Friday, May 19, 2023
Thursday, May 18, 2023
MAMBO YA NJE YAAINISHA FURSA ZINAZOPATIKANA KATIKA MIKUTANO YA KIMATAIFA
Ufafanuzi huo umetolewa Bungeni jijini Dodoma leo tarehe 18 Mei 2023 wakati Mhe. Balozi Mbarouk akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Neema Kichiki Lugangira aliyetaka kujua ni kwa kiasi gani ushiriki wa Tanzania katika Mikutano ya Kimataifa unazingatia upatikanaji wa fursa za kiuchumi na utekelezaji wake.
Mhe. Balozi Mabarouk amesema kuwa, ushiriki wa Tanzania katika Mikutano ya Kimataifa unalenga kupata na kutumia fursa za kiuchumi ikiwa ni pamoja na kupata mitaji, uwekezaji, masoko ya bidhaa na huduma, kukuza utalii, miradi ya kisekta, mikopo ya masharti nafuu na misaada, kujengewa uwezo wa kitaalamu, na upatikanaji wa teknolojia.
Mafanikio mengine ni pamoja na kupata masoko ya bidhaa mbalimbali kama vile mbogamboga, matunda, korosho, nafaka, nguo na mavazi, utalii, malumalu, na bidhaa za kioo. Vilevile, nchi yetu inanufaika kwa kupata wawekezaji katika sekta mbalimbali, ikiwa ni pamoja na utalii, viwanda, kilimo, uvuvi, mifugo, madini, na nishati jadidifu.
Wednesday, May 17, 2023
MAJALIWA, DKT. KIKWETE WAONGOZA WAOMBOLEZAJI MAZISHI YA MEMBE
Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe. Dkt. Jakaya Kikwete na Mke wake Mhe. Salma Kikwete (Mb) wakiweka shada la maua kwenye kaburi la Marehemu Bernard Membe |
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.) akiweka udongo kwenye kaburi la Marehemu Bernard Membe |
Mwili wa Marehemu Bernard Membe ukiwa kwenye ibada maalumu ya kumwombea muda mfupi kabla ya kupunzishwa kwenye nyumba yake ya milele. |
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (wa kwanza kushoto) akishiriki Ibada ya kumwombea Marehemu Bernard Membe |
Ibada maalumu ya kumwombea Marehemu Bernard Membe ikiendelea nyumbani kwake kijiji cha Rondo, Lindi |
Sehemu ya waombolezaji walioshiriki kwenye mazishi ya Marehemu Bernard Membe |
Sehemu ya Viongozi wakiweka mataji ya maua kwenye kaburi la Marehemu Bernard Membe |
Tuesday, May 16, 2023
MCHANGO WA TANZANIA KATIKA MEDANI ZA KIKANDA NA KIMATAIFA UTUNZWE: DKT TAX
Waziri wa Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax ametoa wito kwa Taasisi
mbalimbali nchini kuendelea kutunza kumbukumbu za historia ya Tanzania na
mchango wake katika medani za kikanda na kimataifa ili kuvirithisha vizazi vya
sasa na vijavyo.
Kauli hiyo ameitoa jijini
Dodoma tarehe 16 Mei 2023 wakati wa hafla fupi ya kikabidhi Machapisho ya
Hashim Mbita kwa Taasisi 18 zikiwemo za elimu.
Mhe. Dkt. Tax amesema
kuwa, Tanzania ina historia kubwa na nzuri katika medani za kikanda na
kimataifa ikiwemo mchango wake katika harakati za ukombozi kusini mwa Afrika
hivyo ni jukumu la wadau mbalimbali kuunganisha nguvu ya kutunza kumbukumbu ya
historia hiyo nzuri na kuvirithisha vizazi vya sasa na vijavyo.
Ameeleza kuwa, Wizara
imeamua kuyakabidhi machapisho hayo kwa Taasisi hizo ili yasaidie kurithisha
historia iliyomo kwa vizazi vijavyo, na kujenga hamasa ya uzalendo kwa vizazi
vya sasa na vijavyo.
“Wizara inawakabidhi
nyinyi machapisho haya kama wawakilishi wa wengi. Tunaamini kupitia Vyuo na
Taasisi zenu machapisho haya yatawafikia na kusomwa na Watanzania wengi.
Vilevile kupitia machapisho haya historia kuhusu mchango uliotolewa na Tanzania
katika harakati za ukombozi wa Kusini mwa Afrika na Afrika kwa ujumla itatunzwa
na kukumbukwa daima” amesisitiza Mhe. Dkt. Tax.
Pia ameziomba taasisi hizo
kuwa chachu katika kueneza historia adhimu iliyomo kwenye chapisho hilo kwa
kuhakikisha linasomwa. “Pamoja na kulitumia chapisho hili kama rejea, na kuhamasisha
lisomwe, niwaombe wadau mbalimbali nchini kuona uwezekano wa kuandaa simulizi
au filamu ya chapisho ili kuweza kuwafikia watu wengi hususan vijana”
alisisitiza Mhe. Dkt. Tax.
Aidha, amefafanua kuwa, Chapisho
hilo ambalo pamoja na mambo mengine linaeleza harakati za ukombozi katika nchi
za Angola, Namibia, Afrika ya Kusini, Zimbabwe na Msumbiji na mchango wan chi za
Tanzania, Zambia, Botswana, Lesotho, Malawi na Swaziland, lilipewa jina la
Hashim Mbita kutoka na mchango thabiti na uongozi mahiri wa Hayati Brigedia
Generali Hashim Mbita alioutoa akiwa
Katibu Mtendaji wa Kamati ya Kupigania Uhuru Afrika kuanzia mwaka 1972 hadi
1994.
Mhe. Dkt. Tax pia
ameshukuru na kupongeza mchango uliotolewa
na Viongozi mbalimbali wa Tanzania akiwemo Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius
Kamabarage Nyerere kwenye harakati za ukombozi kusini mwa Afrika kwani fikra na
mtazamo wake kuhusu umuhimu wa uhuru kwa nchi za Afrika zilifanikisha nchi zote
za Afrika kujikomboa dhidi ya ukoloni.
Pia Mhe. Dkt. Tax alitumia
fursa hiyo kuipongeza Kampuni ya Kitanzania ya Uchapishaji ya Mkuki na Nyota kwa
kuchapisha chapisho hilo kwa umahiri.
“Nawashukuru wadau wote
waliofanikisha uchapishaji wa Chapisho la Hashim Mbita ikiwemo Jumuiya ya
Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kwa
kuandaa Chapisho hilo lenye Volume 9 na kwa kutambua mchango wa Tanzania
katika harakati za Ukombozi wa Nchi za Kusini mwa Afrika. Pia kipekee namshukuru Rais Mstaafu wa wa Awamu ya Nne wa
Tanzania, Hayati Benjamin William Mkapa kwa kuniagiza nikiwa Katibu Mtendaji wa
SADC na kunisisitiza kuhakikisha chapisho hili linakamilika baada mchakato wa
awali kusimama ambapo mwaka 2014 kufuatia maagizo hayo, mchakato ulitekelezwa
katika awamu tatu na kukamilika mwaka
2020” alifafanua Dkt. Tax.
Awali akimkaribisha Mhe.
Waziri, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika
Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo amesema kwamba, Wizara imepokea
makasha 28 ya Chapisho la Hashim Mbita lenye Volume 9.
Pia aliongeza kusema
Sektretarieti ya SADC inaendelea na mchakato wa kutafsiri Chapisho la Hashim
Mbita kwa lugha ya Kiswahili ili kuwawezesha watanzania wengi zaidi kulisoma na
kuijua historia ya nchi yao hususan mchango wa Tanznaia katika Harakati za
Ukombozi Kusini mwa Afrika.
Hafa hiyo ilihudhuriwa na
viongozi na wawakilishi kutoka Taasisi mbalimbali zikiwemo Ofisi ya Rais,
Bunge, Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA), Maktaba ya Taifa, Chuo Kikuu cha
Dodoma na Taasisi ya Mwalimu Nyerere.
Sehemu ya wageni waalikwa walioshiriki hafla hiyo wakiwemo Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama |
Sehemu nyingine ya washiriki |
Mhe. Dkt. Tax akimkabidhi Bw. Mbwana Msingwa kutoka Ofisi ya Rais Kasha lenye Volume 9 za Machapisho ya Hashim Mbita |
Makabidhiano yakiendelea kwa wawakilishi wa taasisi mbalimbali ikiwemo Maktaba ya Taifa. |
Makabidhiano ya Machapisho ya Hashim Mbita yakiendelea |
Mwakilishi kutoka Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) naye akikabidhiwa amachapisho ya Hashim Mbita |
BALOZI FATMA RAJAB APOKEA ZAWADI YA TENDE KUTOKA SAUDI ARABIA
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab amepokea zawadi ya tende zilizotolewa na Serikali ya Saudi Arabia katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.
Tende hizo, tani 25 zimetolewa na Mfalme wa Saudi Arabia, Mtukufu Salman bin Abdulaziz Al Saud kupitia Kituo cha Hisani cha Mfalme wa Saudi Arabia na kuwasilishwa nchini na wajumbe maalum wa Taasisi hiyo ya Mfalme Bw. Alrazani Abdulaziz Abdulahman na Alqunur Fahad Abdulahman.
Akipokea zawadi hiyo Balozi Fatma amemshukuru Mtukufu Mfalme Salman kwa kuendelea kutambua urafiki na ushirikiano wa kidiplomasia uliopo kati ya Tanzania na Saudia Arabia.
"Zawadi hii ya tende imetolewa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa niaba ya Watanzania wote, hii inaonesha uhusiano uliopo kati ya nchi zetu kupitia ujumbe mahsusi uliowasili nchini kwa ajili ya kuwasilisha tende hizi” alisema Balozi Fatma.
Vilevile, Balozi Fatma ameeleza kuwa uhusiano kati ya Tanzania na Saudi Arabia unaendelezwa kwa vitendo ambapo Serikali ya Saudi Arabia imekuwa na ziara mbalimbali za wataalam nchini katika sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, afya ambapo wataalamu wa matibabu wamekuwa wakija kufanya huduma za pamoja za upasuaji nchini na katika sekta ya anga Saudi Arabia imeanzisha safari za ndege za moja kwa moja kuja nchini.
Naye Kaimu Balozi Bw. Fahad Alharbi alieleza kuwa Saudi Arabia inatambua umuhimu wa ushirikiano wake na Tanzania katika kukuza uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi na akaahidi kuwa Ofisi ya Ubalozi itaendelea kuhakikisha inadumisha uhusiano huo.
Alisema kuwa kituo cha hisani cha Mfalme Salman ambacho kimekuja na ujumbe wa Mfalme huyo kukabidhi salamu pamoja na tende, kimekuwa kikitoa misaada mbalimbali ya kibinadamu ikiwemo usaidizi wa chakula, dawa na malazi kwa jamii zilizopatwa na majanga.
“Katika nyakati tofauti kituo hicho kimewezesha ziara za madaktari kutoka nchini Saudia Arabia ambao huweka kambi za huduma za matibabu ya upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo” alisema Bw. Fahad.
Pia akaeleza kuwa huduma hiyo ya madakatari itaendelea kutolewa na kwamba hivi karibuni madaktari wengine wanatarajia kuja nchini kuendelea kutoa huduma ya matibabu katika hospitali mbalimbali.
Wakati huohuo Serikali ya Saudi Arabia imekabidhi msaada wa kifedha wenye thamani ya Dola 66, 532 ambazo ni zaidi ya Shilingi milioni 159 kwa lengo la kuimarisha huduma za TEHAMA katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Tanzania na Saudi Arabia zinashirikiana katika sekta za uvuvi, kilimo, mifugo, ujenzi wa miundombinu na masuala ya anga na utalii.
SERIKALI YA TANZANIA IMEJIPANGA KUENDELEA KUNUFAIKA NA FURSA ZA MTANGAMANO WA KIKANDA
Serikali ya Tanzania imejipanga kuendelea kunufaika na fursa zinazotokana na Mtangamano wa Kikanda ili kuwawezesha watanzania kufaidika na uanachama wa Tanzania katika Jumuiya mbalimbali za kikanda.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano
wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt.
Stergomena Tax wakati wa ufunguzi wa semina kuhusu “Nafasi ya Tanzania katika
Mtangamano wa Kikanda” iliyotolewa na Wizara jijini Dodoma kwa Wajumbe
wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kwa lengo la kukuza uelewa
kuhusu masuala ya mtangamano wa kikanda.
Mhe. Dkt. Tax amesema kuwa, mtangamano wa kikanda ni dhana
muhimu katika kukuza uchumi, kuimarisha uhusiano wa kisiasa, amani na usalama
katika mataifa na kwamba Kamati hiyo ni
miongoni mwa wadau muhimu wanaotakiwa kuwa na uelewa mkubwa kuhusu mtangamano
wa kikanda ili kushirikiana na Wizara kueleza fursa na faida zake kwa wananchi.
Ameongeza kusema kwamba kwa Tanzania mtangamano wa kikanda ni
sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje hivyo uelewa wa pamoja kuhusu
dhana hii hususan fursa, faida na changamoto na namna ya kuzitatua unahitajika
ili kufikia malengo kusudiwa.
Vilevile ameeleza kuwa, Tanzania inao mchango mkubwa katika
Mtangamano wa kikanda na inategemewa ambapo pia imeendelea kunufaika na fursa
mbalimbali zinazotokana na uanachama wake katika Jumuiya za Kikanda hususan,
Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika
ikiwemo ajira, biashara, teknolojia, elimu na uwekezaji.
Mhe. Dkt. Tax pia alitumia fursa hiyo kueleza umuhimu wa kila
Jumuiya kwa kusisitiza kuwa kila Jumuiya ina umuhimu na mchango mkubwa kwa
Tanzania kulingana na lengo la kuanzishwa kwake.
“Naomba niweke hoja hii sawa. Kumekuwa na ulinganifu wa
utendaji wa Jumuiya hizi ambapo baadhi ya watu wanaona jumuiya moja ni bora
kuliko nyingine pasipo kujua kwamba kila moja ina umuhimu wake kulingana na
lengo la kuanzishwa,” amesema Dkt. Tax.
Akitoa mfano amesema SADC ilianzishwa kwa lengo la kupigania
ukombozi wa Nchi za Kusini mwa Afrika. Hivyo kwa kiasi kikubwa Jumuiya hii imejikita kwenye masuala ya amani, ulinzi
na usalama na kwamba ni kutokana na lengo hilo nchi za kusini zilikombolewa
katika ukoloni lakini pia nchi wanachama kama Madagascar na Lesotho zilizokuwa
na migogoro zimerejea katika hali ya amani na utulivu.
Kuhusu EAC amesema lengo la kuanzishwa kwake lilikuwa ni
kuimarisha uchumi na biashara, hivyo kila jumuiya ni muhimu kulingana na
majukumu yake.
Pia amesema anaishukuru kamati hiyo kwa kuendelea
kushirikiana na Wizara kwenye masuala mbalimbali yenye maslahi kwa nchi na
kuahidi kuendelea kushirikiana nayo katika masuala mbalimbali yanayohusu
utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje.
Akiwasilisha mada hiyo, Mkufunzi kutoka Chuo cha
Diplomasia cha jijini Dar es Salaam, Bw. Charles Mtakwa amesema zipo faida
nyingi kwa Tanzania kuwa mwanachama katika EAC na SADC ikiwemo ajira, biashara,
elimu, teknolojia na uendelezaji miundombinu ya kikanda.
“Mtangamano wa Kikanda ni dhana muhimu kwa Tanzania na hususan
katika kukuza uchumi kupitia biashara, uwekezaji lakini pia kuboresha ufanisi
wa soko la bidhaa mbalimbali kwani ni muhimu kwa nchi za Afrika kuendelea
kukuza biashara miongoni mwake ambayo bado ipo katika kiwango cha chini cha
asilimia 13 ukilinganisha na nchi za Bara la Asia asilimia 61 na Amerika
asilimia 47” amesema Bw. Mtakwa.
Amesema kupitia Mtangangamano wa kikanda nchi wanachama
huweza kufanya maamuzi ya pamoja ya kisera na kuchochea mageuzi ikiwemo yale ya kiuchumi. Pia kupitia
mtangamano wa kikanda nchi wanachama hushirikiana kuchangia gharama za miradi
mikubwa na miundombinu kama miradi ya umeme na miradi ya barabara na reli.
Ameeleza kuwa, Mtangamano wa Kikanda ambao unalenga katika
kuziwezesha nchi wanachama kushirikiana katika masuala mbalimbali unazo hatua tano ambazo ni biashara huria;
muungano wa forodha;soko la pamoja;muungano wa kifedha na muungano wa kisiasa.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya
Nje, Ulinzi na Usalama, Mhe. Vita Kawawa amesema kuwa anaipongeza na kuishukuru
Wizara kwa kuendelea kutoa semina kuhusu mada mbalimbali za umuhimu na kwamba
Kamati hiyo itaendelea kutoa ushirikiano na ushauri unaohitajika kwa Wizara.
Kwa upande wao, Wajumbe wa Kamati hiyo wameishauri Wizara kushirikiana na wadau mbalimbali kuendelea kutangaza fursa zinazopatikana katika mtangamano wa kikanda na kuendelea kusimamia makubaliano na mikataba iliyokwisha sainiwa katika kanda hizo ili itekelezwe kama ilivyopangwa.
Semina ikiendelea |
Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama wakifuatilia semina kuhusu Mtangamano wa Kikanda |
Semina ikiendelea |
Washiriki wakifuatilia semina |
Mkutano ukiendelea |
Monday, May 15, 2023
MWILI WA MEMBE WAWASILI RONDO, LINDI
Helikopta ya Jeshi iliyobeba mwili wa aliyewahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Marehemu Bernard Membe ikiwasili kijijini kwake Rondo |
Mwili wa Marehemu Bernard Membe ukiwa umebebwa na wananchi ulipowasili kijijini kwake Rondo |
Wananchi wa Rondo na kutoka maeneo mbalimbali nchini wakiwa wamejipanga kupokea mwili wa Marehemu Bernard Membe ulipowasili nyumbani kwake kijiji cha Rondo, Lindi. |
Sehemu ya waombolezaji wakiwa katika hali ya huzuni na majonzi kwenye msiba wa Marehemu Bernard Membe kijijini kwake Rondo, Lindi |