Friday, July 22, 2022

BARABARA YA KIKANDA YA ARUSHA BYPASS CHACHU YA MAENDELEO YA KIUCHUMI KWA NCHI ZA EAC

Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wamesisitiza umuhimu wa kujenga miundombinu bora na ya kisasa ili kuweza kuyafikia malengo ya pamoja ya maendeleo ya kiuchumi katika jumuiya.

 

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika mashariki aliyemaliza muda wake, Mhe. Uhuru Kenyatta wakati wa hafla ya ufunguzi wa barabara ya kikanda ya Arusha Bypass uliofanyika leo tarehe 22 Julai jijini Arusha na kuhudhuriwa na nchi zote wanachana pamoja na mgeni mwalikwa Serikali ya Shirikisho la Somalia.

 

Pia akafafanua kuwa barabara hiyo pamoja na mambo mengine itasaidia kupunguza msongamano wa magari, itaongeza mawasiliano na muingiliano wa kijamii, itakuza biashara, itarahisisha usafiri wa mizigo na kupunguza umasikini kwa nchi wanachama na kujiletea heshima duniani.

 

Naye Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyeji wa mkutano huo, Mhe. Samia Suluhu Hassan katika hotuba yake ameeleza kuwa barabara iliyozinduliwa ina urefu wa kilomita 42.4 na imegharimu kiasi cha shilingi Billioni 197.4 na kwamba imejengwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na Kenya.

 

Vilevile, ameishukuru Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA) na Washirika wa Maendeleo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki “East Africa Trademark” kwa kuendelea kutoa uwezeshaji wa kifedha kukamilisha kwa awamu ya kwanza ya mradi huo na kukubali kuendelea kuwezesha awamu ya pili ya mradi wa barabara inayoanzia Arusha, Horiri, Taveta, Voi yenye urefu wa kilomita 117.

 

Kadhalika, Mhe. Rais Samia ametoa rai kwa wananchi kutumia fursa za miundombinu katika kukuza sekta za utalii, biashara, uwekezaji, usafirishaji wa mizigo na akawataka wananchi kutunza miundombinu iliyopo kuiwezesha serikali kuendelea na ujenzi wa miundombinu katika maeneo mengine kama vile uimarishaji wa miundombinu ya reli, bandari na usafiri wa anga.

 

Maboresho hayo ya miundombinu yatawezesha kuiunganisha Afrika Mashariki na nchi nyingine za Afrika na kulitumia vema soko la eneo huru la biashara la Afrika.

========================================


Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki wakikata utepe kuashiria ufunguzi wa barabara ya EAC Arusha Bypass uliofanyika eneo la Kisongo nje kidogo ya jiji la Arusha tarehe 22 Julai 2022.

Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki wakiwa wamesimama wakati ulipopigwa wimbo wa Taifa na wa Jumuiya ya Afrika Mashariki baada ya kuwasili kwenye hafla ya uzinduzi wa barabara ya EAC Arusha Bypass.

Rais wa Jamhuri ya Muungano, Mhe. Samia Suluhu Hassan (mwenye mask nyeupe) akiwasili eneo la Kisongo nje kidogo ya mji wa Arusha kwenye hafla ya ufunguzi wa barabara ya EAC Arusha Bypass. Kulia kwake ni Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dkt. Peter Mathuki akimuongoza Mhe. Rais Samia jukwaani.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula akiwasili katika eneo la Kisongo nje kidogo ya mji wa Arusha kushiriki hafla ya ufunguzi wa Barabara ya EAC Arusha Bypass.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.