Saturday, November 16, 2013

Tanzania yang`ara eneo bora kiuwekezaji

Mhe. Abdallah Kigoda, Waziri wa Viwanda na Biashara akizungumza kwenye jukwaa la masuala ya biashara la Nchi Wanachama wa  Jumuiya ya Madola  (CBF), jana nchini Sri Lanka.


Tanzania yang`ara eneo bora kiuwekezaji



Tanzania inang’ara na kupanda chati kama eneo bora kiuwekezaji,  kufuatia kujijengea heshima iliyoletwa  na ziara ya Rais wa China Xi Jinping na Barack Obama wa Marekani,  ambao ni viongozi wanaoheshimika kote  duniani .

Haya yalisemwa nchini Sri Lanka kwenye jukwaa la masuala ya biashara la Nchi Wanachama wa  Jumuiya ya Madola  (CBF). Jumuiya hiyo inaundwa na yaliyokuwa makoloni ya Uingereza.

Kadhalika jukwaa hilo lilithibitishiwa kuwa imekuwa rahisi kwa  Tanzania kutambulika kama taifa shindani kiuwekezaji linaloweza kuchuana na majirani zake na mataifa mengine  ya Afrika.

Waziri wa Viwanda na Biashara Dk. Abdallah Kigoda,  alitoa maelezo hayo wakati akizungumza na wajumbe wa jukwaa hilo na kuongeza kuwa faida iliyopatikana kwenye  miradi ya uwekezaji inayoendeshwa na kampuni za ndani na za kigeni imebakizwa nchini kwa ajili  ya kuendeleza uzalishaji.

Hata hivyo, si Waziri Kigoda wala Waziri wa Viwanda na Biashara wa Zanzibar Mwinyikai, alitaja kiasi cha faida hiyo iliyopatikana na kubakizwa nchini kwa ajili ya uwekezaji zaidi.

Aliwaambia wajumbe kuwa serikali inatekeleza mpango wa matokeo makubwa sasa  pia inajizatiti kuimarisha maeneo ya taasisi za fedha, teknolojia ya habari na mawasiliano  na maboresho ya kituo cha taifa cha uwekezaji (TIC)  kukifanya kuwa na uwezo kwa kutoa huduma na mahitaji yote ya wawekezaji.

Sri Lanka pamoja na Tanzania zinaangalia uwezekano wa kuwa na ushirikiano kwenye kuboresha miundombinu na uendeshaji wa bandari ya Dar es Salaam.

Hatua hiyo inakuja wakati Sri Lanka inajenga bandari ya kisasa iitwayo ‘Colombo port city’ ambayo baadhi ya wadau wanaikosoa kuwa itakuwa tishio kwa bandari nyingi ikiwamo   Singapore ambayo ni bandari  huru na kubwa duniani iliyoko kwenye bahari ya Hindi, ikiunganisha mataifa ya Mashariki na Magharibi .

Akizungumza kwenye jukwaa hilo  Mkurugenzi Mtendaji wa TIC  Juliet Kairuki, alisema Tanzania ina uwezekano mkubwa wa kupata wawekezaji zaidi baada ya kuthibitika kuwa ni taifa lisilo na migogoro ya kisiasa.

Alitoa mfano kuwa TIC imepokea maombi ya uwekezaji kwenye nishati ya  joto la asili la ardhini (geothermal) kutoka kampuni ya Marekani wenye thamani ya Dola  milioni 28 (sawa na Sh. bilioni 45.5).


Source:  The Guardian 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.