Tuesday, May 16, 2023

BALOZI FATMA RAJAB APOKEA ZAWADI YA TENDE KUTOKA SAUDI ARABIA

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab akipokea zawadi ya tende kutoka kwa wawakilishi wa Kituo cha Hisani cha Mfalme wa Saudi Arabia. Zawadi hiyo ya tende imetolewa na Serikali ya Saudi Arabia kupitia Kituo hicho na hafla ya makabidhiano imefanyika katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

 
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab akiangalia nyaraka alipopokea zawadi ya tende tani 25 zilizotolewa na Serikali ya Saudi Arabia kupitia Kituo cha Hisani cha Mfalme wa Saudi Arabia katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab (kulia) akizungumza na Kaimu Balozi wa Saudi Arabia nchini Bw. Fahad Alharbi katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam alipofika kukabidhi zawadi ya tende zilizotolewa na Mfalme wa Saudi Arabia kupitia Kituo cha Hisani cha Mfalme wa Saudi Arabia

 Kaimu Balozi wa Saudi Arabia nchini Bw. Fahad Alharbi (kushoto) akizungumza na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab (kulia) katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam alipofika kukabidhi zawadi ya tende zilizotolewa na Mfalme wa Saudi Arabia kupitia Kituo cha Hisani cha Mfalme wa Saudi Arabia

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab (kulia) akiwa na Kaimu Balozi wa Saudi Arabia nchini Bw. Fahad Alharbi wakionesha hundi yenye thamani ya Dola za Marekani 64,000 ambao ni msaada uliotolewa na Serikali ya Saudi Arabia kwa ajili ya kuimarisha huduma za TEHAMA katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab (wa pili kulia) akiwa na Kaimu Balozi wa Saudi Arabia nchini Bw. Fahad Alharbi (wa pili kushoto) wakiwa na Kaimu Mkurugenzi Idara ya Mashariki ya Kati Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bw. Leonce Bilauri na Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Isaack Kalumuna.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab amepokea zawadi ya tende zilizotolewa na Serikali ya Saudi Arabia katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Tende hizo, tani 25 zimetolewa na Mfalme wa Saudi Arabia, Mtukufu Salman bin Abdulaziz Al Saud kupitia Kituo cha Hisani cha Mfalme wa Saudi Arabia na kuwasilishwa nchini na wajumbe maalum wa Taasisi hiyo ya Mfalme Bw. Alrazani Abdulaziz Abdulahman na Alqunur Fahad Abdulahman.

Akipokea zawadi hiyo Balozi Fatma amemshukuru Mtukufu Mfalme Salman kwa kuendelea kutambua urafiki na ushirikiano wa kidiplomasia uliopo kati ya Tanzania na Saudia Arabia.

"Zawadi hii ya tende imetolewa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa niaba ya Watanzania wote, hii inaonesha uhusiano uliopo kati ya nchi zetu kupitia ujumbe mahsusi uliowasili nchini kwa ajili ya kuwasilisha tende hizi” alisema Balozi Fatma.

Vilevile, Balozi Fatma ameeleza kuwa uhusiano kati ya Tanzania na Saudi Arabia unaendelezwa kwa vitendo ambapo Serikali ya Saudi Arabia imekuwa na ziara mbalimbali za wataalam nchini katika sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, afya ambapo wataalamu wa matibabu wamekuwa wakija kufanya huduma za pamoja za upasuaji nchini na katika sekta ya anga Saudi Arabia imeanzisha safari za ndege za moja kwa moja kuja nchini.

Naye Kaimu Balozi Bw. Fahad Alharbi alieleza kuwa Saudi Arabia inatambua umuhimu wa ushirikiano wake na Tanzania katika kukuza uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi na akaahidi kuwa Ofisi ya Ubalozi itaendelea kuhakikisha inadumisha uhusiano huo.

Alisema kuwa kituo cha hisani cha Mfalme Salman ambacho kimekuja na ujumbe wa Mfalme huyo kukabidhi salamu pamoja na tende, kimekuwa kikitoa misaada mbalimbali ya kibinadamu ikiwemo usaidizi wa chakula, dawa na malazi kwa jamii zilizopatwa na majanga.

“Katika nyakati tofauti kituo hicho kimewezesha ziara za madaktari kutoka nchini Saudia Arabia ambao huweka kambi za huduma za matibabu ya upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo” alisema Bw. Fahad.

Pia akaeleza kuwa huduma hiyo ya madakatari itaendelea kutolewa na kwamba hivi karibuni madaktari wengine wanatarajia kuja nchini kuendelea kutoa huduma ya matibabu katika hospitali mbalimbali.

Wakati huohuo Serikali ya Saudi Arabia imekabidhi msaada wa kifedha wenye thamani ya Dola 66, 532 ambazo ni zaidi ya Shilingi milioni 159 kwa lengo la kuimarisha huduma za TEHAMA katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Tanzania na Saudi Arabia zinashirikiana katika sekta za uvuvi, kilimo, mifugo, ujenzi wa miundombinu na masuala ya anga na utalii.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.