Wednesday, July 6, 2022

BALOZI MULAMULA: SERIKALI KUENDELEA KUBORESHA MAZINGIRA WEZESHI KWA SEKTA BINAFSI


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula amefanya mazungumzo na Wawakilishi wa Bodi ya Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) katika ofisi ndogo za Wizara leo tarehe 6 Julai 2022 jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo Waziri Mulamula amewahakikishia Wawakilishi hao kuwa Serikali inaendelea kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi ili kukuza sekta za uzalishaji kwa maslahi mapana ya Taifa.

‘’ Wizara kupitia Balozi zetu nje imeendelea kuhakikisha fursa mbalimbali zinazopatikana nchini zinatangazwa katika maeneo ya uwakilishi ili kuzihakikishia sekta hizo mageuzi makubwa ya  kiuchumi” alisema Balozi Mulamula.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya TPSF, Bi. Angelina Ngalula pamoja na wajumbe alioambatana nao wameipongeza na kuishukuru Serikali ya Awamu ya Sita ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweka mkazo wa kuinua sekta binafsi.

Akifafanua Bi. Ngalula ameeleza juu ya uwepo wa mafanikio katika sekta za biashara, Utalii, uwekezaji, kilimo, madini, huduma, uchukuzi na usafirishaji na ujenzi.

“Sisi sekta binafsi tunaishukuru Serikali yetu kwa kuboresha mazingira ya biashara, sasa tunashuhudia mipaka inafunguka sambamba na ongezeko la watalii kupitia jitihada za makusudi zinazofanyika katika kuitangaza filamu ya “Tanzania the Royal Tour” alisema Bi. Ngalula

Aidha, akafafanua matokeo yaliyopatikana kupitia ziara za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, kwamba kupitia ziara hizo mikutano na makongamano ya biashara yalifanyika katika nchi mbalimbali na yamesaidia kupatikana kwa washirika wa kibiashara kutoka mataifa hayo.

Kupitia mazungumzo hayo Waziri Mulamula na Wawakilishi wa Bodi ya Taasisi ya Sekta Binafsi, wamekubaliana kuanzisha timu maalum ya uratibu na ufuatiliaji wa masuala mbalimbali ya kimkakati kitaifa, kwa lengo la kuimarisha na kukuza diplomasia ya uchumi nchini.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (kati) akizungumza na Wawakilishi wa Bodi ya Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) leo tarehe 6 Julai 2022 katika ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaam. Wa kwanza kushoto ni Mwenyekiti wa Bodi ya TPSF, Bi. Angelina Ngalula.


Waziri Mulamula akizungumza na Wawakilishi wa Bodi ya TPSF kutoka katika Sekta za Huduma, Sekta Umma, Sekta ya Wenye Viwanda Vidogo,Sekta ya Wafanyabiashara Wanawake, Sekta ya Uhandisi na Ujenzi, na ulioambatana, Uongozi wa TPSF uliokuwa umeambatana na Bi. Ngalula.

Kulia ni Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali, Balozi Mindi Kasiga akifafanua jambo katika mazungumzo hayo.


Balozi Mulamula akimkabidhi  Mwenyekiti wa Bodi ya TPSF, Bi. Ngalula vitabu vya Diplomasia ya Uchumi.

Picha ya Pamoja.



No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.