Tuesday, June 14, 2022

WAZIRI MULAMULA AKUTANA NA UONGOZI WA OFISI YA MPANGO WA USIMAMIZI WA MIGOGORO (CMI) YA NCHINI FINLAND

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula akiongea na uongozi wa Ofisi ya Mpango wa Usimamizi wa Migogoro tarehe 13 Juni 2022 kwenye Makao  Makuu ya taasisi hiyo nchini Finland. Mazungumzo yao yalijikita kwenye masuala ya amani na usalama katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika. Pia Mhe. Waziri akaeleza amani na usalama wa ukanda huo ni kipaumbele kwakuwa huziwezesha nchi kupata utulivu wa kufanya shughuli za maendeleo na kuinua uchumi wa Taifa na maisha ya wananchi kwa ujumla.

Kutoka kushoto ni Naibu Mtendaji Mkuu wa Ofisi ya Usimamaizi wa Migogoro, Bi. Hanna Klinge na Mkuu wa Mpango huo Kusini mwa Jwangwa la Sahara, Bi.Tiina Kukkamaa-Bah akitoa taarifa ya utekelezaji wa mipango mbalimbali  katika taasisi hiyo, hususani katika ukanda wa Kusini mwa Afrika na Afrika Mashariki.


Mazungumzo yakiendelea, Kulia kwa Mhe. Waziri ni Balozi wa Tanzania nchini Finland mwenye makazi yake nchini Sweden, Mhe. Grace Alfred Olutu na Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga wakifuatilia mazungumzo

Kutoka kushoto ni Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na America katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme na Afisa Mambo ya Nje, Bi. Tunsume Mwangombole wakifuatilia mazungumzo

Picha ya pamoja

 

WAZIRI MULAMULA ZIARANI NCHINI FINLAND



Helsinki, 14 Juni 2022


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula amewasili nchini Finland kwa ziara ya siku 3 kushiriki Mkutano wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Nchi za Afrika na Nchi za Nordic (NORDIC-AFRICA) unaofanyika kuanzia tarehe 13 hadi 15 Juni 2022 jijini Helsinki, Finland. 


Mkutano huo umeanza na hafla ya ufunguzi iliyofanyika tarehe 13 Juni 2022, ambapo mgeni rasmi alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Finland, Mhe. Pekka Haavisto.

 

Akiwakaribisha wajumbe wa mkutano huo Mhe. Haavisto alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano katika kujiletea maendeleo baina ya nchi hizo marafiki.

 

Aidha, mkutano huu utahusisha nchi 5 za Nordic ambazo ni Finland mwenyeji wa mkutano wa sasa, Sweden, Norway, Iceland na Denmark na nchi za Afrika 25 marafiki wa Nordic. 

 

Mkutano huo wa Mawaziri wa Mambo ya Nje utahusisha Mabalozi wa nchi shiriki za Afrika zinazowakilisha katika nchi za Nordic na Mabalozi wa nchi za Nordic wanaowakilisha katika Nchi shiriki za Afrika.

 

Wazo la kuanzisha mkutano huu lilianza mwaka 2000 ambapo mkutano wa kwanza ulifanyika nchini Sweden mwaka 2001. Baada ya hapo mikutano kama hii inafanyika kwa kupokezana kutoka Bara la Afrika na upande wa Nordic.

 

Mwaka 2019 Tanzania ilikuwa mwenyeji wa mkutano huu ambapo nchi takribani 34 zilishiriki katika mkutano.

 

Wakati huo huo Mhe. Waziri Mulamula ametumia fursa ya ziara hiyo kutembelea Makao Makuu ya Ofisi ya Mpango wa usimamizi wa migogoro nchini Finland na kukutana na uongozi wa mpango huo. Lengo la likiwa kujadili masuala ya amani na usalama katika ukanda wa Afrika Mashariki na ukanda wa kusini mwa Afrika.

 

Katika mazungumzo yake Waziri Mulamula ameeleza kuwa Tanzania inaendelea kuwa mstari wa mbele katika kusimamia masuala ya amani na usalama ili kuwezesha nchi za ukanda huo kufanya shughuli za kiuchumi na kuinua maendeleo ya taifa na wananchi kwa ujumla.


 -Mwisho-


Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 




Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula akifuatilia hotuba wakati wa hafla ya ukaribisho kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Finland na mwenyeji wa Mkutano wa 19 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Nchi za Afrika na Nchi za Nordic (NORDIC - AFRICA), Mhe. Pekka Haavisto unaofanyika tarehe 13 hadi 15 Juni 2022 jijini Helsinki, Finland. Kushoto ni Balozi wa Heshima wa Tanzania nchini Finland, Dkt. Vesa Viitaniemi.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Finland, Mhe. Pekka Haavisto akifungua hafla ya kuwakaribisha wajumbe wa mkutano wa 19 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Nchi za Afrika na Nordic unaofanyika tarehe 13 hadi 15 Juni 2022 jijini Helsinki nchi humo.

Sehemu ya wajumbe wa mkutano huo wakifatilia hotuba ya Mhe. Haavisto.

Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Grace Alfred Olotu (kati) pamoja na Afisa Ubalozi katika ubalozi huo wakisalimiana na wajumbe wengine wa mkutano wakati wa hafla hiyo.

Hafla ikiendelea, Mhe. Waziri Mulamula akisamilimiana na wajumbe wengine wa mkutano huo. Kulia ni Mhe. Balozi Liberata Mulamula.

Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme akifuatilia hafla ya ukaribisho ya mkutano huo.


Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga akisalimiana na mshiriki wa mkutano huo.


 

 

 

Saturday, June 11, 2022

MAKATIBU WAKUU WANAOSIMAMIA SEKTA MBALIMBALI WA NCHI ZA EAC WAKUTANA JIJINI ARUSHA


Mkutano wa 42 wa Kawaida wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki katika ngazi ya Makatibu Wakuu umefanyika leo tarehe 11 Juni 2022 katika Makao Makuu ya Jumuiya jijini Arusha.

Mkutano huo ambao umetanguliwa na mkutano wa Maafisa Waandamizi uliofanyika tarehe 8 na 9 Juni 2022 ulikuwa jukumu maalumu la kupokea na kupitia taarifa, agenda na mapendekezo yaliyotokana na Mkutano wa Maafisa Waandamizi kuhusu masuala mbalimbali ya Jumuiya na hatimaye, kuyawasilisha katika Mkutano wa Mawaziri utakaopangwa kufanyika baadaye mwaka huu. 

Miongoni mwa masuala yaliyojiri katika mkutano huo ni uzingatiwaji wa ripoti mbalimbali ikiwemo ripoti ya kutoa mwelekeo wa kuanza kutumika kwa lugha ya Kifaransa na Kiswahili katika uendeshaji wa shughuli za kiofisi/rasmi za Jumuiya. 

Katika Mkutano huo ujumbe wa Tanzania umeongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe

Viongozi wengine walioambatana naye ni pamoja na, Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Mary Makondo, Katibu Mkuu Afisi ya Rais Kazi, Uchumi na Uwekezaji –Zanzibar Bi. Khadija Rajab Khamis, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Bi. Amina Kh. Shaaban, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw. Gerald Mweli na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi Umma na Utawala Bora Bw. Xavier Daudi. Wengine waliombatana naye ni Balozi Stephen P. Mbundi Mkurugenzi wa Siasa, Ulinzi na Usalama, Bw. Bernard Haule Mkurugenzi Biashara, Uwek ezaji na Sekta za Uzalishaji na Bw. Eliabi Chodota, Mkurugenzi Idara ya Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Jamii, wote wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki pamoja na Maafisa kutoka Wizara mbalimbali. 

Mkutano huo uliofanyika kwa njia mseto (video na ana kwa ana) umehudhuriwa na nchi zote wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, ukiongozwa na Mwenyekiti wake Bw. Saitoti Torume CBS ambaye ni Katibu Mkuu wa Hazina na Mipango kutoka Jamhuri ya Kenya 

Baraza la Mawaziri ni chombo cha kutunga sera za Jumuiya. Baraza hilo linajumuisha Mawaziri wanaosimamia Masuala ya Jumuiya ya Afrika Mashariki au Ushirikiano wa Kikanda.

Miongoni mwa majukumu ya Baraza la Mawaziri la Jumuiya ni kufuatilia na kufanya mapitio ya mara kwa mara juu ya utekelezaji wa programu za Jumuiya na kuhakikisha utendaji kazi mzuri wa Jumuiya
Makatibu Wakuu wanaosimamia sekta mbalimbali katika nchi za Afrika Mashariki wakifurahia jambo kwenye Mkutano wa 42 wa Kawaida wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofanyika jijini
Meza Kuu kutoka kulia ni; Bw. Severin Mbarubukeye Katibu Mkuu anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki, Vijana Michezo na Utamaduni kutoka Burundi, Bi. Edith Mwanje Katibu Mkuu Wizara ya Afrika Mashariki kutoka Uganda, Bw. Saitoti Torume CBS, Katibu Mkuu wa Hazina na Mipango kutoka Kenya, Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe Katibu Mkuu Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na Bw. Adrea Aguer Ariik Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afrika Mashariki ya Jamhuri ya Sudan Kusini wakiwa kwenye Mkutano wa 42 wa Kawaida wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofanyika jijini
Mkutano wa 42 wa Kawaida wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ukiendelea jijini Arusha.
Mkutano wa 42 wa Kawaida wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ukiendelea jijini Arusha.
Mkutano wa 42 wa Kawaida wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ukiendelea jijini Arusha

Friday, June 10, 2022

ITALIA KUANZISHA UPYA SAFARI ZA NDEGE ZANZIBAR

Na Mwandishi wetu, Dar

Katika kukuza na kuendeleza diplomasia ya uchumi Serikali ya Italia imeahidi kuanzisha upya safari za ndege za moja kwa moja kutoka nchini humo hadi Zanzibar kuanzia tarehe 29 Juni 2022.

Ahadi hiyo imetolewa na Inspekta Jenerali kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Italia, Balozi Natalia Quintavalle wakati alipokutana kwa mazungumzo na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb) katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Pamoja na mambo mengine, Balozi Natalia amesema kuwa kuanzishwa kwa safari za ndege za moja kwa moja kutoka Italia hadi Zanzibar zitasaidia kukuza biashara na utalii baada ya kusitishwa kwa safari hizo tangu mwaka 2019 kutokana na changamoto ya Uviko 19.

Nae Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk amesema kuanzishwa upya kwa safari hizo kutachangia kukuza pato la taifa kwani awali kabla ya janga la Uviko 19, Zanzibar ilikuwa inapata watalii 200,000 kwa mwezi kutoka nchini Italia.

“Safari za ndege za moja kwa moja kutoka Italia kuja Zanzibar zinategemea kuanza rasmi tarehe 29 Juni, 2022 na tunaamini kuwa kuanzishwa kwa safari hiyo kutachangia kukuza sekta ya utalii na uchumi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla,” amesema Balozi Mbarouk

Tanzania na Italia zimekuwa zikishirikiana katika nyanja mbalimbali ikiwemo afya, elimu, utalii, viwanda, maji, kilimo, nishati, pamoja na maendeleo ya sekta binafsi. 


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akimueleza jambo na Inspekta Jenerali kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Italia, Balozi Natalia Quintavalle wakati alipokutana kwa mazungumzo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Inspekta Jenerali kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Italia, Balozi Natalia Quintavalle akimfafanulia jambo Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk walipokutana kwa mazungumzo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Mazungumzo baina ya Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk na Inspekta Jenerali kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Italia, Balozi Natalia Quintavalle yakiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk katika picha ya pamoja na Inspekta Jenerali kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Italia, Balozi Natalia Quintavalle baada ya mazungumzo yaliyofanyika katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam



BALOZI MULAMULA AWASILISHA UJUMBE MAALUM WA RAIS SAMIA KWA RAIS WA MISRI

 Na Mwandishi wetu

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) amewasilisha Ujumbe Maalum wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia  Suluhu Hassan kwa Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri Mhe. Abdel Fattah El-Sisi Jijini Cairo.

Pamoja na mambo mengine, Balozi Mulamula aliwasilisha salamu za Mhe. Rais Samia kwa Rais El-Sisi, alisisitiza umuhimu wa kuendelea uhusiano wa kihistoria na ushirikiano katika sekta mbalimbali, za kimkakati hususan Ulinzi na Usalama, Elimu, Nishati na Mifugo. 

Aidha, baada ya mazungumzo na Mhe. Rais El-Sisi alikutana na kwa mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Misri, Mhe. Sameh Shoukri na kisha alifanya mahojiano na waandishi wa habari.

Moja wa Masuala ya msisitizo ni kuiunga mkono Misri kwa kuwa mwenyeji wa Mkutano wa Mazingira COP27 utakaofanyika katika Jiji la Sharma Al Sheikh mwezi Novemba, 2022 na kuahidi kuendeleza ushirikiano katika sekta za Afya, Elimu na nyinginezo kwa manufaaa ya Nchi hizi mbili.

Pia Balozi Mulamula alitumia mazungumzo hayo kuishukuru Misri kwa misaada mbalimbali inayoipatia Tanzania katika sekta za kimkakati pamoja na kuiunga mkono Tanzania katika mipango yake ya maendeleo kwa manufaa ya nchi zote mbili.

Katika Mazungumzo hayo, Balozi Mulamula na Mhe. Shoukri walikubaliana kufanya Mkutano wa Nne wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano (JPC) utakaofanyika Nchini Tanzania mwezi Desemba, 2022 baada ya Mkutano wa Mabadiliko ya Tabia Nchi (COP-27).

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiwasilisha Ujumbe Maalum wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia  Suluhu Hassan kwa Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri Mhe. Abdel Fattah El-Sisi Jijini Cairo

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiwasilisha Ujumbe Maalum wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia  Suluhu Hassan kwa Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri Mhe. Abdel Fattah El-Sisi Jijini Cairo

 Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri Mhe. Abdel Fattah El-Sisi Jijini Cairo akisoma Ujumbe Maalum wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia  Suluhu Hassan. Kushoto ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akifuatilwa na Balozi wa Tanzania nchini Misri, Dkt. Emmanuel Nchimbi. 


OACPS YATENGA EURO MILIONI 157 KUKOPESHA WAKULIMA KUONGEZA MNYORORO WA THAMANI MAZAO YA KILIMO

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Joseph Sokoine akizungumzia maazimio yaliyofikiwa katika Mkutano wa 114 wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya OACPS uliofanyika jijini Brussels nchini Ubelgiji tarehe 8 na 9 Juni 2022 ambapo alimwakilisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula katika mkutano huo.

 

 


 

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Joseph Sokoine (aliyekaa katikati) akiwa na Ujumbe wa Tanzania ulioshiriki Mkutano wa 114 wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya OACPS uliofanyika jijini Brussels nchini Ubelgiji tarehe 8 na 9 Juni 202. Kushoto aliyekaa ni Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji Mhe. Jestas Nyamanga na kulia aliyekaa ni mwakilishi wa Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Marekani Bi Agnes Kiama.



 

Jumuiya ya Nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki (OACPS) umetenga kiasi cha Euro milioni 157 kukopesha wadau wa kilimo katika nchi wanachama kwa masharti nafuu ili kuwekeza kwenye sekta ya kilimo na hivyo kuongeza mnyororo wa thamani katika mazao ya kilimo.

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Joseph Sokoine amesema hilo ni azimio mojawapo lililofikiwa katika Mkutano wa 114 wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya OACPS uliofanyika jijini Brussels nchini Ubelgiji tarehe 8 na 9 Juni 2022 ambapo alimwakilisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula.

Amesema kuwa wadau wa kilimo kutoka Tanzania wanaotaka mikopo hiyo ya masharti nafuu watatakiwa  kuomba fedha hizo kupitia Ubalozi wa Tanzania nchini Ubelgiji na kuweza kushiriki kikamilifu katika mkakati huo wa kuongeza mnyororo wa thamani kwenye mazao ya kilimo

“ Mkutano umeazimia kuanzisha mkakati wa kuongeza mnyororo wa thamani katika mazao ya kilimo, na ili kufanikisha azimio hilo Jumuiya imetenga Euro milioni 157 ambazo zitatoka kama mikopo ya masharti nafuu kwa wakulima ndani ya jumuiya yetu ya OACPS” alisema Balozi Sokoine na kuongeza kuwa wadau wa kilimo kutoka Tanzania wataweza kuomba fedha hizo kupitia Ubalozi wa Tanzania nchini Ubelgiji.

Amesema kuwa Ubalozi ukikamilisha taratibu za uombaji na utoaji wa mikopo hiyo utatoa kwa walengwa ili wafanye maombi ya mikopo hiyo.

Akiongelea mazimio mengine, Balozi Sokoine amesema kuwa ni kuidhinishwa kwa Tanzania katika nafasi ya Uenyekiti wa Kamati ya masuala ya Uvuvi kwa miaka miwili kuanzia 2022 hadi 2024 na hivyo kuwa mwenyeji wa  Mkutano wa Mawaziri wa masuala Uvuvi  unaotarajiwa kufanyika nchini mwaka 2024.

“Hatua hii ni fursa kubwa kwa Tanzania katika kusimamia utekelezaji wa ajenda yake ya uchumi wa buluu na kukuza ushirikiano baina ya nchi za OACPS katika sekta ya uvuvi” alisema. 

Amesema Mkutano huo umejadili changamoto zinazowakabili wafanyabiashara ndani ya jumuiya wakati wa kuingiza bidhaa katika soko la Ulaya na kuja na mikakati  ya kutatua changamoto hizo kwa kufaya tathmini ya kina ili kuzielewa changamoto husika na kuanzisha mfumo wa utoaji tahadhari mapema kwa wafanyabiashara.

 Amesema azimio lingine ni kuanzisha Jukwaa Maalum la Wafanyabiashara ndani ya Jumuiya kwa lengo la kuwakutanisha wafanyabiashara, kubadilishana uzoefu na kukuza mtandao wa masoko ya bidhaa na huduma na kuongeza kuwa   Mkutano pia umeazimia kuunganisha nguvu ya Diaspora kwa kuanzisha jukwaa maalum la kuwezesha Diaspora kukaa pamoja na kubadilishana uzoefu kwenye masuala mbalimbali ikiwemo fursa za uwekezaji ndani ya Jumuiya na kutoa maoni na kufanyiwa kazi.

Mkutano wa Baraza la Mawaziri la nchi wanachama wa OACPS ni chombo cha maamuzi cha Jumuiya hiyo ambacho kinahusika na utekelezaji wa maazimio yanayopitishwa na Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali. Baraza hilo linaundwa na Mawaziri wa Mambo ya Nje kutoka kwa Nchi wanachama na hukutana mara mbili kwa mwaka kujadili utekelezaji wa maazimio  yaliyofikiwa kutoka katika mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya hiyo.

 

 


Thursday, June 9, 2022

TANZANIA YAIKARIBISHA JUMUIYA YA OACPS KUADHIMISHA SIKU YA KISWAHILI DUNIANI

Katibu Mkuu Balozi Joseph Sokoine akimkabidhi kitabu cha kujifunzia lugha ya Kiswahili Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Afrika ya Kati na Mwenyekiti wa Mkutano wa 114 wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya OACPS Mhe. Slyvie Baipo Temon uliofanyika jijini Brussels, Ubelgiji tarehe 7-9 Juni 2022

 

Katibu Mkuu Balozi Joseph Sokoine akimkabidhi kitabu cha kujifunzia kiswahili Balozi wa Jamhuri ya Afrika ya Kati na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Mabalozi nchini Ubelgiji Mhe. Daniel Emery Dede wakati wa Mkutano wa 114 wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya OACPS jijini Brussels

Katibu Mkuu Balozi Joseph Sokoine akimkabidhi kitabu cha kujifunzia kiswahili Katibu Mkuu wa  Jumuiya ya OACPS Bw. Georges Robelo Pinto Chikoti wakati wa Mkutano wa 114 wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya hiyo uliofanyika jijini Brussels, Ubelgiji tarehe 7-9 Juni 2022


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Joseph Sokoine (waliokaa katikati) katika picha ya pamoja na Ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa 114 wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Nchi za OACPS uliofanyika jijini Brussels nchini Ubelgiji tarehe 7-9 Juni 2022. Waliokaa kushoto ni Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji Mhe. Jestas Nyamanga na kulia ni mwakilishi wa Idara ya Ulaya na Marekani Bi. Agnes Kiama.


Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki walioshiriki Mkutano wa 114 wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki (OACPS) uliofanyika Brussels Ubelgiji tarehe 7-9 Juni 2022.

Baadhi ya Wajumbe wa Mkutano wa 114 wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki (OACPS) uliofanyika Brussels Ubelgiji tarehe 7-9 Juni 2022 wakiendelea na mkutano huo.




 

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Joseph Sokoine amezikaribisha nchi wanachama wa Jumuiya ya Nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki (OACPS) kushiriki katika maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani yatakayofanyika Julai 7 2022.

Akitoa mwaliko huo katika Mkutano wa 114 wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya hiyo, Balozi Sokoine amesema Lugha ya Kiswahili imeendelea kukua na hivyo kuwa na wazungumzaji wengi katika sehemu nyingi duniani.

Amesema Tanzania inajivunia uamuzi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni  (UNESCO) wa kuitambua na kuipa  Siku Maalum lugha ya Kiswahili hasa ikizingatiwa kuwa Kiswahili ni lugha ya Taifa Tanzania.

Amesema Maadhimisho hayo yanatarajiwa kukuza zaidi na kuongeza matumizi ya lugha hiyo duniani.

"Leo hii Kiswahili sio lugha ya Taifa ya Tanzania pekee au katika nchi nyingine za Afrika bali pia ni lugha inayozungumzwa na watu wengi katika Afrika Mashariki, Kati na Kusini," alisema Balozi Sokoine. 

Ameongeza  kuwa Kiswahili sasa kinafudishwa katika zaidi ya vyuo vikuu 100 duniani na ni miongoni mwa lugha za kazi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na Umoja wa Afrika.

"Kwa niaba ya Ubalozi wa Tanzania hapa Brussels na Ujumbe wa Tanzania katika Mkutano huu  tunawaalika rasmi nchi wanachama wa OACPS kuungana na Tanzania na  wadau wengine wa Kiswahili kuadhimisha kwa mara kwanza Siku ya Kiswahili duniani," alisema Balozi Sokoine.

Tanzania na Balozi zake zitaungana na wadau wa Kiswahili duniani  kuadhimisha kwa mara ya kwanza  Siku ya Kiswahili duniani. 

Katika Mkutano huo Balozi Sokoine alipata fursa ya kukabidhi vitabu vya awali vya kujifunzia lugha ya Kiswahili vilivyoungwa na Baraza la Kiswahili Tanzania kwa Mwenyekiti wa Mkutano huo ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Afrika ya Kati Mhe. Slyvie Baipo Temon  na  Mwenyekiti wa Jumuiya ya Mabalozi nchini Ubelgiji ambaye pia ni Balozi wa Jamhuri ya Afrika ya Kati nchini Ubelgiji Mhe. Daniel Emery Dede.

Julai 7 ya kila mwaka ilitangazwa na UNESCO kuwa siku maalum ya Maadhimisho ya Kiswahili  duniani.