Wednesday, January 30, 2019

Waziri Mahiga ashiriki Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa EAC



Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga akizungumza kama kiongozi wa ujumbe wa Tanzania kwenye  Kikao Maalum cha 38 cha Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kinachofanyika jijini Arusha kuanzia tarehe 30 Januari 2019 ikiwa ni maandalizi ya Mkutano wa 20 wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki utakaofanyika tarehe 1 Februari 2019. Wengine katika picha ni Kapt. Mstaafu, Mhe. George Mkuchika (kushoto), Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Maejimenti ya Utumishi wa Umma na Mhe. Dkt. Philip Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango. Anayeonekana nyuma ya Mhe. Mkuchika ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe.
Mawaziri hao wakipitia nyaraka mbalimbali wakati wa kikao hicho
Mwenyekiti wa Kikao Maalum cha 38 cha Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kutoka Uganda, Mhe. Kirunda Kivejinja (wa pili kulia), ambaye pia ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao cha Baraza hilo.
Ujumbe wa Burundi ukiwa kwenye kikao hicho cha Baraza la Mawaziri
Ujumbe wa Kenya nao ukifuatilia kikao
Mjumbe kutoka Sudan Kusini (kushoto) akiwa katika meza moja na ujumbe wa Rwanda wakati wa kikao cha Baraza la Mawaziri


Ujumbe wa Uganda nao ukifuatilia kikao

Wajumbe wa Tanzania wakiongozwa na Mawaziri wakifuatilia kikao. Kulia ni Naibuu katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bibi Amina KH. Shaaban
Dkt, Aloyce Nzuki, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii akiwa na Bw. Stephen Mbundi, Mkurugenzi wa Idara ya Siasa, Ulinzi na Usalama, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
Balozi wa Tanzania nchini Uganda, Mhe. Dkt. Aziz Mlima (kushoto) kwa pamoja na Kaimu Mkurugenzi katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakifuatilia kikao cha Baraza la Mawaziri 
Wajumbe wengine wa Tanzania
====================================================


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

KUHUSU MKUTANO MAALUM WA 38 WA  BARAZA LA MAWAZIRI WA JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI

Mkutano Maalum wa 38 wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki unafanyika jijini Arusha kwa lengo la kujadili na kukubabaliana na agenda mbalimbali zitakazowasilishwa kwenye Mkutano wa 20 wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya hiyo utakaofanyika tarehe 1 Februari, 2019.

Mkutano huo ambao unaongozwa na Mwenyekiti kutoka Jamhuri ya Uganda ambaye pia ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Kirunda Kivejinja utajadili agenda mbalimbali muhimu ambazo ni pamoja na ripoti ya utekelezaji wa maamuzi mbalimbali yaliyofikiwa na Baraza hilo kwenye vikao vilivyopita; taarifa kutoka Ofisi ya Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, taarifa kuhusu masuala ya miundombinu, forodha na biashara na ripoti ya kamati ya utawala na fedha.

Agenda zingine ni taarifa ya Baraza kwa Wakuu wa Nchi kuhusu utekelezaji wa maamuzi mbalimbali yanayofiwa kwenye mikutano ya Wakuu hao wa Nchi na Kalenda ya Matukio ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa  kipindi cha kuanzia mwezi Januari hadi Juni 2019.

Mkutano huo wa Mawaziri ulitanguliwa na vikao vya Maafisa Waandamizi kutoka nchi wanachama kilichofanyika tarehe 28 Januari kikifuatiwa na kikao cha Kamati ya Uratibu chini ya Makatibu Wakuu kutoka nchi wanachama kilichofanyika tarehe 29 Januri 2019.

Ujumbe wa Tanzania kwenye mkutano huo  unaongozwa na Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na kuwahusisha pia Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi (Mb), Waziri wa , Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Philip Mpango (Mb), Waziri Fedha na Mipango, Mhe. Kapt. Mstaafu George Mkuchika (Mb), Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Mhe. Joseph Kakunda (Mb), Waziri wa Viwanda na Biashara na Mhe. Innocent Bashungwa, Naibu Waziri wa Kilimo.


Jumuiya ya Afrika Mashariki ambayo inaundwa na nchi sita za Tanzania, Kenya, Uganda, Burundi, Rwanda na Sudan Kusini imeendelea kuhakikisha wananchi katika nchi hizo wananufaika na Jumuiya hiyo hususan katika nyanja za biashara, ulinzi na usalama, viwanda, kilimo, miundombinu na huduma za kijamii.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
Arusha.
30 Januari 2019




Tanzania yavutia makampuni ya Saudi Arabia kuja kuangalia fursa za uwekezaji

Baadhi ya wafanyabiashara wa Saudi Arabia wakisikiliza mada kuhusu fursa,vivutio, sheria na  kanuni  za  uwekezaji nchini  katika kongamano lililofanyika Jumatano tarehe 30 Januari, 2019, jijini Dar es salaam. Ziara hiyo inatokana na juhudi za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Africa Mashariki  kupitia Ubalozi wa Saudi Arabia na wadau wengine wa Kushawishi wafanyabiashara wakubwa kuja kuwekeza nchini katika sekta mbalimbali.



Afisa Uhamasishaji Uwekezaji (TIC) Bi Diana Mwamanaga akiwasilisha mada katika kongamano hilo.


Baadhi ya wawakilishi wa taasisi za serikali wakifuatilia mada zilizokuwa zikiwasilishwa.

Afisa Mipango na Uwekezaji wa Shirika la Viwanda Vidogo(SIDO) Bi. Johari Masenge  akiwasilisha mada katika kongamano hilo.

Tuesday, January 29, 2019

Katibu Mkuu aongoza ujumbe wa Tanzania kikao cha Makatibu Wakuu wa EAC



Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe (aliyekaa mbele), Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiongoza ujumbe wa Tanzania kwenye kikao cha maandalizi kabla ya kushiriki kikao cha Makatibu Wakuu wa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kilichofanyika jijini Arusha tarehe 29 Januari 2019. Pamoja na mambo mengine kikao cha Makatibu Wakuu kilipokea na kujadili taarifa mbalimbali zilizowasilishwa kwao na wajumbe wa ngazi ya Wataalam. Kikao cha Makatibu Wakuu kitafuatiwa na kikao cha Baraza la Mawaziri kitakachofanyika tarehe 30 Januari 2019 kwa ajili ya kuandaa Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki utakaofanyika tarehe 1 Februari 2019.
Bw. Stephen Mbundi (katikati), Kiongozi wa kikao cha ngazi ya wataalam ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Siasa, Ulinzi na Usalama katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akitoa taarifa kwa Makatibu Wakuu. Wengine katika picha ni Dkt. Yamungu Kayandabila (kushoto), Naibu Gavana na Bw. Bernard Haule, Kaimu Mkurugenzi, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Evaristo Longopa (wa pili kulia) akichangia jambo wakati wa kikao cha maandalizi ya ushiriki wa Tanzania kwenye kikao cha Makatibu Wakuu kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Wengine katika picha ni Prof. Sifuni Mchome (wa kwanza kulia), Katibu Mkuu, Wizara ya Katiba na Sheria, Prof. Joseph Buchweshaija, Katibu Mkuu, Wizara ya Viwanda na Biashara na Prof. Siza Tumbo, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Kilimo.
Balozi wa Tanzania nchini Uganda, Mhe. Aziz Mlima (kulia) akifuatilia kikao hicho akiwa pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Aloyce Nzuki na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bi. Amina KH. Shaaban
Wajumbe ambao ni Wataalam kutoka Wizara, Idara na Taasisi mbalimbali za Serikali wakifuatilia kikao

Kikao kikiendelea

Wajumbe wengine wakiwa kwenye kikao

Wajumbe wa kikao wakifuatilia kikao 

Wajumbe kutoak Wizara, Idara na Taasisi za Serikali walioshiriki kikao 


Wajumbe wengine nao wakifuatilia kikao


Wataalam wa masuala mbalimbali kutoka Wizara, Idara na Taasisi za Serikali wakiwa kwenye kikao

Wataalam wakinukuu masuala mbalimbali yaliyokuwa yanajadiliwa kwenye kikao hicho
Kikao kikiendelea


Kikao kikiendelea


Wasaudia watafuta Fursa za Kuwekeza katika Viwanda Tanzania

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Wasaudia watafuta Fursa za Kuwekeza katika Viwanda Tanzania

Ujumbe wa wawekezaji wa makampuni makubwa 15 ya Saudi Arabia utafanya ziara nchini Tanzania tarehe 30 na 31 Januari 2019 kwa madhumuni ya kuangalia fursa ya kuwekeza kwenye viwanda.

Ziara hiyo inatokana na juhudi za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kupitia Ubalozi wa Saudi Arabia na wadau wengine  wa kushawishi wafanyabiashara wakubwa kuja kuwekeza nchini katika sekta mbalimbali.

Ujumbe huo wa watu 20, utakapokuwa nchini pamoja na mambo mengine, utashiriki kongamano la biashara litakalofanyika kwenye Hoteli ya New Africa jijini Dar Es Salaam tarehe 30 Januari 2019 kuanzia saa mbili asubuhi. Kongamano hilo litafuatiwa na mazungumzo ya ana kwa ana baina ya wafanyabiashara wa Tanzania na Saudi Arabia.

Kongamano hilo linaloratibiwa na Chama cha Wafanyabiashara, Wenye Viwanda na Wakulima (TCCIA) litatoa fursa kwa wafanyabiashara hao kusikiliza mada mbalimbali kuhusu fursa, vivutio, sheria na kanuni za uwekezaji nchini kutoka taasisi zinazoratibu masuala ya uwekezaji ikiwemo Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC).

Ujumbe huo pia unatarajiwa kufanya mazungumzo na viongozi wa taasisi mbalimbali; zikiwemo Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Mamlaka ya Kuendeleza Biashara Tanzania (TANTRADE), Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) na Mamlaka ya Uwekezaji na Ukuzaji Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA).

Ziara ya ujumbe huo ni moja ya mikakati ya utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje inayojikita katika diplomasia ya uchumi na inalenga kuhamasisha uwekezaji katika sekta ya viwanda ili kutimiza azma ya Serikali ya awamu ya tano chini ya Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda na uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma.
29 Januari 2019
  

Monday, January 28, 2019

Maandalizi ya Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa EAC yaanza jijini Arusha


Bw. Stephen Mbundi, Mkurugenzi wa Idara ya Siasa, Ulinzi na Usalama katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiongoza  Ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano wa  majadiliano kwa ngazi ya Watalaam wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ikiwa maandalizi ya  Mkutano Maalum wa 38 wa  Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) utakaofanyika tarehe 30 Januari 2019 jijini Arusha. Mkutano huu utafuatiwa na ule wa Makatibu Wakuu tarehe 29 Januari 2019. Pamoja na mambo mengine  mkutano wa 38 wa Baraza la Mawaziri utapitia na kujadili agenda mbalimbali ikiwa ni pamoja na taarifa ya utekelezaji wa maazimio yaliyofikiwa na Baraza hilo kwenye vikao vilivyopita; taarifa kutoka Ofisi ya Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo; taarifa kuhusu masuala ya miundombinu, forodha na biashara na  masuala ya utawala na fedha. Mkutano wa 38 wa Baraza la Mawaziri ni maandalizi ya Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki utakaofanyika jijini Arusha tarehe 1 Februari 2019. Kulia ni Bw. Eliabi Chodota, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Kijamii na kushoto ni Bw. Bernard Haule, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Biashara, Uwekezaji na Sekta za Uzalishaji.
Mwenyekiti wa Kamati ya Wataalam (wa pili kushoto)  akizungumza wakati wa mkutano wa maandalizi ya Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofanyika kwenye Makao Makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki jijini Arusha tarehe 28 Januari 2019
Wajumbe kutoka Burundi wakifuatilia mkutano huo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kwuliofanyika jijini Arusha tarehe 28 Januari 2019  ngazi ya wataalam
Wajumbe kutoka Kenya nao wakifuatilia mkutano wa wataalam
Wajumbe kutoka Uganda wakiwa kwenye mkutano
Wajumbe kutoka Tanzania nao wakifuatilia mkutano huo 
Wajumbe wengine kutoka Tanzania nao wakifuatilia mkutano


Wajumbe wa Tanzania kutoka Wizara, Taasisi na Sekta mbalimbali wakishiriki mkutano kwa ngazi ya wataalam

Wawekezaji kutoka Austria wavutiwa na mazingira ya uwekezaji nchini

Afisa mwandamizi wa Ubalozi wa Austria wenye makazi yake Nairobi, Kenya. Bw. Kurt Muellauer akifungua Kongamano la Biashara lililoandaliwa kwa ushirikiano kati ya Chama cha Wafanyabiashara, Wakulima na Wenyeviwanda Tanzania (TCCIA) na Ubalozi wa Austria. Kongamano hilo nimwendelezo wa jitihada za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kushirikiana na Ubalozi wa Tanzania nchini Ujerumani ambao unawakilisha pia nchini Austria na wadau mbalimbali katika kutekeleza diplomasia ya uchumi. Pamoja na mambo mengine kampuni 8 kati 16 zinatarajiwa kufanya ziara jijini Dodoma tarehe 29 Januari kwa lengo la kukutana na Mawaziri wa Kilimo; Nishati; Fedha na Mipango; Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Watoto na Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Kongamano hilo limefanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es salaam.
Mkurugenzi wa Uhamasishaji Uwekezaji wa TIC, Bw. John Mnali, pamoja na wadau wengine wakimsikiliza kwa makini Bw.Muellauer (hayupo pichani). 
Baadhi ya wawekezaji kutoka Austria nao wakifuatilia kongamano hilo.
Kaimu Rais wa Chama cha Wafanyabiashara, Wakulima na Wenyeviwanda Tanzania (TCCIA), Bw. Octavian Mshiu, akizungumza katika ufunguzi wa kongamano hilo, ambapo alitumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji nchini na kuunga mkono Sera ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, ya Uchumi wa Viwanda nchini.  


 Juu na chini wadau wakiendelea kufuatilia mada mbalimbali wakati wa kongamano

Afisa wa Uhamasishaji Uwekezaji (TIC), Bi. Diana Ladislaus akizungumzia fursa za uwekezaji nchini wakati wa kongamano hilo.
Kongamano likiendelea.
Tunataka tushirikiane ili tuweze kuwekeza nchini Tanzania 
Majadiliano yanayoonesha dalili ya kuzaa matunda ya ushirikiano kati ya Wafanyabiashara wa Tanzania na Austria










Sunday, January 27, 2019

Ziara ya Kampuni kubwa za uwekezaji kutoka Austria na India


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Ziara ya Kampuni kubwa za uwekezaji kutoka Austria na India
Ujumbe wa Makampuni 16 makubwa ya uwekezaji kutoka Austria utafanya ziara ya kikazi hapa nchini kuanzia tarehe 28 hadi 30 Januari, 2019.

Ziara ya ujumbe huo nchini ni mwendelezo wa jitihada za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kushirikiana na Ubalozi wa Tanzania nchini Ujerumani ambao unawakilisha pia nchini Austria na wadau mbalimbali katika kutekeleza diplomasia ya uchumi.  Pamoja na mambo mengine, diplomasia ya uchumi inalenga kwenye kutafuta na kuleta wawekezaji wenye nia ili wawekeze katika maeneo mbalimbali hapa nchini kwa lengo la kukuza uchumi na kuinua kipato cha wananchi.

Makampuni hayo ya Austria yana nia ya kuangalia fursa za uwekezaji hapa nchini katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, mawasiliano ya simu, umeme wa kutumia maji na usafirishaji.

Ukiwa nchini, ujumbe wa Kampuni 8 umeomba kuonana na kufanya majadiliano na viongozi wa Wizara mbalimbali tarehe 29 Januari, 2019 jijini Dodoma akiwemo Mhe. Japhet Ngailonga Hasunga (Mb.), Waziri wa Kilimo; Mhe. Dkt. Medard Kalemani (Mb.), Waziri wa Nishati; Mhe. Dkt. Philip Mpango (Mb.), Waziri wa Fedha na Mipango; Mhe. Ummy Mwalimu (Mb.), Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Watoto na Mhe. Mhandisi Isack Kamwelwe, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Lengo la ujumbe huo kukutana na Mawaziri hao ni kutaka kufahamu kuhusu kazi na miradi mbalimbali inayosimamiwa na kutekelezwa na wizara hizo ili waone namna ya kuwekeza katika maeneo hayo.


Aidha, ujumbe huo utashiriki kwenye Kongamano la Biashara lililoandaliwa kwa ushirikiano kati ya Chama cha Wafanyabiashara, Wakulima na Wenyeviwanda Tanzania (TCCIA) na Ubalozi wa Austria. Kongamano hilo litafanyika kwenye Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam tarehe 28 Januari 2019.

Serikali ya Tanzania na Austria zina mahusiano ya kidiplomasia ya muda mrefu tangu uhuru ambapo Austria imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali kupitia mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs) hapa nchini hususan katika sekta ya kilimo, afya na kuwajengea uwezo wanawake. Ziara ya ujumbe wa makampuni hayo ni dalili njema za kuanza kuimarika zaidi kwa mahusiano kati ya Tanzania na Austria.

Wakati huohuo, Ujumbe wa wawekezaji kutoka Kampuni ya Bureau Facility Services Pvt Ltd (CISB) ya India utafanya ziara hapa nchini kuanzia tarehe 29 Januari hadi 05 Februari 2019. Ziara hiyo ina lengo la kukamilisha utaratibu wa kuwekeza katika maeneo kadhaa ikiwemo ujenzi wa kiwanda cha madawa, kutafuta fursa ya kuwekeza kwenye miundombinu kama vile barabara na madaraja na ujenzi wa nyumba na hoteli. Wajumbe hao wanatarajia kukutana na kufanya mazungumzo na Mawaziri na Viongozi Wakuu Waandamizi wa sekta husika.

Ujumbe huo wa watu watatu utaongozwa na Bw. Alban Rodricks kutoka CISB ambaye alishafanya ziara hapa nchini mara kadhaa. Aidha, Ujumbe huo unatarajiwa kukutana na kufanya mazungumzo na Mhe. Hamisi Kigwangala (Mb.), Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Ummy A. Mwalimu (Mb.), Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto na Mhe. Mhandisi Isack Kamwelwe (Mb.), Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano pamoja na Mhe. Angellah Kairuki (Mb), Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Uwekezaji.

Katika ziara yao hiyo fursa mbalimbali za kiuwekezaji zinatarajia kuibuliwa pamoja na kujadiliana namna bora ya kushirikiana kati ya Tanzania na India.


Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma.
27 Januari 2019

Kuwahudumia Wakimbizi ni jukumu la Wote sio la Nchi moja

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Kuwahudumia Wakimbizi ni jukumu la Wote sio la Nchi moja

Kazi ya kuwahudumia wakimbizi ni Ubinadamu na ni jukumu la kimataifa na ni kitu cha kushangaza kuona nchi zilizoendelea zinaziachia nchi masikini kubeba mzigo wa kugharamia wakimbizi.
Kauli hiyo ilitolewa na Rais Mstaafu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ni Mwenyekiti mwenza wa Baraza la Wakimbizi Duniani (World Refugees Council-WRC), Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete wakati wa kuwasilisha ripoti ya Baraza hilo kwenye Umoja wa Mataifa New York, Marekani tarehe 24 Januari 2019.
Rais Mstaafu alitanabainisha kwamba Baraza lao lilipokea msimamo wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa kukataa mpango wa kukopa Benki ya Dunia ili kuwahudumia wakimbizi wakati yenyewe inadaiwa mikopo ya kimaendeleo iliyonayo. Serikali inaamini kazi ya kuhudumia wakimbizi ni ya kibinadamu kwa kushirikiana na Jumuiya ya Kimataifa badala ya kuibebesha nchi moja mzigo wa madeni.

Taarifa hiyo imebainisha kuwa tatizo la wakimbizi limekuwa kubwa sana duniani wakati huu kuliko wakati wowote ule tangu vita vya Pili vya Dunia.  Mathalan, kuna idadi ya watu milioni 68.5 waliopoteza makwao (Internally displaced persons) mwaka 2017 na kati yao, milioni tatu wamepoteza makwao kwa sababu ya mabadiliko ya hali ya hewa na uchafuzi wa mazingira.
Ripoti inaeleza kuwa, kumekuwa na ongezeko kubwa la wakimbizi na wanaopoteza makwao kusini mwa jangwa la Sahara ambao walifikia milioni 18.4 mwaka 2017 ukilinganisha na idadi ya milioni 14.1 mwaka 2015.
Ripoti inabainisha kuwa ongezeko hilo limetokana na sababu mbalimbali zikwemo upvotevu wa amani katika nchi zao.
 Ripoti inazidi kubainisha kuwa asilimia 30 ya watu wote duniani mwaka 2017 walikuwa wakimbizi na waliopoteza makwao ukilinganisha na asilimia 23 ya mwaka 2015. Kati ya idadi hiyo, wanaotoka Afrika, asilimia 79% wanatoka katika nchi za Somalia, Nigeria, Sudan kusini na Jamhuri ya Afrika ya Kati. 
Ripoti imeeleza nchi zinazopokea wakimbizi wengi kuwa ni pamoja na Uganda, wakimbizi milioni moja na laki nne; Ethiopia, laki Tisa; Tanzania laki tatu na ishirini na Sita elfu; na Rwanda elfu 84.  Baadhi ya nchi zimechukua wakimbizi hao ikiwemo Marekani, Canada, Australia na Finland ingawa idadi yao ni ndogo mno. 
Katika ripoti hiyo, baraza limetoa mependekezo mbalimbali ya kukabiliana na tatizo la wakimbizi duniani.  Mapendekezo makubwa ni pamoja na kudhibiti nchi ambazo zinachochea au kuanzisha migogoro kwa kuweka mfumo thabiti wa kimataifa, kuongeza usuluhishi wa migogoro, kutowanyanyapaa wakimbizi kwa kujenga ukuta na kusaidia juhudi za kutafuta amani katika maeneo yenye migogoro. 
Baraza la Wakimbizi duniani ni chombo kilichoundwa na wataalamu mbalimbali wakiwemo wanasiasa, watafiti na watunga sera kwa lengo la kufanya utafiti wa kina utakaosaidia kubuni njia na mbinu za kitaalamu na za ubunifu zitakazosaidia kukabiliana na kumaliza kabisa tatizo la wakimbizi duniani.
  
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma
27 Januari 2019

Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti Mwenza wa Baraza la Wakimbizi Duniani (World Refugees Council, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete (mstari wa mbele wa kwanza kushoto) akiwa na viongozi mbalimbali jijini New York baada ya Baraza hilo kuwasilisha ripoti kwenye Umoja wa Mataifa ya namna ya kukabiliana na tatizo la wakimbizi duniani. Picha inaonesha kitabu cha ripoti iliyowasilishwa.

Mheshimiwa Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Mhe. Balozi Modest J. Mero (kushoto) na viongozi wengine wa Baraza la Wakimbizi Duniani.

Saturday, January 26, 2019

Dkt. Mahiga amwakilisha Rais katika Jukwaa la Uchumi Duniani

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Dkt. Mahiga amwakilisha Rais katika Jukwaa la Uchumi Duniani

Tanzania imesisitiza umuhimu wa kukabili uhaba wa chakula kwa kuzalisha mazao kwa kutumia utalaamu wa kisasa kwa kuwpatia wakulima pembejeo na masoko ya uhakika ya chakula cha ziada.

Kauli hiyo ilitolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga (Mb) wakati wa kuchangia mjadala unaohusu uhakika wa chakula na changamoto za uhaba wa chakula duniani katika mkutano wa Jukwaa la Uchumi Duniani (World Economic Forum-WEF) unaofanyika Davos, Uswisi kuanzia tarehe 22 hadi 25 Januari 2019.

Mhe. Mahiga alimuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli katika jukwaa hilo ambalo kaulimbiu ya mwaka huu ni Kutengeneza Mazingira ya Utandawazi wa Dunia kwa ajili ya Mapinduzi ya Kisasa ya Nne ya Viwanda “Shaping a Global Architecture in the Age of the Fourth Industrial Revolution”.

Katika mkutano huo, ajenda kuu zilizojadiliwa ni pamoja na Mapinduzi ya Nne ya Viwanda, Agenda ya Afrika ya Maendeleo, Hali ya Ulinzi na Usalama Pembe ya Afrika, changamoto za biashara ya kimataifa, ushirikiano wa Bara la Ulaya na Afrika katika ajenda mpya ya maendeleo.

Tanzania ilialikwa kuchangia mjadala unaohusu uhakika wa chakula na changamoto za uhaba wa chakula duniani pamoja na ajenda ya uwezeshaji wa mawasiliano ya simu za mkononi. Katika ajenda hiyo, Tanzania ilitoa wito wa umuhimu wa teknolojia katika kuboresha utaalamu katika sekta ya kilimo kwa ajili ya kuwawezesha wakulima wadogo waliopo vijijini.

Hili ni Jukwaa la pekee ambalo linakutanisha kwa pamoja Viongozi wa Serikali kutoka mabara yote duniani, Taasisi na Mashirika ya Kimataifa, Viongozi wa Makampuni Makubwa ya Kibiashara kwa ajili ya kujadili maendeleo na mwelekeo wa uchumi duniani.

Kando ya Mkutano huo, Mhe. Dkt. Mahiga alikutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa mashirika na makampuni ambayo yapo Tanzania na yanayohitaji kupanua wigo kama vile Tigo na General Electric na makampuni yanayotafuta fursa za kuwekeza Tanzania. Aidha, alikutana na Rais wa WEF, Mhe. Borge Brende ambapo aliahidi kushawishi wawekezaji kuwekeza Tanzania na kuandaa Jukwaa la wawekezaji wa kimataifa la Tanzania ili waweze kuwekeza Tanzania.

Viongozi wengine waliokutana na Waziri Mahiga ni pamoja na; Bw. Scott Strazik, Rais na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Gesi yenye Makao makuu yake Atlanta, Georgia- Marekani; Bw. Richard Hatchett, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Kupambana na magonjwa ya Mlipuko (Coalition for Epidermic Preparedness Innovations); Bi. Rachel Samren, Makamu wa Rais wa Kampuni ya Kimataifa ya Millicom ambayo TIGO ni Tawi la Kampuni hiyo, na Bw. Mohamed Al-Beity, Mtanzania aliyetambuliwa na Jukwaa la Uchumi Duniani kwa mradi wa kutangaza Utalii wa Tanzania kwa njia ya Mtandao (Tanzania Digital Tourism).


Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma
 26 Januari 2019
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga (Kulia) akichangia Mjadala wa Changamoto za Usalama na uhaba wa Chakula Duniani tarehe 24 Januari 2019 Davos, Uswisi
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine akizungumza na Rais wa WEF, Mhe. Borge Brende tarehe 25 Januari 2019 Davos, Uswisi
Mhe. Waziri Mahiga akifanya mazungumzo na  Bi. Rachel Samren, Makamu wa Rais wa Kampuni ya Kimataifa ya Millicom (Millicom International Cellular S.A) tarehe 25 Januari 2019 Davos, Uswisi.