Friday, November 15, 2013

Idadi kubwa ya watu katika nchi za Afrika na Kiarabu ilete mandeleo, Arab League


Na Ally Kondo, Kuwait

Nchi za Afrika na Kiarabu zimehimizwa kutumia idadi kubwa ya watu wanaoishi katika nchi hizo kama rasilimali ya kujiletea maendeleo ya kiuchumi kwa manufaa ya pande zote mbili. Kauli hiyo ilitolewa na Mwakilishi wa Umoja wa Nchi za Kiarabu wakati alipokuwa anatoa hotuba katika ufunguzi wa Mkutano wa Maafisa Waandamizi wa Ushirikiano baina ya Nchi za Afrika na Kiarabu ulioanza nchini Kuwait siku ya Alhamisi tarehe 14 Novemba, 2013.

 Wakati alipokuwa anafungua rasmi mkutano huo, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Kuwait alieleza kuwa, Serikali ya Kuwait inazithamini na kuzipa kipaumbele nchi za Afrika akitolea mfano namna Mfuko wa Maendeleo wa Kuwait unavyofadhili miradi mingi ya maendeleo ikiwemo ya miundombinu katika nchi za Afrika.

 Naibu Waziri alieleza kuwa theluthi mbili ya nchi za Kiarabu zipo barani Afrika, hivyo alisisitiza umuhimu wa nchi hizo kushirikiana kiuchumi, hususan katika uwekezaji na biashara. Aidha, alisisitiza umuhimu wa mkutano huo kuweka malengo na mikakati thabiti ya utekelezaji ili kukidhi matarajio ya wananchi wa pande zote mbili.

 Kwa upande wa Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Libya ambaye nchi yake ilikuwa Mwenyekiti wa mkutano uliopita, alipongeza ripoti ya pamoja iliyoandaliwa na Sekretariet ya Umoja wa Kiarabu na Kamisheni ya Umoja wa Afrika kwa namna ilivyochambua utekelezaji wa malengo ya Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Ushirikiano baina ya Nchi za Afrika na Kiarabu uliofanyika Sirte, Libya mwaka 2010. Alisisitiza umuhimu wa kuimarisha mikakati ya utekelezaji wa malengo hayo pamoja na kurekebisha mapungufu yaliyobainishwa katika ripoti hiyo ili kuwe na tija kwa wananchi.

 Mwakilishi wa Mabalozi wa Umoja wa Afrika naye aliwasihi wajumbe wa mkutano huo kujadili kwa kina suala la uhamaji ambalo linaonekana kuwa ni changamoto kubwa duniani hivi sasa. Alisisitiza umuhimu wa mkutano huo kutoa mapendekezo ya kukomesha tatizo hilo bila kuathiri maisha ya watu.

 Mkutano wa Maafisa Waandamizi, ambao lengo lake kuu ni kuandaa Mkutano wa Mawaziri wa Mambo ya Nje na Mkutano wa Wakuu wa Nchi  za Afrika na Kiarabu, utamalizika tarehe 15 Novemba, 2013. Mkutano huo, pamoja na masuala mengine, unatarajiwa kujadili namna ya kuoanisha vyombo vya kusimamia utekelezaji wa Mpango Mkakati na Mpango Kazi iliyopitishwa kwenye Mkutano wa Pili wa Ushirikiano baina ya Nchi za Afrika na Kiarabu na pia Kubuni mikakati ya kupata fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya pamoja ya ushirikiano huo.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.