la uwekaji saini na Mgeni wake.
Mhe. Brende naye akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa Habari.
Balozi wa Tanzania nchini Norway mwenye makazi yake nchini Sweden, Mhe. Dora Msechu (wa pili kutoka kulia), Balozi wa Norway nchini Tanzania, Mhe. Hanne Marie Kaarstad (wa kwanza kulia), Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Amerika na Ulaya, Bi. Mary Matari (wa kwanza kushoto) pamoja na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Mindi Kasiga wakifuatilia kwa makini mkutano wa waandishi wa habari na Mawaziri wa Mambo ya Nje.
Sehemu ya ujumbe ulioambatana na Waziri wa Norway nao wakifuatilia mkutano wa waandishi wa habari na Mawaziri wa Mambo ya Nje.
sehemu ya waandishi wa habari wakiwasikiliza kwa makini Mawaziri walipokuwa wakiendelea kuzungumza (hawapo pichani).


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Tanzania na Norway kushirikiana katika masuala ya siasa na diplomasia

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga ameeleza kuwa kusainiwa kwa Mkataba wa Makubaliano (MoU) kuhusu kushirikiana katika Mashauriano ya Kisiasa na Kidiplomasia kati ya Tanzania na Norway kumefungua sura mpya ya mahusiano kati ya nchi hizo mbili. 

Kauli hiyo ameitoa leo jijini Dar Es Salaam wakati anaongea na waandishi wa habari baada ya shughuli ya uwekaji saini wa makubaliano hayo aliyoifanya kwa pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje wa Norway, Mhe. Borge Brende kukamilika.

Alisema kusainiwa kwa MoU hiyo kutazifanya nchi hizo kuwa na mahusiano ya karibu zaidi katika kubadilishana mawazo kuhusu masuala ya kisiasa na kidiplomasia ambayo kimsingi yalikuwepo tokea zamani lakini leo yamerasimishwa. 

Mhe. Mahiga amewambia wanahabari kuwa Tanzania na Norway zimekuwa zikishirikiana kiuchumi, kiteknolojia na kijamii kwa takribani miaka 55 sasa. Baadhi ya maeneo aliyoyataja ambayo nchi hizo zimekuwa zikishirikiana katika kipindi hicho ni pamoja na uzalishaji wa nishati ya umeme hususan vijijini, afya, elimu, kilimo na utunzaji wa misitu.  

Mhe. Mahiga aliendelea kueleza kuwa katika kikao chao, wamejadili maeneo mapya ya ushirikiano yakiwemo utunzaji wa mazingira na kusisitiza umuhimu wa kuimarisha uhusiano wa sekta binafsi za nchi hizo mbili kinyume na awali mahusiano zaidi yalikuwa baina ya Serikali mbili.
Waziri Mahiga ameishukuru Norway kwa jitihada zake ziliozasaidia uvumbuzi na uchimbaji wa gesi asilia nchini kupitia kampuni ya Statoil ambayo imewekeza nchini mtaji mkubwa kuliko mahali popote Afrika.

Alihitimisha hotuba yake kwa kusema kuwa Tanzania itaendelea kufaidika kwa kiasi kikubwa na ushirikiano wake na Norway kwa kuwa nchi hiyo ina utajiri mkubwa katika sekta ya mafuta misitu na teknolojia ya hali ya juu katika sekta mbalimbali.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Norway alieleza kuwa Norway imekuwa ikishirikiana na Tanznaia katika sekta za maendeleo tokea mwaka 1964 na kuahidi kuwa nchi yake itaendelea kuisaidia Tanzania hadi hapo nchi hiyo itakapokuwa na uwezo wa kugharamia miradi yake yenywe. 

Waziri Borge kabla ya kuondoka nchini leo jioni, atashiriki uzinduzi wa programu ya kushirikiana katika masuala ya kodi na uzinduzi wa awamu ya pili ya programu ya kuendeleza mafuta(oil for development program) utakaofanyika katika Hoteli ya Hyatt Regency, Kilimanjaro.  

-Mwisho-

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar es Salaam, 30 Juni 2017



Thursday, June 29, 2017

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Waziri wa Mambo ya Nje wa Norway kuzuru Tanzania

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufalme wa Norway, Mhe. Borge Brende atafanya ziara ya kikazi ya siku mbili nchini tarehe 29 na 30 Juni 2017. Madhumuni ya ziara ya Mhe. Brende ambaye atawasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere tarehe 29 saa tatu usiku ni kuimarisha mahusiano kati ya Norway na Tanzania.

Wakati wa ziara yake, Mhe. Waziri Brende pamoja na mambo mengine atafanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 30 Juni 2017. 

Aidha, siku hiyo hiyo asubuhi, mgeni huyo atafanya mazungumzo na mwenyeji wake, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga (Mb.) kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere na baadaye wataweka saini Mkataba wa Makubaliano (MoU) kuhusu Ushirikiano wa Mashauriano ya Kisiasa na Kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili. 

Mhe. Borge pia atakutana na Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Philip Mpango (Mb.) ambapo kwa pamoja watashiriki katika uzinduzi wa programu ya kushirikiana katika masuala ya kodi na uzinduzi wa awamu ya pili ya programu ya kuendeleza mafuta(oil for development program) utakaofanyika katika Hoteli ya Hyatt Regency, Kilimanjaro tarehe 30 Juni 2017.  Uzinduzi wa programu hizo pia utahudhuriwa na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Mhe. Dkt. Medard Kalemani (Mb.) na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Dkt. Charles Kichere. 

Ratiba ya ziara ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Norway inaonesha pia kwa kushirikiana na Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhe. Charles Mwijage (Mb.) na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Mhe. Dkt. Medard Kalemani watashiriki katika shughuli za kufunga semina ya Mradi wa Kusindika Gesi asilia (LNG) iliyoandaliwa na kampuni ya mafuta ya kutoka Norway inayoitwa Statoil ambayo pia inaendesha shughuli zake hapa nchini. Semina hiyo inafanyika katika Hoteli ya Hyatt Regency jijini Dar es Salaam.
Mhe. Waziri baada ya kukamilisha ratiba yake nchini atarejea Norway siku ya Ijumaa tarehe 30 Juni 2017 saa nne usiku.

-Mwisho-
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar es Salaam, 29 Juni 2017



Waziri Mahiga akutana na kaimu Balozi wa Marekani nchini

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga akizungumza na Kaimu Balozi wa Marekani nchini, Dkt. Inmi K. Patterson, alipokutana naye Wizarani Jijini, Dar es Salaam, tarehe 29 Juni, 2017. Mazungumzo yao yalijikita katika masuala ya ushirikiano ambapo wameahidi kuendeleza ushirikiano katika sekta za maendeleo kwa lengo la kukuza uchumi ili kuendana na kasi ya utendaji wa Serikali zao.   

Mazungumzo yakiendelea, kushoto ni ujumbe uliombatana na Kaimu Balozi, wa kwanza kushoto ni afisa tawala wa ubalozi wa Marekani Bw.Jay Zimmerman, pembeni yake ni afisa habari wa Ubalozi huo, Bi. Lauren Ladenson na kulia ni afisa wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Redempta Tibaigana.

Wednesday, June 28, 2017

Waziri Mahiga ampokea Mjumbe Maalum kutoka Sahrawi

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga (Mb.) amepokea Ujumbe Maalumu kutoka kwa Rais wa Sahrawi ambao uliwasilishwa kwake na Mjumbe Maalum ambaye pia ni Waziri anayeshughulikia masuala ya Afrika, Mhe. Hamdi Mayera. Baada ya kuwasilisha ujumbe huo viongozi hao wawili walifanya mazungumzo yaliyojikita kwenye kuendeleza mahusiaono ya kidiplomasia kati ya Tanzania na Saharawi. Mazungumzo hayo yamehudhuriwa pia na Balozi wa Sahrawi nchini Tanzania Mhe. Brahim Buseif.
Dkt. Mahiga akimsikiliza Mhe.Mayera
Balozi wa Sahrawi hapa nchini Mhe. Buseif (wa kwanza kushoto) pamoja na Dkt. Mahiga wakimsikiliza Mhe. Mayera alipokuwa akiendelea kuzungumza.
Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Afrika, Bw. Suleiman Salehe (wa kwanza kushoto) akifuatiwa na Afisa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Nicholus Katibu wa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Gerald Mbwafu na katikati ni  nao kwa pamoja wa kisikiliza mazungumzo kati ya Mhe. Mayera na Dkt. Mahiga (hawapo pichani).
Waziri Mahiga (wa tatu kutoka kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mjumbe Maalum, Mhe. Mayera (wa tatu kushoto) pamoja na Maafisa Waandamizi kutoka Wizarani pamoja na Balozi Buseif.