Saturday, March 16, 2019

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje akutana kwa mazungumzo na Balozi wa Canada nchini

Mhe. Dkt. Damas D. Ndumbaro (Mb.), Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki amekutana na kufanya mazungumzo na Mhe. Pamela O’Donnell, Balozi wa Canada nchini. Mazungumzo hayo yaliyohudhuriwa pia na Bw. Jestas A. Nyamanga, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika yalifanyika kwenye ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salam tarehe 15 Machi, 2019.

Mazungumzo hayo yalilenga kuimarisha uhusiano wa kihistoria wa Tanzania na Canada ambao ulijengwa tangu enzi za Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius K. Nyerere.

Tanzania na Canada zimekuwa na ushirikiano katika masuala mbalimbali ikiwemo elimu, afya, biashara, uwekezaji, utawala wa Sheria pamoja na haki za binadamu.

Katika mazungumzo hayo, pamoja na mambo mengine, Mhe. Naibu Waziri alisisitiza umuhimu wa ushirikiano unaolenga kuleta tija katika kuinua maisha ya Watanzania.

Mhe. Dkt. Ndumbaro alitumia fursa hiyo kumueleza Balozi huyo kuhusu mafanikio ya Serikali katika kujenga uchumi na kuomba Serikali ya Canada iendelee kutoa ushirikiano kwa Tanzania kwa lengo la kuleta maendeleo zaidi kwa wananchi. Aidha, alimhakikishia  ushirikiano kutoka Wizarani ili kumwezesha kutekeleza majukumu yake kwa manufaa ya ushirikiano wa nchi hizi mbili.
Mhe. Dkt. Damas D. Ndumbaro (Mb), Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akizungumza na Balozi wa Canada hapa nchini, Mhe. Pamela O’Donnel. 
Mazungungumzo kati ya Mhe. Dkt. Ndumbaro na Balozi O'Donnel yakiendelea huku  Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika, Bw. Jestas A. Nyamanga akifuatilia mazungumzo hayo.

 Picha ya pamoja
==================================================


...MKUTANO KATI YA KAIMU MKURUGENZI WA IDARA YA ULAYA NA AMERIKA NA BALOZI WA ITALIA NCHINI

 Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika, Bw. Jestas A. Nyamanga amekutana na kufanya mazungumzo na Mhe. Roberto Mengoni, Balozi wa Italia hapa nchini.

Mazungumzo hayo yaliyofanyika katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam tarehe 15 Machi 2019 yalilenga katika kuimarisha uhusiano baina ya Tanzania na Italia hususan katika masuala ya kimataifa, utamaduni,  biashara na uwekezaji.

Aidha, walikubaliana kuimarisha ushirikiano zaidi na  kuibua maeneo mapya ya ushirikiano kwa maslahi ya mataifa yote mawili.

Bw. Nyamanga alimhakikishia Balozi huyo ushirikiano kutoka kwake na Wizara  kwa ujumla katika masuala mbalimbali yenye maslahi kwa wananchi wa mataifa hayo mawili.


Pichani ni Bw. Jestas A. Nyamanga, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika akiwa kwenye mazungumzo na Balozi wa Italia hapa nchini Mhe. Roberto Mengoni

Bw. Nyamanga akiwa katika picha ya pamoja na Balozi Mengoni mara baada ya kumaliza mazungumzo kati yao

Friday, March 15, 2019

Tanzania yashiriki katika mkutano wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika




Katibu Mtendaji wa  Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Bi. Stergomena Tax, akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano wa  Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC Council of Ministers),  unaofanyika Windhoek, Namibia, kuanzia tarehe 15 -17 Machi, 2019.  
Mkutano huu, unahudhuriwa na Mawaziri wa Mambo ya Nje, Mawaziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji na Mawaziri wa Fedha pamoja nchi 16 wanachama wa SADC ambapo Tanzania inawakilishwa katika mkutano huu na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi (Mb.); Waziri Ofisi ya Rais, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Issa Haji Ussi Gavu; Waziri wa Viwanda na  Biashara, Mhe. George Kakunda (Mb.); na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji (Mb.). 
Masuala yanayojadiliwa katika mkutano huu ni pamoja na  Taarifa ya Utekelezaji wa mipango na mikakati ya SADC; Taarifa ya Kamati ya Fedha kwa mwaka wa fedha 2018/2019 na Kamati ya Usimamizi wa Rasilimali watu; Hatua zilizofikiwa katika mchakato wa Visiwa vya Komoro kujiunga na SADC na Mpango wa Kuanzisha chuo cha Uhawilishwaji cha SADC (SADC  University of Transformation).
Masuala mengine yanayotarajiwa kujadiliwa katika mkutano huu ni pamoja  na; Uendelezaji wa viwanda katika kanda; Utekelezaji wa Mkakati wa Kanda wa Mawasiliano; Mabadiliko ya Kitaasisi katika Umoja wa Afrika(AU); na Majadiliano ya Ubia Mpya Baina ya Nchi za Kundi la Afrika, Carribean na Pasifiki (ACP) na Umoja wa Ulaya (EU), baada ya mkataba wa Cotonou kumalizika mwaka 2020.
Mkutano huu umetanguliwa na Kikao cha Makatibu Wakuu pamoja na maafisa waandamizi  uliofanyika kuanzia tarehe 11 - 14 Machi, 2019, Windhoek. Namibia. Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Faraji Mnyepe, ameongoza ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo.




Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirkiano wa Afrika Mashariki Prof. Kabudi akifuatilia hotuba ya Katibu Mtendaji wa SADC.


Naibu Waziri Mkuu wa Namibia ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo na Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri la SADC, Mhe.Netumbo Nandi-Ndaitwah,  akitoa hotuba wakati wa mkutano huo.
Wajumbe  kutoka nchi za Tanzania, Zambia  na Afrika Kusini, wakifuatilia hotuba ya Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri la SADC, Mhe. Nandi-Ndaitwah.


Mawaziri wa SADC wakiwa katika picha ya pamoja.

Tanzania na Brazil kuendelea kuimarisha ushirikiano

Bw. Jestas A. Nyamanga, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akisalimiana na Mhe. Antonio Augusto Martins Cesar, Balozi mpya wa Brazil hapa nchini walipokutana kwa mazungumzo kwenye ofisi ndogo za Wizara zilizopo Dar es Salaam hivi karibuni. Pamoja na mambo mengine, mazungumzo yao yalijikita katika kuimarisha uhusiano baina ya Tanzania na Brazil hususan katika  sekta ya afya, kilimo biashara na uwekezaji wa viwanda. Kwa upande wake, Mhe. Balozi Cesar aliahidi kutoa ushirikiano kwa Wizara na Serikali kwa ujumla ili kuhakikisha uhusiano baina ya Tanzania na Brazil unafikia malengo yaliyokusudiwa kwa maslahi ya mataifa haya mawili. 
  Bw. Nyamanga akimweleza jambo Mhe. Cesar, Balozi wa Brazil hapa nchini wakati wa mazungumzo yao. 



Wednesday, March 13, 2019

Prof. Kabudi apokea Salamu za Pongezi kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa China

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Prof. Kabudi apokea Salamu za Pongezi kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa China

Mheshimiwa Prof. Palamagamba J. Kabudi (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, leo tarehe 13 Machi, 2019 amekutana na kufanya mazungumzo na Mheshimiwa WANG Ke, Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China.

Mheshimiwa WANG Ke pamoja na masuala mengine amewasilisha kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki barua ya pongezi kutoka kwa Mheshimiwa Wang Yi, Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Watu wa China kufuatia Prof. Kabudi kuteuliwa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. 

Aidha Prof. Kabudi kupitia kwa Mheshimwa Balozi ameshukuru kwa salamu hizo za pongezi alizopokea.

Katika mazungumzo yao, Prof. Kabudi na Balozi WANG Ke, wameahidi kufanya kazi kwa pamoja ili kuimarisha ushirikiano wa kihistoria baina ya nchi hizo mbili. Na kwa pamoja wamesisitiza umuhimu wa kuendelea na jitihada za kuimarisha mahusiano ya kisiasa, kijamii, kiuchumi hususan kwenye maeneo la uwekezaji, biashara, utalii na miundombinu.
                                                                      
Prof. Kabudi ametumia fursa hiyo kuishukuru Jamhuri ya Watu wa China kwa misaada ya kimaendeleo wanayoendelea kuitoa na kwamba Serikali inafurahishwa na Jinsi China inavyounga mkono jitihada zake za kuwaletea wananchi maendeleo na kujenga uchumi.

Tanzania na China zimekuwa na mahusiano ya kidiplomasia tangu mwaka 1964 na mwaka huu zinatarajia kuadhimisha miaka 55 ya ushirikiano huo.

Mheshimiwa Wang amekuwa Balozi wa kwanza kuonana na Mhe. Kabudi tangu kuteuliwa kwake na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuiongoza Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma.
13 Machi 2019
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akipokea barua ya pongezi kutoka kwa Balozi wa China nchini, Mhe. WANG Ke. Balozi wa China aliwasilisha barua hiyo kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Mhe. WANG Yi ambapo anampongeza Prof. Kabudi kwa kuteuliwa kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Mhe. Prof. Kabudi akisoma barua ya pongezi kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa China ambayo iliwasilishwa wizarani na Balozi wa China nchini.

Mhe. Prof. Kabudi akiwa katika mazungumzo na Balozi wa China mara baada ya kupokea barua ya pongezi.



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Prof. Kabudi kushiriki Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika

Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anatarajiwa kuondoka nchini tarehe 14 Machi, 2019 kuelekea Windhoek, Namibia kwa lengo la kuhudhuria Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya  ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) utakaofanyika kuanzia tarehe 15 hadi 17 Machi 2019.

Mkutano huu unatarajiwa kuhudhuriwa na Mawaziri wa Mambo ya Nje, Mawaziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji na Mawaziri wa Fedha pamoja na Makatibu Wakuu kutoka nchi wanachama wote wa SADC. Mkutano huu utatanguliwa na Kikao cha Makatibu Wakuu kitakachofanyika kuanzia tarehe 11 hadi 14 Machi 2019 ambapo Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe anashiriki.

Aidha, mkutano huu utajadili  masuala mbalimbali ikiwemo: Taarifa ya utekelezaji wa mipango na mikakati ya SADC; Taarifa ya Kamati ya Fedha na Kamati ya Usimamizi wa Rasilimali watu; Hatua zilizofikiwa katika mchakato wa Visiwa vya Comoro kujiunga na SADC na Mpango wa Kuanzisha Chuo cha Uhawilishwaji cha SADC (SADC University of Transformation).

Masuala mengine yatakayojadiliwa ni; Utekelezaji wa Mkakati wa Kanda wa Mawasiliano; Mabadiliko ya Kitaasisi katika Umoja wa Afrika; na Majadiliano ya Ubia Mpya Baina ya Nchi za Kundi la Afrika, Carribean na Pasifiki (ACP) na Umoja wa Ulaya (EU) baada ya mkataba wa sasa wa Cotonou kumalizika mwaka 2020.

Mhe. Prof. Kabudi ambaye ataongoza ujumbe wa Tanzania kwenye mkutano huo, atatumia fursa hiyo kuendelea kusisitiza umuhimu wa kuimarisha utangamano na ushirikiano katika Kanda na kufanya Jumuiya ya SADC kuwa chanzo muhimu cha maendeleo kwa wananchi wa nchi wanachama wa jumuiya hiyo.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma, 13 Machi 2019.



Nafasi za masomo na ajira

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Nafasi za masomo na ajira

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki inapenda kuwahimiza Watanzania wenye sifa kuomba fursa za masomo na ajira zinazotolewa na wadau mbalimbali duniani. Fursa zilizopokelewa mwezi Machi 2019 ni kama ifuatavyo:

i.       Mafunzo ya Shahada ya Uzamili yanayotolewa na Chuo Kikuu cha British nchini Misri (British University – Egypt) kwa kipindi cha mwaka wa masomo 2019/2020. Fursa hizi zinaratibiwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, na maombi yanafanyika kwa njia ya  mtandao kupitia tovuti, http://www.bue.edu.eg/;

ii.    Mafunzo ya Shahada ya Kwanza na Uzamili yanayotolewa na Taasisi ya Elimu ya Urusi (Russian Education Institute)                                               kwa kipindi cha mwaka wa masomo 2019/2020 na 2020/2021. Fursa hizi zinaratibiwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Maelezo ya namna ya kuomba fursa hizo yanapatikana katika Wizara zinazoratibu mafunzo hayo. Mwisho wa kufanya maombi kwa mwaka wa masomo 2019/2020 ni tarehe 25 Machi 2019 na tarehe 25 Juni 2020 kwa mwaka wa masomo 2020/2021;

iii. Mafunzo ya Shahada ya Uzamili katika fani ya Usuluhisihi katika Mchakato wa kutafuta Amani (Mediation in Peace Processes) yatakayotolewa nchini Uswisi katika kipindi cha mwaka wa masomo 2019/2021.  Maombi yanafanyika kwa njia ya mtandao kupitia tovuti, http://www.mas-mediation.ethz.ch/.  Mwisho wa kufanya maombi ni tarehe 21 Aprili 2019;

NAFASI ZA AJIRA
iv. Nafasi ya ajira ya Afisa Tathmini (Evaluation Officer, P-3) katika Sekretarieti ya Jumuiya ya Kudhibiti Matumizi ya Silaha za Kemikali (The Secretariat of the Organization for the Prohibition of Chemical Weapons-OPCW). Maelezo ya jinsi ya kuomba yanapatikana katika tovuti, https://opcw-career.talent-soft.com/job/job-officer-industry-p-3_11.aspx. Mwisho wa kutuma maombi ni tarehe 15 Machi 2019; na

v.    Nafasi ya ajira ya Afisa Usalama wa Masuala ya Habari (Information Security Officer, P – 3) katika Sekretarieti ya Jumuiya ya Kudhibiti Matumizi ya Silaha za Kemikali (The Secretariat of the Organization for the Prohibition of Chemical Weapons-OPCW). Maelezo ya jinsi ya kuomba yanapatikana katika tovuti, https://opcw-career.talent-soft.com/job/job-information- security-officer-industry-p-3_18.aspx. Mwisho wa kutuma maombi ni tarehe 26 Machi 2019.
         

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma.
13 Machi 2019

Balozi wa Canada atembelea Wizara ya Mambo ya Nje

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Balozi wa Canada atembelea Wizara ya Mambo ya Nje 

Bw. Jestas A. Nyamanga, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika-Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Canada hapa nchini Mhe. Pamela O’Donnell tarehe 11 Machi 2019.

Mazungumzo hayo yaliyofanyika jijini Dar es Salam yamelenga kuimarisha uhusiano baina ya Tanzania na Canada. Mataifa haya mawili, kwa kipindi kirefu yamekuwa yakishirikiana kwenye masuala ya afya, elimu, ukuzaji wa uchumi, Utawala Bora pamoja na biashara na uwekezaji.

Katika mazungumzo hayo, Balozi wa Canada amemhakikishia Kaimu Mkurugenzi kuwa, Serikali ya Canada inaendelea kuunga mkono jitihada za Serikali ya awamu ya tano katika kuleta Maendeleo na kuondoa umaskini na kwamba Canada itatekeleza kwa ufanisi miradi iliyopo inayotekelezwa kupitia Serikali , Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Asasi zisizo za Kiserikali(NGOs).

Wakati huo huo, Kaimu Mkurugenzi alimkaribisha Balozi huyo mpya nchini na kuishukuru Serikali ya Canada kwa ushirikiano mzuri na wakihistoria uliodumu baina ya Tanzania na Canada .

Aidha, aliishukuru Serikali ya Canada kwa kuisaidia Tanzania katika miradi muhimu na ya kipaumbele hususan miradi ya afya, elimu na ukuzaji wa uchumi. Alimhakikishia ushirikiano thabiti wa Wizara na Serikali kwa jumla katika kuhakikisha miradi iliyopo inatekelezwa kwa ufanisi na mingine mipya inaibuliwa.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma.
13 Machi 2019

Bw. Jestas A. Nyamanga, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika akimkaribisha Balozi wa Canada hapa nchini Mhe. Pamela O’ Donnell

Bw. Jestas A. Nyamanga, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika-Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Canada hapa nchini Mhe. Pamela O’Donnell.


Bw. Jestas A. Nyamanga, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika akiendelea kufanya majadiliano na Balozi wa Canada hapa nchini Mhe. Pamela O’ Donnell.

Prof. Kabudi akutana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mheshimiwa Prof. Palamagamba J. Kabudi (Mb)  amekutana na kufanya mazungumzo na Mheshimiwa Mikhail Bogdanov, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Shirikisho la Urusi katika Ofisi Ndogo ya Wizara Jijini Dar es Salaam.
Katika mazungumzo hayo, Waheshimiwa Mawaziri 
wamezungumzia masuala mbalimbali yaliyolenga kuboresha na kuimarisha uhusiano na ushirikiano baina ya mataifa haya mawili, hususan, katika Nyanja ya kidiplomasia, nishati, biashara na uwekezaji. Naibu Waziri huyo yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya siku  mbili. 
Waheshimiwa Mawaziri wanaendelea na mazungumzo hayo, huku ujumbe aliofuatana nao Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi ukifuatilia mazungumzo hayo


Kutoka kushoto ni Balozi wa Tanzania nchini Urusi, Mej. Jenerali mstaafu Simon Mumwi, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika, Bw. Jestas Nyamanga, Balozi wa Urusi nchini Tanzania, Mhe. Yuri Popov na Afisa wa Ubalozi wa Urusi nchini Tanzania wakifuatilia mazungumzo ya Waheshimiwa Mawaziri.

Tuesday, March 12, 2019

Prof. Kabudi na Dkt. Mahiga wakabidhiana majengo ya ofisi za Wizara zao Mtumba

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga akimkabidhi Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, mchoro wa jengo la Ofisi za Wizara ya Mambo ya  Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki zinazojengwa kwenye Mji wa Serikali uliopo Mtumba, Dodoma. Makabidhiano hayo yalifanyika tarehe 12 Machi 2019. Baada ya kukabidhiwa Prof. Kabudi alipongeza jitihada za Wizara chini ya usimamizi wa Mhe. Dkt. Mahiga kwa hatua kubwa iliyofikiwa kwenye ujenzi huo.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Prof. Sifuni Mchome akitoa maelezo mafupi kwa Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mhe. Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Katiba na Sheria walipofika  kwenye ofisi za Wizara ya Katiba na Sheria zinazojengwa kwenye mji wa Serikali uliopo, Mtumba jijini Dodoma kwa ajili ya makabidhiano.
Mhe. Prof. Kabudi na Mhe. Dkt. Mahiga wakiwa kwenye moja ya chumba cha jengo la  ofisi za Wizara  zinazojengwa Mtumba


Mhe. Prof. Kabudi akisalimiana na mmoja wa Wakurugenzi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa alipotembelea ofisi za Wizara zinazojengwa Mtumba
Mhe. Prof. Kabudi akiongozana na Mhe. Dkt. Mahiga kuelekea kwenye jengo la Wizara, Mtumba
Mhe. Prof. Kabudi akisaini kitabu cha wageni na kutoa maoni yake kuhusu maendeleao ya ujenzi  wa ofisi hizo 
Mhe. Prof. Kabudi na Mhe. Dkt. Mahiga wakiwa katika picha ya pamoja na Wakuu wa Idara na Vitengo na mafundi wanaojenga jengo la ofisi za Wizara zilizopo Mtumba
Muonekano wa jengo la ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki linalojengwa kwenye mji wa Serikali uliopo Mtumba, Dodoma











Prof. Kabudi na Dkt. Mahiga wakabidhiana ofisi

Waziri wa Katiba na Sheria ambaye awali alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga (kulia) akikabidhi Taarifa ya Makabidhiano ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe.  Prof. Palamagamba Kabudi ambaye awali alikuwa Waziri wa Katiba na Sheria. Makabidhiano hayo yalifanyika jijini Dodoma tarehe 12 Machi 2019.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba Kabudi (kushoto) akimkabidhi Taarifa ya Makabidhiano ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga. 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akiweka saini Kitabu cha mahudhurio mara baada ya kukabidhiwa ofisi jijini Dodoma.
Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga akiongea na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi mara baada ya makabidhiano ya ofisi.
Wakuu wa Idara na Vitengo wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakishuhudia makabidhiano ya ofisi kati ya Waziri wa Katiba na Sheria na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akiongea na Wakuu wa Idara na Vitengo (hawapo pichani) baada ya kukabidhiwa ofisi na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga.
Wakuu wa Idara na Vitengo wakimsikiliza Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki (hayupo pichani).
Wakuu wa Idara na Vitengo wakimsikiliza Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiongea na Wakuu wa Idara na Vitengo wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu, Bi Savera Kazaura akitoa maelezo kwa  Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Waziri wa Katiba na Sheria kabla zoezi la makabidhiano kuanza.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akisalimiana na baadhi ya watumishi mara baada ya kuwasili katika Ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Anayemkaribisha  ni mmoja wa watumishi hao, Bw. Shaban Mtambo.
Bi. Chiku Kiguhe akisalimiana na Mhe. Prof. Kabudi.
Bw. Habibu Ibrahim akisalimiana na Mhe. Waziri.
Bw. Maulidi Mkenda akisalimiana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiongea na baadhi ya watumishi waliojitokeza kumpokea mara alipowasili kwa mara ya kwanza katika ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje jijini Dodoma.
Bw. Caesar Waitara akisalimiana na Mhe. Prof. Kabudi