Monday, July 6, 2015

Rais Kikwete aongoza Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi wa EAC kuhusu Burundi


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Mhe.Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete pamoja na baadhi ya Wawakilishi wa Wakuu wa Nchi Wanachama wakiimba Wimbo wa Jumuiya  hiyo tayari kwa kuanza Mkutano wao Dharura wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya hiyo uliofanyika Ikulu, Dar es Salaam tarehe 06 Julai, 2015.
 Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dkt.Richard Sezibera akisoma Maazimio  yaliyofikiwa katika Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi wa EAC huku Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Rais Kikwete (wa tano kutoka kushoto waliokaa) pamoja na viongozi wengine wakisikiliza kwa makini. Pamoja na mambo mengine Wakuu wa Nchi wamemteua Rais Museveni kusimamia majadiliano ya makundi yanayopingana nchini Burundi na Uchaguzi wa Rais ufanyike tarehe 30 Julai, 2015 badala ya tarehe 15 Julai mwaka huu.
 Katibu mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Balozi Liberata Mulamula (katikati) kwa pamoja na  Katibu Mkuu wa Wizara ya Afrika Mashariki, Bi.Joyce Mapunjo (kulia) pamoja na wajumbe wengine waliohudhuria mkutano huo wakiimba wimbo wa Jumuiya.
  Balozi wa Kenya nchini Tanzania, Mhe. Chirau Ali Mwakere pamoja na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa Kenya, Mhe. Phyllis Kandie 

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bi. Zuhura Bundala akiwa na Wajumbe wengine kabla ya mkutano kuanza
 Balozi wa Tanzania nchini Rwanda, Mhe.Ali Siwa (katikati) na Balozi wa Tanzania nchini Uganda, Mhe.Ladislaus Komba (kulia)  wakati wa mkutano huo.
 Afisa Mwandamizi kwenye Ubalozi wa Tanzania nchini Burundi, Bi. Victoria Mwakasege akiwa na Afisa Mwandamizi, Ofisi ya Rais wakisikiliza maazimio ya wakuu wa nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki yakisomwa.
 Afisa Mwandamizi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Bw.Mkumbwa Ally akijadiliana jambo na Afisa wa Mambo ya Nje, Bi.Samira Diria muda mfupi kabla ya mkutano huo kuanza.
Sehemu ya Wajumbe waliohudhuria mkutano huo uliofanyika Ikulu, Jijini Dar es Salaam.
Maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
 Picha ya pamoja.

Picha na Reuben Mchome
==================================

Wakuu wa Nchi wa EAC wamteua Rais Museveni kusimamia majadiliano nchini Burundi

Mkutano wa Tatu wa Dharura wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kujadili hali ya kisisasa nchini Burundi umefanyika Jijini Dar es Salaam tarehe 06 Julai, 2015 chini ya Uenyekiti wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete.

Katika Mkutano huo ambao umehudhuriwa pia na Rais wa Uganda, Mhe. Yoweri Kaguta Museveni na Mawaziri wa Mambo ya Nje na wale wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki kutoka nchi zote wanachama, umeazimia masuala mbalimbali kwa ajili ya kuhakikisha hali ya kisiasa na utulivu  nchini Burundi inarejea.

Katika mkutano huo, Wakuu wa Nchi wamemteua Rais wa Uganda, Mhe. Yoweri Kaguta Museveni kusimamia majadiliano ya makundi yanayopingana nchini Burundi.

Pia wakuu hao wa nchi wameitaka Serikali ya Burundi kuyanyang’anya silaha makundi yote nchini humo kikiwemo kikundi kinachojiita Imbonera Kure”. Aidha, wameomba Umoja wa Afrika (AU) usimamie zoezi hili kwa kupeleka Timu ya Waangalizi wa Kijeshi ili kuhakikisha linafanikiwa. 

Azimio jingine ni kuvitaka vyombo vya usalama chini ya Sekretarieti ya Maziwa Makuu (ICGLR) kutafiti na kuhakiki uwepo wa kikundi cha waasi cha FDLR nchini Burundi.

Aidha, Wakuu wa Nchi wameitaka Serikali ya Burundi kuahirisha Uchaguzi wa Rais  uliopangwa kufanyika tarehe 15 Julai, 2015 na sasa ufanyike tarehe 30 Julai, 2015 ili kutoa muda kwa msuluhishi kusimamia majadiliano kama ilivyopangwa.

Wakuu hao wa nchi pia wametaka yeyote atakayeshinda nafasi ya Urais nchini Burundi kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa itakayojumuisha vyama vilivoshiriki kwenye Uchaguzi na vile ambavyo havikushiriki.

Pia, Wakuu wa nchi wameitaka Serikali ya Burundi kuheshimu Mkataba wa Amani na Maridhiano wa Arusha wa mwaka 2000 na kutoifanyia marekebisho ya aina yoyote Katiba ya Burundi.

Vilevile, Wakuu hao wa nchi wameiomba AU kuidhinisha na kupitisha maamuzi haya ya EAC na kwamba Jumuiya hiyo ya Afrika Mashariki itatuma Timu ya Waangalizi katika Uchaguzi wa Rais nchini Burundi.

-Mwisho-








No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.