Saturday, December 14, 2019

DKT. SHEIN KUFUNGUA RASMI KONGAMANO LA SITA LA DIASPORA TANZANIA

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, kesho tarehe 15 Desemba 2019, anatarajiwa kufungua rasmi Kongamano la sita la Diaspora Tanzania mjini Zanzibar.

Wizara ya mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi -Zanzibar wamekuwa wakiandaa makongamano ya Disapora kwa kuwakutanisha kila mwaka Watanzania waishio ughaibuni kujadili mambo mbalimbali ikiwemo masuala ya uwekezaji, Utalii, Kilimo na mengine ya maendeleo.

Kongamano hili ni muendelezo wa makongamano mengine matano yaliyofanyika jijini Dar es Salaam, Unguja na Pemba katika miaka ya kuanzia 2014 hadi 2018.
Lengo la kongamano hili la sita ni kuhamasisha na kushirikisha Diaspora katika shughuli za maendeleo nchini. Dhamira ya kongamano hili kuendeleza ushirikiano uliopangwa na Diaspora na wawekezaji kama wadau wa maendeleo nchini chini ya kauli mbiu ya "mtu kwao ndio ngao".

Kongamano hili linatarajiwa kuwa na washiriki zaidi ya 350 wakiwemo Diaspora, Viongozi wa Kitaifa, Wadau mbalimbali kutoka Serikalini na Sekta Binafsi ambapo pamoja na mambo mengine, watajadili mazingira ya uwekezaji na fursa za uwekezaji na utalii ziliopo nchini.

Leo tarehe 14 Desemba 2019 Diaspora na wadau wengine waliowasili wanafanya ziara ya kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii ikiwa ni pamoja na Zanzibar Village Icon na mashamba ya viungo mbalimbali vya chakula.

Mwezi Augusti, 2018 watanzania waishio ughaibuni (Diaspora) walikutana Chake Chake, kisiwani Pemba katika kongamano la tano la Diaspora kufuatia  utaratibu uliowekwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya  Zanzibar  kuwakutanisha kila mwaka Watanzania waishio ughaibuni.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.