Wednesday, September 15, 2021

WAKAZI WA MARA WANUFAIKA NA MAADHIMISHO YA "SIKU YA MARA"

Septemba 15 kila mwaka Tanzania na Kenya hufanya maadhimisho ya Siku ya Mara (Mara Day), ambayo pia huusisha maonesho ya bidhaa mbalimbali sambamba na utoaji elimu inayolenga kuhimiza umuhimu wa kuhifadhi mazingira ya Bonde la Mto Mara. 

Sherehe za maadhimisho haya ambayo hufanyika kwa zamu baina ya Tanzania na Kenya, mwaka huu 2021, Maadhimisho ya 10 ya Siku ya Mara yanafanyika katika Wilaya ya Tarime, mkoani Mara. Kama ilivyo ada ya maadhimisho haya kuendeshwa kwa ushirikiano baina ya pande mbili (Tanzania na Kenya) mwaka huu pia kumekuwa na ushiriki wa pande zote mbili. 

Madhimisho ya Kumi ya Siku ya Mara mwaka huu 2021 yanaongozwa na Kauli Mbiu isemayo “Tuhifadhi Mto Mara kwa Utalii na Uchumi Endelevu” 

Akizungungumza kwenye maadhimisho hayo Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso ametoa wito kwa Mkuu wa Mkoa, Wakuu wa Wilaya, Wenyeviti wa Halmashauri pamoja na Wenyeviti wa Vijiji kuhakikisha wanashughulikia kwa mtazamo chanya suala la utunzaji wa mazingira na vyanzo vya maji katika maeneo yetu.

“Suala la kuhifadhi ya mazingira ya Bonde la Mto Mara ikiwa ni pamoja na vyanzo vya maji limekua likitiliwa mkazo na Serikali ili kuhakikisha kuwa maji yaliyopo yanahifadhiwa na kutunzwa kwa mujibu wa sheria. Wito wangu kwenu ni kwamba tuendeleze ushirikiano katika uhifadhi wa mazingira ili pawepo na vyanzo vya maji vya uhakika, vyenye maji ya kutosha na yenye ubora wakati wote kwa ajili ya maendeleo” alisema Mhe. Aweso

Akizungumza kwenye ufunguzi wa maadhimisho hayo Mkuu wa Wilaya ya Tarime ambaye pia ni Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mara Mheshimiwa Lt. Col. Michael Mangwela Mtenjela amebainisha baadhi ya mafanikio yaliyofikiwa tokea kuanza kwa Maadhimisho haya mwaka 2012 kuwa ni pamoja na; ongezeko la upandaji miti, ongezeko la watalii, kuongezeka kwa ushirikiano baina ya jamii za pande zote mbili zinazozunguka Bonde la Mto Mara na uwekwaji wa mawe ya kuonesha mipaka (bikoni) katika eneo la Bonde. 

“Mwaka huu Idadi ya miti na vigingi imeongezeka ikilinganishwa na mwaka 2020 ambapo miti 2600 ilipandwa pamoja na vigingi 20 katika Wilaya ya Butiama. Ongezeko hili linatokana na juhudi za makusudi zinazochukuliwa na Mkoa wa Mara katika kuhifadhi ikolojia ya Bonde la Mto Mara na Mkoa mzima wa Mara” alieleza Mheshimiwa Lt.Col. Mtenjela.

Kwa upande wake Balozi wa Tanzania nchini Kenya Mhe. Dkt. John Simbachawene ameeleza kuwa Mara Day ni jukwaa linatoa fursa nzuri ya utetezi na ushirikiano kati ya watendaji wa serikali, asasi za kiraia, sekta binafsi, washirika wa maendeleo na mashirika yasiyo ya kiserikali katika mashirikiano ya kuimarisha usimamizi na maendeleo ya rasilimali za maji katika Bonde la Mto Mara. 

Katika kuadhimisha Siku ya Mto Mara mwaka 2021, sambamba na shughuli zingine zilizokuwa zikiendelea Mkoa wa Mara umepanda miti 13,000 na kuweka vigingi 70 katika vijiji vya Mrito na Kerende vilivyopo wilayani ya Tarime.

Akizungumza katika hafla ya ufunguzi wa madhimisho hayo Bi. Bhoke Mwita amkazi wa Tarime ameelezea kuridhishwa kwake na mafanikio aliyoyaona tokea kuanzishwa kwa maadhimisho ya Siku ya Mara. Ambapo ameeleza kuwa hapo awali pamoja na kunufaika na Mto Mara hawakutambua umuhimu wa kutunza mazingira yanayo uzunguka hivyo kusababisha uharibifu wa Ikolojia ya Bonde, tofauti na ilivyo sasa ambapo kupitia Maadhimisho haya wamejifunza na kuhamasika kutunza mazingira ya Bonde la Mto Mara. 

Tunazishukuru sana Serikali zetu ya Tanzania na Kenya kwa kuridhia kufanyika kwa Maadhimisho haya, licha kupata fursa ya kushiriki maonesho tunapata elimu kubwa kuhusu umuhimu wa kulinda Bonde la Mto Mara, sasa tumefikia mahali ambapo sisi wenyewe tunakuwa mlinzi dhidi ya kila mmoja kuzuia uharibifu katika mazingira ya Bonde la Mto. Kwa mafanikio tuanayoendelea kuyaona na kunufaika nayo hatuna budi kuendelea kuhifadhi mazingira kwa ajili ya mandeleo yetu wenyewe. Alisema Bi. Bhoke Mwita

Mto Mara ambao ni eneo muhimu kwa maendeleo ya kiuchumi pamoja na baioanuai zilizopo unaanzia katika chemchem ya Enapuyapui iliyopo kwenye misitu ya Milima ya Mau nchini Kenya, ambapo maji ya Mto huo hutiririka kupitia pori la akiba la Hifadhi ya Taifa ya Maasai-Mara kwa upande wa Kenya na hatimaye katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti (SENAPA) kwa upande wa Tanzania, kabla ya kumwaga maji yake katika Ziwa Victoria. Mto huu unapita katika Wilaya nne kwa upande wa Tanzania ambazo ni Serengeti, Tarime, Rorya na Butiama.

Maadhimisho haya yanatokana na Mkutano wa 10 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Bonde la Ziwa Victoria lililoamua kuwe na Maadhimisho ya Siku ya Mara kila mwaka ifikapo tarehe 15 Septemba katika Mkutano uliofanyika Mei 4,2021 jijini Kigali, Rwanda ili kuhamasisha na kutoa elimu kwa wadau juu ya utunzaji wa mazingira na rasilimali maji katika Bonde la Mto Mara.
Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso (Mb) akisalimiana na Bw. Eliabi Chodota Kaimu Mkurugenzi wa Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Kijamii katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, wakati alipowasili katika viwaja vya Chuo cha Uwalimu cha Tarime kwenye Maadhimisho ya 10 ya Siku ya Mara
Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso (Mb) akisaini kitabu cha wageni kwenye Maadhimisho ya 10 ya Siku ya Mara yaliyofanyika Wilayani Tarime, Musoma
Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso (wapili kulia) akiwa ameambatana na viongozi na watendaji mbalimbali wa Serikali wakati akielekea kuona bidhaa mbalimbali za wafanyabiashara walioshiriki maonesho ya Maadhimisho ya Siku ya Mara
Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso (Mb) akisisitiza jambo wakati akizungumza na Wananchi wa Tarime (hawapo pichani) kwenye kilele cha Maadhimisho ya 10 ya Siku ya Mara


Balozi wa Tanzania nchini Kenya Mhe. Dkt. John Simbachawene akizungumza na wananchi waliojitokeza kushiriki kilele cha Maadhimisho ya 10 ya Siku ya Mara yaliyofanyika katika viwaja vya Chuo cha Uwalimu cha Tarime, Musoma.
Balozi wa Tanzania nchini Kenya Mhe. Dkt. John Simbachawene (wakwanza kulia) akifuatilia Maadhimisho ya 10 ya Siku ya Mara yaliyokuwa yakiendelea katika viwaja vya Chuo cha Uwalimu cha Tarime, Musoma
Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso (Mb) akifuatilia maelezo kuhusu huduma mbalimbali za Mamlaka ya Kodi Tanzania (TRA) alipotembelea banda la Mamlaka hiyo kwenye kilele cha Maadhimisho ya 10 ya Siku ya Mara
Mkuu wa Wilaya ya Tarime Mhe. Lt. Col. Michael Mangwela Mtenjela akizungumza na wananchi waliojitokeza kwenye ufunguzi wa Maadhimisho ya 10 ya Siku ya Mara yaliyofanyika katika viwaja vya Chuo cha Uwalimu cha Tarime, Musoma. 
Kaimu Mkurugenzi wa Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Kijamii Bw. Eliabi Chodota (wakwanza) katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akifuatilia matukio mbalimbali yaliyokuwa yakiendela kwenye kilele cha Maadhimisho ya 10 ya Siku ya Mara yaliyofanyika katika viwanja vya Chuo cha Uwalimu cha Tarime, Musoma

Meza Kuu wakifuatilia matukio mbalimbali yaliyokuwa yakiendela kwenye Maadhimisho ya 10 ya Siku ya Mara yaliyofanyika katika viwanja vya Chuo cha Uwalimu cha Tarime, Musoma

Waziri mwenye Dhamana ya Usimamizi wa Rasilimali Maji Mhe. Job Kiyiapi kutoka Kenya akizungumza na wananchi (hawapo pichani) waliojitokeza kushiriki kilele cha Maadhimisho ya 10 ya Siku ya Mara yaliyofanyika katika viwaja vya Chuo cha Uwalimu cha Tarime, Musoma.
Meza Kuu wakijumuika kuchea na kikundi cha kwaya kilichokuwa kikitoa burudani kwenye Maadhimisho ya 10 ya Siku ya Mara yaliyofanyika katika viwanja vya Chuo cha Uwalimu cha Tarime, Musoma

BALOZI FATMA RAJAB AFUNGUA WARSHA YA KITAIFA YA UWEKAJI GHARAMA KATIKA MPANGO MKAKATI ELEKEZI WA MAENDELEO WA KANDA WA SADC

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab amefungua warsha kwa maafisa wa Serikali wanaoshiriki zoezi la uwekaji gharama katika mpango mkakati elekezi wa maendeleo wa kanda wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Africa SADC – RISDP ( Regional Indicative Strategic Development Plan 2020 - 2030).

Warsha hiyo inayoratibiwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambaye pia ni mratibu wa masuala ya kikanda kitaifa imeanza leo tarehe 15 hadi 22 Septemba, 2021 mjini Morogoro. Pia imehudhuriwa na maafisa kutoka wizara zinazosimamia maeneo/sekta za vipaumbele zilizoainishwa katika Mkataba wa SADC wa mwaka 1992.

Maeneo ya vipaumbele ni pamoja na; Amani, Usalama na Utawala Bora; Maendeleo ya Viwanda na Mtangamano wa Masoko; Maendeleo ya Miundombinu katika kusaidia Mtangamano wa Kikanda; Maendeleo ya Jamii na Watu; Jinsia, Vijana, Mazingira na Mabadiliko ya Tabia nchi na Usimamizi wa hatari ya Maafa; na Usimamizi wa kimkakati wa Mpango Mkakati Elekezi wa Maendeleo wa Kanda.

“Nimeelezwa kuwa Warsha hii inajumuisha sekta mbalimbali za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hasa zile zinazohusika moja kwa moja na utekelezaji wa itifaki na sera mbalimbali za Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika. Ni faraja kuona mpo katika ari kubwa kwa ajili ya kuikamilisha kazi hii muhimu, hivyo mkaweke mbele maslahi ya Taifa wakati wa kupanga gharama kwenye maeneo husika.” Alisema Balozi Fatma

Lengo kuu la mpango huu ni kuimarisha ushirikiano katika Kanda kwa ajili ya kuharakisha juhudi za kupunguza umaskini na hatimaye kufikia malengo ya maendeleo ya kiuchumi na yasiyo ya kiuchumi. Mpango huu mpya umekuja baada ya ule wa awali wa mwaka 2015 – 2020 kumalizika muda wake. Kimsingi mpango huu mpya umetokana na Dira ya SADC ya mwaka 2020 - 2030 (Vision 2050)

Kadhalika, Balozi Fatma alitumia fursa hiyo kuwashukuru Shirika la Ujerumani (GIZ) kwa kukubali kufadhili shughuli hii na akawaahidi kuwa Serikali itaendelea kuwapa ushirikiano kwenye programu na miradi mbalimbali inayotekelezwa nchini na kikanda.

Zoezi hili linafanyika kufuatia maelekezo ya Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Mendeleo kusini mwa Africa (SADC) uliofanyika mwezi Agosti 2021 Lilongwe, Malawi. Mkutano huo ulizitaka nchi wanachama kukamilisha zoezi hilo na kuwasilisha maoni yao kwa Sekretarieti ya SADC kabla ya tarehe 30 Septemba 2021.


Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab akizungumza wakati wa Hafla ya Ufunguzi wa Warsha ya Kitaifa ya Uwekaji Gharama katika mkakati elekezi wa maendeleo wa kanda wa SADC - RISDP 2020 -2030 inayofanyika kuanzia tarehe 15 hadi 22 Septemba 2021 mjini Morogoro
Mshauri Elekezi ambaye pia ni Kaimu Mkuu wa Chuo cha Takwimu Mashariki mwa Afrika, Dkt. Tumaini Katunzi akifuatilia hotuba ya ufunguzi.

Balozi Fatma akiteta jambo na Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Agnes Kayola na Afisa Mwandamizi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Khalifa Kondo.

Afisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Joshua Mponela akielezea ratiba ya warsha kwa washiriki wakati wa ufunguzi.

Washiriki wakifuatilia ufunguzi wa warsha hiyo.

Washiriki wakifuatilia ufunguzi wa warsha.

Washiriki wakifuatilia ufunguzi wa warsha.

 

TPFS YARIDHISHWA NA JUHUDI ZA SERIKALI ZA KUKUZA SEKTA BINAFSI

 Na Mwandishi wetu, Dar

Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) imekiri uwepo wa ongezeko la biashara kati ya Tanzania na nchi za Ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Ushoroba wa kusini zikiwemo nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) tangu Serikali ya awamu ya sita ilipoingia madarakani.

Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) Bi. Angelina Ngalula amesema kuwa ukuaji wa biashara kati ya Tanzania na nchi jirani zikiwemo Kenya, Burundi na Uganda umeongezeka na kwamba ushirikiano kati ya Tanzania na Mataifa hayo umezidi kuimarika ukiashiria kukua kwa diplomasia ya uchumi.

“Sasa hivi ukiangali ukuaji wa biashara chini ya uongozi wa Serikali ya awamu ya sita, Serikali inaishirikisha ipasavyo Sekta binafsi katika kukuza na kuendeleza biashara na uwekezaji nchini,” amesema Bi. Ngalua

Ameongeza kuwa ushirikiano ambao Serikali imekuwa ikiutoa kwa sekta binafsi umechangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa kiwango cha biashara kati ya Tanzania na Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki pamoja na ushoroba wa kusini ikihusisha nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).

Bi. Ngalula amepongeza hatua ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan ya kuamua kuambatana na wawekezaji na wafanyabiashara kutoka katika Taasisi ya Sekta Binafsi kwa kuwa hatua hiyo imesaidia kuwakutanisha na kuwaunganisha na wenzao wa Mataifa mengine tofauti na nyakati zilizopita ambapo kila mfanyabiashara alijitafutia fursa peke yake.

Kwa uapnde wake Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (Mb) ameihakikishia Taasisi ya Sekta Binafsi ushirikiano mkubwa kutoka Serikalini kwa kuwa Serikali inaamini uwepo wa sekta binafsi imara ni kichocheo kikubwa cha ukuaji wa uchumi imara wa Nchi.

Balozi Mulamula ameitaka TPSF kuhakikisha kuwa inakuwa na kanzi data ili kurahisisha azma ya Serikali ya kuiunganisha sekta hiyo na wafanyabiashara pamoja na wawekezaji kutoka katika mataifa mengine ulimwenguni.

Katika tukio jingine, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula amekutana kwa mazungumzo na Mkurugenzi anayeshughulikia masuala ya maendeleo ya uchumi Dkt. Stefan Oswald aliyefuatana na Mkurugenzi anayeshughulikia masuala ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje wa Ujerumani kwa lengo la kuzungumzia masuala mbalimbali ikiwemo ushirikiano wa kidiplomasia na maendeleo ya Uchumi.

Dkt. Oswald amemuambia Balozi Mulamula kuwa Tanzania imekuwa ni Nchi ya kwanza kwa viongozi hao wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Ujerumani kuifanya na hiyo imetokana na ishara ya  mabadiliko ya kidiplomasia na ushirikiano wa Maendeleo na Mataifa mengine duniani iliyooneshwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Ameongeza kuwa mazungumzo kati ya Mhe. Samia Suluhu Hassan na Kansela wa Ujerumani Mhe Angela Merkel ambayo yalilenga kutoa kipaumbele cha uwepo wa mazingira wezeshi ya biashara na uwekezaji yamekuwa kichocheo cha Viongozi hao kufanya ziara hapa nchini.

Dkt.Stefan amesema Ujerumani iko tayari kushirikiana na Tanzania pamoja na Nchi za Afrika kuzisaidia kuimarisha uchumi kutokana na kuathiriwa na UVIKO 19.

Pamoja na mambo mengine, mazungumzo ya viongozi hao yaligusia masuala la ulinzi na usalama katika ukanda wa maziwa makuu na kutafuta suluhisho la kudumu kwa wakimbizi wa Burundi.   

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata  akiwa katika mazungumzo na Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) Bi. Angelina Ngalula katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Mazungumzo baina ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata  akiwa katika mazungumzo na Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) Bi. Angelina Ngalula yakiendelea 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula akizungumza na Mkurugenzi anayeshughulikia masuala ya maendeleo ya uchumi Dkt. Stefan Oswald aliyefuatana na Mkurugenzi anayeshughulikia masuala ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje wa Ujerumani  


Mazungumzo baina ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula na Mkurugenzi anayeshughulikia masuala ya maendeleo ya uchumi Dkt. Stefan Oswald yakiendelea



UFARANSA KIUANZISHA SAFARI YA NDEGE KUJA ZANZIBAR

Na Mwandishi Wetu, Dar

Serikali ya Ufaransa kupitia Shirika lake la ndege ‘Fance Airline’ inategemea kuanzisha safari mpya ya ndege kutoka Ufaransa moja kwa moja hadi Zanzibar kuanzia 19 Oktoba 2021.

Hayo yamebainishwa na Balozi Mteule wa Ufaransa hapa nchini Mhe. Nabil Hajlaouvi wakati alipokuwa anawasilisha nakala ya Hati za utambulisho kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Balozi Nabil amemhakikishia Mhe. Waziri Mulamula kuwa Airfance inaanzisha safari ya ndege ya moja kwa moja kutoka Ufaransa kuja Zanzibar –Tanzania ambapo katika uzinduzi wa safari hiyo utaongozwa na Waziri wa mambo ya Nje uwa Ufaransa tarehe 19 Oktoba 2021.

Pia Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki amepokea nakala ya Hati za Utambulisho kutoka kwa Balozi mteule wa Somalia hapa nchini mhe. Zahra Ali Hassan ambapo pamoja na mambo mengine, Balozi Zahra amemhakikishia Waziri Mulamula kuwa Somalia itaendelea kuhakikisha kuwa mahusiano yake na Tanzania yanazidi kuimarika.

Katika tukio jingine, Balozi Mulamula amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Umaja wa Ulaya hapa nchini mhe. Manfredo Fanti wamejadiliana masuala mbalimbali ya ushirikiano katika sekta mbalimbali ikiwemo miundombinu pamoja ufadhili wa miradi mbalimbali ya maendeleo hapa nchini.

Balozi Mulamula pia amekutana na kufanya mazungumzo baadhi ya Mabalozi wa nchi za Nordic hapa nchini ambao ni Balozi wa Denmark, hapa nchini Mhe. Mette Norgaard Dissing-Spandet, Balozi wa Norway hapa nchini, Mhe. Elisabeth Jacobsen, Balozi wa Sweden hapa nchini Mhe. Anders Sjoberg

Kwa upande wake Balozi wa Denmark, hapa nchini Mhe. Mette Norgaard Dissing-Spandet amemhakikishia Waziri Mulamula kuwa pamoja na kuwa Denmark imesema kuwa itafunga ubalozi wake hapa nchini ifikapo 2024, bado nchi hiyo itaendelea kushirikiana kwa karibu na Tanzania na katika kukuza miradi mbalimbali ya maendeleo iliyopo baina ya mataifa hayo kwa maslahi mapana ya pande zote mbili.

Aidha, Waziri Mulamula amekutana kwa mazungumzo na Balozi wa Norway hapa nchini, Mhe. Elisabeth Jacobsen, Balozi wa Sweden hapa nchini Mhe. Anders Sjoberg ambapo viongozi hao wamejadiliana masuala mbalimbali ya kukuza na kuendeleza uhusiano wa kidiplomasia uliopo baina ya Tanzania na mataifa yao.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula akimsikiliza Balozi Mteule wa Ufaransa hapa nchini Mhe. Nabil Hajlaouvi mara baada ya kuwasilisha nakala ya Hati za utambulisho katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam



 

Monday, September 13, 2021

BALOZI SOKOINE AFUNGUA KIKAO KAZI CHA WADAU WA IORA

 

Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Joseph Sokoine akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha wadau wa ndani wa Jumuiya ya Nchi zilizopo kwenye mwambao wa Bahari ya Hindi (IORA) kinachofanyika mjini Zanzibar

 

Katibu Mkuu Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Bw. Aboud S. Jumbe (kushoto) akiwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Joseph Sokoine katika kikao kazi cha wadau wa ndani wa Jumuiya ya Nchi zilizopo kwenye mwambao wa Bahari ya Hindi (IORA) 

Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Agness Kayola akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha wadau wa ndani wa Jumuiya ya Nchi zilizopo kwenye mwambao wa Bahari ya Hindi (IORA)kinachofanyika mjini Zanzibar

Mkurugenzi wa Idara ya Mambo ya Nje Zanzibar Balozi Masoud A Balozi (kushoto) akiwa na Mkurugenzi wa Ushirikiano wa Kikanda Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Agness Kayola wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha wadau wa ndani wa Jumuiya ya Nchi zilizopo kwenye mwambao wa Bahari ya Hindi (IORA) kinachofanyika mjini Zanzibar


Wadau wa ndani wa Jumuiya ya Nchi zilizopo kwenye mwambao wa Bahari ya Hindi (IORA) kutoka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakimsikiliza Mratibu wa masuala ya IORA Tanzania Balozi Agness  Kayola kinachofanyika mjini Zanzibar
Wadau wa ndani wa Jumuiya ya Nchi zilizopo kwenye mwambao wa Bahari ya Hindi (IORA) kutoka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika picha ya Pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Joseph Sokoine baada ya ufunguzi wa kikao kazi chao kinachofanyika mjini Zanzibar


 Na mwandishi wetu, Zanzibar

Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Joseph Sokoine amefungua kikao kazi cha wadau wa ndani wa Jumuiya ya Nchi zilizopo kwenye mwambao wa Bahari ya Hindi (IORA) na kuwataka washiriki wa kikao hicho kutoa msukumo na kipaumbele kwa shughuli zinazoratibiwa na Jumuiya hiyo.

Balozi Sokoine amesema hayo mjini Zanzibar alipokuwa akifungua kikao kazi hicho na kuongeza kuwa kufanya hivyo watakuwa wanalinda kwa vitendo maslahi ya Taifa na kuimarisha ushirikiano uliopo kati ya Tanzania, Nchi Wanachama na Washirika wa Mazungumzo na hivyo kuleta tija kwa Tanzania.

Amesema uanachama wa Tanzania kwenye Jumuiya hiyo ni muhimu kwa maendeleo ya diplomasia, ushirikiano wa kikanda na kimataifa hasa ikizingatiwa kuwa inakutanisha nchi mbalimbali kubwa zilizoendeleana kwamba  Tanzania inaweza kutumia fursa ya Jukwaa la IORA kuimarisha ushirikiano wa nchi na nchi na Washirika wa Mazungumzo ambao wana nguvu kiuchumi na wameendelea kisayani na kiteknolojia.

Amewataka wadau hao kuandaa Mapendekezo ya Miradi yenye sifa na vigezo vya kupatiwa ufadhili kwenye Mfuko Maalum wa Jumuiya ya IORA ili kusaidia kuwezesha, kuhudumia wananchi na kuwezesha  jamii inayozunguka maeneo ya ukanda wa bahari,  uhifadhi wa mazingira ya bahari, uvunaji endelevu wa rasilimali za bahari, uwezeshaji wananchi kiuchumi na maeneo mengine mtambuka yenye tija na maslahi kwa wananchi.

Awali akizungumza katika kikao kazi hicho Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda Balozi Agness Kayola alisema Kikao Kazi hiko kina lengo la kuimarisha ushiriki wa Nchi kwenye Jumuiya ya IORA; kuimarisha ushirikiano wa kisekta kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kuimarisha vikundi kazi ili kuweza kunufaika na uanachama wa Tanzania katika IORA.

Alisema kwa sasa, IORA ina vikundi kazi vinane (8) ambavyo vinafanya kazi chini ya Uratibu wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda - Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Amevitaja vikundi hivyo kuwa ni Ulinzi na Usalama; Biashara na Uwekezaji; Kazi cha Utalii na Utamaduni; Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi; Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ubunifu; Uvuvi; Maafa na Uchumi wa Bluu  

Kikao kazi hicho kinajadili mada zinazohusiana na upatikanaji wa fursa za uwekezaji zilizopo kwenye uchumi wa bluu; sheria, kanuni na taratibu za kuvuna na kuhifadhi rasilimali zilizopo kwenye bahari hususan kwenye ukanda wa bahari kuu; sera na mwongozo wa kufanikisha utekelezaji wa masuala ya uchumi wa bluu pamoja na umuhimu wa kuhifadhi mazingira ya bahari kwa maendeleo endelevu na usalama wa eneo la bahari.

Jumuiya ya Nchi zilizopo kwenye Mwambao wa Bahari ya Hindi inaundwa na nchi 23 ambazo ni Australia,  Afrika Kusini, Bangladesh, Comoro, India, Indonesia, Iran, Kenya, Madagascar, Malaysia, Maldieves, Msumbiji, Mauritius, Oman, Seychelles, Singapore, Somalia, Sri Lanka, Tanzania na Thailand, Umoja wa Falme za Kiarabu, Yemen na Ufaransa kupitia Visiwa vya Reunion ambavyo inavimiliki.

 

 

KAMATI YA BUNGE YA MAMBO YA NJE, ULINZI NA USALAMA (NUU) YAPIGWA MSASA

 Na Mwandishi Wetu, Dar

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeipiga msasa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) kwa kuipatia mafunzo maalumu yenye malengo mbalimbali hasa katika kutetea maslahi ya Taifa.

Pamoja na mambo mengine, mafunzo hayo pia yatajikita  katika masuala ya Itifaki, mawasiliano ya Kidiplomasia, usalama wa Kimtandao na Diplomasia ya Uchumi  ili kuwajengea uwezo wabunge wa kamati hiyo katika kutekeleza majukumu yao ya Kamati na Bunge kikamilifu.

Akifungua mafunzo hayo ya siku tano Jijini Dar es Salaam, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (Mb) amesema kuwa kupitia mafunzo hayo kamati itapata ujuzi juu ya masuala mbalimbali yanayohusu Kamati maslahi ya Taifa, masuala ya Itifaki, mawasiliano ya Kidiplomasia, usalama wa Kimtandao na Diplomasia ya Uchumi  ili kuwajengea uwezo katika kutekeleza majukumu yenu ya Kamati na Bunge kikamilifu.

“Ninayo furaha kuwajulisha kuwa mtapata fursa ya kuelimishwa juu ya mambo Uchumi wa Buluu, mada itakayotolewa na Wizara yenye dhamana ya usimamizi wa uchumi wa buluu kutoka Zanzibar ambayo imepiga hatua katika utekelezaji wake,” Amesema Balozi Mulamula.

Balozi Mulamula ameongeza kuwa, Wizara inaamini kuwa wajumbe wa Kamati na washiriki wote wa mafunzo wataendelea kutumia ujuzi watakaoupata kuishauri Wizara na kuwa Mabalozi wazuri ndani na nje ya Bunge katika kulinda taswira ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Niihakikishie Kamati kuwa Wizara itaendelea kushirikiana nanyi kikamilifu hasa katika kipindi hiki tunapoandaa Sera yetu ya Mambo ya Nje. Tunaamini kuwa ushiriki wenu utaiwezesha nchi yetu kuwa wa sera iliyosheheni masuala muhimu yatakayoiwezesha nchi kunufaika,” ameongeza Balozi Mulamula

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) Bw. Mussa Zungu amesema kamati anayoiongoza inafanya kazi kuwa kwa maslahi mapana ya nchi na kuahidi kuwa vichocheo vya maslahi ya nchi vinalindwa kwa maslahi mapana ya nchi.

“Kamati inatoa ushauri ‘cross-cutting’ kwa maana inagusa kila eneo kwa taifa letu, jambo lolote lile linalohusiana na masuala ya foreign huwa tunashauri, mambo ya ulinzi na usalama…..kwa hiyo inatoa mambo yak echini kwa chini kwa malengo ya kuisaidia serikali,” Amesema Bw. Zungu

Mafunzo haya muhimu kwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) yameandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kushirikiana na Chuo cha Diplomasia na yatafanyika kuanzia tarehe 13 – 17 Septemba 2021 jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) akijadili jambo na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) Bw. Mussa Zungu (Mb) Jijini Dar es Salaam


Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) wakimsikiliza Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (Mb) hayupo pichani

Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Mipango kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bibi. Agnela Nyoni akitoa hotuba kabla ya kumkaribisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula kuongea na wajumbe wa Kamati ya NUU


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula akiwasilisha hotuba ya ufunguzi wa mafunzo maalum ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) Jijini Dar es Salaam


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) Jijini Dar es Salaam



Sunday, September 12, 2021

Shule ya Kimataifa ya Wakimbizi kujengwa Tanzania

Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi, Mhe. Irene Kasyanju (kulia) akiwa katika mazungumzo na Balozi wa Shirika la Elimu, Utamadani na Sayansi la Umoja wa Nchi za Kiarabu, Mhe. Amir Fehri alipotembelea Ofisi ya Ubalozi nchini Uholanzi.

Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi, Mhe. Irene Kasyanju akimpa zawadi ya kahawa ya Tanzania Balozi Fehri

Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi, Mhe. Irene Kasyanju akipokea barua kwa ajili ya kuwasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Shule ya Kimataifa ya Wakimbizi kujngwa Tanzania

 

Balozi wa Shirika la Elimu, Utamaduni na Sayansi la Umoja wa Nchi za Kiarabu (The Arab League Educational, Cultural and Scientific Organization-ALECSO), Mhe. Amir Fehri anakusudia kukutana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan ili aombe ridhaa ya kujenga shule ya kimataifa kwa ajili ya wakimbizi-watoto nchini Tanzania.

Balozi huyo kijana (17) na maarufu duniani, raia wa Tunisia alibainisha hayo alipokutana na kufanya mazungumzo hivi karibuni na Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi, Mhe. Irene Kasyanju.

“Naomba kupatiwa nafasi ya kukutana na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan ili kumuomba nasaha zake (moral support) katika kampeni yangu ya kusambaza salaam ya Amani na Uvumilivu duniani, lakini zaidi kuomba ridhaa ya Mheshimiwa Rais ili niweze kujenga shule yenye hadhi ya kimataifa kwa ajili ya wakimbizi-watoto nchini Tanzania”, Balozi Fehri alisema.

Akielezea kuhusu matarajio yake hayo, alisema, shule hiyo itakuwa inatoa vyeti vya kimataifa ili kuwasaidia watoto hao ama kupata kazi nchini Tanzania au wakirejea katika nchi zao. Aidha, Mhe. Fehri ameomba apatiwe nafasi ya kukutana na wanafunzi wa shule na vyuo mbalimbali nchini Tanzania ili kuwaelimisha kuhusu unyanyasaji unaofanyika mashuleni (bullying) na madhara yake pamoja na njia za kukabiliana na kadhia hiyo.

Kwa upande wake, Balozi Kasyanju alimpongeza Mheshimiwa Fehri kwa jitihada zake thabiti na kumshukuru kwa mapenzi yake juu ya Tanzania, lakini zaidi kwa dhamira yake ya kujenga shule ya wakimbizi nchini Tanzania.

Alisema ni kweli kwamba, Tanzania imekuwa ikipokea wakimbizi kwa zaidi ya miaka 40 na moja ya changamoto kubwa inayojitokeza ni pale ambapo wakimbizi hao wanaporejea katika nchi zao kwa hiari, wanashindwa kujumuika ipasavyo na jamii zao kutokana na ukosefu wa elimu stahiki itakayowawezesha pamoja na mambo mengine kupata ajira. 

 

Balozi Kasyanju alitumia fursa hiyo pia kumpongeza sana Balozi Fehri kwa umaarufu wake duniani kama vile; kuteuliwa kuwa Balozi wa Francophonie ulimwenguni; kuweza kuchapisha vitabu 4 akiwa na umri wa miaka 12, ambavyo vilimpa tuzo 25 za kimataifa katika fasihi kama Sanaa na Barua za Tuzo ya Kimataifa ya Ufaransa, 2014; na kuzungumza lugha saba (Kikurdi-Kifaransa-Kichina-Kiingereza-Kijerumani-Kiarabu-Kilatini) sifa iliyomuwezesha kuwasiliana na viongozi wakubwa duniani. 

 

Balozi Fehri anashirikiana na Rais wa Tume ya Ulaya, kupitia Mfuko wa Amir Fehri (Amir Fehri Foundation) kufungua shule ya kwanza ya Kimataifa huko Mossoul, Iraq. Shule hiyo itakuwa ishara halisi ya elimu kwani itajengwa ndani ya kambi za wakimbizi na itatoa nafasi mpya kwa watoto wote wakimbizi.

 


 

Friday, September 10, 2021

VACANCY ANNOUNCEMENT AT THE OACPS SECRETARIAT


 

MTOTO BARKA SEIF MWENYE KIPAJI CHA MPIRA WA MIGUU ATEMBELEA UBALOZI WA TANZANIA NCHINI UHOLANZI


Mtoto Barka Seif mwenye umri wa miaka 7 ambaye anakipaji cha kucheza mpira wa miguu,akisalimiana na Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi Mhe. Erine Kasyanju alipotembelea ubalozini hapo. Barka Seif yuko Nchini Uholanzi katika klabu ya Ajax.
Mtoto Barka Seif mwenye umri wa miaka 7 ambaye anakipaji cha kucheza mpira wa miguu,akiteta jambo na Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi Mhe. Erine Kasyanju alipotembelea ubalozini hapo. Barka Seif yuko Nchini Uholanzi katika klabu ya Ajax.
Mtoto Barka Seif mwenye umri wa miaka 7 ambaye anakipaji cha kucheza mpira wa miguu,akisaini kitabu cha Wageni katika Ubalozi wa Tanzania Nchini Uholanzi. Barka Seif yuko Nchini Uholanzi katika klabu ya Ajax.

Mtoto Barka Seif mwenye umri wa miaka 7 ambaye anakipaji cha kucheza mpira wa miguu,akiwa katika picha ya pamoja na Balozi wa Tanzania Nchini Uholanzi Mhe. Erine Kasyanju alipotembelea ubalozini hapo. Barka Seif yuko Nchini Uholanzi katika klabu ya Ajax.