Monday, June 10, 2024

KATIBU MKUU MAMBO YA NJE AONGOZA UJUMBE WA TANZANIA KIKAO CHA SADC MASUALA YA SIASA NA DIPLOMASIA

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo ameongoza ujumbe wa Tanzania kushiriki Kikao cha Pamoja cha Kamati Ndogo ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kuhusu masuala ya Siasa na Diplomasia kilichofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 10 Juni 2024.


Akifungua kikao hicho ambacho kimefanyika kwa ngazi ya Makatibu Wakuu , Mwenyekiti ambaye ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Zambia,  Bi. Etambuyu Gundersen aliwataka wajumbe kujadili na kutoa mapendekezo katika agenda mbalimbali zilizowasilishwa kwao ili hatimaye mapendekezo hayo yawasilishwe kwenye kikao cha Mawaziri kitakachofanyika mwezi Julai 2024 kwa ajili ya kuridhiwa.

 

Akichangia hoja kwenye kikao hicho, Balozi Shelukindo amezishukuru na kuzipongeza Nchi Wanachama wa SADC kwa kufanikisha uundwaji na uzinduzi wa Sanamu ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere uliofanyika mwezi Februari 2024 katika Makao Makuu ya Umoja wa Afrika jijini Addis Ababa, Ethiopia.

 

Amesema  uzinduzi huo ambao ulihudhuriwa na idadi kubwa  ya wakuu wa nchi  wa Afrika  ulidhihirisha namna ambavyo  wanaenzi mchango mkubwa uliotolewa na Hayati Mwalimu Nyerere kwenye Ukombozi wa  Nchi za Kusini mwa Afrika.

 

Kadhalika amesema  Tanzania inaendelea na mawasilianao ya ndani ili kukamilisha Mpango  wa Taifa  wa Utekelezaji wa Azimio la Umoja wa Mataifa Namba 1325 kuhusu kuwawezesha Wanawake kushiriki  katika juhudi  za  kutatua, kuzuia na kudhibiti migogoro duniani huku akizipongeza nchi zilizokamilisha Mpango huo ikiwemo Zimbawe na Madagascar.

 

Vilevile, ametumia fursa hiyo kuzipongeza Jamhuri ya Afrika Kusini na Jamhuri ya Madagascar kwa kufanikisha uchaguzi mkuu wa Rais na Wabunge uliofanyika kwenye nchi hizo kwa amani na utulivu  tarehe 29 Mei 2024 mtawalia.

 

Amesema, kikanda uchaguzi katika nchi hizi mbili umeakisi viwango vya kimataifa vya demokrasia pamoja na kanuni na miongozo ya SADC kuhusu uchaguzi unaofuata misingi ya demokrasia.

 

Kikao hicho ambacho kimefanyika kwa ajili ya kuandaa mkutano wa Mawaziri unaotarajiwa kufanyika mwezi Julai 2024,  kimehudhuriwa na Nchi za Tanzania, Lesotho, Eswatini, Botswana, Angola, Namibia, Afrika Kusini, Shelisheli ,  Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Zambia na Zimbabwe.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo akizungumza wakati wa Kikao cha Pamoja cha Kamati Ndogo ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kuhusu masuala ya Siasa na Diplomasia kilichofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 10 Juni 2024
Katibu Mkuu, Balozi Shelukindo akichangia hoja wakati wa Kikao cha Pamoja cha Kamati Ndogo ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kuhusu masuala ya Siasa na Diplomasia kilichofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 10 Juni 2024. Kulia ni Afisa Mambo ya Nje anayeshughulikia Dawati la SADC, Bi. Shazma Msuya akinukuu taarifa ya kikao hicho. 

 
Kikao kikiendelea

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.