Monday, July 4, 2022

BALOZI MULAMULA: WIZARA KUENDELEA KUHAMASISHA WAWEKEZAJI

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) amesema Wizara itaendelea kuhakikisha kuwa sekta za uwekezaji, biashara na utalii zinazidi kuimarika.

Balozi Mulamula alitoa kauli hiyo wakati alipotembelea banda la Wizara katika maonesho ya 46 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam.

Akiwa katika banda la Wizara, Waziri Mulamula amewapongeza watumishi wanaoiwakilisha Wizara katika maonesho hayo na kuongeza kwamba Wizara imekuwa ikijivunia kuwa sehemu ya kutafuta wawekezaji na wafanyabiashara ili kuja kuwekeza nchini kama ambavyo kauli mbiu ya maonesho hayo inavyosema ‘Tanzania: Mahali sahihi pa Biashara na Uwekezaji’

“Wizara kupitia Balozi zake Nje ya nchi inaendelea kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali katika kuhakikisha kuwa tunapata wawekezaji wa kutosha kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan imejitahidi kuboresha mazingira ya biashara na uwekeza” alisema Balozi Mulamula

Pamoja na mambo mengine, Mhe. Waziri aliwasihi watumishi wa Wizara kuendelea kufanya kazi kwa kuzingatia weledi, juhudi na bidii na kuendelea kuzitangaza fursa za biashara, uwekezaji pamoja na vivutio vya utalii vinavyopatikana nchini.

Katika tukio jingine Balozi Mulamula alishiriki katika hafla ya ufunguzi wa Maonesho ya 46 ya Biashara ya Sabasaba yaliyofunguliwa na Katibu Mtendaji wa Sekretarieti ya Eneo Huru la Biashara Afrika (AfCFTA) Mhe. Wamkele Mene tarehe 03 Juni, 2022 Jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akisaini kitabu cha wageni alipotembelea banda na Wizara inayoiongoza katika maonesho ya 46 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika picha ya pamoja na watumishi wa Wizara katika maonesho ya 46 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akizungumza na watumishi wa Wizara alipotembelea banda la wizara katika maonesho ya 46 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akizungumza na Watumishi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AlCC) katika maonesho ya 46 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam

Katibu Mtendaji wa Sekretarieti ya Eneo Huru la Biashara Afrika (AfCFTA) Mhe. Wamkele Mene akisalimiana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula wakati wa hafla ya ufunguzi wa maonesho ya 46 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam





No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.