Friday, November 24, 2017

Katibu Mkuu wa Mambo ya Nje ziarani China kushiriki Mkutano wa FOCAC

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Adolf Mkenda akifungua Mkutano wa kuvutia wawekezaji uliofanyika Ubalozi wa Tanzania nchini China na kuhudhuriwa na wawakilishi wa Makampuni 100 yenye nia ya kuwekeza Barani Afrika. Prof. Mkenda yupo nchini China kwa ajili ya kuhudhuria Mkutano wa 12 wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika FOCAC unaofanyika kwa ngazi ya Watendaji.
Prof. Mkenda akizungumza na Kiongozi wa Benki ya AIIB iliyoanzishwa kwa lengo  la kutoa mikopo kwa miradi ya miundombinu kwa nchi wanachama wa Belt and Road. Benki hiyo imeikaribisha Tanzania kujiunga nayo ili iweze kufaidika na fursa za mikopo nafuu. Vilevile, Prof. Mkendaamekutana na uongozi wa Kampuni ya Hainan Group inayomiliki mashirika mbalimbali ya ndege na Hoteli zaidi ya 1000 ulimwenguni. Katika mazungumzo hayo Prof. Mkenda amewashawishi wawekeze kwenye ujenzi wa Hoteli katika maeneo ya Utalii Zanzibar na Tanzania Bara.
Ujumbe ukifuatilia mazungumzo kati ya Prof. Mkenda na Kiongozi wa Benki ya AIIB (hawapo pichani).  Kutoka kushoto ni Prof. Elisante Ole Gabriel, Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Dkt. Lu Yongqing, aliyekuwa Balozi wa China nchini Tanzania na Mhe. Mbelwa Kairuki, Balozi wa Tanzania nchini China.
Ujumbe kutoka Benki ya AIIB
Prof. Mkenda akizungumza na Waandishi wa Habari mara baada ya kufungua Mkutano wa Kuvutia Wawekezaji uliofanyika kwenye Ubalozi wa Tanzania nchini China.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Mhe. Chen Xiaodong akifungua Mkutano wa Maafisa Waandamizi wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika unaofanyika tarehe 24 Novemba, 2017 Beijing, China. Baada ya ufunguzi kiongozi huyo amefanya mazungumzo ya kukuza ushirikiano na nchi nne Tanzania ikiwa ya kwanza kukutana nayo. Katika mazungumzo kati ya Prof. Mkenda na Mhe. Xiaodong, China imeahidi kuendeleza ushirikiano katika nyanja  za uchumi hususan kwenye ujenzi wa miundombinu ikiwemo ujenzi wa Eneo Maalum la Uwekezaji Bagamoyo.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Adolf Mkenda akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Mhe. CHEN Xiaodong mara baada ya kukamilisha mazungumzo ya ushirikiano kati ya Tanzania na China.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.