Monday, July 11, 2022

UBALOZI WA TANZANIA NCHINI ISRAEL ULIVYOADHIMISHA SIKU YA KISWAHILI DUNIANI

Wadau mbalimbali nchini Israel wamepongeza jitihada za Serikali ya Tanzania katika kukuza na kuienzi Lugha ya Kiswahili.

Pongezi hizo zimetolewa na wadau hao wakati wa Maadhimisho ya kwanza ya Siku ya Kiswahili Duniani yaliyofanyika tarehe katika Makazi ya Balozi wa Tanzania nchini humo tarehe 07Julai 2022

Kwa upande wake, Balozi wa Tanzania nchini Israel, Mhe. Alex Gabriel Kalua amesema kuwa ametumia maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani kukukutana na kujadiliana na wadau mbalimbali kuhusu namna bora ya kukuza na kuendeleza Lugha hiyo adhimu.

Aidha, Mhe. Balozi Kalua ambaye alijumuika na viongozi kutoka Serikali ya Israel, wadau mbalimbali wanaoshirikiana na Tanzania, Watanzania wanaoishi nchini humo na wageni mbalimbali, alitumia maadhimisho  hayo kugawa vitabu vya kujifunzia Kiswahili kikiwemo cha “Jifunze Kiswahili, Hazina ya Afrika: Kitabu cha Kwanza”, pamoja na kushiriki chakula cha Kitanzania na wadau hao.

Kadhalika, Mhe. Balozi Kalua alitoa hotuba yake kwa lugha ya Kiswahili ambayo ilitafsiriwa kwa Kiebrania.

Naye Mkurugenzi wa Ukanda wa Afrika Mashariki katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Israel, Bibi Amit Gil Bayaz ambaye ni miongoni mwa viongozi kutoka Serikali ya Israel walioshiriki aliipongeza Tanzania kwa maadhimisho hayo.

Maadhimisho hayo yalihitishwa kwa Wadau mbalimbali  kushiriki chakula na vinywaji vya kitanzania  ambapo walieleza kufurahishwa na ukarimu wa watanzanaia na kufurahia vinywaji na chakula cha kitanzania kilichoandaliwa kwa ajili yao.

Balozi wa Tanzania nchini Israel, Mhe. Alex Gabriel Kalua akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani yaliyofanyika kwenye Makazi ya Balozi nchini humo tarehe 7 Julai 2022 na kuwashirikisha wadau mbalimbali. Wengine katika picha ni Mwakilishi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Israel ambaye ni Mkurugenzi wa Ukanda wa Afrika Mashariki, Bibi Amit Gil Bayaz (wa pili kutoka kushoto), Rais wa Klabu ya Mabalozi waliopo Israel, Mhe. Balozi Yzihack Elden (kushoto) na Mwakilishi wa Balozi wa Heshima, Mhe. Chirich Nuriel Kasbian (wa pili kulia)


Mhe. Balozi Kalua akimkabidhi kitabu cha kujifunza Kiswahili, Mkurugenzi wa Ukanda wa Afrika Mashariki, Bibi Amit Gil Bayaz.

Mhe. Balozi Kalua akimkabidhi kitabu cha kujifunza Kiswahili, Rais wa Klabu ya Mabalozi waliopo Israel, Mhe. Yitzhack Elden


Mhe. Balozi Kalua akiwa na wadau mbalimbali aliowakabidhi vitabu

Wawakilishi kutoka Jeshi la Israel walioshiriki maadhimisho ya siku ya Kiswahili wakiwa na Mwambata Jeshi wa Ubalozi wa Tanzania nchini, Israel, Brig. Jen. Mziray


Wadau mbalimbali wakionesha vitabu vya kujifunza Kiswahili walivyokabidhiwa

 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.