Friday, May 19, 2023

DKT SAMIA AZINDUA MAANDALIZI YA MKUTANO WA WAKUU WA NCHI AFRIKA KUHUSU RASILIMALI WATU

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amezindua Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali watu (Africa Heads of State Human Capital Summit) utakaofanyika nchini tarehe 25 - 26 Julai, 2023. 

Mhe. Dkt. Samia ametoa wito kwa viongozi wa Afrika kuendelea kuchukua hatua kwa kuwekeza kwa watu na kutoa kipaumbele kwa vijana na wanawake.

Mhe. Rais pia amewataka viongozi wa Afrika kuchukua hatua zaidi ili kukabiliana na changamoto zinazowakabili watu wengi kwa kuwekeza zaidi katika kuboresha afya za watu, maji safi na salama, elimu bora na ujuzi muhimu kwa maendeleo ya rasilimali watu.

“Viongozi wa Afrika lazima tuendelee kuchukua hatua kwa kuwekeza kwa watu na kutoa kipaumbele kwa vijana na wanawake. Nitoe wito kwa viongozi wa Afrika kuchukua hatua zaidi ili kukabiliana na changamoto zinazokabili rasilimali watu kwa kuwekeza zaidi katika kuboresha afya za watu, kuwaletea maji safi na salama, kutoa elimu bora na ujuzi muhimu kwa maendeleo ya rasilimali watu,” alisema Mhe. Samia 

Rais Samia amesema taarifa za Umoja wa Mataifa zinaonesha kuwa nchi nyingi za Afrika ukitoa za Afrika Kaskazini zinakabiliwa na changamoto katika utekelezaji wa malengo ya milenia ya uendelezaji rasilimali watu hali ikiwa chini ya wastani hasa katika maeneo ya elimu, afya na ulinzi wa jamii. 

“Hali ya afya ya uzazi, uwepo wa maji safi na salama na usimamizi wa maji taka bado ni changamoto kwa nchi nyingi huku ujumuishi wa kijinsia ukiwa na kasi ndogo na utekelezaji wa sheria za kulinda wanawake na watoto wa kike dhidi ya ubaguzi, unyanyasaji wa kijinsia, ndoa za utotoni na ukeketaji ukiwa mdogo na kuongeza kuwa kuwa hali ya ukamilishaji wa malengo ya milenia namba , 4, 5, 6 na 8 kwa nchi za Afrika hairidhishi na inaonesha hatari ya kutokamilika kwa malengo hayo kufikia mwaka 2030,” alisema Dkt. Samia.

Akizungumza katika uzinduzi wa Mkutano huo, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Stergomena Tax (Mb.) alisema kuwa kufanyika kwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika wa Rasilimali Watu mwezi Julai 2023, kunatokana na jitihada za Serikali kuboresha ushirikiano na kuzingatia umuhimu wa rasilimali watu katika kukuza uchumi na umuhimu wa kuwekeza kwa watu.

 “Kufanyika kwa mkutano huo hapa nchini, kunatokana na jitihada za serikali katika kuboresha ushirikiano na kuzingatia umuhimu wa rasilimali watu katika kukuza uchumi wa na kuona umuhimu wa kuwekeza kwa watu,” 

Alisema kufanyika kwa mkutano huo kutatoa fursa kwa wakuu wa nchi kubadilishana ujuzi na uzoefu kuhusu rasilimali watu na kutoka na maazimio madhubuti kuhusu cha kufanya kuendeleza rasilimali watu.

Dkt. Tax aliongeza kuwa Azma ya agenda 2063 inalenga kuzibadilisha nchi za Afrika na kuwa na nguvu za kiuchumi lakini azma hiyo inahitaji uwekezaji wa makusudi katika ujuzi na uwezo ili kutumia fursa za kijamii na kiuchumi katika bara la Afrika.

Naye Waziri wa Fedha na Mipango  Dk. Mwigulu Nchemba (Mb.) alisema Tanzania imekuwa mwenyeji wa mkutano huo kutokana na vipaumbele vya Rais Dkt. Samia alivyoweka katika maeneo ya afya na  makundi mbalimbali ya vijana na wanawake.

Alisema mbali ya Rais kufanya mabadiliko mbali mbali yaliyofanyika nchini lakini pia tumeshuhudia uwekezaji mkubwa wa fedha ukielekezwa katika eneo la elimu ili watoto wengi zaidi wanufaike kwa kupata elimu.

Awali Mkurugenzi wa Benki ya Dunia katika nchi za Tanzania, Malawi, Zambia na Zimbabwe, Bw. Nathan Belete alisema Bara la Afrika lina nguvu kazi kubwa ambapo zaidi ya asilimia 75 ya watu wake wanafanya kazi katika sekta rasmi na kwamba nchi za Afrika zinapaswa kuungana na kufanya kazi kwa pamoja ili kumaliza changamoto zinazokabili rasilimali watu.

“Bara la Afrika lina nguvu kazi kubwa, tunaona kuwa asilimia 75 ya watu katika bara hili wanafanya kazi katika sekta rasmi, hivyo Nchi  zinapaswa kuungana na kufanya kazi kwa pamoja ili kuzimaliza changamoto zinazokabili rasilimali watu kwa urahisi katika ukanda huo,” alisema. 

Alisema nchi za Afrika lazima zifanyie kazi suala la unyanyasaji wa kijinsia kwa kuwekeza katika elimu, afya na kuwawezesha wananchi wake kupata maarifa, ujuzi na afya bora.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia Viongozi, Mabalozi pamoja na Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa kabla ya kuzindua Mkutano wa Maandalizi kwa ajili ya Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali watu (Africa Heads of State Human Capital Summit), Jijini Dar es Salaam. Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali Watu unatarajiwa kufanyika tarehe 25-26 Julai, 2023 Jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akizungumza wakati wa Mkutano wa Maandalizi ya Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali watu (Africa Heads of State Human Capital Summit), Jijini Dar es Salaam

Sehemu ya Viongozi, Mabalozi pamoja na Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa wakifuatilia Hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa uzinduzi wa Mkutano wa Maandalizi kwa ajili ya Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali watu (Africa Heads of State Human Capital Summit), Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akizungumza na Balozi wa Canada nchini, Mhe. Kyle Nunas kabla ya uzinduzzi wa Mkutano wa Maandalizi ya Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Rasilimali watu (Africa Heads of State Human Capital Summit), Jijini Dar es Salaam


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.