Saturday, July 23, 2022

RAIS NDAYISHIMYE AKABIDHIWA UENYEKITI WA EAC

Rais wa Jamhuri ya Burundi, Mhe. Jen. Evariste Ndayishimye amekabidhiwa nafasi ya Uenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Mwenyekiti aliyemaliza muda wake Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. Uhuru Kenyatta wakati wa Mkutano wa 22 wa Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki uliomalizika tarehe 22 Julai 2022.

 

Akikabidhi nafasi hiyo Mhe. Kenyatta aliwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya jumuiya hiyo wakati wa uongozi wake ambapo alieleza kwamba Jumuiya imefanikiwa kukamilisha mchakato wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kuwa mwanachama, Kuondolewa kwa vikwazo vya kibiashara 13 kati ya 22 vilivyokuwepo awali, kutafuta ufumbuzi wa pamoja katika changamoto za Covid–19 na kuanzisha mchakato utakaowezesha nchi wanachama kupata chanjo ya Covax.

 

Masuala mengine ya utekelezaji ni; Kuhakikisha Burundi inafanikiwa kushiriki katika Shirikisho la Afrika Mashariki, kusimamia ushiriki wa asasi za kiraia na ushiriki wa sekta binafsi katika utekelezaji wa majukumu ya kikanda.

 

Naye Rais wa Burundi, Mhe. Jen. Ndayishimye baada ya kupokea majukumu hayo ya nafasi ya Mwenyekiti, alimshukuru Mhe. Kenyatta kwa uongozi bora na kwa mafanikio yaliyopatikana katika uongozi wake.

 

Aidha, akazishukuru nchi wanachama wa Jumuiya hiyo kwa kuiamini Burundi kuongoza, na akaeleza uelekeo wa utekelezaji wa majukumu katika kipindi chake cha uongozi utazingatia masuala yafuatayo; Kukuza mtangamano wa Afrika Mashariki na kuimarisha ujirani mwema; kuharakisha mkakati wa viwanda katika Jumuiya; Kuzingatia ombi la Jamhuri ya Shirikisho la Somalia kujiunga na Jumuiya hiyo na Usimamizi wa agenda ya amani na usalama ili kuondoa migogoro.

Masuala mengine yatakayosimamiwa ni pamoja na; Kuimarisha mfumo wa mageuzi ya kitaasisi, Kuendelea kusisitiza umuhimu wa maridhiano ya kitaifa ili kuweza kuyafikia maridhiano ya kisiasa katika ngazi ya jumuiya, Ushirikishwaji wa Wanawake na Vijana; na Wake za viongozi kushirikishwa katika utekelezaji wa malengo ya jumuiya.

 

Naye Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akihutubia katika mkutano huo alimuaga Mhe. Kenyatta kwakuwa anaelekea kipindi cha mwisho cha uongozi wake nchini Kenya  kuitakia nchi hiyo uchaguzi mkuu mwema unaotarajiwa kufanyika mwezi Agosti 2022.

 

Pamoja na mambo mengine mkutano huo umemchagua Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. Uhuru Kenyatta kuwa msimamizi wa mazungumzo ya amani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC); umefanya uapisho wa majaji wa Mahakama ya Afrika Mashariki ambao ni; Mhe. Jaji Leonard Gacuko kutoka Burundi na Mhe. Jaji Cheborion Barishaki kutoka Uganda.

 

Pia mkutano huo ulikabidhi zawadi kwa wanafunzi wa sekondari walioshinda katika nafasi mbalimbali kwenye mashindano ya uandishi wa insha kwa lugha ya Kiswahili, kiingereza na kifaransa. Walishiriki hao ni wale ambao walishiriki mashindano hayo kuanzia mwaka 2019 hadi 2021 lakini hawakukabidhiwa zawadi kufuatia kutoitishwa kwa mikutano ya Wakuu wa Nchi ya ana kwa ana kutokana na changamoto ya maambukizi yaCovid-19.

===========================================


Rais wa Jamhuri ya Kenya na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki aliyemaliza muda wake wa uongozi, Mhe. Uhuru Kenyatta akikabidhi vitendea kazi kwa Mwenyekiti mpya wa Jumuiya hiyo Rais wa Jamhuri ya Burundi, Mhe. Evariste Ndayishimye. Makabidhiano hayo yamefanyika wakati wa Mkutano wa 22 wa Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofanyika tarehe 22 Julai jijini Arusha.

Rais wa Jamhuri ya Kenya na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki aliyemaliza muda wake wa uongozi, Mhe. Uhuru Kenyatta akimpongeza Mwenyekiti mpya wa Jumuiya hiyo Rais wa Jamhuri ya Burundi, Mhe. Evariste Ndayishimye kwa kuaminiwa kushika nafasi hiyo. Anayeshuhudia ni Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dkt. Peter Mathuki.


Rais wa Jamhuri ya Burundi na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe. Evariste Ndayishimye akiongoza Mkutano wa 22 wa Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki baada ya kukamilika kwa makabidhiano ya nafasi hiyo ya Mwenyekiti.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.