Friday, April 12, 2019

Profesa Kabudi amekutana Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb.) akisalimiana na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Balozi Seif Ali Iddi alipofika kujitambulisha rasmi baada ya kuteuliwa kuwa Waziri wa Wizara hiyo. 
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi wa kwanza kulia akimwelezea jambo Prof. Palamagamba John Kabudi, wa kwanza kushoto ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mh. Balozi Ramadhan Muombwa Mwinyi. 

Waziri wa Mabo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Profesa Palamagamba John Kabudi wa Pili kutoka Kushoto akielezea msimamo wa Wizara yake katika kuzitangaza fursa za Uwekezaji zilizopo Zanzibar. Wa kwanza kushoto ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mwinyi.

Profesa Palamagamba John Kabudi wa Pili kutoka Kushoto akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo yake na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi.
=====================

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Profesa Palamagamba John Kabudi  (Mb.) amesema Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imefanikiwa kuwa Taifa moja linaloendelea kudumu muda wote kutokana na misingi imara iliyowekwa na Waasisi wa Taifa hilo.
Amesema yapo Makabila mengi katika Mikoa na Wilaya mbali mbali Nchini lakini muungano wa lugha moja inayozungumzwa na Wananchi wake Bara na Zanzibar imekuwa mfano kwa Mataifa mengine Duniani.
Profesa Palamagamba John Kabudi ameeleza hayo wakati akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi, Vuga Mjini Zanzibar alipofika kujitambulisha baada ya kuteuliwa na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. John Pombe Magufuli kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
Ameongeza kuwa yapo Mataifa mengi Duniani yaliyowahi kuunganisha Nchi zao akitolea Mfano iliyokuwa Yugoslavia na sasa imesambaratika pia Senegal na Gambia kwa upande Afrika lakini zimeshindwa kuendeleza Muungano wao.
Waziri Palamagamba John Kabudi alisema wakati Serikali zote mbili zikiendelea kuheshimu kwa kuweka Kumbukumbu za Waasisi hao ambao ni Hayati Mzee Abeid Amani Karume na Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Vizazi vya sasa vinapaswa kujifunza tabia ya Viongozi hao walioacha misingi imara ya kitaifa. 

Akigusia suala la Diplomasia ya Uchumi ambayo kwa sasa Tanzania imeelekeza nguvu zake kupitia Balozi zake zilizoko nje ya mipaka ya Tanzania Profesa Palamagamba John Kabudi amesema Serikali inaendeleza mfumo wa kushawishi Wawekezaji ili kuunga mkono jitihada za Taifa za kuwa na Tanzania ya Viwanda ifikapo Mwaka 2025.
Amesema mkakati wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wa Kuimarisha Uchumi wake unapaswa kuungwa mkono na Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania katika muelekeo wa kuelekea kwenye Maendeleo ya haraka.
Akigusia Sekta ya Utalii kufanya vyema Zanzibar, Waziri Palamagamba amesema Sekta hiyo ni muhimu hivi sasa kwa mapato ya Taifa na nilazima iwekewe utaratibu wa pamoja utakaosaidia kuuza haiba ya pande zote mbili za Muungano.
Alisema vipo vivutio vinavyopaswa kutangazwa kwa pamoja Bara na Zanzibar ambavyo vinaweza kutoa nguvu ya ushawishi wa Watalii kufanya ziara ya kutembelea sehemu zote mbili kwa wakati mmoja.
Waziri huyo wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki alielezea faraja yake kutokana na Zanzibar kupiga hatua kubwa katika kuimarisha Sekta ya Utalii inayotoa ajira kubwa hasa kwa Vijana.
Akitoa shukrani zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema ushawishi wa Uwekezaji ndani ya Visiwa vya Zanzibar unapaswa kuungwa mkono na Ofisi zote za Kibalozi za Tanzania zilizopo Mataifa mbali mbali Duniani.
Alisema Zanzibar ni sehemu ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo ushawishi wake kwa Wawekezaji na Mataifa ya kigeni unawajibika kusimamiwa na Mabalozi wa Tanzania kupitia Wizara yake ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Balozi Seif alimueleza Profesa Palamagamba John Kabudi kwamba Zanzibar kupitia Viongozi wake wote waliopita na waliopo hivi sasa bado wanaendeleza sera na Mikakati iliyoachwa na Muasisi wa Mapinduzi ya Zanzibar Hayati Mzee Abeid Amani Karume.
Alisema uimarishaji wa Miundombinu ya Mawasiliano, Ujenzi wa Nyumba za Kisasa za Maendeleo, Afya, Elimu pamoja na huduma za Maji safi na salama ni miongoni mwa Sekta zinazoendelea kuimarishwa na Viongozi wote.
Balozi Seif Ali Iddi alimweleza Profesa Palamagamba John Kabudi, kuwa Miradi iliyobuniwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikiwemo ujenzi wa Miji Mipya kama ule wa Ng’ambo tuitakayo katika eneo la Kwahani na Mtaa wa Chumbuni imelenga kustawisha maisha ya Wananchi wake ili kuachana na matumizi mabaya ya Ardhi ndogo iliyopo visiwani humo.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma
12 Aprili, 2019.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.