Tuesday, November 12, 2013

Mkutano wa Ushirikiano baina ya Nchi za Afrika na Kiarabu



Na Ally Kondo, Kuwait

Mkutano wa Ushirikiano baina ya Nchi za Afrika na Kiarabu (Afro – Arab Summit) umeanza nchini Kuwait siku ya Jumatatu tarehe 11 Novemba, 2013 kwa Mfuko wa Maendeleo wa Kuwait (Kuwait Fund) kuandaa Kongamano la Uchumi na Uwekezaji. Mkutano huo unafanyika katika ngazi mbalimbali ukianzia na mkutano wa ngazi ya maafisa waandamizi baadaye  Mawaziri na kuhitimishwa na Mkutano wa Ngazi ya Wakuu wa Nchi na Serikali ambao umepangwa kufanyika tarehe 19 na 20 Novemba, 2013.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mohammed Gharib Bilal atamwakilisha Rais Jakaya Mrisho Kikwete katika mkutano wa ngazi ya Wakuu wa Nchi na Serikali.

Mkutano wa mwaka huu wa Afro –Arab Summit ni watatu kufanyika ambapo wa kwanza ulifanyika Misri katika miaka ya 70 na wa pili ulifanyika mjini Sirte, Libya mwaka 2010. Katika Mkutano wa Libya, Wakuu wa Nchi na Serikali walijiwekea malengo mbambali ambayo utekelezaji wake utatathiminiwa katika mkutano wa mwaka huu nchini Kuwait.

Mkutano wa mwaka huu wenye kaulimbiu isemayo “Wabia katika Maendeleo na Uwekezaji” unadhamiria kuweka mikakati madhubuti ya kushirikiana baina ya nchi za Afrika na Kiarabu katika maeneo mbalimbali ikiwemo kilimo, bishara, uwekezaji, siasa na masuala ya kijamii.

Kwa upande wa sekta ya kilimo, nchi hizo zinakusudia kuimarisha ushirikiano ili kuongeza uzalishaji katika sekta ya kilimo kwa kutumia ardhi kubwa na yenye rutuba iliyopo katika nchi za Afrika ambazo hazina mitaji yakutosha kama zilivyo nchi za Kiarabu. Lengo kubwa la mkakati huo ni kukomesha njaa ya mara kwa mara inayozikumba nchi za Afrika pamoja na kuondoa hali ya wasiwasi wa tishio la njaa linaloweza kutokea katika nchi za Kiarabu.

Katika mkutano huo pia nchi za Afrika na Kiarabu zitajadili namna zitakavyoweza kushirikiana kwa pamoja katika kukabiliana na kudhibiti majanga ya asili ambayo yanapotokea husababisha uharibifu mkubwa wa maisha ya watu na mali zao.

Sanjari na mkutano huo, Serikali za Tanzania na Kuwait zinatarajia kuweka saini Mikataba miwili ya Kukuza na Kulinda Vitega Uchumi; na Ushirikiano katika Sekta ya Utalii. Mikataba hiyo itakaposainiwa itahamisisha uwekezaji pamoja na kuongeza idadi ya watalii kwa manufaa ya nchi hizi mbili. 
   

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.