Friday, July 29, 2022

TANZANIA, USWISI KUENDELEZA USHIRIKIANO


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Uswisi zimeahidi kuendeleza zaidi ushirikiano katika nyanja mbalimbali ikiwemo teknolojia ya habari na mawasiliano, elimu, afya, ujenzi wa miundombinu, utawala bora na haki za binandamu, uhuru wa vyombo vya habari, kilimo na utalii kwa maslahi mapana ya pande zote mbili. 

Ahadi hiyo imetolewa kwa nyakati tofauti na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula na Balozi wa Uswisi nchini Mhe. Didier Chassot kwenye hafla ya kuadhimisha Siku ya Taifa ya Uswisi iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 28 Julai 2022. 


Waziri Mulamula alisema Tanzania na Uswisi zimekuwa na uhusiano mzuri wa kidiplomasia na zimeendelea kushirikiana katika nyanja za teknolojia ya habari na mwasiliano, elimu, afya, ujenzi wa miundombinu, utawala bora na haki za binandamu, uhuru wa vyombo vya habari, kilimo na utalii. 

“Uswisi imekuwa mdau mkubwa katika masuala ya uchumi na kijamii ambapo kampuni mbalimbali kutoka Uswisi zimewekeza hapa nchini na zimekuwa zikichangia kutoa ajira kwa watanzania na kuongeza pato la taifa,” alisema Waziri Mulamula 

Kwa upande wake Balozi wa Uswisi nchini Mhe. Didier Chassot alisema Uswis imefurahishwa na ushirikiano mzuri inaoupata kutoka Serikali ya Tanzania na kuahidi kuwa itaendelea kudumisha uhusiano huo kwa maslahi ya mataifa yote mawili

Balozi Chassota aliongeza kuwa Uswiss itaendelea kushirikiana na Tanzania na kuunga mkono juhudi mbalimbali za kukuza maendeleo ya kijamii, kisiasa na kiuchumi zinazofanywa na Serikali ya Tanzania.

Hafla hiyo ilihudhuriwa Mabalozi mbalimbali na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa wanaoziwakilisha nchi zao hapa nchini, asasi za kiraia, na wafanyabiashara. 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula akitoa hotuba yake katika hafla ya kuadhimisha Siku ya Taifa ya Uswisi iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 28 Julai 2022
Balozi wa Uswisi nchini Mhe. Didier Chassot akitoa hotuba yake katika hafla ya kuandimisha Siku ya Taifa ya Uswisi iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 28 Julai 2022
Hafla ya kuadhimisha Siku ya Taifa ya Uswisi iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 28 Julai 2022 ikiendelea. 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula na alozi wa Uswisi nchini Mhe. Didier Chassot wakifurahia jambo kwenye hafla ya kuadhimisha Siku ya Taifa ya Uswisi iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 28 Julai 2022

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.