Friday, June 24, 2022

BALOZI MULAMULA ATAKA MIGOGORO KATIKA NCHI ZA JUMUIYA YA MADOLA IMALIZWE

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula amesema kuwa, licha ya wanachama wa Jumuiya ya Madola kufanya kazi nzuri katika kuimarisha misingi ya demokrasia, amani na utawala bora katika nchi zao, bado kuna changamoto nyingi zinazohitaji kutafutiwa ufumbuzi ili misingi hiyo ya maisha iweze kufanya kazi kwa ukamilifu wake.

Ametoa kauli hiyo leo tarehe 23 Juni 2022 jijini Kigali katika kikao cha Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Jumuiya ya Madola kilichukuwa kinajadili masuala ya demokrasia, amani na utawala bora.

Waziri Mulamula alizitaja baadhi ya changamoto hizo na kusisitiza umuhimu wa familia ya Jumuiya ya Madola kuziangalia kwa makini na kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu, kuwa ni pamoja na migogoro isiyoisha, ukosefu wa usalama na udhaifu wa vyombo vinavyosimamia masuala ya utawala wa sheria.

Balozi Mulamula katika maelezo yake alitambua jitihada zinazofanywa na jumuiya za kikanda na kimataifa za kutumia njia za kidiplomasia kuzuia migogoro na kuzisihi nchi za jumuiya hiyo kongwe kurejea katika misingi yake ya awali, ili kuhakikisha kuwa amani na utulivu vinatawala muda wote kwenye nchi hizo.

Aidha, Waziri Mulamula alitumia mkutano huo wa Mawaziri wa Mambo ya Nje, kuzishauri nchi wanachama kuangalia uwezekano wa kutumia taratibu za kujitathmini zinazotumika kwenye jumuiya nyingine za kujipima kiutawala bora.

Alitoa mifano ya taratibu hizo kuwa ni pamoja na Mpango wa Nchi za Afrika za Kujitathmini Kiutawala Bora (APRM); mpango wa hiyari wa nchi zinazotekeleza malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) wa kujipima utekelezaji wa malengo hayo; mpango wa nchi wanachama wa Baraza la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu wa kujitathmini kila baada ya kipindi fulani.

Aliwafahamisha Mawaziri wenzake kuwa, Tanzania imefanyiwa tathmini hivi karibuni na Baraza la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu na kupitia tathmini hiyo, Tanzania ilipata fursa ya kueleza mazuri yaliyofanyika kuhusu utawala bora na haki za binadamu. Alisema pia kuwa nchi yake ilipata fursa ya kujifunza mazuri ya nchi nyingine kuhusu utawala bora.

Balozi Mulamula alitihitimisha hotuba yake kwa kuwakumbusha Mawaziri kuhusu programu zilizobuniwa na Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola na umuhimu wa kuzihuisha na kuzipa nguvu. Progaramu hizo ni pamoja na misaada katika uchaguzi ikiwa ni pamoja na kuhamasisha nchi wanachama kuendesha chaguzi za huru na haki, kutoa misaada ya kiufundi katika uandaaji wa sera, misaada katika programu za mabadiliko ya sheria, kuunda taasisi imara za kitaifa za kusimamia masuala ya haki za binadamu na kuzijengea nchi uwezo wa kutoa haki bila upendeleo.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiwa katika kiti cha Tanzania wakati wa Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Madola unaofanyika nchini Rwanda tarehe 20 hadi 25 Juni 2022.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akisalimiana na Mawaziri wenzake wanaoshiriki katika mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Madola unaofanyika nchini Rwanda tarehe 20 hadi 25 Juni 2022.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiwa na makabrasha ya mkutano akilekea kwenye Kiti cha Tanzania kwa ajili ya kushiiki mkutano wa Mawaziri wa sJumuiya ya Madola unaofanyika nchini Rwanda.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akihojiwa na mwandishi wa Kituo cha Runimga cha Channel 10, Bw. Ezekiel Mwamboko. Aliyemshikia kipaza sauti ni Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,, Balozi Mindi Kasiga.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiwa katika picha ya pamoja na Mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchi za Jumuiya ya Madola wanaoshiriki katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa jumuiya hiyo unaofanyika nchini Rwanda tarehe 20 hadi 25 Juni 2022.


 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.