Friday, March 15, 2019

Tanzania yashiriki katika mkutano wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika




Katibu Mtendaji wa  Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Bi. Stergomena Tax, akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano wa  Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC Council of Ministers),  unaofanyika Windhoek, Namibia, kuanzia tarehe 15 -17 Machi, 2019.  
Mkutano huu, unahudhuriwa na Mawaziri wa Mambo ya Nje, Mawaziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji na Mawaziri wa Fedha pamoja nchi 16 wanachama wa SADC ambapo Tanzania inawakilishwa katika mkutano huu na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi (Mb.); Waziri Ofisi ya Rais, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Issa Haji Ussi Gavu; Waziri wa Viwanda na  Biashara, Mhe. George Kakunda (Mb.); na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji (Mb.). 
Masuala yanayojadiliwa katika mkutano huu ni pamoja na  Taarifa ya Utekelezaji wa mipango na mikakati ya SADC; Taarifa ya Kamati ya Fedha kwa mwaka wa fedha 2018/2019 na Kamati ya Usimamizi wa Rasilimali watu; Hatua zilizofikiwa katika mchakato wa Visiwa vya Komoro kujiunga na SADC na Mpango wa Kuanzisha chuo cha Uhawilishwaji cha SADC (SADC  University of Transformation).
Masuala mengine yanayotarajiwa kujadiliwa katika mkutano huu ni pamoja  na; Uendelezaji wa viwanda katika kanda; Utekelezaji wa Mkakati wa Kanda wa Mawasiliano; Mabadiliko ya Kitaasisi katika Umoja wa Afrika(AU); na Majadiliano ya Ubia Mpya Baina ya Nchi za Kundi la Afrika, Carribean na Pasifiki (ACP) na Umoja wa Ulaya (EU), baada ya mkataba wa Cotonou kumalizika mwaka 2020.
Mkutano huu umetanguliwa na Kikao cha Makatibu Wakuu pamoja na maafisa waandamizi  uliofanyika kuanzia tarehe 11 - 14 Machi, 2019, Windhoek. Namibia. Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Faraji Mnyepe, ameongoza ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo.




Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirkiano wa Afrika Mashariki Prof. Kabudi akifuatilia hotuba ya Katibu Mtendaji wa SADC.


Naibu Waziri Mkuu wa Namibia ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo na Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri la SADC, Mhe.Netumbo Nandi-Ndaitwah,  akitoa hotuba wakati wa mkutano huo.
Wajumbe  kutoka nchi za Tanzania, Zambia  na Afrika Kusini, wakifuatilia hotuba ya Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri la SADC, Mhe. Nandi-Ndaitwah.


Mawaziri wa SADC wakiwa katika picha ya pamoja.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.