Friday, May 4, 2018

Waziri Maas ahitimisha ziara ya siku mbili nchini Tanzania

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Mhe. Heiko Maas akiingia kwenye Ndege aliyokuja nayo tayari kwa kuanza safari ya kurejea nchini Ujerumani mara baada ya kumaliza ziara yake ya siku mbili nchini.
Waziri Maas akiagana na Afisa Mambo ya Nje Bi. Lilian Kimaro, anayeshughulikia dawati la nchi hiyo.
Waziri Haeko Maas akiwa katika picha ya pamoja na maafisa wa Wizara ya Mambo ya Nje.
Watumishi wa Ubalozi wa Ujerumani nchini Tanzania wakiongozwa na Balozi wao wakiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Amerika na Ulaya Bw. Jestas Nyamanga(wa kwanza kulia) pamoja na maafisa Mambo ya Nje Bi. Lilian Kimaro na Bw. Lucas Mayenga mara baada ya kuagana na Waziri Maas.




Thursday, May 3, 2018

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani awasili nchini kuanza ziara ya kikazi

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Zanzibar, Mhe. Issa Haji Gavu (kushoto) akimpokea Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani, Mhe. Heiko Maas alipowasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kuanza ziara ya kikazi ya siku mbili nchini tarehe 03 na 04 Mei, 2018.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani, Mhe. Heiko Maas akisalimiana na Balozi wa Ujerumani nchini, Mhe. Detlef Waechteralipowasili nchini kwa ziara ya siku mbili. Anayeshuhudia ni Mhe. Waziri Gavu.
Mhe. Waziri Maas akisalimiana na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Jestas Nyamanga.


Mhe. Waziri Maas akisalimiana na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Mindi Kasiga huku Bw. Nyamaga akishuhudia
Mhe. Waziri Gavu akizungumza na Mhe. Waziri Maas mara baada ya kumpokea rasmi nchini kwa ajili ya kuanza ziara yake ya siku mbili.


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU FURSA ZA MAFUNZO




TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

FURSA ZA UFADHILI WA MAFUNZO KWA WATUMISHI WA UMMA

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imepokea fursa za ufadhili wa masomo ya muda mrefu katika sekta ya miundombinu chini ya program iitwayo “Global Infrasructure Development Scholarship Program (GIDSP) kutoka Jamhuri ya Korea.

Mafunzo haya ambayo ni kwa ajili ya Watumishi wa Umma yatafanyika katika Chuo Kikuu cha Seoul (UOS) nchini Korea kuanzia mwezi Agosti 2018 hadi Desemba 2019. 

Waombaji wa mafunzo haya wanatakiwa kutuma maombi yao moja kwa moja kwenye Chuo Kikuu cha Seoul (UOS). Maelezo ya ziada kuhusu mafunzo haya na namna ya kutuma maombi yanapatikana kupitia tovuti ya http://isus.uos.ac.kr au maombi yatumwe kwa barua pepe ifuatayo: mipd@uos.ac.kr. Mwisho wa kutuma maombi ni tarehe 18 Mei, 2018.  

Mafunzo haya yanaratibiwa na  Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar es Salaam
03 Mei, 2018


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU ZIARA YA WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA UJERUMANI NCHINI



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI 

Taarifa kuhusu ziara ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani nchini

Waziri wa Mambo ya Nje wa Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani, Mhe. Heiko Maas anatarajia kufanya  ziara ya kikazi ya siku mbili  nchini tarehe 03 na 04 Mei, 2018. 

Lengo la ziara hiyo ni kuimarisha uhusiano uliopo kati ya Tanzania na Ujerumani na kuibua maeneo mapya ya ushirikiano. Waziri huyo atakuja nchini kwa ndege binafsi akiambatana na ujumbe wa watu hamsini (50). 

Hii ni ziara ya kwanza ya Waziri huyo nchini Tanzania na Barani Afrika tangu ateuliwe tarehe 14 Machi, 2018 kwenye wadhifa wa sasa kutoka kwenye wadhifa aliokuwa nao awali wa Waziri wa Sheria. Kwenye ziara yake hii ya awali Barani Afrika, atatembelea nchi mbili tu ambazo ni Tanzania na Ethiopia ambayo ni  Makao Makuu ya Umoja wa Afrika (Afican Union).  Hii inadhihirisha dhamira ya Ujerumani na hasa Waziri huyo mpya wa Mambo ya Nje kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na Tanzania.

Wakati wa ziara hiyo nchini, Mhe. Maas ataonana kwa mazungumzo rasmi na mwenyeji wake, Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga (Mb.), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na baadaye kwa pamoja watakutana na vyombo vya habari kuelezea madhumuni ya ziara ya Waziri huyo nchini.

Aidha, tarehe o4 Mei, 2018, Mhe. Waziri Maas anatarajiwa kuweka shada la maua kwenye Mnara wa Askari (Askari Monument) Jijini Dar es Salaam pamoja na kutembelea Shule ya Sekondari ya Majaribio ya Chang’ombe. 

Siku hiyo hiyo, Mhe. Maas ataondoka Dar es Salaam kuelekea Arusha. Akiwa Arusha Mhe. Waziri Maas atakutana na viongozi wa Mahakama ya Kesi Masalia za Mauaji ya Kimbari (United Nations Mechanism for International Criminal Tribiunals-MICT) na Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu (African Court on Human and Peoples’ Rights). Pamoja na kutembelea Makao Makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. 

Tanzania na Ujerumani zimekuwa na mahusiano mazuri na ya muda mrefu na Tanzania ni kati ya nchi zinazoongoza kwa kunufaika na miradi ya maendeleo inayofadhiliwa na Serikali ya Ujerumani kwenye nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara. Tangu kuanza kwa mahusiano kati ya nchi hizi mbili, Ujerumani imekuwa ikiisadia Tanzania katika maeneo mbalimbali ikiwemo afya, elimu, miundombinu, nishati mbadala, mapambano dhidi ya vitendo vya ujangili na uwindaji haramu.

Mhe. Maas ataondoka nchini tarehe 04 Mei, 2018 kurejea Ujerumani.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar es Salaam, 02 Mei, 2018
-Mwisho-

Wednesday, May 2, 2018

Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Nje washiriki Sherehe za Mei Mosi

Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakisherehekea Siku ya Wafanyakazi Duniani iliyofanyika katika Uwanja wa Uhuru, Jijini Dar es  Salaam. Kaulimbiu ya maadhimisho ya mwaka huu ni "Kuunganishwa kwa Mifuko ya Jamii Kulenge Kuboresha Mafao ya Wafanyakazi"


Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakiwa kati maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani
Juu na Chini ni Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakionesha furaha yao wakati wa maadhimisho ya siku yao duniani.


Maadhimisho yakiendelea.
Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje wakipita mbele ya Mgeni Rasmi ambaye hayupo pichani.


Juu na Chini Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakiwa na nyuso za furaha.




Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kuadhimisha siku ya wafanyakazi duniani




Monday, April 30, 2018

Ubalozi wa Tanzania nchini India ulivyoadhimisha Siku ya Muungano


Mhe. Baraka Luvanda (kulia), Balozi wa Tanzania nchini India akimpokea Mhe. Shri Vijay Goel, Waziri wa Nchi, Masuala ya Bunge na Takwimu wa India katika hafla ya kuadhimisha Siku ya Taifa ya Tanzania iliyofanyika jijini New Delhi tarehe 26 Aprili 2018.
Mhe. Baraka Luvanda (kulia), Balozi wa Tanzania nchini India akiwa katika mazungumzo na Mhe. Shri Vijay Goel, Waziri wa Nchi, Masuala ya Bunge na Takwimu wa India kabla ya kuanza rasmi kwa hafla ya kuadhimisha Siku ya Muungano wa Tanzania.

Balozi Luvanda akiwahutubia washiriki wa hafla ya kuadhimisha Siku ya Muungano wa Tanzania

Balozi Luvanda akigongesheana glasi na Waziri wa Nchi, Masuala ya Bunge na Takwimu wa India ikiwa ni ishara ya kuutakia mema Muungano wa Tanzania uweze kudumu milele.
Mhe. Shri Vijay Goel, Waziri wa Nchi, Masuala ya Bunge na Takwimu wa India (katikati) akionesha jarida kuhusu miaka 54 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar lililoandaliwa na Ubalozi wa Tanzania nchini India na kuzinduliwa rasmi katika hafla hiyo.
Hafla ikiendelea
Mhe. Baraka Luvanda (kulia), Balozi wa Tanzania nchini India akimkabidhi zawadi ya kinyago Mhe. Shri Vijay Goel, Waziri wa Nchi, Masuala ya Bunge na Takwimu wa India.

Picha ya pamoja.