Tuesday, June 14, 2022

WAZIRI MULAMULA ZIARANI NCHINI FINLAND



Helsinki, 14 Juni 2022


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula amewasili nchini Finland kwa ziara ya siku 3 kushiriki Mkutano wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Nchi za Afrika na Nchi za Nordic (NORDIC-AFRICA) unaofanyika kuanzia tarehe 13 hadi 15 Juni 2022 jijini Helsinki, Finland. 


Mkutano huo umeanza na hafla ya ufunguzi iliyofanyika tarehe 13 Juni 2022, ambapo mgeni rasmi alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Finland, Mhe. Pekka Haavisto.

 

Akiwakaribisha wajumbe wa mkutano huo Mhe. Haavisto alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano katika kujiletea maendeleo baina ya nchi hizo marafiki.

 

Aidha, mkutano huu utahusisha nchi 5 za Nordic ambazo ni Finland mwenyeji wa mkutano wa sasa, Sweden, Norway, Iceland na Denmark na nchi za Afrika 25 marafiki wa Nordic. 

 

Mkutano huo wa Mawaziri wa Mambo ya Nje utahusisha Mabalozi wa nchi shiriki za Afrika zinazowakilisha katika nchi za Nordic na Mabalozi wa nchi za Nordic wanaowakilisha katika Nchi shiriki za Afrika.

 

Wazo la kuanzisha mkutano huu lilianza mwaka 2000 ambapo mkutano wa kwanza ulifanyika nchini Sweden mwaka 2001. Baada ya hapo mikutano kama hii inafanyika kwa kupokezana kutoka Bara la Afrika na upande wa Nordic.

 

Mwaka 2019 Tanzania ilikuwa mwenyeji wa mkutano huu ambapo nchi takribani 34 zilishiriki katika mkutano.

 

Wakati huo huo Mhe. Waziri Mulamula ametumia fursa ya ziara hiyo kutembelea Makao Makuu ya Ofisi ya Mpango wa usimamizi wa migogoro nchini Finland na kukutana na uongozi wa mpango huo. Lengo la likiwa kujadili masuala ya amani na usalama katika ukanda wa Afrika Mashariki na ukanda wa kusini mwa Afrika.

 

Katika mazungumzo yake Waziri Mulamula ameeleza kuwa Tanzania inaendelea kuwa mstari wa mbele katika kusimamia masuala ya amani na usalama ili kuwezesha nchi za ukanda huo kufanya shughuli za kiuchumi na kuinua maendeleo ya taifa na wananchi kwa ujumla.


 -Mwisho-


Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 




Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula akifuatilia hotuba wakati wa hafla ya ukaribisho kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Finland na mwenyeji wa Mkutano wa 19 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Nchi za Afrika na Nchi za Nordic (NORDIC - AFRICA), Mhe. Pekka Haavisto unaofanyika tarehe 13 hadi 15 Juni 2022 jijini Helsinki, Finland. Kushoto ni Balozi wa Heshima wa Tanzania nchini Finland, Dkt. Vesa Viitaniemi.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Finland, Mhe. Pekka Haavisto akifungua hafla ya kuwakaribisha wajumbe wa mkutano wa 19 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Nchi za Afrika na Nordic unaofanyika tarehe 13 hadi 15 Juni 2022 jijini Helsinki nchi humo.

Sehemu ya wajumbe wa mkutano huo wakifatilia hotuba ya Mhe. Haavisto.

Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Grace Alfred Olotu (kati) pamoja na Afisa Ubalozi katika ubalozi huo wakisalimiana na wajumbe wengine wa mkutano wakati wa hafla hiyo.

Hafla ikiendelea, Mhe. Waziri Mulamula akisamilimiana na wajumbe wengine wa mkutano huo. Kulia ni Mhe. Balozi Liberata Mulamula.

Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme akifuatilia hafla ya ukaribisho ya mkutano huo.


Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga akisalimiana na mshiriki wa mkutano huo.


 

 

 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.