Wednesday, August 3, 2022

WAZIRI WA USAFIRISHAJI ZAMBIA AFANYA ZIARA BANDARI, TAZARA

Na Mwandishi Wetu, Dar

Waziri wa Uchukuzi na Usafirishaji wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Frank Tayali amefanya ziara ya kutembelea Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Kampuni binafsi ya Kimataifa ya Kuhudumia Makontena Tanzania (TICTS) pamoja na Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (Tazara) Jijini Dar es Salaam.

Katika ziara hiyo Mhe. Tayali aliambatana na mwenyeji wake Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa (Mb) ambapo pamoja na mambo mengine, viongozi hao wametembelea maeneo hayo ikiwa ni siku moja tu tangu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan pamoja na Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema walipowaelekeza Mawaziri wa Sekta hiyo kushughulika changamoto zinazoikabilia miundombinu ya kiuchumi baina ya nchi hizo ikiwemo reli ya Tazara na Bomba la mafuta la Tazama.

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa amemhakikishia Waziri mwenzake kuwa Tanzania ipo tayari kushirikiana na Zambia katika kutafuta mikakati ya kuifufua reli ya Tazara na kuhakikisha kuwa wafanyabishara kutoka Tanzania na Zambia wananufaika na reli ya Tazara.

“Tanzania na Zambia ni washirika na ndugu hivyo sisi kama watanzania tupo hapa kuwahudumia na pia tupo tayari kushirikiana nanyi kuhakikisha kuwa uchumi wetu unakua……………. kupanua wigo wa biashara baina ya mataifa yetu,” amesema Prof. Mbarawa.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania, Bw. Plasduce Mbossa amesema kuwa Zambia ni nchi moja wapo kati ya nchi zainazotumia Bandari ya Tanzania kwa asilimia kubwa ambapo Bandari inatambua mchango mkubwa wa wafanyabiashara kutoka Zambia wanavyotumia bandari ya Tanzania na kuwa Bandari inawaahidi ushirikiano katika kukuza na kuendeleza biashara baina ya Tanzania na Malawi.

Kwa upande wake Waziri wa Uchukuzi na Usafirishaji wa Zambia, Mhe. Tayali amesema Tazara ni nyenzo muhimu katika kuinua uchumi wa mataifa yote mawili, hivyo kufufuliwa kwa reli ya Tazara kutasaidia kuinua uchumi wa mataifa yote hususan kwa wafanyabiashara na wawekezaji. 

“Zambia tutafanya kazi kwa bidii kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kutafuta mikakati mbalimbali ya kuifufua Tazara ili kuendelea kunufaisha watanzania na wazambia kwani bila kufanya hivyo maendeleo ya mataifa hayo yatadhorora,” amesema Mhe. Tayali

Aidha, viongozi hao wamewaagiza Makatibu Wakuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kutoka Tanzania na Zambia kushirikiana na Uongozi wa Tazara kuunda Kamati ya kufuatilia mikakati ya ufufuaji wa Reli ya Tazara mapema iwezekananyo ili kuanza kutekeleza maagizo ya viongozi wakuu wa nchi yaliyotolewa jana tarehe 2 Aug, 2022 wakati wa Ziara rasmi ya kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Zambia nchini Tanzania jana. 

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa (kulia) na mgeni wake Waziri wa Uchukuzi na Usafirishaji wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Frank Tayali (kushoto) wakichukua dondoo walipofanya ziara katika Mamlaka ya Bandari Tanzania. Mhe. Tayali ametembelea bandari ya Tanzania kwa lengo la kujionea jinsi bandari hiyo inavyotekeleza majukumu yake

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa na mgeni wake Waziri wa Uchukuzi na Usafirishaji wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Frank Tayali wakimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (Tazara) Mhandisi Bruno Tching'andu (aliyesimama) alipokuwa akieleza jinsi Tazara inavyotekeleza majukumu yake


Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa na mgeni wake Waziri wa Uchukuzi na Usafirishaji wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Frank Tayali wakipata taarifa fupi kuhusu Kampuni binafsi ya Kimataifa ya Kuhudumia Makontena Tanzania (TICTS) inavyotekeleza majukumu yake wakati walipotembelea ofisi za TICTS Jijini Dar es Salaam

Kikao cha Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa na mgeni wake Waziri wa Uchukuzi na Usafirishaji wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Frank Tayali kikiendelea katika Ofisi za Tazara Jijini Dar es Salaam



Tuesday, August 2, 2022

RAIS SAMIA, HICHILEMA WAKUBALIANA KUBORESHA UHUSIANO

Na Mwandishi wetu, Dar 

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema wamekutana na kufanya mazungumzo kuhusu kufufua ushirikiano baina ya nchi hizo ambao ulikuwa umelegalega.

Mazungumzo hayo yamefanyika Ikulu Jijini Dar es salaam ambapo Mhe. Hichilema alikuja kwa ziara rasmi ya kiserikali ya siku moja.

Rais Samia amesema kuwa Tanzania na Zambia ni nchi ambazo zilikuwa karibu zikiwa na urafiki na undugu ambao ulianzishwa na waasisi wa mataifa hayo Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere kwa upande wa Tanzania na Hayati Keneth Kaunda wa Zambia.

“Wazee hawa ndio walioshirikiana kuleta ukombozi kusini mwa bara la Afrika lakini kwa upande wao katika nchi zetu mbili wakatuanzishia mambo ambayo walitaka yadumu milele na yatuunganishe,” amesema Rais Samia.

Rais Samia ameongeza kuwa katika kurudisha undugu wameangalia maeneo yote ambayo yatachochea kurudi huko kwa kuangalia uhusiano wa kisiasa na kuongoza wananchi wao katika kuelewana vyema.

Mbali na hayo Rais Samia amesema wamejadili masuala ya usalama wa nchi hizo na kuangalia changamoto za kiusalama zinazokabili ukanda wao ikiwemo ugaidi na kukubaliana kushirikiana.

Wawili hao walizungumzia pia masuala ya uchumi ambapo walikubaliana kufufua upya miundombinu ya kiuchumi baina ya nchi hizo ikiwemo reli ya TAZARA na Bomba la mafuta la TAZAMA.

Rais Samia alisema wamekubaliana kuboresha reli ya TAZARA kwa kuijenga kwa kiwango cha kisasa (SGR) ili kuendana na mahitaji ya sasa ya kidunia.

“Tumekubaliana tuboreshe TAZARA kama tunaifanyia marekebisho reli iliyopo lakini tukakubaliana kwamba kwa dunia ya leo reli ni SGR, kwahiyo tutakuwa na mradi wa pamoja tutafute pesa kwa pamoja kupitia PPP pengine na marafiki waliotujengea reli hiyo tuone jinsi tutakavyoboresha kwa kiwango cha SGR,” amesema Rais Samia.

Kuhusu Bomba la mafuta la TAZAMA marais hao wamekubaliana kuwa lililopo ni dogo ikilinganishwa na mahitaji na hivyo kuona haja ya kujenga lingine kubwa kwani kwa sasa bomba la TAZAMA halifanyi kazi kama ilivyokusudiwa kutokana na mabadilko ya sera za Nishati za Zambia.

“Tumekubaliana bomba lile (TAZAMA) ni dogo sana kwahiyo kuna haja ya kujenga kubwa litakalopeleka mafuta kwa wingi na bandari ya Dar es Salaam na miundombinu iliyopo Tanzania iwasaidie kupunguza ughali wa mafuta katika nchi yao,” ameongeza Rais Samia

Kadhalika viongozi hao walijadili kuhusu biashara na uwekezaji ambapo pamoja na mambo mengine,  wameangalia vikwazo vya kikodi na visivyo vya kikodi na kukubaliana mamlaka zinazoshulika na kodi na forodha kukutana na kuangalia mambo ya kuondoa ili kuruhusu biashara baina ya nchi hizo kufanyika vizuri.

Rais Samia alisema wamewazungumzi pia wafanyabishara wadogowadogo wanaovuka mipaka na kubaini kuwa masharti wanayopewa ni makubwa kuanzia vibali vya kuingia hadi tozo.

“Tumeagiza Mawaziri wakae na kuangalia jinsi ya kusaidia biashara ziendelee bila matatizo,” amesema Rais Samia.

Vilevile wamejadili changamoto za madereva na kukubaliana taasisi za madereva za Zambia na Tanzania ziwekwe pamoja zizungumze na Serikali zote mbili na kuona ni jinsi gani changamoto zinazowakabili zinaondolewa.

Rais Samia ameongeza kuwa katika mazungumzo yao waligusia mambo ya kilimo ambapo wameona kuwa wote ni wazalishaji wa soya ambayo ina soko nje ya nchi zetu, na kwamba Zambia wapo vizuri katika uzalishaji wa mbegu.

“Tumekubaliana tusishindane lakini tuongezeane uwezo, wenzetu ni mabingwa wa uzalishaji wameendelea kidogo wana mbegu nzuri na tumezungumza kwamba linapokuja suala la mbegu mnatutoza sana akaniambia basi tuzungumze tuuziane kirafiki na kindugu.”

“Tumekubaliana kufanya kazi kwa pamoja na kama mmoja ana soko amwambie mwingine kuna soko hapa na sisi leo tumeofa soko la nyama, ng’ombe na kondoo tuna soko kubwa tumelipata Saudia Arabia tumewaalika wenzetu waje twende tukalitumie hilo soko,” amesema Rais Samia

Kwa upande wake Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema amesema viongozi wa nchi hizo mbili  ni kizazi ambacho kinatakiwa kuendeleza  urithi ulioachwa na waasisi  Keneth Kaunda na Julius Nyerere.

“Tumekubaliana na dada yangu Rais Samia kuendeleza urafiki wetu katika mambo mbalimbali kama vile masuala ya utamaduni kwa sababu ukienda maeneo kama Nakonde au Tunduma kuna familia ambazo shangazi anaishi upande wa Zambia na mjomba anaishi upande wa Tanzania kwa hiyo sisi ni ndugu.

“Tunaangalia pia namna ya kutumia umoja wetu kupitia majukwaa kama SADC, Nchi za ukanda wa Maziwa Makuu na Ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki hasa ikizingatiwa Tanzania ni nchi wanachama kote, sisi hatupo baadhi lakini tunaweza kufaidika na uwepo wa Tanzania kwenye umoja huo,” amesema Rais Hichilema 

Rais Hichilema ameongeza kuwa Zambia imepanga kuimarisha uhusiano na Tanzania na kufanya kazi kwa pamoja kwa maslahi mapana ya mataifa yote mawili.

Aidha, Mhe. Hichilema amesema kuwa Tanzania imefanikiwa kwenye sekta ya madini ambapo imewawezesha wachimbaji wadogo na kuwainua hadi kuwa wachimbaji wakubwa.

Katika hafla hiyo pia Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb.) pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Zambia, Mhe. Stanley Kakubo  wamesaini mikataba mitatu ya ushirikiano katika sekta ya ulinzi na usalama pamoja na sanaa na utamaduni.

Akifafanua kuhusu ziara hiyo, Waziri Mulamula alisema mikataba miwili inahusu ulinzi na usalama ambapo nchi hizo zitashirikiana kwenye masuala ya kijeshi pamoja na mafunzo kwa maofisa wa ngazi za juu kwenye masuala ya ulinzi na usalama wakati mkataba wa tatu utahusu masuala ya sanaa na utamaduni.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan pamoja na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Hakainde Hichilema wakisalimiana na viongozi mbalimbali waliofika kwenye mapokezi baada ya Mhe. Hichilema kuwasili katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan pamoja na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Hakainde Hichilema wakisalimiana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula baada ya Mhe. Hichilema kuwasili katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa amesimama pamoja na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema wakati nyimbo za Taifa (Tanzania na Zambia) zikiimbwa mara baada ya kuwasili katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Wanahabari (hawapo pichani) katika ziara ya Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema Ikulu Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Zambia, Mhe. Stanley Kakubo  wakionesha mikataba waliyosaini. Mikataba hiyo ni ya ushirikiano katika sekta ya ulinzi na usalama pamoja na sanaa na utamaduni

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akiagana na Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema mara baada ya kuhitimisha ziara yake ya siku moja Jijini Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akiagana na Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema mara baada ya kuhitimisha ziara yake ya siku moja Jijini Dar es Salaam



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI





 

Friday, July 29, 2022

TANZANIA, URUSI KUONGEZA MAENEO YA USHIRIKIANO

Serikali ya Tanzania na Urusi zimekubaliana kuongeza maeneo ya ushirikiano katika sekta za biashara na uwekezaji,utalii pamoja na utamaduni.

Makubaliano hayo yamefikiwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk alipokutana kwa mazungumzo na Balozi wa Urusi nchini, Mhe. Andrey Levonovish Avetsyan katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Balozi Mbarouk amesema kuwa Tanzania na Urusi zimekuwa na ushirikiano wa muda mrefu wa kihistoria ambao uliasisiwa na Waasisi wa Mataifa hayo mawili…….“ kutokana na uhusiano mzuri tulionao umechangia kuimarisha sekta ya utalii, elimu pamoja na afya,” alisema Balozi Mbarouk

Balozi Mbarouk aliongeza kuwa Tanzania na Urusi zitaendelea kujikita zaidi kufungua maeneo mapya ya ushirikiano katika sekta za biashara, uwekezaji, utalii na masuala mengine ya kiuchumi kwa maslahi mapana ya mataifa hayo.

Kwa upande wake Balozi wa Urusi nchini, Mhe. Andrey Levonovish Avetsyan ameishukuru Tanzania kwa ushirikiano ambao imekuwa ikimpatia tangu aliwasili na kuongeza kuwa Urusi itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kukuza na kuendeleza ushirikiano wa kufanya kazi kwa pamoja kwa manufaa ya mataifa mawili.

“Naamini kuwa mimi ni kiungo cha kuimarisha na kuendeleza uhusiano baina ya Urusi na Tanzania…..tumekuwa tukishirikiana katia sekta mbalimbali ikiwemo biashara na uwekezaji, elimu na afya utalii na utamaduni naahidi kuwa Urusi itaendelea kushirikiana na Tanzania kwa maslahi mapana ya pande zote mbili,” Amesema Balozi Avetsyan

Balozi Avetsyan ameongeza kuwa katika mwaka huu Serikali ya Urusi imepanga kutoa fursa za masomo kwa wanafunzi wa kitanzania takribani 70.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akizungumza na Balozi wa Urusi nchini, Mhe. Andrey Levonovish Avetsyan katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Mazungumzo baina ya Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk na Balozi wa Urusi nchini, Mhe. Andrey Levonovish Avetsyan yakiendelea katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Balozi wa Urusi nchini, Mhe. Andrey Levonovish Avetsyan akizungumza na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk katika picha ya pamoja na Balozi wa Urusi nchini, Mhe. Andrey Levonovish Avetsyan


TANZANIA, USWISI KUENDELEZA USHIRIKIANO


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Uswisi zimeahidi kuendeleza zaidi ushirikiano katika nyanja mbalimbali ikiwemo teknolojia ya habari na mawasiliano, elimu, afya, ujenzi wa miundombinu, utawala bora na haki za binandamu, uhuru wa vyombo vya habari, kilimo na utalii kwa maslahi mapana ya pande zote mbili. 

Ahadi hiyo imetolewa kwa nyakati tofauti na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula na Balozi wa Uswisi nchini Mhe. Didier Chassot kwenye hafla ya kuadhimisha Siku ya Taifa ya Uswisi iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 28 Julai 2022. 


Waziri Mulamula alisema Tanzania na Uswisi zimekuwa na uhusiano mzuri wa kidiplomasia na zimeendelea kushirikiana katika nyanja za teknolojia ya habari na mwasiliano, elimu, afya, ujenzi wa miundombinu, utawala bora na haki za binandamu, uhuru wa vyombo vya habari, kilimo na utalii. 

“Uswisi imekuwa mdau mkubwa katika masuala ya uchumi na kijamii ambapo kampuni mbalimbali kutoka Uswisi zimewekeza hapa nchini na zimekuwa zikichangia kutoa ajira kwa watanzania na kuongeza pato la taifa,” alisema Waziri Mulamula 

Kwa upande wake Balozi wa Uswisi nchini Mhe. Didier Chassot alisema Uswis imefurahishwa na ushirikiano mzuri inaoupata kutoka Serikali ya Tanzania na kuahidi kuwa itaendelea kudumisha uhusiano huo kwa maslahi ya mataifa yote mawili

Balozi Chassota aliongeza kuwa Uswiss itaendelea kushirikiana na Tanzania na kuunga mkono juhudi mbalimbali za kukuza maendeleo ya kijamii, kisiasa na kiuchumi zinazofanywa na Serikali ya Tanzania.

Hafla hiyo ilihudhuriwa Mabalozi mbalimbali na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa wanaoziwakilisha nchi zao hapa nchini, asasi za kiraia, na wafanyabiashara. 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula akitoa hotuba yake katika hafla ya kuadhimisha Siku ya Taifa ya Uswisi iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 28 Julai 2022
Balozi wa Uswisi nchini Mhe. Didier Chassot akitoa hotuba yake katika hafla ya kuandimisha Siku ya Taifa ya Uswisi iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 28 Julai 2022
Hafla ya kuadhimisha Siku ya Taifa ya Uswisi iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 28 Julai 2022 ikiendelea. 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula na alozi wa Uswisi nchini Mhe. Didier Chassot wakifurahia jambo kwenye hafla ya kuadhimisha Siku ya Taifa ya Uswisi iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 28 Julai 2022

Thursday, July 28, 2022

WAZIRI MULAMULA AMUAGA BALOZI WA PAKISTAN NCHINI TANZANIA

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) amemuaga Balozi wa Pakistan hapa nchini Mhe. Mohammad Saleem anayemaliza kipindi chake cha kuhudumu. 

Katika tukio hilo ambalo limefanyika kwenye Ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaam Waziri Mulamula amemshukuru Balozi Saleem kwa utumishi uliotuka na kumpongeza kwa mafanikio makubwa aliyoyapata katika utendaji wake ambayo yataacha alama na kumbukumbu ya kudumu kwenye historia ya uhusiano wa kidiplomasia baina ya Tanzania na Pakistan.

“Wazara na Serikali kwa ujumla tunajivunia utendaji wako, katika kipindi chako ulichohudumu hapa nchini licha ya kudumisha na kukuza uhusiano baina yetu na Pakistan umefanya kazi nzuri sana ya kuibua fursa na mikakati mbalimbali ambayo imeleta manufaa kwa wananchi wetu, kama vile fursa za nafasi za masomo, kuendeleza shughuli za uvuvi nchini na kukuza biashara baina ya Tanzania na Pakistan” Alisema Waziri Mulamula

Balozi Saleem kwa upande wake ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano mzuri iliompa katika kipindi chote alichokuwa nchini kuteleza majukumu yake. Aidha ameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita chini usimamizi mahiri wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri inayoendelea kuifanya ya kuleta maendeleo nchini. 

Waziri Mulamula amemuhakikishi Balozi Saleem kuwa Serikali ya Tanzania itaendelea kushirikiana kwa karibu na Pakistan kwa manufaa ya maslahi mapana ya pande zote mbili.

Wakati huo huo Waziri Mulamula amempokea na kufanya mazungumzo na Balozi wa Misri nchini Tanzania Mhe. Mohamed Gaber katika ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaam. Wawili hao wamejadili musaula mbalimbali yenye maslahi kwa pande zote mbili ikiwemo uwekezaji, biashara, elimu na mafunzo, ushirikiano katika sekta ya utamaduni na michezo na maendeleo ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali inayotekelezwa na Kampuni za Misri hapa nchini.

Aidha wamekubaliana kuendelea kufuatilia utelezaji wa makubaliano na mikataba mbalimbali liyosainiwa wakati wa ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan aliyoifanya nchini Misri mwezi Novemba 2021. 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) akimsikiliza Balozi wa Pakistan anayemaliza kipindi chake cha kuhudumu nchini Mhe. Mohammad Saleem alipokuwa akimuaga katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam
Mazungumo baina Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula Balozi wa Pakistan anayemaliza kipindi chake cha kuhudumu nchini Mhe. Mohammad Saleem yakiendelea katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) na Balozi wa Misri nchini Tanzania Mhe. Mohamed Gaber wakiwa katika picha ya pamoja na Maafisa wa Ubalozi na Wizara
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) na Balozi wa Misri nchini Tanzania Mhe. Mohamed Gaber wakiwa katika mazungumzo yaliyofanyika katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) na Balozi wa Misri nchini Tanzania Mhe. Mohamed Gaber wakiwa katika picha ya pamoja

WAZIRI MULAMULA ASHIRIKI MKUTANO WA BARAZA LA AMANI NA USALAMA LA UMOJA WA AFRIKA KUJADILI HALI YA AMANI NA USALAMA NCHINI SOMALIA


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) akichangia hoja kwenye mkutano wa 1094 wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 27 Julai 2022.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) ameshiriki Mkutano wa 1094 wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 27 Julai 2022. 

Mkutano huo ulilenga kupokea na kujadili taarifa ya Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika kuhusu hali ya amani na usalama ya nchini Somalia na shughuli za Kikosi cha Mpito cha Umoja wa Afrika nchini Somalia (The African Union Transition Mission in Somalia –ATMIS).

Taarifa hiyo ambayo iliyowasilishwa na Mhe. Mahmoud Ali Youssouf, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Jamhuri ya Djibouti ambaye ni Mwenyekiti wa Baraza la Amani na Usalama kwa mwezi Julai 2022, pamoja na mambo mengine iliangazia masuala yafuatayo; Hali ya kisiasa ya nchini Somalia na kukamilika kwa mchakato wa Uchaguzi Mkuu (political Development and update on National Elections), Hali ya Usalama na Maendeleo ya Shughuli za Pamoja katika Kusaidia Mpango wa Mpito wa Somalia na Usanifu wa Usalama wa Kitaifa.

Masuala mengine ni kuangazia hali ya Maendeleo katika utekelezaji wa Pendekezo la Pamoja na Dhana ya Uendeshaji, Masuala yanayohusiana na kuimarisha Hali ya Kibinadamu nchini Somalia na Ufadhili endelevu wa Kikosi cha Mpito cha Umoja wa Afrika nchini SomaliaAkichangia katika mkutano huo Waziri Mulamula alianza kwa kumpongeza Mhe. Hassan Sheikh Mohamud wa Somalia kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Serikali ya Shirikisho la Somalia. Vilevile alitumia nafasi hiyo kuelezea matumaini ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa nchi hiyo baada ya kukamilisha vyema zoezi la uchaguzi sasa kunawapa fursa na hali mpya ya kuweka nguvu katika kutekeleza mambo muhimu kama yalivyoainishwa katika Mpango wa Mpito wa Somalia, kama vile kujenga taasisi za serikali, na kuongeza nguvu katika maandalizi ya makabidhiano ya serikali kwa amani na usalama. 

Aidha, Waziri Mulamula alitoa wito kwa Kikosi cha Mpito cha Umoja wa Afrika nchini Somalia (ATMIS), Umoja wa Mataifa na Serikali ya Shirikisho la Somalia kufanya kazi kwa pamoja katika kushughulikia masuala muhimu yatakayo leta amani ya kudumu sambamba na kutazama suala la vikwazo vya silaha dhidi vilivyowekwa dhidi ya Somalia.

Mkutano huo umetoa wito kwa Umoja wa Mataifa kuzingatia kwa haraka maombi ya Serikali ya Shirikisho la Somalia kuhusu kuondolewa vikwazo vya silaha vilivyowekwa dhidi ya nchi yao, ili kuiongezea nchi hiyo uwezo wa kutosha wa kukabiliana vilivyo na tishio la usalama linaloletwa na kundi la kigaidi la Al Shabaab.

Vilevile mkutano uliipongeza Serikali ya Shirikisho la Somalia kwa kumchagua Naibu Spika mwanamke wa kwanza katika historia ya nchi hiyo. Pia ulisisitizo kuhusu umuhimu wa Serikali ya Somalia kuendelea kutambua nafasi ya wanawake, vijana, mashirika ya kiraia pamoja na vyombo vya habari katika mchakato wa mpito ambao utaifanya Somalia kufikia lengo la asilimia 30 kama ilivyokubaliwa katika Makubaliano ya Uchaguzi wa tarehe 17 Septemba 2020 na 27 Mei 2021. 

Tanzania ni miongoni mwa wajumbe 15 wa Baraza hilo. Wajumbe wengine ni Burundi, Cameroon, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Djibouti, Gambia, Ghana, Morocco, Namibia, Nigeria, Senegal, Afrika Kusini, Tunisia, Uganda na Zimbabwe.
Mkutano wa 1094 wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 27 Julai 2022 ukiwa unaendelea.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) akichangia jambo kwenye mkutano wa 1094 wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 27 Julai 2022

Wednesday, July 27, 2022

BALOZI MULAMULA AFUNGUA MAFUNZO YA UANDISHI WA HABARI ZA KIDIPLOMASIA

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akisalimiana na Balozi Patrick Tsere alipowasili katika ufunguzi wa mafunzo ya uandishi wa habari za kidiplomasia kwa waandishi wa habari nchini yaliyoandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na kufanyika katika Chuo cha Diplomasia jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akifungua mafunzo ya uandishi wa habari za kidiplomasia kwa waandishi wa habari nchini yaliyoandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na kufanyika katika Chuo cha Diplomasia jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akifungua mafunzo ya uandishi wa habari za kidiplomasia kwa waandishi wa habari nchini. Kulia ni Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Serikali Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mindi Kasiga na kushoto ni Kaimu Mkuu wa  Chuo cha Diplomasia Dkt. Anita Lugimbana


Balozi Peter Kalaghe akiwaeleza waandishi wa habari jinsi ya kuandika taarifa za kidiplomasia wakati wa mafunzo ya uandishi wa habari za kidiplomasia kwa waandishi wa habari nchini na kufanyika katika Chuo cha Diplomasia Dar es Salaam





Watoa mada katika mafunzo ya waandishi wa habari nchini wakifuatilia ufunguzi wa mafunzo hayo uliofamywa na Waziri Mulamula hayupo pichani

Balozi Patrick Tsere (kushoto) akiwa na Balozi Mindi Masiga (kulia) wakimfuatilia Balozi Peter Kalaghe (hayupo pichani) akizungumza na waandishi wa habari katika mafunzo ya waandishi wa habari ya kuandika habari za kidiplomasia yaliyoandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikianio wa Afrika Mashariki jijini Dar es Salaam

Baadhi ya washiriki mafunzo ya uandishi wa habari za kidiplomasia kwa waandishi wa habari nchini wakimfuatilia Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula akifungua mafunzo ya waandishi wa habari yaliyoandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na kufanyika katika Chuo cha Diplomasia jijini Dar es Salaam


Mkurugenzi wa Mawasiliano Serikalini Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mindi Kasiga akizungumza wakati wa mafunzo kwa waandishi wa habari ya kuandika habari za kidiplomasia yaliyoandaliwa na Wizara na kufanyika katika Chuo cha Diplomasia cha Dar es Salaam

Balozi Patrick Tsere akiongea na waandishi wa habari juu ya kuandika habari kwa kuzingatia uzalendo katika kulinda taswira ya Tanzania wakati wa mafunzo kwa waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini yanayofanyika katika Chuo cha diplomasia jijini Dar es Salaam

Kaimu Mkurugenzi wa Sera na Mipango , Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bw. Justine Kisoka akizungumza katika mafunzo ya waandishi wa habari yaliyoandaliwa na wizara na kufanyika katika chuo cha diplomasia jijini Dar es salaam
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (aliyekaa katikati) katika picha ya pamoja na waandishi wa habari nchini baada ya kufungua mafunzo ya uandishi wa habari za kidiplomasia kwa waandishi wa habari nchini


 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula amefungua mafunzo ya uandishi wa habari za kidiplomasia kwa waandishi wa habari nchini.

Akifungua mafunzo hayo ya siku mbili yanayofanyika katika Chuo cha Diplomasia jijini Dar es Salaam, Balozi Mulamula amewataka watendaji wa Wizara kuhakikisha wanaimarisha mahusiano kati ya wizara na vyombo vya habari.

'Tuwe pamoja siku zote tuendelee kushirikiana, vyombo vya habari ni wadau muhimu, tufanye kazi pamoja kwa manufaa ya nchi yetu,' alisema.

Amesema waandishi wa habari wanajukumu la kuilinda na kuitetea taswira ya Tanzania kupitia kazi zao na kuwataka waandishi wa habari nchini kuzingatia taswira ya nchi wakati wanatekeleza majukumu yao.
"Wanahabari, tuko hapa kuelimishana juu ya kuandika habari za kidiplomasia, niwaombe kwanza mhakikishe mnailinda taswira ya nchi, hii ni nchi yetu wote, ikiharibika taswira yake hata wewe uliyeandika pia utakutana na athari zake, hata uende wapi utajulikana kama Mtanzania. Mnapoandika mzingatie uzalendo na miiko ya taaluma ya uandishi wa habari," alisema Balozi Mulamula.

Pia aliongeza kusema mafunzo haya ambayo yatakuwa endelevu yanalenga pamoja na mambo mengine kutoa uelewa kuhusu masuala ya diplomasia ikiwemo Itifaki, Diplomasia ya Umma, Uzalendo na Mawasiliano ya kimkakati baina ya Tanzania na nchi zingine.

Kadhalika, aliwashukuru waandishi wa habari kote nchini kwa ushirikiano uliopo kati yao na wizara na kuwataka kuzingatia mafunzo yatakayotolewa kwao.


"Nawashukuru kwa ushirikiano na kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa Wizara na Sera ya Mambo ya Nje inayosisitiza katika Diplomasia ya Uchumi. Nawaomba mzingatie mafunzo haya kwani yatakuwa na tija kubwa kwenu," alisisitiza Balozi Mulamula.

Awali akimkaribisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Serikali Waziri ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mindi Kasiga alieleza kuwa mafunzo hayo yameandaliwa kwa ajili ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari nchini katika eneo la kuandika habari za kidiplomasia.

Amesema mafunzo hayo yatakuwa endelevu kwani kufanya hivyo kutasaidia kuboresha uandishi na kuwa daraja kati ya Wizara na waandishi wa habari na hivyo kuwafikia wananchi wengi.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki yamewashirikisha waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari vya hapa nchini.

 

 

 

 

WAZIRI MULAMULA ATOA WITO KWA AFRIKA KUTHAMINI MCHANGO WA WANAWAKE KATIKA KUJENGA UCHUMI


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) ametoa wito kwa Jumuya ya Afrika kutambua na kuthamini mchango wa Wanawake kwenye maendeleo ya uchumi. 

Waziri Mulamula ameyasema hayo alipokuwa akifungua Mkutano wa Uchumi wa Wanawake Afrika (Pan-African Women Economic Summit 2022) uliofanyika tarehe 26 Julai 2022 jijini Dar es Salaam. Waziri Mulamula ameeleza kuwa pamoja na mchango mkubwa unaotolewa na wanawake kwenye maendeleo, bado katika maeneo mengi barani Afrika hawatambui na kuthamini ipasavyo mchango huo hivyo kufifisha jitihaza za kundi hilo muhimu na lenye idadi kubwa barani katika kujenga uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla.

Waziri Mulamula aliendelea kubainisha kuwa endapo mchango wa wanawake ungetambuliwaingewapa motisha zaidi ya kuendelea kushiriki katika shughuli za maendeleo kwenye jamii na kajikwamua dhidi ya umaskini uliokithiri na hali ngumu ya maisha. 

Pamoja na hayo Waziri Mulamula akifafanua zaidi hoja yake alieleza kuwa kutambua mchango wa wanawake kwenye uchumi ni muhimu kwa mamlaka mbalimbali kuanza kufikiria namna ya kuwavutia wanawake kuendesha shughuli zao katika sekta rasmi. 

"Wanawake wa Kiafrika ni wajasiriamali wa hali ya juu, wanamiliki theluthi moja ya biashara zote barani Afrika, Hata hivyo wajasiriamali wanawake wana uwezekano mkubwa wa kuendesha biashara ndogo ndogo katika sekta isiyo rasmi, wakijihusisha na shughuli za ongezeko la thamani la chini ambazo huvuna faida ndogo. Wanaelekea kuwa wajasiriamali wa lazima, badala ya fursa, wakiongozwa na biashara ndogo na ukosefu wa njia mbadala” Alisema Waziri Mulamula.

Kwa upande Mkurugenzi wa Tanzania Women CEO’s Roundtable Bi. Emma Kawawa akizungumza kwenye hafla ufunguzi wa mkutano huo, alieleza kuwa lengo la mkutano huo ni pamoja na kuwahamasisha wanawake kushiri katika shughuli rasmi za uzalishaji mali. 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akipokelewa na Waandaaji wa Mkutano wa Uchumi wa Wanawake Afrika alipowasili katika mkutano uliofanyika jijini Dar es Salaam. Tarehe 26 Julai 2022
Sehemu ya washiriki wa Mkutano wa Uchumi wa Wanawake Afrika wakifualia mjadala ulikokuwa ukiendelea
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akiwa katika picha ya pamoja waandaaji na baadhi ya washiriki wa Mkutano wa Uchumi wa Wanawake Afrika uliofanyika jijini Dar es Salaam
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) akisisitiza jambo wakati wa akifungua Mkutano wa Uchumi wa Wanawake Afrika (Pan-African Women Economic Summit 2022) uliofanyika jijini Dar es Salaam