Thursday, May 18, 2023

MAMBO YA NJE YAAINISHA FURSA ZINAZOPATIKANA KATIKA MIKUTANO YA KIMATAIFA

Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akijibu swali bungeni jijini Dodoma lililoulizwa na Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Neema Kichiki Lugangira tarehe 18 Mei 2023. 
=================================


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk amefafanua fursa mbalimbali zinazopatikana nchini kupitia ushiriki wa Tanzania katika mikutano ya kimataifa.

Ufafanuzi huo umetolewa Bungeni jijini Dodoma leo tarehe 18 Mei 2023 wakati Mhe. Balozi Mbarouk akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Neema Kichiki Lugangira aliyetaka kujua ni kwa kiasi gani ushiriki wa Tanzania katika Mikutano ya Kimataifa unazingatia upatikanaji wa fursa za kiuchumi na utekelezaji wake.

Mhe. Balozi Mabarouk amesema kuwa, ushiriki wa Tanzania katika Mikutano ya Kimataifa unalenga kupata na kutumia fursa za kiuchumi ikiwa ni pamoja na kupata mitaji, uwekezaji, masoko ya bidhaa na huduma, kukuza utalii, miradi ya kisekta, mikopo ya masharti nafuu na misaada, kujengewa uwezo wa kitaalamu, na upatikanaji wa teknolojia.

Mafanikio mengine ni pamoja na kupata masoko ya bidhaa mbalimbali kama vile mbogamboga, matunda, korosho, nafaka, nguo na mavazi, utalii, malumalu, na bidhaa za kioo. Vilevile, nchi yetu inanufaika kwa kupata wawekezaji katika sekta mbalimbali, ikiwa ni pamoja na utalii, viwanda, kilimo, uvuvi, mifugo, madini, na nishati jadidifu. 

Wednesday, May 17, 2023

MAJALIWA, DKT. KIKWETE WAONGOZA WAOMBOLEZAJI MAZISHI YA MEMBE


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa na Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe. Dkt. Jakaya Kikwete wameongoza mamia ya waombolezaji katika mazishi ya aliyewahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard Membe yaliyofanyika kijijini kweke Rondo, mkoani Lindi yaliyofanyika jana Jumanne tarehe 16 Mei 2023.

Akitoa salamu za Serikali kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Mhe. Majaliwa amesema kifo cha Bernard Membe kimewacha Watanzania na wana Lindi na simanzi, majonzi na huzuni isiyo na kifani.

"Kipekee Mhe. Rais Samia anawashukuru wananchi wote wa Lindi kwa utulivu mliouonesha wakati huu wa msiba wa Mzee Membe wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Lindi kwa kuhakikisha shughuli ya mazishi inaenda vizuri kama ilivyokusudiwa, tunawashukuru na Mwenyezi Mungu aendelee kuwajaalia faraja na uvumilivu katika kipindi hiki cha majonzi mnachopitia," alisema Mhe. Waziri Mkuu.

Mhe. Majaliwa ameongeza kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Mpango naye ameungana na Rais Samia kutoa pole kwa wana Lindi na wana Mtama na amewasihi kuendelea kuyaenzi mazuri yote aliyofanya enzi za uhai wake.

Marehemu Membe atakumbukwa kwa mengi hususani utumishi wake uliotukuka na hasa katika taasisi za Kimataifa alizohudumu wakati wa uhai wake ambapo pia ametumikia Watanzania katika nafasi mbalimbali na kuleta maendeleo. 

“Mchango wa marehemu Membe ni mkubwa hasa katika Jimbo la Mtama," alisema Mhe. Majaliwa.

Mhe. Waziri Mkuu aliongeza kuwa CCM imeelezea kazi nzuri aliyoifanya kwa nafasi mbalimbali alizoshika wakati wa utumishi wake, umahiri na weledi, alikuwa pia na siasa za kistaarabu hakika Chama kimempoteza kiongozi makini na hodari na utumishi uliotikuka, hakika alikuwa kiongozi wa kuigwa.

Kwa upande wake, Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe. Dkt. Jakaya Kikwete alisema alifahamiana na Marehemu Membe muda mrefu na tangu wakati huo wamekuwa wakisaidiana mambo mengi katika kazi na nje ya kazi.

"Alikuwa msaada mkubwa kwangu wakati wote wa utumishi. Alifanya mambo makubwa na alileta medali za kimataifa kutokana na uchapa kazi wake wa kujitoa kwa moyo wake wote," alisema Dkt. Kikwete.

Mhe. Dkt. Kikwete aliongeza kuwa Marehemu alikuwa mwanadiplomasia mahiri na aliyekuwa na mikakati mizuri iliyokuwa na mafanikio makubwa kwa taifa.......na alikuwa msomi mzuri lakini pia alikuwa mcha Mungu," alisisitiza Dkt. Kikwete.

Dkt. Kikwete aliongeza kuwa Marehemu Membe aliweka maslahi ya Tanzania mbele na hakutaka mchezo na maslahi ya taifa lake, alikuwa jasiri, hakika taifa limepoteza moja kati ya watu muhimu.

Akitoa salamu za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.) alisema Marehemu Membe alitoa mchango mkubwa katika Wizara ya Mambo ya Nje na mchango huo utakumbukwa daima.

"Marehemu alikuwa mchapa kazi, mpenda watumishi wake, kiongozi mahiri na mwanadiplomasia nguli....na Kipindi cha uongozi wake, Serikali ilipata medali nyingi za Kimataifa kutokana na uchapa kazi wake," alisema Balozi Mbarouk.

Balozi Mbarouk aliongeza kuwa Marehemu Membe alikuwa ni Mwalimu na mfano bora wa kuigwa, hivyo kwa niaba ya watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki waliopo nchini na Nje ya nchi, Wizara inatoa pole kwa familia, Mungu awajalie uvumilivu wakati huu mgumu wa msiba.

Naye Katibu wa Itikadi na Uenezi wa (NEC), CCM Taifa, ndgu Sophia Mjema alisema Marehemu Membe aliyeshika nafasi mbalimbali kwenye Chama za Ubunge, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa, Mjumbe wa Sektrtariet ya Halmashauri Kuu ya Taifa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Taifa Ali fanya kazi y’a kukitetea Chama chake na daima watamkumbuka kwa hilo. 

"Membe alifanya kazi ya kutetea Chama chake CCM, alikuwa kiongozi makini na hodari, alikuwa mwana CCM kweli kweli, CCM itamkumbuka ndgu Membe kwa uanachama wake na uongozi wake mahiri...aliweza kukitetea Chama chake na kuiunganisha CCM na vyama rafiki katika Dunia," alisema ndugu. Mjema

Ndgu Mjema alisema kuwa CCM itaendelea kumkumbuka kwa kazi nzuri aliyoifanya.

Ibada ya mazishi ya Marehemu Membe ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Zainabu Telack, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mhe. Kanali Mstaafu Ahmed Abbas; Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mhe. Batilda Buriani; Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Anthony Mtaka.

Wengine ni Waziri wa TAMISEMI Mhe. Angela Kairuki, Waziri wa Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwan Kikwete, Mhe. William Lukuvi, Mbunge Isimani; Wakuu wa Wilaya mbalimbali na wakuu wa taasisi za Serikali na viongozi wa vyama mbalimbali vya siasa
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa (Mb.) akiwasili nyumbani kwa Marehemu Bernard Membe kijiji cha Rondo, Lindi ambapo aliongoza mamia ya waombolezaji kwenye  mazishi ya Mwanadiplomasia huyo ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa
Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe. Dkt. Jakaya Kikwete akiwasili nyumbani kwa Marehemu Bernard Membe kijiji cha Rondo, Lindi ambapo aliongoza mamia ya waombolezaji kwenye  mazishi ya Mwanadiplomasia huyo ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.) akitoa salamu za pole kwa familia na waombolezaji muda mfupi baada  ya Ibada ya kumwombea Marehemu Bernard Membe iliyofanyika nyumbani kwake Rondo, Lindi
Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe. Dkt. Jakaya Kikwete na Mke wake Mhe. Salma Kikwete (Mb) wakiweka shada la maua kwenye kaburi la Marehemu Bernard Membe
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.) akiweka udongo kwenye kaburi la Marehemu Bernard Membe
Mwili wa Marehemu Bernard Membe ukiwa katika eneo la ibada maalumu ya kumwombea muda mfupi kabla ya kupunzishwa kwenye nyumba yake ya milele. 
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.) akisalimiana  na baadhi ya waombolezaji alipowasili nyumbani kwa Marehemu Bernard Membe Rondo, Lindi kwenye  mazishi ya Mwanadiplomasia huyo ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa
Mwili wa Marehemu Bernard Membe ukiwa kwenye ibada maalumu ya kumwombea muda mfupi kabla ya kupunzishwa kwenye nyumba yake ya milele. 
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (wa kwanza kushoto) akishiriki Ibada ya kumwombea Marehemu Bernard Membe


Ibada maalumu ya kumwombea Marehemu Bernard Membe ikiendelea nyumbani kwake kijiji cha Rondo, Lindi
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa (Mb.) akitoa salamu za pole kwa familia na waombolezaji muda mfupi baada  ya Ibada ya kumwombea Marehemu Bernard Membe iliyofanyika nyumbani kwake Rondo, Lindi
Naibu Waziri Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk na Mkurugenzi wa Kitengo cha Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi James Bwana wakiweka shada la maua kwenye kaburi la Marehemu Bernard Membe
Sehemu ya waombolezaji walioshiriki kwenye mazishi ya Marehemu Bernard Membe
Sehemu ya Viongozi wakiweka mataji ya maua kwenye kaburi la Marehemu Bernard Membe
Waziri wa TAMISEMI Mhe. Anjela Kairuki (Kulia) na Balozi wa Tanzania nchini China Mhe. Mbelwa Kairuki (katika) wakiwasili nyumbani kwa Marehemu Bernard Membe Kijiji cha Rondo, Lindi kushiriki kwenye  mazishi ya Mwanadiplomasia huyo ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa

Tuesday, May 16, 2023

MCHANGO WA TANZANIA KATIKA MEDANI ZA KIKANDA NA KIMATAIFA UTUNZWE: DKT TAX


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax ametoa wito kwa Taasisi mbalimbali nchini kuendelea kutunza kumbukumbu za historia ya Tanzania na mchango wake katika medani za kikanda na kimataifa ili kuvirithisha vizazi vya sasa na vijavyo.


Kauli hiyo ameitoa jijini Dodoma tarehe 16 Mei 2023 wakati wa hafla fupi ya kikabidhi Machapisho ya Hashim Mbita kwa Taasisi 18 zikiwemo za elimu.


Mhe. Dkt. Tax amesema kuwa, Tanzania ina historia kubwa na nzuri katika medani za kikanda na kimataifa ikiwemo mchango wake katika harakati za ukombozi kusini mwa Afrika hivyo ni jukumu la wadau mbalimbali kuunganisha nguvu ya kutunza kumbukumbu ya historia hiyo nzuri na kuvirithisha vizazi vya sasa na vijavyo.


Ameeleza kuwa, Wizara imeamua kuyakabidhi machapisho hayo kwa Taasisi hizo ili yasaidie kurithisha historia iliyomo kwa vizazi vijavyo, na kujenga hamasa ya uzalendo kwa vizazi vya sasa na vijavyo.


“Wizara inawakabidhi nyinyi machapisho haya kama wawakilishi wa wengi. Tunaamini kupitia Vyuo na Taasisi zenu machapisho haya yatawafikia na kusomwa na Watanzania wengi. Vilevile kupitia machapisho haya historia kuhusu mchango uliotolewa na Tanzania katika harakati za ukombozi wa Kusini mwa Afrika na Afrika kwa ujumla itatunzwa na kukumbukwa daima” amesisitiza Mhe. Dkt. Tax.


Pia ameziomba taasisi hizo kuwa chachu katika kueneza historia adhimu iliyomo kwenye chapisho hilo kwa kuhakikisha linasomwa. “Pamoja na kulitumia chapisho hili kama rejea, na kuhamasisha lisomwe, niwaombe wadau mbalimbali nchini kuona uwezekano wa kuandaa simulizi au filamu ya chapisho ili kuweza kuwafikia watu wengi hususan vijana” alisisitiza Mhe. Dkt. Tax.


Aidha, amefafanua kuwa, Chapisho hilo ambalo pamoja na mambo mengine linaeleza harakati za ukombozi katika nchi za Angola, Namibia, Afrika ya Kusini, Zimbabwe na Msumbiji na mchango wan chi za Tanzania, Zambia, Botswana, Lesotho, Malawi na Swaziland, lilipewa jina la Hashim Mbita kutoka na mchango thabiti na uongozi mahiri wa Hayati Brigedia Generali Hashim Mbita  alioutoa akiwa Katibu Mtendaji wa Kamati ya Kupigania Uhuru Afrika kuanzia mwaka 1972 hadi 1994.


Mhe. Dkt. Tax pia ameshukuru na kupongeza  mchango uliotolewa na Viongozi mbalimbali wa Tanzania akiwemo  Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kamabarage Nyerere kwenye harakati za ukombozi kusini mwa Afrika kwani fikra na mtazamo wake kuhusu umuhimu wa uhuru kwa nchi za Afrika zilifanikisha nchi zote za Afrika kujikomboa dhidi ya ukoloni.


Pia Mhe. Dkt. Tax alitumia fursa hiyo kuipongeza Kampuni ya Kitanzania ya Uchapishaji ya Mkuki na Nyota kwa kuchapisha chapisho hilo kwa umahiri.


“Nawashukuru wadau wote waliofanikisha uchapishaji wa Chapisho la Hashim Mbita ikiwemo Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kwa  kuandaa Chapisho hilo lenye Volume 9 na kwa kutambua mchango wa Tanzania katika harakati za Ukombozi wa Nchi za Kusini mwa Afrika. Pia kipekee  namshukuru Rais Mstaafu wa wa Awamu ya Nne wa Tanzania, Hayati Benjamin William Mkapa kwa kuniagiza nikiwa Katibu Mtendaji wa SADC na kunisisitiza kuhakikisha chapisho hili linakamilika baada mchakato wa awali kusimama ambapo mwaka 2014 kufuatia maagizo hayo, mchakato ulitekelezwa katika  awamu tatu na kukamilika mwaka 2020” alifafanua Dkt. Tax.


Awali akimkaribisha Mhe. Waziri, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo amesema kwamba, Wizara imepokea makasha 28 ya Chapisho la Hashim Mbita lenye Volume 9.


Pia aliongeza kusema Sektretarieti ya SADC inaendelea na mchakato wa kutafsiri Chapisho la Hashim Mbita kwa lugha ya Kiswahili ili kuwawezesha watanzania wengi zaidi kulisoma na kuijua historia ya nchi yao hususan mchango wa Tanznaia katika Harakati za Ukombozi Kusini mwa Afrika.


Hafa hiyo ilihudhuriwa na viongozi na wawakilishi kutoka Taasisi mbalimbali zikiwemo Ofisi ya Rais, Bunge, Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA), Maktaba ya Taifa, Chuo Kikuu cha Dodoma na Taasisi ya Mwalimu Nyerere. 


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi Machapisho Hashim Mbita kwa Taasisi mbalimbali za hapa nchini. Hafla hiyo ambayo ilizishirikisha Taasisi 18 kutoka Tanzania Bara na Zanzibar ilifanyika jijini Dodoma tarehe 16 Mei 2023

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi machapisho ya Hashim Mbita kwa Taasisi mbalimbali nchini. Katikati ni Mhe. Dkt. Tax na kulia ni Mhe. Vincent Mbogo, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Sehemu ya wageni waalikwa walioshiriki hafla hiyo wakiwemo Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama

Sehemu nyingine ya washiriki

Wawakilishi wa Taasisi zilizoshiriki hafla ya kukabidhi machapisho ya Hashim Mbita wakifuatailia tukio. kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Talha Waziri

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Talha Waziri akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi machapisho ya Hashim Mbita kwa Taasisi mbalimbali.


Mhe. Dkt. Tax akimkabidhi Bw. Mbwana Msingwa kutoka Ofisi ya Rais Kasha lenye Volume 9 za Machapisho ya Hashim Mbita

Mhe. Dkt. Tax akiwakabidha Kasha lenye Volume 9 za Machapisho ya Hashim Mbita Wawakilishi kutoka Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakiwemo Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Mabo ya Nje, Ulinzi na Usalama wakiongozwa na Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Mbogo (kulia)

Makabidhiano yakiendelea kwa wawakilishi wa taasisi mbalimbali ikiwemo Maktaba ya Taifa.

Makabidhiano ya Machapisho ya Hashim Mbita yakiendelea

Mwakilishi kutoka Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) naye akikabidhiwa amachapisho ya Hashim Mbita

 

BALOZI FATMA RAJAB APOKEA ZAWADI YA TENDE KUTOKA SAUDI ARABIA

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab akipokea zawadi ya tende kutoka kwa wawakilishi wa Kituo cha Hisani cha Mfalme wa Saudi Arabia. Zawadi hiyo ya tende imetolewa na Serikali ya Saudi Arabia kupitia Kituo hicho na hafla ya makabidhiano imefanyika katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

 
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab akiangalia nyaraka alipopokea zawadi ya tende tani 25 zilizotolewa na Serikali ya Saudi Arabia kupitia Kituo cha Hisani cha Mfalme wa Saudi Arabia katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab (kulia) akizungumza na Kaimu Balozi wa Saudi Arabia nchini Bw. Fahad Alharbi katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam alipofika kukabidhi zawadi ya tende zilizotolewa na Mfalme wa Saudi Arabia kupitia Kituo cha Hisani cha Mfalme wa Saudi Arabia

 Kaimu Balozi wa Saudi Arabia nchini Bw. Fahad Alharbi (kushoto) akizungumza na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab (kulia) katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam alipofika kukabidhi zawadi ya tende zilizotolewa na Mfalme wa Saudi Arabia kupitia Kituo cha Hisani cha Mfalme wa Saudi Arabia

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab (kulia) akiwa na Kaimu Balozi wa Saudi Arabia nchini Bw. Fahad Alharbi wakionesha hundi yenye thamani ya Dola za Marekani 64,000 ambao ni msaada uliotolewa na Serikali ya Saudi Arabia kwa ajili ya kuimarisha huduma za TEHAMA katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab (wa pili kulia) akiwa na Kaimu Balozi wa Saudi Arabia nchini Bw. Fahad Alharbi (wa pili kushoto) wakiwa na Kaimu Mkurugenzi Idara ya Mashariki ya Kati Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bw. Leonce Bilauri na Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Isaack Kalumuna.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab amepokea zawadi ya tende zilizotolewa na Serikali ya Saudi Arabia katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Tende hizo, tani 25 zimetolewa na Mfalme wa Saudi Arabia, Mtukufu Salman bin Abdulaziz Al Saud kupitia Kituo cha Hisani cha Mfalme wa Saudi Arabia na kuwasilishwa nchini na wajumbe maalum wa Taasisi hiyo ya Mfalme Bw. Alrazani Abdulaziz Abdulahman na Alqunur Fahad Abdulahman.

Akipokea zawadi hiyo Balozi Fatma amemshukuru Mtukufu Mfalme Salman kwa kuendelea kutambua urafiki na ushirikiano wa kidiplomasia uliopo kati ya Tanzania na Saudia Arabia.

"Zawadi hii ya tende imetolewa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa niaba ya Watanzania wote, hii inaonesha uhusiano uliopo kati ya nchi zetu kupitia ujumbe mahsusi uliowasili nchini kwa ajili ya kuwasilisha tende hizi” alisema Balozi Fatma.

Vilevile, Balozi Fatma ameeleza kuwa uhusiano kati ya Tanzania na Saudi Arabia unaendelezwa kwa vitendo ambapo Serikali ya Saudi Arabia imekuwa na ziara mbalimbali za wataalam nchini katika sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, afya ambapo wataalamu wa matibabu wamekuwa wakija kufanya huduma za pamoja za upasuaji nchini na katika sekta ya anga Saudi Arabia imeanzisha safari za ndege za moja kwa moja kuja nchini.

Naye Kaimu Balozi Bw. Fahad Alharbi alieleza kuwa Saudi Arabia inatambua umuhimu wa ushirikiano wake na Tanzania katika kukuza uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi na akaahidi kuwa Ofisi ya Ubalozi itaendelea kuhakikisha inadumisha uhusiano huo.

Alisema kuwa kituo cha hisani cha Mfalme Salman ambacho kimekuja na ujumbe wa Mfalme huyo kukabidhi salamu pamoja na tende, kimekuwa kikitoa misaada mbalimbali ya kibinadamu ikiwemo usaidizi wa chakula, dawa na malazi kwa jamii zilizopatwa na majanga.

“Katika nyakati tofauti kituo hicho kimewezesha ziara za madaktari kutoka nchini Saudia Arabia ambao huweka kambi za huduma za matibabu ya upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo” alisema Bw. Fahad.

Pia akaeleza kuwa huduma hiyo ya madakatari itaendelea kutolewa na kwamba hivi karibuni madaktari wengine wanatarajia kuja nchini kuendelea kutoa huduma ya matibabu katika hospitali mbalimbali.

Wakati huohuo Serikali ya Saudi Arabia imekabidhi msaada wa kifedha wenye thamani ya Dola 66, 532 ambazo ni zaidi ya Shilingi milioni 159 kwa lengo la kuimarisha huduma za TEHAMA katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Tanzania na Saudi Arabia zinashirikiana katika sekta za uvuvi, kilimo, mifugo, ujenzi wa miundombinu na masuala ya anga na utalii.

SERIKALI YA TANZANIA IMEJIPANGA KUENDELEA KUNUFAIKA NA FURSA ZA MTANGAMANO WA KIKANDA

Serikali ya Tanzania imejipanga kuendelea kunufaika na fursa zinazotokana na Mtangamano wa Kikanda ili kuwawezesha watanzania kufaidika na uanachama wa Tanzania katika Jumuiya mbalimbali za kikanda.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika   Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax wakati wa ufunguzi wa semina kuhusu “Nafasi ya Tanzania katika Mtangamano wa Kikanda” iliyotolewa na Wizara jijini Dodoma kwa Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kwa lengo la kukuza uelewa kuhusu masuala ya mtangamano wa kikanda.

Mhe. Dkt. Tax amesema kuwa, mtangamano wa kikanda ni dhana muhimu katika kukuza uchumi, kuimarisha uhusiano wa kisiasa, amani na usalama katika mataifa  na kwamba Kamati hiyo ni miongoni mwa wadau muhimu wanaotakiwa kuwa na uelewa mkubwa kuhusu mtangamano wa kikanda ili kushirikiana na Wizara kueleza fursa na faida zake kwa wananchi.

Ameongeza kusema kwamba kwa Tanzania mtangamano wa kikanda ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje hivyo uelewa wa pamoja kuhusu dhana hii hususan fursa, faida na changamoto na namna ya kuzitatua unahitajika ili kufikia malengo kusudiwa.

Vilevile ameeleza kuwa, Tanzania inao mchango mkubwa katika Mtangamano wa kikanda na inategemewa ambapo pia imeendelea kunufaika na fursa mbalimbali zinazotokana na uanachama wake katika Jumuiya za Kikanda hususan, Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ikiwemo ajira, biashara, teknolojia, elimu na uwekezaji.

Mhe. Dkt. Tax pia alitumia fursa hiyo kueleza umuhimu wa kila Jumuiya kwa kusisitiza kuwa kila Jumuiya ina umuhimu na mchango mkubwa kwa Tanzania kulingana na lengo la kuanzishwa kwake.

“Naomba niweke hoja hii sawa. Kumekuwa na ulinganifu wa utendaji wa Jumuiya hizi ambapo baadhi ya watu wanaona jumuiya moja ni bora kuliko nyingine pasipo kujua kwamba kila moja ina umuhimu wake kulingana na lengo la kuanzishwa,” amesema Dkt. Tax.

Akitoa mfano amesema SADC ilianzishwa kwa lengo la kupigania ukombozi wa Nchi za Kusini mwa Afrika. Hivyo kwa kiasi kikubwa Jumuiya  hii imejikita kwenye masuala ya amani, ulinzi na usalama na kwamba ni kutokana na lengo hilo nchi za kusini zilikombolewa katika ukoloni lakini pia nchi wanachama kama Madagascar na Lesotho zilizokuwa na migogoro zimerejea katika hali ya amani na utulivu.

Kuhusu EAC amesema lengo la kuanzishwa kwake lilikuwa ni kuimarisha uchumi na biashara, hivyo kila jumuiya ni muhimu kulingana na majukumu yake.

Pia amesema anaishukuru kamati hiyo kwa kuendelea kushirikiana na Wizara kwenye masuala mbalimbali yenye maslahi kwa nchi na kuahidi kuendelea kushirikiana nayo katika masuala mbalimbali yanayohusu utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje.

Akiwasilisha mada hiyo, Mkufunzi kutoka Chuo cha Diplomasia cha jijini Dar es Salaam, Bw. Charles Mtakwa amesema zipo faida nyingi kwa Tanzania kuwa mwanachama katika EAC na SADC ikiwemo ajira, biashara, elimu, teknolojia na uendelezaji miundombinu ya kikanda.

“Mtangamano wa Kikanda ni dhana muhimu kwa Tanzania na hususan katika kukuza uchumi kupitia biashara, uwekezaji lakini pia kuboresha ufanisi wa soko la bidhaa mbalimbali kwani ni muhimu kwa nchi za Afrika kuendelea kukuza biashara miongoni mwake ambayo bado ipo katika kiwango cha chini cha asilimia 13 ukilinganisha na nchi za Bara la Asia asilimia 61 na Amerika asilimia 47” amesema Bw. Mtakwa.

Amesema kupitia Mtangangamano wa kikanda nchi wanachama huweza kufanya maamuzi ya pamoja ya kisera na kuchochea  mageuzi ikiwemo yale ya kiuchumi. Pia kupitia mtangamano wa kikanda nchi wanachama hushirikiana kuchangia gharama za miradi mikubwa na miundombinu kama miradi ya umeme na miradi ya barabara na reli.

Ameeleza kuwa, Mtangamano wa Kikanda ambao unalenga katika kuziwezesha nchi wanachama kushirikiana katika masuala mbalimbali  unazo hatua tano ambazo ni biashara huria; muungano wa forodha;soko la pamoja;muungano wa kifedha na muungano wa kisiasa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, Mhe. Vita Kawawa amesema kuwa anaipongeza na kuishukuru Wizara kwa kuendelea kutoa semina kuhusu mada mbalimbali za umuhimu na kwamba Kamati hiyo itaendelea kutoa ushirikiano na ushauri unaohitajika kwa Wizara.

Kwa upande wao, Wajumbe wa Kamati hiyo wameishauri Wizara kushirikiana na wadau mbalimbali kuendelea kutangaza fursa zinazopatikana katika mtangamano wa kikanda na kuendelea kusimamia makubaliano na mikataba iliyokwisha sainiwa katika kanda hizo ili itekelezwe kama ilivyopangwa.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb.) akifungua semina kuhusu Nafasi ya Tanzania katika Mtangamano wa Kikanda iliyoandaliwa na Wizara kwa Wajumbe wa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama 9NUU) iliyofanyika Dodoma hivi katibuni

Semina ikiendelea

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, Mhe. Vita Kawawa akizungumza wakati wa semina iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Wajumbe wa Kamati hiyo kuhusu Mtangamano wa Kikanda.

Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama wakifuatilia semina kuhusu Mtangamano wa Kikanda
Semina ikiendelea
Washiriki wakifuatilia semina
katibu Mkuu wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo akichangia jambo wakati wa semina kuhusu Mtangamano wa Kikanda. Kushito kwake ni Naibu katibu Mkuu, Balozi Fatma Mohammed Rajab akifuatiwa na Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Mipango, Bw. Haji Janabi

Mkutano ukiendelea















Monday, May 15, 2023

MWILI WA MEMBE WAWASILI RONDO, LINDI


Mwili wa aliyewahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Marehemu Bernard Membe umewasili kijijini kwake Rondo mkoani Lindi kwa ajili ya mazishi yanayotarajiwa kufanyika kesho tarehe 16 Mei, 2023.

Mwili wa Marehemu Membe umewasili kijijini hapo majira ya saa  06.40 mchana na Helikopta ya Jeshi na kupokelewa na mamia ya waombolezaji kutoka sehemu mbalimbali wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Limdi, Mhe. Shaibu Ndemanga

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye (Mb.) aliongoza ujumbe uliosafiri na mwili wa marehemu Membe kutoka Jijini Dar es Salaam hadi Rondo mkoani Lindi. Mhe. Nape ni Mbunge wa Jimbo la Mtama ambalo awali liliongozwa na Marehemu Membe kwa miaka 15 mfululizo (2000-2015).

Mwili marehemu mara baada ya kuwasili nyumbani kwake ulipokelewa na wanafamilia kwa simanzi, huzuni pamoja na vilio.

Mwili huo utalala nyumbani kwake hadi kesho tarehe 16 Mei 2023 atakapopumzishwa katika nyumba yake ya milele.

Marehemu Membe aliaga Dunia tarehe 12 Mei, 2023 wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Kairuki, Jijini Dar es Salaam.
Helikopta ya Jeshi iliyobeba mwili wa aliyewahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Marehemu Bernard Membe ikiwasili kijijini kwake Rondo

Mwili wa Marehemu Bernard Membe ukiwa umebebwa na wananchi ulipowasili kijijini kwake Rondo
Wananchi wa Rondo na kutoka maeneo mbalimbali nchini wakiwa wamejipanga kupokea mwili wa Marehemu Bernard Membe ulipowasili nyumbani kwake kijiji cha Rondo, Lindi. 

Sehemu ya waombolezaji wakiwa katika hali ya huzuni na majonzi kwenye msiba wa Marehemu Bernard Membe kijijini kwake Rondo, Lindi