Monday, August 14, 2017

RAIS WA MISRI AWASILI NCHINI NA KUPOKEWA NA MWENYEJI WAKE RAIS DKT. MAGUFULI


 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimpokea mgeni wake Rais wa Misri Abdel Fattah Al Sisi mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere(JNIA) jijini Dar es Salaam. 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na mgeni wake Rais wa Misri Abdel Fattah Al Sisi mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere(JNIA) jijini Dar es Salaam. 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa amesimama na mgeni wake wake Rais wa Misri Abdel Fattah Al Sisi wakati nyimbo za mataifa mawili ya Tanzania na Misri zikipigwa uwanjani hapo
 Rais wa Misri Abdel Fattah Al Sisi akikagua gwaride la Heshima mara baada ya nyimbo za Taifa kupigwa katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere(JNIA) jijini Dar es Salaam.
Rais wa Misri Abdel Fattah Al Sisi akiangalia vikundi vya ngoma za asili mara baada ya kuwasili nchini.
 TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI 

Tanzania na Misri kushirikiana katika viwanda

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli amesema kuwa Misri ina historia kubwa katika Nyanja mbalimbali za maendeleo yaliyofikiwa na mwanadamu katika dunia ya leo.

Kauli hiyo aliitoa jana Ikulu, Dar Es Salaam akiwa pamoja na mgeni wake, Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Mhe. Abdel Fatah Al Sisi ambaye yupo nchini kwa ziara ya kitaifa ya siku mbili tarehe 14 na 15 Agosti 2017.

Rais Magufuli alisema kuwa ukizungumzia maendeleo ya uhandisi huwezi kukosa kuitaja Misri na ushahidi hadi leo upo namna ujenzi wa piramidi ulivyofanyika. Aidha, katika masuala ya dini, Rais Magufuli alisema kuwa maandiko yanabainisha kuwa Yesu Kristu alikimbilia nchi hyo alipotaka kuuwawa na Herode. 

“Kwa kuwa hata Manabii walikimbilia Misri nimeona nami shida zangu nizikimbizie huko na Mhe. Al Sisi amekubali tushirikiane ili kwa pamoja tutatue changamoto za kiuchumi zinazotukabili”. Rais Magufuli alisema.
Viongozi hao wawili wamekubaliana kushirikiana katika masuala mbalimbali ikiwemo ufugaji, kilimo, afya, elimu, utalii, ulinzi na matumizi ya maji ya mto Nile.

Kwa upande wa Ufugaji, Misri imekubali kuanzisha kiwanda kikubwa cha kusindika nyama nchini ili kukidhi mahitaji makubwa ya nyama nchini Misri na pia kutoa ajira, mapato na soko kwa wafugaji wa hapa nchini.
Aidha, Tanzania itaendelea kujifunza kutoka Misri katika sekta ya kilimo, hususan utaalamu wa umwagiliaji. “Nchi ya Misri ina eneo kubwa kidogo kuliko Tanzania lakini asilimia 95 ya eneo hilo ni jangwa ambalo huwezi kufanya shughuli za kilimo. Licha ya eneo linalotumika kwa kilimo kuwa dogo, lakini nchi hiyo inazalisha chakula cha kutosha na ziada ya kuuza nje”. Rais Magufuli alisema.

Kuhusu masuala ya afya, Misri imeahidi kuanzisha kiwanda cha kutengeneza dawa za binadamu nchini Tanzania ambapo Rais Magufuli alisema kiwanda hicho kitakapokamilika na kuanza kazi, kitaokoa fedha nyingi za Serikali zinazotumika kwa ajili kuagiza dawa nje ya nchi.
Suala la matumizi ya maji ya mto Nile, Rais Magufuli alieleza kuwa wamekubaliana na mgeni wake kuwa wataendelea kujadiliana ili kupata utaratibu mzuri wa kutumia maji hayo utakaokuwa na maslahi kwa nchi zote zinazopitiwa na mto huo.

Viongozi hao pia wamekubaliana kubadilishana uzoefu katika sekta ya utalii ambapo Misri imepiga hatua kubwa katika sekta hiyo. Kwa mujibu wa takwimu zilizopo, Misri inapokea watalii zaidi ya milioni 10 kila mwaka ukilinganisha na idadi ya watalii milioni 2 ambayo Tanzania inapata kwa mwaka. Hivyo, Tanzania ina mambo mengi ya kujifunza kutoka Misri ili kuongeza idadi ya watalii wa kutembelea Tanzania kwa mwaka.

Rais Nagufuli alihitimisha hotuba yake kwa kueleza kuwa Ziara ya Mhe. Al Sisi imeimarisha uhusiano mzuri uliopo kati ya nchi hizi mbili ambao uliasisiwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na Rais wa zamani wa Misri, Marehemu Gamal Abdel Nasser. Alisisitiza umuhimu wa kushirikiana kibiashara kati ya nchi hizo mbili ambapo kwa takwimu zilizopo kiwango cha biashara kwa mwaka ni Dola milioni 778 na uwekezaji wa Misri nchini ni Dola milioni 887, viwango ambavyo bado ni vya chini mno.

Kwa upande wake, Rais wa Misri alipongeza hatua mbalimbali zinazochokuliwa na Rais Magufuli za kuiendeleza nchi kiuchumi pamoja na kupambana na rushwa na ufisadi. Aidha, aliahidi kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuimarisha mtangamano ndani ya Afrika na kupata msimamo mmoja wa Bara la Afrika katika masuala mbalimbali ya kimataifa.    
Mwisho-

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar es Salaam, 15 Agosti 2017









Waziri Mahiga akutana na Mjumbe Maalum kutoka Serikali ya Japan

Waziri wa Mambo wa Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga akizungumza na Mjumbe Maalum wa Serikali ya Japan, Mhe. Ichiro Aisawa alipofika Wizarani hivi karibuni. Katika mazungumzo yao walizungumzia masuala mbalimbali yanayohusu ushirikiano kati ya nchi hizi mbili ikiwemo miradi ya maendeleo inayofadhiliwa na Japan.
Bw. Ichiro Aisawa nae akizungumza. Kushoto ni Balozi wa Japan nchini, Mhe. Masaharu Yoshida
Mhe. Mahiga akifafanua jambo wakati wa mazungumzo. Kulia ni Bi. Justa Nyange, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Waziri Mahiga akiagana na Bw. Ichiro Aisawa mara baada ya kumaliza mazungumzo yao.



Friday, August 11, 2017

Taarifa kuhusu ziara ya Kitaifa ya Mhe. Abdel Fattah Al Sisi, Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri nchini


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI 

Taarifa kuhusu ziara ya Kitaifa ya Mhe. Abdel Fattah Al Sisi, Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri nchini 

Kufuatia mwaliko wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Abdel Fattah Al Sisi, Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri atafanya Ziara ya Kitaifa nchini Tanzania wiki ijayo. Hii itakuwa ni ziara ya kwanza ya Mheshimiwa Abdel Fattah Al Sisi nchini Tanzania tangu Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli aingie madarakani. 

Lengo la ziara hii ni kuimarisha na kukuza zaidi mahusiano mazuri yaliyopo ya kidiplomasia, kiuchumi na kijamii kati ya nchi hizi mbili, ziara hii pia itatoa fursa kwa viongozi wetu kujadili masuala mbalimbali yanayohusu nchi hizi mbili, ya kikanda na kimataifa.

Mheshimiwa Rais Al Sisi atawasili nchini kupokelewa na mwenyeji wake, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Aidha, Mheshimiwa Rais Al Sisi mchana atakuwa na mazungumzo (tete-a-tete) na mwenyeji wake kabla ya kushiriki mazungumzo rasmi (official talks) na baadae jioni Mheshimiwa Rais Al Sisi atahudhuria dhifa ya kitaifa itakayoandaliwa na mwenyeji wake. 

Tanzania na Misri zina mahusiano mazuri ya kidiplomasia ya muda mrefu ambayo yamezidi kuimarika hasa katika miaka ya karibuni. Ushirikiano huu unatokana na misingi ya mahusiano na mashirikiano ya karibu sana kati ya Marehemu Baba wa Taifa na muasisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Kiongozi mashuhuri wa Misri na muasisi wa Jamhuri ya Taifa  la Kiarabu ya Misri, Marehemu Gamal Abdel Nasser. Uhusiano wa nchi hizi mbili umejengwa katika misingi ya ushirikiano na maelewano katika Nyanja za kijamii, kiuchumi, kisiasa, kiulinzi na kiusalama pamoja na medani za siasa za ushirikiano kimataifa, kutetea haki za binadamu, kuimarisha umoja na maendeleo ya Afrika, ukombozi wa Bara la Afrika na kupinga ukoloni, dhuluma na aina zote za ukandamamizaji duniani. Uhusiano huu umejengwa katika Nyanja zote za uhusiano katika sekta za huduma za kijamii na kiuchumi zikiwemo elimu, afya, kilimo, mawasiliano, usafiri, ulinzi na usalama na ushirikiano wa kimataifa.

Misri ni nchi ya pili yenye uchumi mkubwa Barani Afrika. Takwimu za mwaka 2016, zinaonesha kwamba pato la taifa (GDP) la Misri lilikuwa Dola za Kimarekani Billioni 266.213. Sekta kubwa kabisa katika uchumi wa Misri ni sekta ya huduma ( huduma za benki, mawasiliano, usafirishaji na utalii) ambayo inachangia takribani asilimia 52.5 kwenye GDP. Viwanda (manufacturing) inachangia asilimia 36.3, na kilimo asilimia 11.2.

Tanzania na Misri zinashirikiana katika ngazi za taasisi za serikali ambazo ni Taasisi ya Udhibiti wa utawala ya Misri (Administration Control Authority of Egypt) ambayo inashirikiana na Taasisi ya kupambana na kuzuia Rushwa ya Tanzania (TAKUKURU), Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na Hospitali ya Rufaa ya Mnazi mmoja zimesaini makubaliano ya Ushirikiano na Hospitali ya El Shatby ya Chuo Kikuu cha Alexandria nchini Misri, Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) kina mashirikiano ya kubadilishana wataalamu na usimamizi wa pamoja wa Shahada za juu za uzamili na uzamivu na Chuo Kikuu cha Azhar cha Misri, Jeshi la Wananchi wa Tanzania kupitia SUMA JKT wamesaini Makubaliano ya Ushirikiano na Kampuni ya Polyserve ya Misri .

Aidha, kutokana na takwimu za kituo cha Uwekezaji (TIC) kimesajili jumla ya miradi nane kati ya mwaka 1990 hadi 2017, miradi hii ina jumla ya thamani ya Dola za Kimarekani 887.02 na kutoa ajira zipatazo 953, uwekezaji huo ni katika maeneo ya Kilimo, viwanda(mbao, mbolea, madini, dhahabu na shaba) na sekta ya Huduma.

Hivyo ziara hii ina umuhimu mkubwa sana hasa katika wakati huu ambapo msisitizo wa Serikali ni katika kujenga uchumi wa viwanda.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dar es Salaam
11 Agosti, 2017
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Aziz P. Mlima akiongea na waandishi wa habari kuhusu ziara ya Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Mhe. Abdel Fattah Al Sisi itakayofanyika nchini wiki ijayo.

Balozi Mlima akiendelea na mazungumzo yake na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.


Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali na Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Mindi Kasiga akifafanua jambo kwa waandishi wa habari.(hawapo pichani)

Wednesday, August 9, 2017

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola kutembelea Tanzania

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Aziz Mlima akizungumza kwenye mkutano na Waandishi wa Habari, kuhusu ziara ya kikazi ya Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Mhe. Patricia Scotland anayewasili nchini tarehe 10 - 12 Agosti, 2017
Kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Deusidedit Kaganda.Kushoto ni Mkuu wa Kitengo cha Habari na Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Mindi Kasiga
Juu na chini ni sehemu ya waandishi wa habari waliohudhuria mkutano huo.


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Taarifa kuhusu ziara ya Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola nchini

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Mheshimiwa Patricia Scotland anatarajiwa kufanya ziara ya kikazi ya siku tatu nchini kuanzia tarehe 10 hadi 12 Agosti, 2017. 

Lengo la ziara hiyo ni kueleza Viongozi wa Ngazi za Juu wa Taifa kuhusu  mageuzi yanayofanywa na Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola na vipaumbele vya Jumuiya hiyo kwa sasa; Hatua zinazochukuliwa ili kuimarisha kazi za Jumuiya hiyo na kutoa taarifa kuhusu Mkutano wa Wakuu Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Madola unaotarajiwa kufanyika London, Uingereza mwezi Aprili, 2018.

Mageuzi hayo yanajumuisha kuondoa vyeo vya Naibu Makatibu Wakuu watatu na kupunguza idadi ya Wakurugenzi kutoka 12 hadi 6. Mageuzi haya yataiwezesha Jumuiya kuokoa kiasi cha Pauni milioni 3 kwa mwaka. Mageuzi mengine ni ya kuanzisha nafasi tano za Maafisa Waandamizi kutoka maeneo ya kijiografia ya Jumuiya ya Madola kwa maana ya Afrika, Ulaya na Amerika, Karibeani, Asia na Pacific Kusini. Nafasi hizi zitaziba zile za Naibu Makatibu Wakuu.

Wakati wa ziara hiyo, Mhe. Scotland atakutana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa mazungumzo tarehe 11 Agosti, 2017, Ikulu, Dar es Salaam.

Aidha, Mhe. Scotland ataonana na Mawaziri mbalimbali kwa nyakati tofauti ikiwa ni pamoja na Mhe. Prof. Joyce Ndalichako, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. January Makamba, Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira.

Mhe. Scotland na ujumbe wake wataondoka nchini tarehe 12 Agosti, 2017 kuelekea Msumbiji.

Historia fupi kuhusu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Mhe. Patricia Scotland alichaguliwa kwenye nafasi hiyo mwezi Novemba, 2015 wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali (CHOGM) uliofanyika nchini Malta. Kabla ya kuchaguliwa kwake Jumuiya hiyo iliongozwa na Bw. Kamalesh Sharma ambaye alishikilia nafasi hiyo kuanzia mwaka 2008 hadi 2016.

Jumuiya ya Madola

Jumuiya ya Madola ni Umoja ulioanzishwa mwanzoni mwa karne ya 20. Jumuiya hiyo inajumuisha Uingereza pamoja na nchi ambazo zilikuwa koloni la Uingereza. Uanachama wa Jumuiya hiyo kwa sasa hauzingatii kigezo cha koloni hivyo nchi yoyyote inaweza kujiunga na Jumuiya ya Madola kama itapenda. Malkia ndiye Kiongozi Mkuu wa Jumuiya ya Madola.

Jukumu kubwa la Jumuiya ya Madola ni kuhakikisha nchi wanachama zinajikwamua kisiasa, kiuchumi na kijamii kwa kutumia jukwaa la majadiliano, makubaliano na utekelezaji.

Ushiriki wa Tanzania katika Jumuiya ya Madola


Jumuiya ya Madola inajumuisha nchi 52 Tanzania ikiwa ni mwanachama wa Jumuiya hiyo tangu mwaka 1961. Tangu kujiunga kwake, Tanzania imewahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya Jumuiya hiyo. Miongoni mwa nafasi hizo ni ile ya Uenyekiti wa Kundi la Mawaziri la Utekelezaji la Jumuiya ya Madola (Commonwealth Ministrial Action Group (CMAG). Kundi hili lilijumuisha Mawaziri tisa ambao walipewa jukumu la kusimamia misingi mikuu ya Jumuiya ya Madola. Tanzania ilishikilia nafasi hii kuanzia mwaka 2013 hadi 2015.

Pia Tanzania ni mjumbe kwenye Bunge la Jumuiya ya Madola (CPA). Kutokana na mchango mkubwa wa Tanzania kwenye Jumuiya ya Madola, kuanzia mwaka 2007 hadi 2014 Marehemu Dkt. William F. Shija aliteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Bunge hilo. Aidha, mwaka 2009 Tanzania ilikuwa mwenyeji wa Mkutano wa 55 wa Bunge la Jumuiya ya Madola uliofanyika Jijini Arusha.

Aidha, miongoni mwa faida ambazo Tanzania imepata kutokana na kujiunga na Jumuiya hii ni pamoja na kukuza biashara na uwekezaji na nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola zikiwemo Uingereza, India, Kenya na Afrika Kusini. Nchi hizi ni miongoni mwa  nchi  zilizowekeza zaidi kwa biashara nchini Tanzania.

Tanzania imenufaika kwenye masuala ya  Teknolojia kupitia Taasisi ya Commonwealth of Learning (COL) ambayo inahamasisha mafunzo ya wazi na ya mbali miongoni mwa nchi wanachama. Pia Jumuiya ya Madola ina  mchango mkubwa kwenye mageuzi katika  Sekta ya Umma na utoaji mafunzo, kozi na misaada mbalimbali ya kiufundi kupitia Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola na Mfuko wa ushirikiano wa Kiufundi wa  Jumuiya ya Madola (CFTC).

Tanzania imekuwa mshiriki mzuri wa michezo maarufu ya Jumuiya ya Madola ambayo inalenga kuhamasisha ushirikiano na urafiki miongoni mwa nchi wanachama. Itakumbukwa kuwa mwaka 1974 Bw. Filbert Bayi alivunja rekodi  kwa kukimbia mita 1,500 mashindano yaliyofanyika huko Christchurch, New Zealand. 

Michezo ya Madola hufanyika kila baada ya miaka minne. Tanzania inajiandaa kushiriki kwenye michezo  ya Madola itakayofanyika mwezi Aprili, 2018 huko Gold Coast, Australia.

-Mwisho-

Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dar es Salaam

09 Agosti, 2017

Monday, August 7, 2017

Hafla ya Uwekaji wa Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Bomba la Mafuta

 TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Hafla ya Uwekaji wa Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Bomba la Mafuta

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ameitaja tarehe ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa bomba la kusafirisha mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi bandari ya Tanga nchini Tanzania kuwa ni siku ya maendeleo ya kweli kwa Tanzania na Uganda na nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa ujumla.

Uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa bomba hilo litakalokuwa na urefu wa kilomita 1445 litakalogharimu takribani Shilingi trilioni 8 za Tanzania ulifanywa na Rais Magufuli na Rais wa Uganda, Mhe. Yoweri Kaguta Museveni katika eneo la Chongoleani mkoani Tanga siku ya Jumamosi tarehe 05 Agosti 2017 na kushuhudiwa na umati mkubwa wa watu wakiwemo viongozi wakuu wa Serikali na vyama vya siasa kutoka pande zote mbili.

Rais Magufuli alieleza kuwa hadi kufikia hatua ya uwekaji wa jiwe la msingi wa ujenzi wa bomba hilo, vikwazo vingi vilijitokeza, hivyo anamshukuru Rais Museveni kwa kuipa kipaumbele Tanzania kwa kuwa bomba hilo lingeweza kupita mahali pengine ambako umbali ungekuwa mfupi kwa zaidi ya kilomita 500.

Aliendelea kueleza kuwa licha ya Tanzania kutoa vivutio vingi kwa Uganda ikwemo kusamehe baadhi ya kodi kama za ongezeko la thamani lakini ujenzi wa bomba hilo utakuwa na manufaa makubwa kwaTanzania katika kipindi cha ujenzi unaotarajiwa kuanza mwezi Januari 2018 na kukamilika mwaka 2020 na baada ya kukamilika kwa ujenzi huo.

"Tutapata mamilioni ya Dola yatakayotokana na ada ya usafirishaji ambayo ni Dola 12.5 kwa pipa moja na inakadiriwa kwa siku yatasafirishwa mapipa 216,000". Rais Magufuli alisema.

Manufaa mengine ni pamoja na ajira ambapo inakadiriwa watu kati ya elf 10 hadi 15 watapata ajira za kudumu bomba litakapokamilika na ajira za muda mfupi za watu zaidi ya elf 30 katika kipindi cha ujenzi.

Aidha, bomba litakuza biashara ya bidhaa mbalimbali ikiwemo saruji na vifaa vingine vitakavyotumika katika ujenzi wa bomba,  ujenzi wa nyumba za kupangisha na kuchochea ujenzi wa viwanda ambavyo malighafi zake zinatokana na mabaki yanayotokana na usafishaji wa mafuta kama vile viwanda vya mbolea. 

Vile vile, bomba linatarajiwa kupunguza gharama za uendeshaji katika sekta ya anga kutokana na unafuu wa mafuta na linakuja wakati mwafaka kwa kuwa Tanzania imeshaanza kulifufua shirika lake la ndege na Uganda ipo mbioni pia kulifufua shirika lake. Imeelezwa kuwa moja ya sababu ya Mashirika ya ndege ya nchi za Mashariki ya Kati kufanya vizuri kibiashara inatokana na unafuu wa mafuta ya ndege.

Mhe. Rais alitoa wito kwa wakandarasi watakaojenga bomba hilo kuharakisha  ujenzi ili uweze kukamilika kabla ya muda uliopangwa wa miaka mitatu.

"Kuna sababu gani ya kutumia muda wote huo wakati fedha zipo na wakandarasi wote mnatoka nchi kubwa zilizopiga hatua ya maendeleo, Tuoeni zabuni kwa wakandarasi wengini (sub contractors) ili ujenzi ukamilike kwa muda mfupi". Rais Magufuli alishauri. 

Wakandarasi watatu, wawili kutoka Ufaransa, Total na Cnooc na mwingine kutoka Uingereza, Tullow Oil kwa pamoja watajenga bomba hilo.

Mhe. Magufuli alibainisha kuwa Tanzania na Uganda zipo katika mazungumzo ili wataalamu wa Kiganda waliogundua mafuta hayo mwaka 2006 waje Tanzania kufanya utafiti kwenye maziwa ya Tanganyika na Eyasi ambayo yana viashiria vya kuwepo kwa mafuta.

Rais Magufuli alihitimisha hotuba yake kwa kumuhakikishia Mhe. Museveni kuwa Tanzania ni nchi iliyokamilika kiulinzi, hivyo Waganda wasiwe na wasi wasi kuhusu usalama wa bomba hilo ambalo litapita katika mikoa 8 ya Tanzania , wilaya 24 na vijiji 124.

Kwa upande wake, Rais Museveni aliishukuru Tanzania kwa kutoa vivutio vingi ili ujenzi wa bomba hilo uendelee kwani bila ya hivyo mafuta hayo hayatakuwa na faida ukizingatia bei ya mafuta katika soko la dunia imeshuka.

Alisema sababu kubwa ya bara la Afrika kuwa masikini hadi leo ni kutumia bidhaa isiyozalisha na kuzalisha bidhaa isiyotumia. 

Kwa mujibu ya takwimu alizotoa, nchi za Afrika Mashariki zinaagiza bidhaa zenye thamani ya Dola za Marekani milioni 33 na inauza bidhaa zenye thamani ya Dola milioni 13.8 tu kwa mwaka. Fedha hizo zinafaidisha nchi zilioendelea kuimarisha uchumi wao na kuziacha nchi za Afrika kubaki masikini.

Kutokana na hali hiyo, Rais Museveni alizisihi nchi za Afrika zibadilishe mfumo wa uchumi kwa kujenga viwanda na kuuziana bidhaa. Hivyo, ana matumaini makubwa  kuwa ujenzi wa bomba hilo litaongeza kipato kitakachotumika kuchochea mabadiliko ya kiuchumi ndani ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Martine Shigella aliwahakikishia Marais wawili kuwa mkoa umejipanga kutoa huduma stahiki kwa wageni wote watakaoingia mkoani humo kwa ajili ya ujenzi wa bomba hilo.

"Tumejipanga kuzalisha chakula cha kutosha na tumetenga maeneo ya kujenga nyumba za makazi, hivyo wawekezaji jitokezeni kuchukua maeneo hayo". Mkuu wa Mkoa alihimiza. Aliwasihi watu wa Tanga wasomeshe watoto wao ili waweze kuwa na vigezo vya kupata ajira zitakazotokana na ujenzi wa bomba hilo.

Alihitimisha kwa kumuomba Rais Magufuli asaidie kuimarisha bandari ya Tanga angalau iwe na kina cha mita 12 ili iweze kuhudumia meli zote zitakazotumika kubeba shehena za vifaa vya kujengea bomba la mafuta.


 -Mwisho-
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Tanga, 05 Agosti, 2017.

Viongozi Wakuu wa Serikali wakiwa katika mstari kwa ajili ya kuwapokea Waheshimiwa Marais wa Tanzania na Uganda kwenye viwanja vilivyofanyika hafla ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi Tanga nchini Tanzania. Mwenye ushungi ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan na Madam Balozi Grace Martin, Mkuu wa Itifaki

Rais wa Jamhuri ya Muungno wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli (kulia) akiwa kwenye Meza Kuu na Mgeni wake, Rais wa Uganda, Mhe. Yoweri Kaguta Museveni (katikati) na Makamu wa Rais, Mama Samia Hassan Suluhu.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Martine Shigella akitoa neno la ukaribisho kwa Marais wa Uganda na Tanzania na wageni waalikwa waliohudhuria hafla ya uwekaji jiwe la msingi la ujenzi wa bomba la mafuta iliyofanyika katika eneo la Chongoleani mkoani Tanga tarehe 05 Agosti 2015.

Bw. Guy Mourice, Rais wa Kampuni ya Total na Msimamizi  wa ujenzi wa bomba hilo akitoa maelezo mafupi kuhusu ujenzi wa bomba hilo utaskavyotekelezwa.

Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi, Mhe. Abdulrahman Kinana akiwasalimia viongozi na wananchi waliofurika viwanjani hapo kushuhudia hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa bomba la mafuta.

AWaziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa akiwasalimia wananchi.

Makamu wa Rais, Mhe. Samia Hassan Suluhu akiwasalimia wananchi.

Rais wa Jamhuri ya Uganda akisoma hotuba yake kwenye hafla ya uwekasji wa jiwe las msingi la ujenzi wa bomba ls mafuta ghafi kutoka Uganda hadi Tanga.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli akisoma hotuba katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi wa ujenzi wa bomba lamfuta kutoka Uganda hadi Tanzania.

Mkuu wa Mkoa wa Dar Es Salaam, Mhe. Paul Makonda akipeana Mkono na Bw. Ruge Mutahaba wa Cloud FM. Wawili hao walitakiwa  na Mhe. Rais Magufuli kumaliza tofauti zao.

Viongozi mbalimbali wakiwemo Waheshimiwa Mawaziri, Naibu Mawaziri, Wakuu wa Mikoa, Wilaya na Wabunge walioshiriki hafla hiyo.

Sehemu ya umati wa wananchi waliohudhuria hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi.

Burdani ndani ya viwanja vya Chongoleani.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli (kulia) na Rais wa Jamhuri ya Uganda, Mhe. Yoweri Kaguta Museveni wakiweka jiwe la Msingi kuashiria uzinduzi wa ujenzi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Hoima, Uganda hadi Tanga, Tanzania.

Waheshimiwa Marasi wakishikana mikono baada ya kuweka jiwe la msingi.

Thursday, August 3, 2017

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje akutana kwa mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Kifaru

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Susan Kolimba akizungumza na Dkt. Viktor Korcek, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Kifaru ambaye pia ana nia ya kuwa Mwakilishi wa Heshima wa Tanzania katika Jamhuri ya Czech.
Mazungumzo yakiendelea
Dkt. Korcek nae akimweleza jambo Dkt. Kolimba.
Picha ya pamoja