Wednesday, December 11, 2019

KATIBU MKUU DKT. MNYEPE ASHIRIKI MKUTANO WA HAKI ZA BINADAMU BEIJING, CHINA.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe yuko nchini China kushiriki Mkutano wa Pili wa Jukwaa la Haki za Binadamu kwa nchi zinazoendelea unaofanyika jijini Beijing nchini humo. 

 Mkutano huu ulioandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje ya China kwa kushirikiana na Ofisi ya Habari ya Baraza la Taifa la nchini humo, unalenga kuzikutanisha  nchi zinazoendelea kwa lengo la kubadilishana taarifa na kujadili kwa pamoja masuala ya Haki za Binadamu.

Dkt. Mnyepe  ambaye pia aliwasilisha salaam za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli katika Mkutano huo amesema, Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi zingine duniani katika kulinda na kutetea Haki za Binadamu na utawala bora sambamba na kuendelea kuheshimu, na kufuata Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu kutoingilia masuala ya ndani ya nchi.

Akizungumza katika mkutano huo Dkt. Mnyepe, ameelezea hatua mbalimbali zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano ambazo kwa kiasi kikubwa zimechangia kuboresha mazingira ya upatikanaji wa huduma za msingi kwa wananchi. 

Hatua hizo ni pamoja  na utelezaji wa sera ya elimu bure, uboreshwaji wa mazingira ya uwekezaji na biashara, kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma za afya, na ujenzi wa miundombinu ya barabara na nishati ambayo itarahisisha na kupunguza gharama za upatikanaji wa huduma kwa wananchi.

Aidha, Katibu Mkuu Dkt. Mnyepe katika mkutano huo ameendelea kusisitiza dhamira ya Tanzania ya kuitaka Jumuiya ya Kimataifa kuondoka vikwazo dhidi ya Zimbabwe. 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe akizungumza kwenye Mkutano wa Pili wa Jukwaa la Haki za Binadamu kwa nchi zinazoendelea unaofanyika jijini Beijing, China.
Sehemu ya hadhira iliyojitokeza kwenye Mkutano wa Pili wa Jukwaa la Haki za Binadamu kwa nchi zinazoendelea wakifuatilia hotuba iliyokuwa ukitolewa na Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe akizungumza kwenye Mkutano wa Pili wa Jukwaa la Haki za Binadamu kwa nchi zinazoendelea unaofanyika jijini Beijing, China.    

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.