Friday, September 8, 2023

AFRIKA INA ARDHI KUBWA YA KULISHA DUNIA, RAIS SAMIA

Rais wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amezihimiza nchi za Afrika kushirikiana ili kukabiliana na aibu ya baa la njaa, kwakuwa bara hilo lina asilimia 65 ya ardhi inayofaa kwa kilimo duniani, asilimia 60 ya utajiri wa rasilimali na maziwa makubwa, nguvu kazi ya kutosha ya vijana na madini yanayoweza kuingizia fedha nyingi za kuwekeza katika kilimo barani humo.

Rais Samia ametoa kauli hiyo alipohutubia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula ngazi ya Marais uliofanyika jijini Dar Es Salaam tarehe 07 Septemba 2023.

Mhe. Rais Samia amesikitishwa na hali ya Afrika ya kuwa Bara la walalamikaji badala ya kuweka mikakati na kutafuta mbinu za kujiiletea mapinduzi ya kijani. Alisema watu takribani milioni 283 barani Afrika wana lala na njaa kila siku, wengine wanapata utapia mlo na baadhi yao kufariki kwa kukosa chakula, jambo ambalo amelitaja ni la aibu na halikubaliki kwa dunia ya leo.

Mhe. Rais Samia amezitaka nchi za Afrika kuzigeuza changamoto zinazoikabili dunia kuwa fursa kwao, kwa kuwekeza zaidi katika kilimo, hususan kwa kuwawezesha vijana na kuwatatulia matatizo yao. Matatizo hayo yanayowakabili vijana ni pamoja na ukosefu wa taarifa sahihi, ardhi, mitaji, athari za mabadiliko ya tabianchi na kuibuka kwa magonjwa duniani.

Dkt. Samia amebainisha kuwa ili kufikia malengo ya usalama wa chakula barani Afrika, nchi za Afrika hazina budi kutathmini vipaumbele vyake na kutunga sera zinazoendena na mahitaji ya sasa ya dunia.

Alisema ni muhimu kwa nchi za Afrika kutekeleza ahadi ilizojiwekea ambazo zimebainishwa katika Progaramu ya Maendeleo ya Kilimo ya Umoja wa Afrika ya Mwaka 2003, Azimio la Malabo la mwaka 2014 kuhusu kuongeza kasi ya ukuaji wa sekta ya kilimo na mikakati mingine kuhusu kilimo.

Miongozo ya maazimio hayo yanaelekeza nchi za Afrika kuongeza bajeti ya kilimo hadi asilimia 10, kukuza sekta ya kilimo kwa asilimia 6, kuimarisha ukuaji jumuishi wa sekta ya kilimo, kuhamasisha na kushirikisha sekta binafsi katika kilimo, kutoa fursa za ajira kwa vijana angalau kwa asilimia 30 katika minyororo ya uongezaji thamani katika mifumo ya kilimo na kuongeza biashara ya bidhaa na huduma za kilimo barani Afrika.

Mhe. Rais alieleza kuwa Tanzania inatekeleza maazimio hayo kwa kuongeza bajeti ya sekta ya kilimo, kutekeleza agenda Namba 1030 ya kuongeza ukuaji wa sekta ya kilimo kwa asilimia 10 ifikapo mwaka 2030, kuingia katika masoko ya chakula ya kikanda na ya kimataifa ili kukidhi mahitaji ya chakula katika nchi mbalimbali.

Aidha, alieleza kuwa ili kuchochea sekta ya kilimo nchini, Serikali inatekeleza programu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwawezesha vijana na wanawake kupitia mpango wa Jenga Kesho iliyo bora (BBT) ambayo imezinduliwa na kutekelezwa katika mikoa mbalimbali nchini.

Rais Samia ambaye aliungana na Rais wa Kenya, Mhe. William Ruto, Rais wa Burundi, Mhe. Evariste Ndayishimiye na Rais wa Senegal, Mhe. Macky  Sall na Rais wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi aliahidi kuwa Afrika ipo tayari kuzalisha chakula cha kutosha na kuacha kutegemea bidhaa hiyo muhimu kutoka nje. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam

Washiriki mbalimbali wakifuatilia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam
Washiriki wakiwa wamesimama kwa ajili ya kuimba Wimbo wa Taifa wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam
Viongozi mbalimbali akiwemo Rais wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi (kushoto) na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (wa pili kutoka kushoto) wakifuatilia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam
Rais wa awamu ya nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete na Rais wa Zanzibar, Mhe. Hussein Mwinyi wakiteta jambo wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam

Wakifuatilia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam


Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga akifuatilia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam

Wanadiplomasia mbalimbali wakifuatilia Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam






Thursday, September 7, 2023

TANZANIA IMEJIPANGA KUTUMIA TEHAMA KUBORESHA KILIMO


 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na vijana wanaoshiriki Mkutano wa Mifumo ya Chakula Barani Afrika (AGRF 2023) uliofanyika katika ukumbi wa JNICC jijini Dar es Salaam


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na vijana wanaoshiriki Mkutano wa Mifumo ya Chakula Barani Afrika (AGRF 2023) uliofanyika katika ukumbi wa JNICC jijini Dar es Salaam


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amewaeleza vijana wanaoshiriki Mkutano wa Mifumo ya Chakula Barani Afrika (AGRF 2023) kuwa Serikali ya Tanzania imejipanga kutumia vyema Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) ili kuboresha sekta ya Kilimo na kukuza upatikaji wa chakula nchini.

Mhe. Dkt. Samia ametoa kauli hiyo alipozungumza na vijana walioko katika Sekta ya kilimo kuhusu jitihada za kukabiliana na changamoto za kutafuta masoko ya mazao ya kilimo wanaoshiriki Mkutano wa Mifumo ya Chakula barani Afrika (AGRF 2023) unaofanyika Jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 5 – 8 Septemba 2023.

Mhe. Rais amesema matumizi ya teknolojia ya kisasa katika sekta ya Kilimo yataleta matokeo chanya na kutoleo mfano wa kutumia trekta za ‘automatic’ na zinavyosaidia kuleta tija katika sekta ya kilimo.

Amesema Serikali ya Tanzania inategemea kufikia mwaka 2025 kuhakikisha robo tatu ya mbegu zinazotumiwa na wakulima zinazalishwa nchini zikiwa na ubora unaokidhi mahitaji kwa kutumia ICT.

Mhe. Samia akiongelea madhumuni ya programu ya Jenga Kesho iliyo Bora (BBT) amesema imelenga kuwawezesha vijana kushiriki katika kilimo na kuongeza kuwa program hiyo ilianzishwa kwa lengo la kuinua maisha ya vijana na kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo nchini.

Rais Samia ameongeza kuwa pamoja na mambo mengine, malengo ya kimkakati ya BBT ni kuwavuta vijana kushiriki kwenye miradi ya kilimo chenye tija na faida kwa maisha yao.

BBT ilianzishwa mwaka 2022, na tangu ilipoanzishwa imechukua vijana 1,252 na vijana wengine 812 wamejiandikisha kupata mafunzo hayo yanayotolewa kwa miezi minne.

Kadhalika, Rais Samia ameongeza kuwa Tanzania imejipanga kuiendeleza sekta ya kilimo siyo tu kwa manufaa yake bali kwa manufaa ya bara la Afrika na Dunia kwa ujumla.

TANZANIA IMEJIPANGA KUTUMIA TEHAMA KUBORESHA KILIMO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amewaeleza vijana wanaoshiriki Mkutano wa Mifumo ya Chakula Barani Afrika (AGRF 2023) kuwa Serikali ya Tanzania imejipanga kutumia vyema Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) ili kuboresha sekta ya Kilimo na kukuza upatikaji wa chakula nchini.

Mhe. Dkt. Samia ametoa kauli hiyo alipozungumza na vijana walioko katika Sekta ya kilimo kuhusu jitihada za kukabiliana na changamoto za kutafuta masoko ya mazao ya kilimo wanaoshiriki Mkutano wa Mifumo ya Chakula barani Afrika (AGRF 2023) unaofanyika Jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 5 – 8 Septemba 2023.

Mhe. Rais amesema matumizi ya teknolojia ya kisasa katika sekta ya Kilimo yataleta matokeo chanya na kutoleo mfano wa kutumia trekta za ‘automatic’ na zinavyosaidia kuleta tija katika sekta ya kilimo.

Amesema Serikali ya Tanzania inategemea kufikia mwaka 2025 kuhakikisha robo tatu ya mbegu zinazotumiwa na wakulima zinazalishwa nchini zikiwa na ubora unaokidhi mahitaji kwa kutumia ICT.

“Kutokana na matumizi ya teknolojia ya kisasa tunategemea hadi kufikia mwaka 2025 Serikali itahakikisha robo tatu ya mbegu zinazotumiwa na wakulima zinazalishwa nchini zikiwa na ubora unaokidhi mahitaji kwa msaada wa Tehama,” alisema Rais Samia.

Mhe. Samia akiongelea madhumuni ya programu ya Jenga Kesho iliyo Bora (BBT) amesema imelenga kuwawezesha vijana kushiriki katika kilimo na kuongeza kuwa program hiyo ilianzishwa kwa lengo la kuinua  maisha ya vijana na kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo nchini.

“Madhumuni ya BBT ni kuwawezesha vijana kushiriki katika sekta ya kilimo ili kuweza kuinua Maisha yao na kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo,” alisema Rais Samia

Rais Samia ameongeza kuwa pamoja na mambo mengine, malengo ya kimkakati ya BBT ni kuwavuta vijana kushiriki kwenye miradi ya kilimo chenye tija na faida kwa maisha yao.

BBT ilianzishwa mwaka 2022, na tangu ilipoanzishwa imechukua vijana 1,252 na vijana wengine 812 wamejiandikisha kupata mafunzo hayo yanayotolewa kwa miezi minne.

Kadhalika, Rais Samia ameongeza kuwa Tanzania imejipanga kuiendeleza sekta ya kilimo siyo tu kwa manufaa yake bali kwa manufaa ya bara la Afrika na Dunia kwa ujumla. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na vijana wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula Afrika (AGRF) unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere kuanzia tarehe 5 - 8 Septemba, 2023 Jijini Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akichangia mjadala wa masuala ya kilimo na vijana wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula Afrika (AGRF) unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere, Jijini Dar es Salaam 








RAIS RUTO AWASILI NCHNI KUSHIRIKI AGRF 2023

Rais wa Jamhuri ya Kenya Mheshimiwa William Ruto amewasili nchini kuhudhuria Mkutano wa Mifumo ya Chakula Afrika unaofanyika nchini kuanzia tarehe 5-8 Septemba 2023.

Baada ya kuwasili nchini, Mhe. Ruto amepokelewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam. 

Mhe. Ruto ni miongoni mwa Wakuu wa Nchi na Serikali, Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa na Marais na Mawaziri Wakuu wastaafu kutoka barani Afrika wanaohudhuria mkutano huo mkubwa unaojadili Mifumo ya Chakula Afrika (AGRF 2023).

Rais wa Jamhuri ya Kenya Mheshimiwa William Ruto akisalimiana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam kushiriki Mkutano wa Mifumo ya Chakula Afrika unaofanyika nchini kuanzia tarehe 5-8 Septemba 2023



Rais wa Jamhuri ya Kenya Mheshimiwa William Ruto akitambulishwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba kwa viongozi mbalimbali baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Kenya Mheshimiwa William Ruto akisalimiana na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam





Wednesday, September 6, 2023

RAIS WA SENEGAL AWASILI NCHINI KUHUDHURIA AGRF 2023

Rais wa Jamhuri ya Sénégal Mhe.Macky Sall  amewasili nchini kuhudhuria Mkutano wa Mifumo ya Chakula Afrika unaofanyika nchini kuanzia tarehe 5-8 Septemba 2023.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Dar es Salaam Mhe. Sall alilakiwa na Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Angellah Kairuki.

Mhe.Sall  ni miongoni mwa Wakuu wa Nchi na Serikali, Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa na Marais na Mawaziri Wakuu wastaafu kutoka barani Afrika wanaohudhuria mkutano huo mkubwa unaojadili mifumo ya chakula duniani








WAZIRI MAKAMBA AKUTANA KWA MAZUNGUMZO NA WAZIRI WA VIWANDA NA TEKNOLOJIA YA JUU WA SERIKALI YA UAE

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) amekutana na kuzungumza na Waziri wa Viwanda na Tekinolojia ya Juu wa Serikali ya Umoja wa Falme za Kiarabu, Mhe. Sultan Ahmed Al Jaber Jijini Nairobi, Kenya.

Waziri Makamba amekutana na Mhe. Al Jaber pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabia Nchi unaofanyika Nairobi, Kenya.

Pamoja na mambo mengine, Mhe. Waziri Makamba ameihakikishia UAE kuwa Tanzania itashiriki Mkutano wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi (COP 28) mwezi Disemba 2023, ambapo miongoni mwa masuala itakayoyatilia mkazo ni ufadhili wa miradi ya nishati safi ya kupikia kwa akina mama vijijini.

Aidha, Mheshimiwa Waziri Makamba amesisitiza kuwa Tanzania itaungana na nchi za Afrika na nchi nyingine zinazoendelea duniani, kuhimiza Nchi Wanachama, hususan zilizoendelea kutekeleza ahadi za kupunguza hewa ukaa, kuchangia fedha kwa ajili ya Uhimilivu na kukabiliana na mabadiliko ya Tabianchi na upatikanaji wa teknolojia kwa ajili ya jitihada hizo. 

Kwa upande wake, Mhe. Sultan Ahmed Al Jaber, aliishukuru Tanzania kwa kuahidi kushiriki Mkutano wa COP 28 na kwamba Umoja wa Falme za Kiarabu umejipanga kuhakikisha Mkutano wa COP 28 unaleta matokeo chanya katika jitihada za kukabiliana na athari za mabadiliko ya Tabianchi Duniani. 

Aidha, Mhe. Al Jaber aliahidi kuunga mkono masuala ya kipaumbele ya Tanzania katika Mkutano huo kwa kuzingatia uhusiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na UAE.

Mhe. Al Jaber ni Rais ajaye wa Mkutano wa Cop 28 unaotarajiwa  kufanyika Dubai, mwezi Disemba 2023. 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) akizungumza na na Waziri wa Viwanda na Tekinolojia ya Juu wa Serikali ya Umoja wa Falme za Kiarabu, Mhe. Sultan Ahmed Al Jaber Jijini Nairobi, Kenya. Mazungumzo ya viongozi hao yamefanyika pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabia Nchi unaofanyika Nairobi, Kenya unaofanyika Nchini humo kuanzia tarehe 4 – 8 Septemba 2023.




Rais wa Jamhuri ya Burundi Mhe. Evariste Ndayishimiye amewasili nchini kuhudhuria Mkutano wa Mifumo ya Chakula Afrika unaofanyika nchini kuanzia tarehe 5-8 Septemba 2023.

Katika Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere Dar es Salaam Mhe. Ndayishimiye amepokelewa na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Albert Chalamila.

Mhe. Ndayishimiye ni miongoni mwa Wakuu wa Nchi na Serikali, Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa na Marais na Mawaziri Wakuu wastaafu kutoka barani Afrika wanaohudhuria mkutano huo mkubwa unaojadili mifumo ya chakula duniani

Rais wa Jamhuri ya Burundi Mhe. Evariste Ndayishimiye akiteremka kwenye ndege baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Jijini Dar es Salaam kuhudhuria Mkutano wa Mifumo ya Chakula Afrika unaofanyika nchini kuanzia tarehe 5-8 Septemba 2023

Rais wa Jamhuri ya Burundi Mhe. Evariste Ndayishimiye akisalimiana na viongozi mbalimbali baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Jijini Dar es Salaam kuhudhuria Mkutano wa Mifumo ya Chakula Afrika unaofanyika nchini kuanzia tarehe 5-8 Septemba 2023



Rais wa Jamhuri ya Burundi Mhe. Evariste Ndayishimiye akizungumza na Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavende baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Jijini Dar es Salaam kuhudhuria Mkutano wa Mifumo ya Chakula Afrika unaofanyika nchini kuanzia tarehe 5-8 Septemba 2023



MWANI KUWAKOMBOA WANAWAKE KIUCHUMI ZANZIBAR, MAMA MARIAM MWINYI

Mke wa Rais wa Zanzibar, Mama Mariam Mwinyi ametoa wito kwa wadau kusaidia kilimo cha mwani Zanzibar, zao ambalo amelitaja kuwa linaongoza kwa kuwa na virutubisho vingi kuliko mazao mengine yote duniani.

Mama Mariam Mwinyi ametoa kauli hiyo leo Septemba 06, 2023 alipokuwa anaelezea hatua zinazochukuliwa na taasisi yake ya Maisha Bora kusaidia kilimo cha mwani kwa wananwake kisiwani Zanzibar.

Mama Mariam Mwinyi ambaye alikuwa mmoja wa jopo la watu waliokuwa wanajadili mada kuhusu kubadilisha mifumo ya chakula kwa ajili ya kuleta lishe bora wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula unaondelea katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere tarehe 05 hadi 08 Septemba 2023.

Alisema taasisi yake ilianzishwa miaka miwili iliyopita kwa lengo la kuunga mkono jitihada za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ambayo moja ya malengo yake ni kuendeleza uchumi wa buluu.

“Zanzibar inaongoza barani Afrika kwa kilimo cha zao la mwani ambalo ni chanzo cha tatu kwa kuingizia fedha za kigeni kisiwa chetu, huku asilimia 90 ya watu wanaojihusisha na kilimo hicho ni wanawake”, Mama Mariam Mwinyi alisema.

Aliendelea kueleza kuwa taasisi ya Maisha Bora inasaidia takribani vikundi 16 vyenye watu 20 kila kimoja katika maeneo mbalimbali ili viweze kufaidika kiuchumi na kilimo hicho.

Misaada hiyo ni pamoja na kuvirasimisha vikundi vyao, kuwawezesha kupata mikopo kwa ajili ya kununulia vifaa vya kisasa, mafunzo ya kuogelea pamoja na kuwapatia boti ili waweze kuendesha kilimo chao mbali zaidi baharini kwa sababu ufukweni mwa bahari, hali ya hewa sio muafaka kwa kilimo cha mwani.

Miasaada mingine ni vichanja vya kukaushia mwani na mashine za kuchakata mwani ili kwawezesha kuuza mwani iliyoongezwa thamani ambayo inakuwa na bei nzuri sokoni.

Mama Mariam Mwinyi alihitimisha wasilisho lake kwa kueleza kuwa mwani ni mkombozi wa maisha duni ya wanawake, lishe duni na udumavu kwa watoto kufuatia matumzi tofauti ya zao hilo ikiwa ni pamoja na vipodozi, mbolea na chakula chenye virutubisho vya kutosha.

Mke wa Rais wa Zanzibar, Mama Mariam Mwinyi akijadili mada kuhusu kubadilisha mifumo ya chakula kwa ajili ya kuleta lishe bora wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula unaondelea katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere tarehe 05 hadi 08 Septemba 2023


Mke wa Rais wa Zanzibar, Mama Mariam Mwinyi (katikati) akiwa na wanajopo wenzake wakati wa kujadili mada kuhusu kubadilisha mifumo ya chakula kwa ajili ya kuleta lishe bora wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula unaondelea katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere tarehe 05 hadi 08 Septemba 2023. Kushoto ni Waziri wa Maendeleo ya Kimataifa wa Norway, Mhe. Anne Beathe Tvinnereim

Watu mbalimbali wakisikiliza mada kuhusu kubadilisha mifumo ya chakula kwa ajili ya kuleta lishe bora wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula unaondelea katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere tarehe 05 hadi 08 Septemba 2023.

 

Tuesday, September 5, 2023

TANZANIA IMEDHAMIRIA KUMALIZA TATIZO LA NJAA IFIKAPO 2030

Serikali ya Tanzania imeazimia kutimiza lengo namba 2 la Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDG-2) la kuondoa njaa nchini ifikapo mwaka 2030.

 

Kauli hiyo imetolewa leo Septemba 05, 2023 na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango alipofungua Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam.

 

Kufikia lengo hilo, Makamu wa Rais amesema Serikali imechukua hatua mbalimbali kwa lengo sio tu la kuondoa njaa nchini, bali pia kuwa hazina ya chakula katika kanda na duniani kwa ujumla.

 

Ametaja hatua zilizochukuliwa na Serikali kuwa ni pamoja na kukifanya kilimo kuwa uti wa mgongo na injini ya ukuaji wa uchumi jumuishi. Akifafanua vizuri hatua hiyo, Mheshimiwa Makamu wa Rais alisema asilimia 65 ya watu nchini wamejiajiri katika sekta ya kilimo inayokua kwa asilimia 5 kwa mwaka na hivyo kuchangia asilimia 30 ya mapato ya mauzo ya nje, huku asilimia 65 ya malighafi zinazotumika viwandani nchini zikitoka katika sekta ya kilimo ambayo mchango wake katika pato ghafi la nchi ni asilimia 27 na 21 kwa Tanzania Bara na Zanzibar mutawalia.

 

Hatua nyingine iliyochukuliwa na Serikali ni kuongeza bajeti ya kilimo kwa asilimia 70 kutoka Dola za Marekani milioni 120 mwaka 2021/2022 hadi kufikia milioni 397 mwaka 2023/2024. Amesema hatua hiyo inalenga kuongeza kasi ya mabadiliko ya mifumo katika sekta ya kilimo ili pamoja na mambo mengine, sekta hiyo ikue kwa asilimia 10 kwa mwaka kutoka ukuaji wa asilimia 5.4 ya sasa.

 

Aidha, Mhe. Dkt. Mpango alieleza kuwa Serikali imeweka sera zinazolenga kuinua sekta ya kilimo nchini, kuendesha kilimo kinachozingatia athari za mabadiliko ya tabianchi na kuongeza uwekezaji katika tafiti na elimu kwa wakulima na umma kwa ujumla.

 

Awali, kabla ya Mhe. Makamu wa Rais hajakaribishwa kuhutubia jukwaa hilo, Waziri wa Kilimo, Mhe. Hussein Bashe alisema Afrika haiwezi kufikia azma ya mabadiliko ya mifumo katika sekta ya kilimo kama wanawake na vijana hawatashirikishwa ipasavyo na kuwasihi viongozi wa Afrika washirikiane badala ya kushindana.

 

Naye, Rais wa AGRA, Dkt. Agnes Kalibata amesema mkutano wa mwaka huu ni mkubwa na wa aina yake kuliko mikutano yote iliyofanyika katika miaka ya nyuma. Alisema zaidi ya watu 5000 kutoka nchi 70 duniani walijitokeza kujisajili ili kushiriki Mkutano huo na kusababisha sekretarieti kufunga zoezi la usajili kutokana na idadi ya watu kuwa kubwa kuliko iliyotarajiwa. Awali ilikadiriwa kuwa watu 3000 ndiyo watakaojisajili kushiriki mkutano huo.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Philip Isdor Mpango akisoma hotuba wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Philip Isdor Mpango na Rais wa AGRA, Dkt. Agnes Kalibata  wakizindua ripoti ya hali ya kilimo ya Afrika (Africa Agriculture Status Report- AASR)

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Philip Isdor Mpango akiwa katika picha ya pamoja na viongozi mbalimbali walioshiriki hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Jukwaa la Mifumo ya Chakula unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere.

Waziri wa Fedha, Mhe. Mwigulu Nchemba akisoma baadhi ya mambo kutoka katika kishikwambi huku Mkutano wa Jukwa la Mifumo ya Chakula ukiendelea katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere.
Waziri wa Kilimo, Mhe. Hussein Bashe akifuatilia Mkutano wa Jukwa la Mifumo ya Chakula unaendelea katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere.



MAKATIBU WAKUU SADC WAKUTANA KWA DHARURA KUJADILI HALI YA ULINZI NA USALAMA NCHINI DRC

Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo ameongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa Kamati ya Utatu ya Makatibu Wakuu wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini Mwa Afrika (SADC) uliofanyika kwa mtandao.

Balozi Shelukindo ameshiriki katika Mkutano huo akiwa katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine, mkutano umejadili hali ya ulinzi na usalama mashariki mwa DRC. 

Mkutano huo umefuatiwa na Mkutano wa Kamati ya Mawaziri wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC (SADC MCO) ambapo ujumbe wa Tanzania katika Mkutano huo umeongozwa na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb.) kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.)

Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo akichangia jambo katika Mkutano wa Kamati ya Utatu ya Makatibu Wakuu wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini Mwa Afrika (SADC) uliofanyika kwa mtandao katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Talha Waziri.


Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo akiongoza ujumbe katika Mkutano wa Kamati ya Utatu ya Makatibu Wakuu wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini Mwa Afrika (SADC) uliofanyika kwa mtandao katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Talha Waziri.

Mkutano wa Kamati ya Utatu ya Makatibu Wakuu wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini Mwa Afrika (SADC) ukiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam



WAZIRI MAKAMBA ATEMBELEA ENEO LITAKALOJENGWA UBALOZI NAIROBI , KENYA


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (wa tatu kushoto) katika picha ya pamoja na maafisa Ubalozi na wakandarasi alipotembelea kiwanja cha Ubalozi wa Tanzania kilichopo eneo la UpperHill, Nairobi Kenya.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (wa tatu kushoto) katika picha ya pamoja na maafisa Ubalozi na wakandarasi alipotembelea kiwanja cha Ubalozi wa Tanzania kilichopo eneo la UpperHill, Nairobi Kenya.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (wa tatu kushoto) katika picha ya pamoja na maafisa Ubalozi na wakandarasi alipotembelea kiwanja cha Ubalozi wa Tanzania kilichopo eneo la UpperHill, Nairobi Kenya.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba atembelea kiwanja cha Ubalozi wa Tanzania kilichopo UpperHill, Nairobi Kenya. Ziara hiyo ameifanya tarehe 4 Septemba 2023 kwa lengo kukagua maandalizi ya kuanza ujenzi wa jengo la Ubalozi na kitega uchumi

Akiwa kwenye kiwanja hicho, Waziri Makamba amejionea baadhi ya mahitaji na vifaa muhimu ambavyo vimeanza kukusanywa na Mkandarasi tayari kuanza ujenzi huo.

Mhe. Waziri yuko Nairobi, nchini Kenya kuhudhuria Mkutano wa Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabia Nchi unaofanyika Jijini Nairobi.

Monday, September 4, 2023

TANZANIA KUIUNGA MKONO SAUDI ARABIA EXPO 2023

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeahidi kuiunga mkono Saudi Arabia kuwa mwenyeji wa Maonesho ya Kimataifa ya Biashara mwaka 2030 (EXPO 2030).

Ahadi hiyo imeelezwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo alipoelezea yaliyojiri katika mkutano kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Mjumbe Maalum wa Mfalme wa Saudi Arabia, Mhe. Ahmed Abdulaziz Kattan uliofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam.

Balozi Shelukindo amesema katika kikao hicho Mhe. Rais amemhakikishia mjumbe huyo maalum kuwa Tanzania itashiriki mkutano ya Nchi za Kiarabu na Afrika (Afro Arab Summit) na Mkutano kati ya Saudi Arabia na Nchi za Afrika itakayofanyika Jijini Riyadh mwezi Novemba 2023.

“Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amemhakikishia mjumbe huyo Maalum kuwa Tanzania itaiunga mkono Saudi Arabia kuwa mwenyeji wa Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya mwaka 2030 alisema Dkt. Shelukindo.

Balozi Shelukindo pia aliongeza kuwa Mhe. Rais amemhakikishia mjumbe huyo kuwa Tanzania itashiriki Mkutano kati ya Nchi za Kiarabu na Afrika (Afro Arab Summit) na Mkutano kati ya Saudi Arabia na Nchi za Afrika inayotarajiwa kufanyika Jijini Riyadh, Saudi Arabia mwezi Novemba 2023.

Naye Mjumbe Maalum wa Mfalme wa Saudi Arabia, Mhe. Ahmed Abdulaziz Kattan amesema Saudi Arabia inaishukuru Serikali ya Tanzania kwa kukubali kuiunga mkono kuwa mwenyeji wa Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya mwaka 2030 (EXPO 2030)

“Kwa niaba ya Serikali ya Saudi Arabia tunaishukuru sana Serikali ya Tanzania kwa kuahidi kutuunga mkono kuwa mwenyeji wa Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya mwaka 2030 (EXPO 2030),” alisema Mhe. Kattan.

Aliongeza kuwa Saudi Arabia inamshukuru Mheshimiwa Rais kwa kitendo cha kukubali Tanzania ishiriki katika Mikutano kati ya Nchi za Kiarabu na Afrika (Afro Arab Summit) na Mkutano kati ya Saudi Arabia na Nchi za Afrika itakayofanyika Jijini Riyadh mwezi Novemba 2023

“Kwa niaba ya Serikali ya Saudi Arabia namshukuru Mheshimwa Rais kwa kukubali kutuunga mkono kuwa mwenyeji wa Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya EXPO 2030 na kukubali kushiriki mikutano kati ya Nchi za Kiarabu na Afrika (Afro Arab Summit) na Mkutano kati ya Saudi Arabia na Nchi za Afrika itakayofanyika Jijini Riyadh mwezi Novemba 2023,” aliongeza Mhe. Kattan.

Amesema katika kikao hicho wamejadili pia masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Saudi Arabia na Tanzania katika nyanja mbalimbali.  

Tanzania na Saudi Arabi zimekuwa na uhusiano mzuri na zimekuwa zikishirikiana katika sekta mbalimbali hususan utalii, biashara za bidhaa za nyama, matunda na mazao mengine ya chakula.

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo akizungumza na Mjumbe Maalum wa Mfalme wa Saudi Arabia, Mhe. Ahmed Abdulaziz Qattan katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Mazungumzo baina ya Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo na Mjumbe Maalum wa Mfalme wa Saudi Arabia, Mhe. Ahmed Abdulaziz Qattan yakiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam. Wengine pichani ni Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Mhe. Ali Jabir Mwadini na Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mindi Kasiga.

Mazungumzo baina ya Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo na Mjumbe Maalum wa Mfalme wa Saudi Arabia, Mhe. Ahmed Abdulaziz Qattan yakiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam. Wengine pichani ni Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Mhe. Ali Jabir Mwadini na Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mindi Kasiga.

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo na Mjumbe Maalum wa Mfalme wa Saudi Arabia, Mhe. Ahmed Abdulaziz Qattan wakieleza yaliyojiri katika mkutano kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Mjumbe Maalum wa Mfalme wa Saudi Arabia Ikulu Jijini Dar es Salaam