Friday, March 10, 2023

TANZANIA YAFUNGUA RASMI OFISI ZA UBALOZI NCHINI NAMIBIA

Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imefungua rasmi Ofisi za Ubalozi jijini Windhoek, Namibia.

Hafla ya ufunguzi wa ofisi hizo za ubalozi ulihudhuriwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Namibia, Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah, Mabalozi wa nchi za Afrika, viongozi wa Serikali ya Tanzania na viongozi wa jumuiya ya Watanzania wanaoishi nchini humo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri Dkt. Tax ameishukuru Jamhuri ya Namibia hususan Wizara ya Mambo ya Nje kwa ushirikiano ilioutoa katika hatua zote za kuanzisha ofisi hiyo na kuelezea kuwa kushiriki kwao katika tukio hilo la kihistoria la ufunguzi ni hatua muhimu katika kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia baina ya nchi hizo.

Amesema  Tanzania kama mama wa lugha ya Kiswahili inaendelea na jitihada  za kuhakikisha lugha hiyo inatangazwa na kuenea kwa kasi kupitia Balozi zake, vyuo vya kimataifa na majukwaa mbalimbali ya kimataifa.

“Wakati huu ambapo Serikali za Tanzania na Namibia zipo kwenye mazungumzo ya lugha ya Kiswahili kuwa sehemu ya lugha ya chaguo katika shule za Namibia, Ubalozi umefungua maktaba ndogo yenye vitabu na majarida ya Kiswahili kwa ajili ya watu wenye nia ya kujifunza kiswahili kuja kujisomea” alisema Dkt. Tax

Naye Mhe. Dkt. Ndaitwah akizungumza katika hafla hiyo alieleza kuwa kwasasa nchi hizo mbili zina makazi ya ubalozi katika miji mikuu ambapo ni hatua muhimu katika kukuza na kuimarisha ushirikiano baina ya nchi hizo na watu wake.

Kadhalika, amempomgeza Balozi wa Tanzania nchini Namibia, Mhe. Dkt. Modestus Kipilimba kwa kuchagua jengo lenye ubora na la kisasa kwa ajili ya ofisi za ubalozi huo ambalo ni rafiki kwa mazingira.

‘’ Tanzania ikiwa mpambanaji wa bara la Afrika na Kusini mwa Afrika siku zote imekuwa pamoja nasi na hivyo sisi wanamibia tutakapokuja kujisomea na kufanya tafiti katika maktaba hii ya Kiswahili inayofunguliwa leo tutakuwa katika mazingira salama” alisema Mhe. Ndaitwah.

Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Namibia ulianza utekelezaji wa majukumu yake ya kidiplomasia tarehe 20 Februari 2020 na kufanya Mhe. Dkt. Modestus Kipilimba kuwa Balozi wa kwanza kuwaiwakilisha Tanzania katika nchi hiyo.

Hafla ya ufunguzi wa Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Namibia imefanyika pembezoni mwa Mkutano wa Tatu wa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Namibia unaofanyika jijini Windhoek Namibia kuanzia tarehe 8 hadi 10 Machi 2023 ambapo Mhe. Dkt. Tax anaongoza ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo.

Wakati huo huo, Waziri Dkt. Tax alifanya mazungumzo na viongozi wa Jumuiya ya Watanzania wanaoishi nchini Namibia ambao walijitambulisha kitaaluma ni Madaktari wa Binadamu.

Pamoja na mambo mengine Mhe. Waziri aliwasihi kuendelea kuwa mabalozi wazuri wa Tanzania wanapokuwa nje ya nchi na kuendelea na zoezi la kujiandikisha linalofanyika kwa watanzania wenye taaluma mbalimbali waliopo nje ya nchi ili waweze kutambulika na kuisaidia nchi yao katika taaluma hizo pale wanapohitajika.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (kushoto) pamoja na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Namibia, Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah wakikata utepe kuashiria ufunguzi rasmi wa ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Namibia.
   

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akihutubia wakati wa hafla ya ufunguzi wa ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Namibia. Mhe. Dkt. Tax ameishukuru Jamhuri ya Namibia kwa ushirikiano ilioutoa katika hatua za kuanzisha ubalozi huo  na uwepo wao katika tukio hilo muhimu na la kihistoria kwa nchi hizo mbili.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Namibia, Mhe. Netumbo Nandi-Ndaitwah akihutubia wakati wa hafla ya ufunguzi wa ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Namibia. Mhe. Dkt. Ndaitwah ameeleza kuwa uwepo wa ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Namibia ni ishara kubwa na muhimu katika kuendeleza na kuimarisha uhusiano uliopo kwa maslahi ya nchi hizo na watu wake.


     Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (kushoto) na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Namibia, Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah wakisoma kitabu cha Kiswahili katika makataba ya kiswahili iliyopo katika ofisi za ubalozi wa Tanzania nchini Namibia mara baada ya kukata utepe kuashiria ufunguzi wa ofisi hiyo.


 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Namibia, Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah katika picha ya pamoja na Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Namibia, Mhe. Dkt. Modestus Kipilimba (kushoto) wakati wa hafla ya ufunguzi wa ofisi za Ubalozi jijini Windhoek, Namibia.


     Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Namibia, Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah katika picha ya pamoja na Mabalozi wa nchi za Afrika wanaowakilisha nchini Namibia wakati wa hafla ya ufunguzi rasmi wa ofisi za Ubalozi jijini Windhoek, Namibia.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Namibia, Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah katika picha ya pamoja na Watumishi wa ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Namibia wakati wa hafla ya ufunguzi rasmi wa ofisi za Ubalozi jijini Windhoek, Namibia.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Namibia, Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah katika picha ya pamoja na Watanzania wanaoishi nchini Namibia wakati wa hafla ya ufunguzi rasmi wa ofisi za Ubalozi jijini Windhoek, Namibia.


 


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.